Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI

Viumbe vya Kiroho—Ni Marafiki ao Maadui Wetu?

Viumbe vya Kiroho—Ni Marafiki ao Maadui Wetu?
  • Malaika wanatusaidia namna gani?

  • Mashetani wanawachochea watu wafanye nini?

  • Je, tunapaswa kuogopa mashetani?

1. Kwa nini ni vizuri tuwajue malaika?

KWA kawaida unapomujua mutu ni vizuri pia uijue familia yake. Vilevile, unapomujua Yehova Mungu ni vizuri uijue pia familia yake iliyo huko mbinguni, yaani, malaika. Katika Biblia malaika wanaitwa “wana wa Mungu.” (Ayubu 38:7) Basi, malaika hao wana kazi gani katika kusudi la Mungu? Je, malaika wamewasaidia wanadamu wakati wa zamani? Malaika wanaweza kukusaidia namna gani?

2. Ni nani aliyewaumba malaika, na ni wangapi?

2 Maandiko mengi katika Biblia yanazungumuza juu ya malaika. Basi, acha tuchunguze maandiko fulani kati ya hayo ili tuwajue vizuri. Ni nani aliyewaumba? Andiko la Wakolosai 1:16 linasema hivi: “Kwa njia yake [Yesu Kristo] vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani.” Kwa hiyo, ni Yehova Mungu aliyeumba malaika, kupitia Mwana wake muzaliwa wa kwanza. Mungu aliumba malaika wangapi? Biblia inaonyesha kama Mungu aliumba mamia ya mamilioni ya malaika, na wote wana nguvu nyingi.​—Zaburi 103:20. *

3. Andiko la Ayubu 38:4-7 linafundisha nini juu ya malaika?

3 Biblia, Neno la Mungu, inatuambia kama wakati Mungu alipoumba dunia, ‘wana wote wa Mungu walianza kupaaza sauti kwa kushangilia.’ (Ayubu 38:4-7) Hilo linaonyesha kama malaika walikuwako tangu zamani sana mbele ya kuumbwa kwa wanadamu, na hata mbele ya kuumbwa kwa dunia. Andiko hilo pia linaonyesha kama malaika wanaweza kufurahi ao kusikia huzuni, kwa sababu linasema ‘walipiga vigelegele pamoja kwa shangwe.Tunaona kama “wana wote wa Mungu” walishangilia pamoja. Wakati huo, malaika wote walikuwa katika familia yenye umoja; wote walikuwa wanamutumikia Yehova Mungu.

MALAIKA WANATUSAIDIA NA KUTULINDA

4. Namna gani Biblia inaonyesha kama malaika waaminifu wanapendezwa na mambo ambayo sisi wanadamu tunafanya?

4 Tangu walipojionea kuumbwa kwa wanadamu wa kwanza, malaika waaminifu wamependezwa sana na mambo ya wanadamu wanaozidi kuongezeka na pia wamependezwa na kutimizwa kwa kusudi la Mungu. (Methali 8:30, 31; 1 Petro 1:11, 12) Lakini, kadiri wakati ulivyopita, malaika waliona namna wanadamu wengi walikuwa wakiacha kumutumikia Muumbaji wao mwenye upendo. Hakika, jambo hilo liliwahuzunisha malaika hao waaminifu. Hata hivyo, wakati mutu mumoja tu anamurudilia Yehova, malaika wanafurahi sana. (Luka 15:10) Kwa kuwa malaika wanahangaikia hivyo hali nzuri ya wale wanaomutumikia Mungu, tunaelewa kwa nini mara nyingi Mungu aliwatumia malaika ili kuwatia nguvu na kuwasaidia watumishi wake waaminifu walio duniani. (Waebrania 1:7, 14) Tuchukue mifano fulani.

‘Mungu wangu mwenyewe alimutuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.’​—Danieli 6:22

5. Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha kama malaika wapo tayari kusaidia watumishi wa Mungu?

5 Malaika wawili walimusaidia Loti, mutu mwenye haki, pamoja na binti zake ili waokoke; wakati miji ya Sodoma na Gomora iliyojaa uovu ilipoharibiwa, malaika waliwaondoa humo. (Mwanzo 19:15, 16) Miaka mingi kisha hapo, nabii Danieli alitupwa katika shimo la simba, lakini simba hao hawakumufanya kitu, yeye mwenyewe alisema: ‘Mungu wangu mwenyewe alimutuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.’ (Danieli 6:22) Malaika alimufungua mutume Petro na kumutoa katika gereza. (Matendo 12:6-11) Tena malaika walimutia Yesu moyo alipoanza kazi yake ya kuhubiri duniani. (Marko 1:13) Muda mufupi mbele ya Yesu kufa, malaika alimutokea na ‘akamutia nguvu.’ (Luka 22:43) Kwa kweli, musaada huo wa malaika ulimufariji Yesu katika nyakati hizo za maana sana za maisha yake!

6. (a) Namna gani malaika wanawalinda watumishi wa Mungu leo? (b) Tutapenda kupata jibu ya maulizo gani?

6 Leo, malaika hawawatokei tena watumishi wa Mungu duniani kama zamani. Hata hivyo, malaika hao wenye nguvu wanaendelea kuwalinda watumishi wa Mungu; wanawalinda hasa na mambo yanayoweza kuharibu uhusiano wao na Mungu. Biblia inasema hivi: ‘Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomuogopa, na yeye huwaokoa.’ (Zaburi 34:7) Kwa nini maneno hayo yanapaswa kututia moyo? Kwa sababu kuna viumbe vya kiroho wabaya walio hatari wanaokusudia kutuangamiza! Wao ni nani? Walitoka wapi? Namna gani wanajaribu kututendea vibaya? Ili kupata majibu ya maulizo hayo, acha tuzungumuzie kwa kifupi jambo lililotokea mwanzoni mwa historia ya wanadamu.

VIUMBE VYA KIROHO AMBAO NI MAADUI WETU

7. Ni watu wangapi Shetani alifikia kufanya wamuache Mungu?

7 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 3, malaika mumoja alikomalisha tamaa ya kuwatawala wengine na hivyo akamuasi Mungu. Mwishowe, malaika huyo akaitwa Shetani Ibilisi. (Ufunuo 12:9) Kwa muda wa miaka 1 600 hivi, tangu wakati alipomudanganya Eva, Shetani alifikia kufanya watu karibu wote wamuache Mungu; wachache tu kama vile Abeli, Enoko, na Noa ndio waliobaki waaminifu.​—Waebrania 11:4, 5, 7.

8. (a) Namna gani malaika fulani waligeuka kuwa mashetani? (b) Ili wasikufe katika Garika ya siku za Nao, malaika hao wabaya walifanya nini?

8 Katika siku za Noa, malaika wengine walimuasi Yehova. Waliacha nafasi yao katika familia ya Mungu huko mbinguni, wakaja duniani, na wakavaa miili ya wanadamu. Sababu gani? Katika andiko la Mwanzo 6:2, tunasoma hivi: “Wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” Lakini, Yehova Mungu hakuachilia malaika hao waendelee na matendo yao maovu na waendelee kuwadanganya wanadamu. Alileta garika kubwa duniani, ikawafagia wanadamu wote wabaya, lakini akawalinda watumishi wake waaminifu. (Mwanzo 7:17, 23) Kwa hiyo, malaika hao waasi, ao mashetani, waliondoa miili ya wanadamu waliyovaa na wakarudi tena mbinguni katika mwili wao wa kiroho. Walijitia hivyo upande wa Ibilisi, ambaye sasa alikuwa ‘mutawala wa roho waovu.’​—Mathayo 9:34.

9. (a) Ni jambo gani liliwapata malaika hao wabaya waliporudi mbinguni? (b) Tutajifunza nini juu ya mashetani?

9 Malaika hao wasiotii waliporudi mbinguni, walikataliwa kuingia tena katika familia ya Mungu, kama vile mutawala wao Shetani alivyokataliwa. (2 Petro 2:4) Leo, malaika hao hawana uwezo wa kuvaa tena miili ya wanadamu, hata hivyo, wanawashawishi wanadamu kufanya mambo mabaya. Kwa kweli, Shetani akiwa mwenye kusaidiwa na mashetani hao, ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9; 1 Yohana 5:19) Namna gani? Mara nyingi, mashetani hao wanatumia njia mbalimbali ili kuwapoteza watu. (2 Wakorintho 2:11) Tuone sasa njia fulani ambazo wanatumia.

NAMNA MASHETANI WANAVYOWADANGANYA WATU

10. Namna gani mutu anaweza kuzungumuza na mashetani?

10 Ili kuwadanganya watu malaika hao wabaya, ao mashetani wanatumia mazoea yanayowavutia watu wazungumuze nao. Mutu anaweza kuzungumuza moja kwa moja na mashetani hao ao kupitia muchawi. Biblia inakataza kabisa mazoea ya kuzungumuza na mashetani na inatuambia tujiepushe na kila kitu kinachopatana na mazoea hayo. (Wagalatia 5:19-21) Mashetani wanatumia njia hiyo kama vile muvuaji wa samaki anavyotumia chambo (ao chakula) kwenye ndoano. Muvuaji wa samaki anatumia vyambo vya aina mbalimbali ili kunasa samaki wa aina mbalimbali. Vilevile mashetani wanatumia njia mbalimbali ili watu wavutiwe kuzungumuza nao na kuwafanya hivyo kuwa watumwa wao.

11. Uaguzi ni nini, na sababu gani tunapaswa kuepuka uaguzi?

11 Uaguzi ni aina moja ya chambo ambacho mashetani wanatumia. Uaguzi ni nini? Ni kujaribu kujua habari za wakati ujao ao jambo fulani lisilojulikana. Kuna aina mbalimbali za uaguzi: kuangalia nyota, kutabiri kwa kutumia karata, kwa kutazama kitu kilicho kama kioo, kwa kutazama mikono, kwa kutafsiri ndoto ao ishara za ndege. Hata ikiwa watu wengine wanawaza kama uaguzi hauna hatari yoyote, Biblia inaonyesha kuwa watu wenye kuagua wanafanya uhusiano na mashetani. Kwa mufano, andiko la Matendo 16:16-18 linamutaja ‘roho [pepo] muovu wa uaguzi’ ambaye alimuwezesha kijakazi kufanya “ufundi wa kubashiri.” Lakini, wakati pepo huyo alimutoka, kijakazi huyo alipoteza uwezo aliokuwa nao wa kutabiri.

Mashetani wanatumia njia mbalimbali ili kuwadanganya watu

12. Kujaribu kuzungumuza na watu waliokufa kuna hatari gani?

12 Mashetani wanadanganya pia watu kwa kuwachochea waulize mambo kutoka kwa watu waliokufa. Watu walio katika kilio cha mutu fulani aliyekufa waliyemupenda sana, mara nyingi wanakubali haraka mambo ya uongo juu ya watu waliokufa. Muchawi aliye na uwezo wa kuzungumuza na mashetani anaweza kuwaambia jambo fulani ao kuongea kwa sauti iliyo kama ya mutu huyo aliyekufa. Jambo hilo linawafanya watu wengi waamini kama watu waliokufa wanaendelea kuishi na kama kuzungumuza nao kunaweza kutuliza huzuni ya waliobaki. Lakini “faraja” kama hiyo ni ya uongo na ni hatari. Sababu gani? Kwa sababu mashetani wanaweza kuiga sauti ya mutu aliyekufa na kumupa muchawi anayezungumuza nao habari juu ya mutu huyo. (1 Samweli 28:3-19) Zaidi ya hilo, katika Sura ya 6, tulijifunza kama watu waliokufa hawaendelei kuishi. (Zaburi 115:17) Basi, mutu “yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu” anadanganywa na roho wabaya na anatenda kinyume na mapenzi ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 18:10, 11; Isaya 8:19) Kwa hiyo, fanya angalisho ili usinaswe na chambo hicho hatari ambacho mashetani wanatumia.

13. Watu wengi ambao hapo mbele walikuwa wakiogopa mashetani walifikia kufanya nini?

13 Malaika hao wabaya hawawadanganyi tu watu lakini pia wanawaogopesha. Leo, Shetani na mashetani wake wanajua kama wanabaki tu na “kipindi kifupi cha wakati” mbele ya kuachishwa kazi yao; kwa hiyo wanakuwa wakali zaidi. (Ufunuo 12:12, 17) Hata hivyo, watu wengi ambao hapo mbele walikuwa wakiogopa sana roho hao wabaya, sasa hawawaogopi tena. Ni jambo gani lililowasaidia? Mutu aliye na mazoea ya kuzungumuza na roho wabaya ao pepo anaweza kufanya nini?

NAMNA YA KUWAPINGA ROHO WABAYA

14. Namna gani mutu anaweza kuachana na mambo ya uchawi, kama Wakristo wapya wa Efeso?

14 Biblia inatufundisha namna ya kuwapinga roho wabaya na namna ya kuachana nao. Wazia mufano wa Wakristo wa wakati wa mitume katika muji wa Efeso. Wengine kati yao, mbele ya kuwa Wakristo, walikuwa na mazoea ya kuzungumuza na roho wabaya. Walipoamua kuachana na mazoea hayo, walifanya nini? Biblia inasema hivi: ‘Hesabu kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi wakaleta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mutu.’ (Matendo 19:19) Kwa kuharibu vitabu vyao vya mambo ya uchawi, Wakristo hao wapya waliwawekea mufano wale wote wanaotaka kupinga roho wabaya leo. Watu wanaotaka kumutumikia Yehova wanapaswa kuharibu kila kitu kinachopatana na mambo ya mashetani. Kwa mufano: vitabu, magazeti, sinema, foto ao picha, miziki; vitu vinavyowachochea watu kuzungumuza na roho wabaya, kuvutiwa na kufurahishwa na jambo hilo. Pia hirizi zinapaswa kuharibiwa ao kifaa chochote kinachovaliwa ili kumulinda mutu asipatwe na mabaya.​—1 Wakorintho 10:21.

15. Tunapaswa kufanya nini ili kuyapinga majeshi ya roho wabaya?

15 Miaka fulani ilipopita, kisha Wakristo hao kuharibu vitabu vyao vya mambo ya uchawi, mutume Paulo aliwaandikia hivi: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12) Mashetani hawakuwaacha mara moja. Walitafuta tu kuwaangusha Wakristo hao. Kwa hiyo, Wakristo hao walipaswa tena kufanya nini? Mutume Paulo alisema: ‘Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mutaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu [Shetani].’ (Waefeso 6:16) Ikiwa ngao yetu ya imani ni yenye nguvu, ndipo tutaweza kuyapinga majeshi ya roho wabaya.​—Mathayo 17:20.

16. Namna gani tunaweza kuifanya imani yetu iwe nguvu?

16 Sasa, ni nini inayoweza kuifanya imani yetu iwe nguvu? Kujifunza Biblia. Musingi ukiwa nguvu, ukuta pia utakuwa nguvu. Vivyo hivyo, imani yetu itakuwa nguvu ikiwa musingi wayo uku nguvu, yaani, ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, Biblia. Ikiwa tunasoma na kujifunza Biblia kila siku, imani yetu itakuwa pia nguvu. Imani yetu itakuwa kama ukuta wenye nguvu, itatukinga ili tusinaswe na mambo ya roho wabaya.​—1 Yohana 5:5.

17. Ni jambo gani lingine inafaa kufanya ili kushindana na roho wabaya?

17 Wakristo hao wapya wa Efeso walipaswa kufanya nini tena? Kwa sababu walikuwa wanaishi katika muji wenye kujaa mambo ya mashetani, walikuwa na lazima ya ulinzi zaidi. Kwa hiyo mutume Paulo aliwaandikia hivi: ‘Kwa kila namna ya sala na dua, endelezeni sala kila wakati katika roho.’ (Waefeso 6:18) Kwa kuwa sisi pia tunaishi katika dunia inayojaa mambo ya mashetani, tunapaswa kumuomba Yehova kwa bidii ili atulinde tunaposhindana na roho hao wabaya. Hakika, tunapaswa kutumia jina la Yehova katika sala zetu. (Methali 18:10) Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kumuomba Mungu ‘atukomboe kutokana na yule muovu,’ Shetani Ibilisi. (Mathayo 6:13) Yehova hatakosa kujibu sala kama hizo za bidii.​—Zaburi 145:19.

18, 19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa hakika kama tutashinda vita tunayopigana na roho hao wabaya? (b) Ni ulizo gani litajibiwa katika sura inayofuata?

18 Roho wabaya ni hatari, hata hivyo hatupaswi kuwaogopa ikiwa tunamupinga Ibilisi na kumukaribia Mungu kwa kufanya mapenzi yake. (Yakobo 4:7, 8) Nguvu za roho wabaya zina mipaka. Waliazibiwa wakati wa garika ya siku za Noa, na sasa wanangojea hukumu yao ya mwisho wakati ujao. (Yuda 6) Tena, kumbuka kama malaika wenye nguvu wa Yehova wanatulinda. (2 Wafalme 6:15-17) Malaika hao wanapenda kabisa tuwashinde roho hao wabaya. Ni kama vile wanatutia moyo ili tusichoke. Kwa hiyo, tubaki karibu na Yehova na familia yake ya viumbe vya kiroho. Tuepuke pia kila aina ya kuzungumuza na roho wabaya na tutumie kila siku shauri la Neno la Mungu katika maisha yetu. (1 Petro 5:6, 7; 2 Petro 2:9) Tukifanya hivyo, hakika tutashinda vita tunayopigana na malaika waovu.

19 Lakini, kwa nini Mungu ameachilia mambo mabaya na malaika hao wabaya waendelee kuwatesa watu sana? Ulizo hilo litajibiwa katika sura inayofuata.

^ fu. 2 Andiko la Ufunuo 5:11 linasema juu ya malaika waaminifu hivi: “Hesabu yao ilikuwa makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu.” Kwa hiyo, Biblia inaonyesha kama Mungu aliumba mamia ya mamilioni ya malaika.