Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI

Jinsi Viumbe wa Roho Wanavyohusika Maishani Mwetu

Jinsi Viumbe wa Roho Wanavyohusika Maishani Mwetu
  • Je, malaika huwasaidia watu?

  • Roho waovu wamekuwa na uvutano gani kwa wanadamu?

  • Je, tuna sababu ya kuwaogopa roho waovu?

1. Kuna faida gani kujifunza kuhusu malaika?

KWA kawaida kumjua mtu kunatia ndani kuijua familia yake pia. Vivyo hivyo, kumjua Yehova Mungu hutia ndani kuwajua vizuri zaidi malaika ambao ni sehemu ya familia yake. Biblia huwaita malaika hao ‘wana wa Mungu.’ (Ayubu 38:7) Kwa hiyo, wana jukumu gani katika kusudi la Mungu? Je, wametimiza lolote katika historia ya wanadamu? Je, malaika wanahusika maishani mwako? Ikiwa ndivyo, jinsi gani?

2. Malaika walitoka wapi, na ni wangapi?

2 Malaika hutajwa katika Biblia mara nyingi sana. Hebu tuchunguze baadhi ya maandiko hayo ili tujifunze mengi zaidi kuwahusu. Malaika walitoka wapi? Andiko la Wakolosai 1:16 linasema hivi: “Kwa njia yake [Yesu Kristo] vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani.” Kwa hiyo, viumbe wote wa roho wanaoitwa malaika waliumbwa moja kwa moja na Yehova Mungu kupitia Mwana wake mzaliwa wa kwanza. Kuna malaika wangapi? Biblia inaonyesha kwamba mamia ya mamilioni ya malaika waliumbwa, na wote wana nguvu nyingi.—Zaburi 103:20. *

3. Andiko la Ayubu 38:4-7 linatuambia nini kuhusu malaika?

3 Neno la Mungu, Biblia, linatuambia kwamba msingi wa dunia ulipowekwa, ‘wana wote wa Mungu walianza kupaaza sauti kwa kushangilia.’ (Ayubu 38:4-7) Kwa hiyo malaika walikuwako muda mrefu kabla ya wanadamu kuumbwa, hata kabla ya kuumbwa kwa dunia. Andiko hilo la Biblia linaonyesha pia kwamba malaika wana hisia kwa sababu linasema “walipiga vigelegele pamoja kwa shangwe.” Ona kwamba “wana wote wa Mungu” walishangilia pamoja. Wakati huo, malaika wote walikuwa sehemu ya familia yenye umoja iliyokuwa ikimtumikia Yehova Mungu.

UTEGEMEZO NA ULINZI WA MALAIKA

4. Biblia inaonyeshaje kwamba malaika waaminifu wanapendezwa na utendaji wa wanadamu?

4 Tangu waliposhuhudia kuumbwa kwa wanadamu wa kwanza, viumbe wa roho walio waaminifu wamependezwa sana na familia ya wanadamu inayoongezeka na wamependezwa pia na kutimizwa kwa kusudi la Mungu. (Methali 8:30, 31; 1 Petro 1:11, 12) Hata hivyo, kadiri wakati ulivyopita, malaika waliona kwamba wanadamu wengi walikuwa wakiacha kumtumikia Muumba wao mwenye upendo. Bila shaka jambo hilo liliwahuzunisha malaika waliokuwa waaminifu. Kwa upande mwingine, hata mwanadamu mmoja tu anapomrudia Yehova, “shangwe hutokea kati ya malaika.” (Luka 15:10) Kwa kuwa malaika hupendezwa sana na hali nzuri ya wale wanaomtumikia Mungu, haishangazi kwamba Yehova amekuwa akiwatumia malaika kuwaimarisha na kuwalinda watumishi wake waaminifu walio duniani. (Waebrania 1:7, 14) Fikiria mifano kadhaa.

“Mungu wangu mwenyewe alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.”—Danieli 6:22

5. Biblia inataja mifano gani ambayo inaonyesha jinsi malaika wanavyowategemeza watumishi wa Mungu?

5 Malaika wawili walimsaidia yule mwanamume mwadilifu Loti pamoja na binti zake waokoke kuharibiwa kwa majiji yaliyojaa uovu ya Sodoma na Gomora, kwa kuwaongoza kutoka katika eneo hilo. (Mwanzo 19:15, 16) Karne nyingi baadaye, nabii Danieli alitupwa katika shimo la simba, hata hivyo hakupatwa na madhara yoyote naye alisema hivi: “Mungu wangu mwenyewe alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:22) Katika karne ya kwanza W.K., malaika alimweka huru mtume Petro kutoka gerezani. (Matendo 12:6-11) Isitoshe, malaika walimtia nguvu Yesu mwanzoni mwa huduma yake hapa duniani. (Marko 1:13) Pia, muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu, malaika alimtokea, “akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Lazima hilo lilimfariji Yesu kama nini katika nyakati hizo muhimu sana maishani mwake!

6. (a) Malaika huwalindaje watumishi wa Mungu leo? (b) Tutachunguza maswali gani sasa?

6 Leo, malaika hawawatokei kihalisi watumishi wa Mungu walio duniani. Ingawa hawaonekani, malaika wa Mungu wenye nguvu bado huwalinda watumishi wake, hasa dhidi ya madhara yoyote ya kiroho. Biblia inasema hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.” (Zaburi 34:7) Kwa nini maneno hayo yanapaswa kutufariji sana? Kwa sababu kuna roho waovu hatari, wanaotaka kutuangamiza! Ni nani hao? Wanatoka wapi? Wanajaribu kutuumiza jinsi gani? Ili kupata majibu, na tuchunguze kifupi jambo lililotokea mwanzoni mwa historia ya wanadamu.

VIUMBE WA ROHO AMBAO NI ADUI ZETU

7. Shetani alifanikiwa kadiri gani kuwageuza watu waache kumtumikia Mungu?

7 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 3 ya kitabu hiki, mmoja wa malaika alikuza tamaa ya kuwatawala wengine na hivyo akamwasi Mungu. Baadaye, malaika huyo akaja kuitwa Shetani Ibilisi. (Ufunuo 12:9) Kwa karne 16 tangu alipomdanganya Hawa, Shetani alifanikiwa kuwageuza karibu watu wote waache kumtumikia Mungu isipokuwa waaminifu wachache, kama vile Abeli, Enoko, na Noa.—Waebrania 11:4, 5, 7.

8. (a) Malaika fulani walikujaje kuwa roho waovu? (b) Roho waovu walilazimika kufanya nini ili kuokoka Mafuriko ya siku za Noa?

8 Katika siku za Noa, malaika wengine walimwasi Yehova. Waliacha mahali pao katika familia ya Mungu ya kimbingu, wakaja duniani, na kujivika miili yenye nyama. Kwa nini? Tunasoma hivi katika Mwanzo 6:2: “Wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” Hata hivyo, Yehova Mungu hakuachilia matendo ya malaika hao na ufisadi wao uendelee kati ya wanadamu. Alileta mafuriko duniani, akawafagilia mbali wanadamu wote waovu na kuwahifadhi watumishi wake waaminifu. (Mwanzo 7:17, 23) Hivyo, malaika hao waasi, au roho waovu, walilazimika kuiacha miili yao yenye nyama na kurudi mbinguni wakiwa viumbe wa roho. Walikuwa wamejiunga na Ibilisi, aliyekuwa “mtawala wa roho waovu.”—Mathayo 9:34.

9. (a) Ni nini kilichowapata roho waovu waliporudi mbinguni? (b) Tutachunguza nini kuhusiana na roho waovu?

9 Waliporudi mbinguni, malaika hao waasi walitengwa na familia ya Mungu, kama alivyotengwa Shetani, mtawala wao. (2 Petro 2:4) Ingawa kwa sasa hawawezi kujivika miili ya kibinadamu, bado wana uvutano mbaya sana kwa wanadamu. Shetani, akisaidiwa na roho hao waovu, ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9; 1 Yohana 5:19) Jinsi gani? Malaika hao hutumia hasa njia ambazo zinakusudiwa kuwapotosha wanadamu. (2 Wakorintho 2:11) Hebu tuchunguze baadhi ya njia hizo.

JINSI ROHO WAOVU WANAVYOPOTOSHA

10. Kuwasiliana na pepo huhusisha nini?

10 Roho waovu hutumia mazoea ya kuwasiliana na pepo ili kuwapotosha watu. Mazoea hayo huhusisha roho waovu, kwa njia ya moja kwa moja au kupitia mwanadamu mwingine. Biblia hushutumu mazoea ya kuwasiliana na pepo nayo hutuonya tujiepushe na kila kitu kinachohusiana na mazoea hayo. (Wagalatia 5:19-21) Roho waovu hutumia mazoea ya kuwasiliana na pepo kama vile mvuvi anavyotumia chambo kwenye ndoana. Mvuvi hutumia vyambo vya aina mbalimbali ili kunasa samaki wa namna mbalimbali. Vivyo hivyo, roho waovu hutumia njia mbalimbali za kuwasiliana na pepo ili kuwanasa watu wa namna zote.

11. Uaguzi ni nini, na kwa nini tunapaswa kuuepuka?

11 Chambo kimoja kinachotumiwa na roho waovu ni uaguzi. Uaguzi ni nini? Ni kujaribu kujua habari za wakati ujao au jambo lisilojulikana. Uaguzi unatia ndani kuangalia nyota, kusoma kadi za karata, kutazama mpira wa kioo, kusoma viganja vya mkono, kutafuta ndege au ishara mbaya, na kufasiri ndoto. Ingawa watu wengi hufikiri kwamba uaguzi hauna madhara yoyote, Biblia huonyesha kwamba wabashiri hushirikiana na roho waovu. Kwa mfano, andiko la Matendo 16:16-18 linamtaja “roho mwovu wa uaguzi” ambaye alimwezesha kijakazi kufanya “ufundi wa kubashiri.” Lakini, roho huyo mwovu alipomtoka, alipoteza uwezo wa kubashiri.

Roho waovu hutumia njia mbalimbali kuwadanganya watu

12. Kwa nini ni hatari kujaribu kuwasiliana na wafu?

12 Njia nyingine ambayo roho waovu hutumia kuwapotosha watu ni kuwachochea watafute habari za wafu. Mara nyingi, watu wanaoomboleza kifo cha mpendwa wao huamini mambo ya uwongo kuhusu waliokufa. Mtu mwenye uwezo wa kuwasiliana na pepo anaweza kutoa ujumbe wa pekee au anaweza kuongea kwa sauti kama ya mtu aliyekufa. Ndiyo sababu watu wengi husadiki kwamba wafu wako hai na kwamba kuwasiliana nao kutawasaidia walio hai kuvumilia huzuni yao. Lakini “faraja” ya aina hiyo ni ya uwongo na ni hatari. Kwa nini? Kwa sababu roho waovu wanaweza kuiga sauti ya mtu aliyekufa na kumpa mtu anayewasiliana na pepo habari kumhusu mfu huyo. (1 Samweli 28:3-19) Isitoshe, kama tulivyojifunza katika Sura ya 6, wafu hawaendelei kuishi. (Zaburi 115:17) Kwa hiyo, “yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu” amepotoshwa na roho waovu na anatenda kinyume cha mapenzi ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 18:10, 11; Isaya 8:19) Basi, uwe mwangalifu usije ukanaswa na chambo hicho hatari kinachotumiwa na roho waovu.

13. Watu wengi ambao zamani waliwaogopa roho waovu wamefaulu kufanya nini?

13 Mbali na kuwapotosha watu, roho waovu huwatisha pia. Leo, Shetani na roho wake waovu wanajua kwamba wana “kipindi kifupi cha wakati” kabla hawajakomeshwa, na sasa ni wakatili kuliko wakati mwingine wowote. (Ufunuo 12:12, 17) Hata hivyo, maelfu ya watu ambao hapo zamani walikuwa wakiwaogopa roho waovu, sasa hawawaogopi kamwe. Ni nini kimewasaidia? Mtu anaweza kufanya nini hata ikiwa anashiriki katika mazoea ya kuwasiliana na pepo?

JINSI YA KUWAPINGA ROHO WAOVU

14. Tunawezaje kuacha kuwasiliana na roho waovu kama walivyofanya Wakristo wa Efeso katika karne ya kwanza?

14 Biblia inatueleza jinsi ya kuwapinga roho waovu na jinsi ya kuvunja uhusiano nao. Fikiria mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza katika jiji la Efeso. Baadhi yao walikuwa na mazoea ya kuwasiliana na pepo kabla ya kuwa Wakristo. Walipoamua kuacha mazoea hayo, walifanya nini? Biblia inasema: “Hesabu kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi wakaleta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mtu.” (Matendo 19:19) Kwa kuharibu vitabu vyao vya uchawi, Wakristo hao wapya waliwawekea mfano wale wanaotaka kuwapinga roho waovu leo. Watu wanaotaka kumtumikia Yehova wanapaswa kuharibu kila kitu kinachohusiana na mazoea ya kuwasiliana na pepo. Vitu hivyo vinatia ndani vitabu, magazeti, sinema, vibandiko, na miziki inayowachochea watu kuwasiliana na pepo na kuona mazoea hayo kuwa yenye kuvutia na kusisimua. Vitu vingine ambavyo pia vinapaswa kuharibiwa ni hirizi au chochote kinachovaliwa ili kumlinda mtu asipatwe na mabaya.—1 Wakorintho 10:21.

15. Tunahitaji kufanya nini ili kuwapinga roho waovu?

15 Miaka kadhaa baada ya Wakristo wa Efeso kuharibu vitabu vyao vya uchawi, mtume Paulo aliwaandikia hivi: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12) Roho waovu hawakuwa wamekata tamaa. Bado walikuwa wakijaribu kuwanasa. Kwa hiyo, Wakristo hao walihitaji kufanya nini? Paulo alisema, “Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu [Shetani].” (Waefeso 6:16) Kadiri ngao yetu ya imani ilivyo na nguvu, ndivyo tutakavyowapinga roho waovu kwa nguvu.—Mathayo 17:20.

16. Tunawezaje kuwa na imani yenye nguvu?

16 Basi, tunawezaje kuimarisha imani yetu? Kwa kujifunza Biblia. Ili ukuta uwe imara, ni lazima msingi wake uwe na nguvu. Vivyo hivyo, ili imani yetu iwe na nguvu ni lazima tuwe na msingi imara, ambao ni ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, Biblia. Tukisoma na kujifunza Biblia kila siku, imani yetu itakuwa na nguvu. Sawa na ukuta imara, imani hiyo itatukinga dhidi ya uvutano wa roho waovu.—1 Yohana 5:5.

17. Ni hatua gani nyingine tunayohitaji kuchukua ili kuwapinga roho waovu?

17 Wakristo wa Efeso walihitaji kuchukua hatua gani nyingine? Walihitaji ulinzi zaidi kwa sababu walikuwa wakiishi katika jiji lililojaa mazoea ya roho waovu. Kwa hiyo Paulo aliwaambia hivi: ‘Kwa kila namna ya sala na dua, endelezeni sala kila wakati katika roho.’ (Waefeso 6:18) Kwa kuwa sisi pia tunaishi katika ulimwengu uliojaa mazoea ya roho waovu, tunahitaji kumwomba Yehova kwa bidii ili atulinde dhidi ya roho hao waovu. Bila shaka, tunahitaji kulitumia jina la Yehova katika sala zetu. (Methali 18:10) Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kumwomba Mungu ‘atukomboe kutokana na yule mwovu,’ Shetani Ibilisi. (Mathayo 6:13) Yehova atajibu sala hizo tunazotoa kwa bidii.—Zaburi 145:19.

18, 19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba tutashinda vita dhidi ya viumbe waovu wa roho? (b) Sura inayofuata itajibu swali gani?

18 Roho waovu ni hatari, hata hivyo, ikiwa tunampinga Ibilisi na kumkaribia Mungu kwa kufanya mapenzi Yake, hatutaishi kwa woga. (Yakobo 4:7, 8) Nguvu za roho waovu zina mipaka. Waliadhibiwa katika siku za Noa, nao watapata hukumu yao ya mwisho. (Yuda 6) Pia, kumbuka kwamba malaika wenye nguvu wa Yehova hutulinda. (2 Wafalme 6:15-17) Malaika hao wangependa sana kuona tukifaulu kuwashinda roho waovu. Malaika hao waadilifu wanatushangilia. Basi, na tukae karibu na Yehova na familia yake ya viumbe waaminifu wa roho. Na tuepuke pia kila namna ya kuwasiliana na pepo na sikuzote tutumie shauri la Neno la Mungu maishani mwetu. (1 Petro 5:6, 7; 2 Petro 2:9) Tukifanya hivyo, tutashinda vita tunavyopigana na viumbe waovu wa roho.

19 Lakini kwa nini Mungu ameachilia roho waovu na uovu ambao umefanya watu wateseke sana? Swali hilo litajibiwa katika sura inayofuata.

^ fu. 2 Andiko la Ufunuo 5:11 linasema hivi kuhusu malaika waadilifu: “Hesabu yao ilikuwa makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu.” Kwa hiyo, Biblia inaonyesha kwamba mamia ya mamilioni ya malaika waliumbwa.