Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA MOJA

Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?

Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?
  • Je, Mungu ndiye anayesababisha kuteseka ulimwenguni?

  • Ni masuala gani yaliyozushwa katika bustani ya Edeni?

  • Mungu atakomeshaje kuteseka kwa wanadamu?

1, 2. Watu wanateseka jinsi gani leo, na hilo huwafanya waulize maswali gani?

BAADA ya vita vya kikatili katika nchi moja, maelfu ya wanawake na watoto waliouawa walizikwa kwenye kaburi la ujumla lililozingirwa na misalaba. Kila msalaba ulikuwa na swali hili: “Kwa nini?” Nyakati nyingine swali hilo huumiza sana. Watu huuliza swali hilo lenye kuhuzunisha wakati vita, msiba, ugonjwa, au uhalifu unaposababisha vifo vya wapendwa wao wasio na hatia, nyumba zao zinapoharibiwa au wanapoteseka sana katika njia nyingine kwa sababu ya vita. Wanataka kujua kwa nini wanapatwa na misiba hiyo.

2 Kwa nini Mungu anawaacha watu wateseke? Ikiwa Yehova Mungu ana nguvu zote, ana upendo, hekima, na haki, kwa nini ulimwengu umejaa chuki na ukosefu wa haki? Je, umewahi kujiuliza maswali hayo?

3, 4. (a) Sababu gani si vibaya kuuliza kwa nini Mungu anawaacha wanadamu wateseke? (b) Yehova anahisije kuhusu uovu na kuteseka?

3 Je, ni vibaya kuuliza kwa nini Mungu anawaacha wanadamu wateseke? Watu fulani huogopa kwamba kuuliza swali kama hilo kutaonyesha kwamba hawana imani au hawamheshimu Mungu. Hata hivyo, unaposoma Biblia utaona kwamba watumishi waaminifu wa Mungu waliuliza maswali kama hayo. Kwa mfano, nabii Habakuki alimuuliza Yehova hivi: “Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana hutokea, kwa nini mzozo huendelezwa?”—Habakuki 1:3.

Yehova atakomesha kabisa kuteseka

4 Je, Yehova alimkemea nabii mwaminifu Habakuki kwa kuuliza maswali hayo? Hapana. Badala yake Mungu aliyatia maneno manyoofu ya Habakuki katika Biblia iliyoandikwa kwa mwongozo wa roho. Pia, Mungu alimsaidia kuelewa mambo zaidi na kuwa na imani zaidi. Yehova anataka kukusaidia vivyo hivyo. Kumbuka, Biblia inafundisha kwamba ‘anakujali.’ (1 Petro 5:7) Hakuna mwanadamu anayechukia uovu na kuteseka kwa wanadamu kama Mungu anavyoyachukia mambo hayo. (Isaya 55:8, 9) Kwa nini basi watu wanateseka sana ulimwenguni?

KWA NINI WATU WANATESEKA SANA?

5. Watu fulani husema ni kwa nini watu wanateseka, lakini Biblia inafundisha nini?

5 Watu wa dini mbalimbali wamewauliza viongozi na walimu wao wa dini kuhusu kinachosababisha watu wateseke sana. Mara nyingi, wanaambiwa kwamba ni mapenzi ya Mungu na kwamba ndiye aliyepanga zamani mambo yatakayowapata wanadamu kutia ndani misiba yenye kuhuzunisha. Wengi huambiwa kwamba njia za Mungu haziwezi kueleweka au Mungu husababisha vifo vya watu, hata watoto, ili wakae pamoja naye huko mbinguni. Hata hivyo, kama ulivyojifunza, Yehova Mungu hasababishi mabaya. Biblia inasema: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu, na Mweza-Yote kutenda isivyo haki!”—Ayubu 34:10.

6. Kwa nini watu wengi humlaumu Mungu isivyofaa kwa sababu ya mambo yanayosababisha kuteseka ulimwenguni?

6 Je, unajua ni kwa nini watu humlaumu Mungu isivyofaa kwa sababu ya mambo yote yanayosababisha kuteseka ulimwenguni? Mara nyingi, wao humlaumu Mungu Mweza-Yote kwa sababu wanafikiri kwamba yeye ndiye anayeutawala ulimwengu huu. Hawajui kweli ya msingi ambayo Biblia hufundisha. Ulijifunza kweli hiyo katika Sura ya 3 ya kitabu hiki. Shetani Ibilisi ndiye anayeutawala ulimwengu huu.

7, 8. (a) Ulimwengu unaonyeshaje utu wa mtawala wake? (b) “Wakati na tukio lisilotazamiwa” pamoja na kutokamilika kwa wanadamu kumesababishaje kuteseka?

7 Biblia hueleza hivi waziwazi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Unapofikiria hilo, je, huoni ni kwa nini ulimwengu uko jinsi ulivyo leo? Ulimwengu unaonyesha utu wa kiumbe huyo wa roho asiyeonekana, “anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Shetani ana chuki, ni mwongo, na mkatili. Kwa hiyo, ulimwengu ulio chini yake umejaa chuki, uwongo, na ukatili. Hiyo ni sababu moja inayowafanya wanadamu wateseke sana leo.

8 Kama ilivyozungumziwa katika Sura ya 3, sababu ya pili ni kwamba wanadamu si wakamilifu nao wamekuwa watenda-dhambi tangu uasi ulipoanza katika bustani ya Edeni. Wanadamu wenye dhambi hung’ang’ania utawala, na hilo hutokeza vita, ukandamizaji, na kuteseka. (Mhubiri 4:1; 8:9) Sababu ya tatu ni “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Katika ulimwengu usiotawaliwa na Yehova, watu wanaweza kuteseka kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.

9. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ana sababu nzuri ya kuwaacha wanadamu waendelee kuteseka?

9 Inatia moyo kujua kwamba Mungu hasababishi kuteseka. Hasababishi vita, uhalifu, ukandamizaji, au hata misiba ya kiasili inayowafanya watu wateseke. Hata hivyo, tunahitaji kujua, Kwa nini Yehova anawaacha wanadamu waendelee kuteseka? Ikiwa yeye ndiye Mweza-Yote, ana nguvu za kukomesha kuteseka. Lakini, kwa nini hachukui hatua? Lazima Mungu mwenye upendo ambaye tumejifunza juu yake awe na sababu nzuri.—1 Yohana 4:8.

SUALA MUHIMU LAZUKA

10. Shetani alipinga nini, na jinsi gani?

10 Ili kufahamu ni kwa nini Mungu amewaacha wanadamu waendelee kuteseka, tunahitaji kujikumbusha jinsi kuteseka kulivyoanza. Shetani alipowachochea Adamu na Hawa wamwasi Yehova, suala muhimu lilizuka. Shetani hakupinga nguvu za Yehova. Hata Shetani mwenyewe anajua kwamba nguvu za Yehova hazina kifani. Badala yake, Shetani alipinga haki ya Yehova ya kutawala. Kwa kudai kwamba Mungu ni mwongo anayewanyima raia zake mambo mazuri, Shetani alikuwa akidai kwamba Yehova ni mtawala mbaya. (Mwanzo 3:2-5) Shetani alidokeza kwamba hali ya wanadamu ingekuwa bora pasipo utawala wa Mungu. Alishambulia enzi kuu ya Yehova, haki yake ya kutawala.

11. Kwa nini Yehova hakuwaangamiza waasi hao katika Edeni?

11 Adamu na Hawa walimwasi Yehova. Ni kana kwamba walisema: “Hatuhitaji kutawaliwa na Yehova. Tunaweza kujiamulia mema na mabaya.” Yehova angetatuaje suala hilo? Angewafundishaje viumbe wake wote wenye akili kwamba waasi hao walikosea na kwamba kwa kweli njia yake ndiyo bora? Huenda mtu akasema kwamba afadhali Mungu angewaangamiza mara moja waasi hao na kuanza upya. Lakini Yehova alikuwa ametaja kusudi lake kwamba uzao wa Adamu na Hawa ujaze dunia, naye alitaka waishi katika paradiso duniani. (Mwanzo 1:28) Yehova hutimiza makusudi yake sikuzote. (Isaya 55:10, 11) Isitoshe, kuwaangamiza waasi hao katika Edeni hakungejibu suala lililokuwa limezuka kuhusu haki ya Yehova ya kutawala.

12, 13. Toa mfano unaoonyesha ni kwa nini Yehova amemruhusu Shetani autawale ulimwengu huu na kwa nini Mungu amewaruhusu wanadamu wajitawale.

12 Hebu tufikirie mfano mmoja. Wazia kwamba mwalimu anawafundisha wanafunzi wake jinsi ya kufanya hesabu fulani ngumu. Mwanafunzi mmoja mwerevu lakini mwasi anadai kwamba mwalimu amekosea. Anadai kwamba mwalimu ameshindwa, na mwasi huyo anasisitiza kwamba anajua njia bora zaidi ya kufanya hesabu hiyo. Wanafunzi fulani wanafikiri kwamba anasema kweli, nao pia wanaasi. Mwalimu afanye nini? Akiwafukuza waasi hao kutoka darasani, wanafunzi wengine wataonaje? Je, hawataamini kwamba mwanafunzi mwenzao na wale waliojiunga naye wanasema kweli? Huenda wale wanafunzi wengine walio darasani wakaacha kumwamini mwalimu wao wakifikiri kwamba anaogopa kuonyeshwa makosa yake. Basi mwalimu angemruhusu mwasi huyo awaonyeshe wanafunzi wenzake jinsi yeye mwenyewe anavyoweza kufanya hesabu hiyo.

Watu wakiomboleza makaburini

13 Yehova amefanya kama mwalimu huyo anavyofanya. Kumbuka kwamba kuna wengi waliohusika mbali na waasi hao katika Edeni. Mamilioni ya malaika walikuwa wakitazama. (Ayubu 38:7; Danieli 7:10) Njia ya Yehova ya kushughulikia uasi huo ingekuwa na matokeo makubwa sana kwa malaika wote na hatimaye viumbe wote wenye akili. Kwa hiyo, Yehova amefanya nini? Amemruhusu Shetani aonyeshe jinsi anavyoweza kuwatawala wanadamu. Mungu amewaruhusu pia wanadamu wajitawale wenyewe wakiwa chini ya uongozi wa Shetani.

14. Kuna faida gani kwa Yehova kuwaruhusu wanadamu wajitawale wenyewe?

14 Katika mfano uliotolewa, mwalimu anajua kwamba yule mwanafunzi mwasi na wale wanaomuunga mkono wamekosea. Lakini pia anajua kwamba kuwapa nafasi ya kujaribu kuthibitisha madai yao kutawafaidi wanafunzi wote darasani. Waasi hao wakishindwa, wale wanafunzi wengine wote wataona kwamba ni mwalimu wao tu anayestahili kulifundisha darasa. Baadaye, mwalimu akiwafukuza waasi kutoka darasani, wanafunzi wataelewa sababu iliyomfanya awafukuze. Vivyo hivyo, Yehova anajua kwamba wanadamu na malaika wote wanyoofu watafaidika wakiona kwamba Shetani na waasi wenzake wameshindwa na kwamba wanadamu hawawezi kujitawala wenyewe. Kama Yeremia wa zamani, watajifunza ukweli huu muhimu: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.

KWA NINI YEHOVA AMEWAACHA WANADAMU WATESEKE KWA MUDA MREFU?

15, 16. (a) Kwa nini Yehova amewaacha wanadamu wateseke kwa muda mrefu? (b) Kwa nini Yehova hazuii mambo kama vile uhalifu?

15 Hata hivyo, kwa nini Yehova amewaacha wanadamu wateseke kwa muda mrefu? Na kwa nini hazuii mambo mabaya yasitendeke? Katika ule mfano tuliotoa, fikiria mambo mawili ambayo yule mwalimu hangefanya. Kwanza, hangemzuia yule mwanafunzi mwasi kutoa madai yake. Pili, mwalimu hangemsaidia mwasi huyo kuthibitisha madai yake. Vivyo hivyo, kuna mambo mawili ambayo Yehova ameazimia kutofanya. Kwanza, hajamzuia Shetani na wale wanaomuunga mkono kujaribu kuthibitisha kwamba wanasema kweli. Ndiyo sababu ameruhusu wakati upite. Kwa maelfu ya miaka katika historia, wanadamu wamejaribu kila aina ya utawala, au serikali za wanadamu. Wanadamu wamefanya maendeleo katika sayansi na katika nyanja nyinginezo, lakini ukosefu wa haki, umaskini, uhalifu, na vita vimeongezeka sana. Sasa imeonekana wazi kwamba utawala wa wanadamu umeshindwa.

16 Pili, Yehova hamsaidii Shetani kuutawala ulimwengu huu. Kama Mungu angezuia uhalifu usitokee, je, hangekuwa anaunga mkono madai ya waasi hao? Je, watu hawangefikiri kwamba labda wanadamu wanaweza kujitawala bila matatizo? Kama Yehova angefanya hivyo, angekuwa anaunga mkono uwongo, na “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.”—Waebrania 6:18.

17, 18. Yehova atachukua hatua gani ili kuondoa madhara ya utawala wa wanadamu na uvutano wa Shetani?

17 Lakini vipi kuhusu madhara ya uasi huo wa muda mrefu kumwelekea Mungu? Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova ni Mweza-Yote. Kwa hiyo, anaweza na ataondoa mambo yanayowafanya wanadamu wateseke. Kama tulivyojifunza, badala ya dunia kuendelea kuharibiwa itageuzwa iwe Paradiso. Matokeo ya dhambi yataondolewa kupitia imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu na ufufuo utatangua matokeo ya kifo. Hivyo, Mungu atamtumia Yesu ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’ (1 Yohana 3:8) Yehova atatimiza yote hayo wakati unaofaa kabisa. Tunafurahi kwamba hakuchukua hatua kabla ya wakati unaofaa kwa sababu subira yake imetupatia nafasi ya kujifunza kweli na kumtumikia. (2 Petro 3:9, 10) Kwa sasa, Mungu amekuwa akiwatafuta kwa bidii waabudu wanyoofu na kuwasaidia wavumilie mambo yoyote yanayowakumba na yanayowafanya wateseke katika ulimwengu huu wenye taabu.—Yohana 4:23; 1 Wakorintho 10:13.

18 Huenda wengine wakauliza, Je, mateso haya yote yangezuiwa iwapo Mungu angewaumba Adamu na Hawa kwa njia ya kwamba hawangeweza kuasi? Ili kujibu swali hilo unahitaji kukumbuka kwamba Yehova amekupa zawadi fulani yenye thamani.

UTAITUMIAJE ZAWADI AMBAYO MUNGU AMEKUPA?

Mungu atakusaidia kuvumilia unapoteseka

19. Yehova ametupa zawadi gani yenye thamani, na kwa nini tunapaswa kuithamini?

19 Kama tulivyoona katika Sura ya 5, wanadamu waliumbwa wakiwa na uhuru wa kuchagua. Je, unaiona zawadi hiyo kuwa yenye thamani? Mungu ameumba wanyama wengi sana, nao wanaongozwa hasa na silika. (Methali 30:24) Mwanadamu ametengeneza mashine zinazoweza kufuata maagizo. Je, tungefurahi ikiwa Mungu angetuumba hivyo? Hapana, tunafurahi kwa kuwa tuna uhuru wa kuamua tutakuwa watu wa aina gani, tutaishi maisha ya aina gani, tutakuwa na marafiki wa aina gani, na kadhalika. Tunapenda kuwa na uhuru, na Mungu anataka tuwe na uhuru.

20, 21. Tunawezaje kuitumia vizuri zaidi zawadi ya uhuru wa kuchagua, na kwa nini tunapaswa kufanya hivyo?

20 Yehova hapendi watu wamtumikie kwa kulazimishwa. (2 Wakorintho 9:7) Kwa mfano: Ni nini kinachoweza kumfurahisha mzazi zaidi—mtoto anaposema “nakupenda” kwa sababu ameambiwa aseme hivyo au anaposema hivyo mwenyewe kutoka moyoni? Kwa hiyo, ni muhimu kufikiria swali hili, Wewe utatumiaje uhuru wa kuchagua ambao Yehova amekupa? Shetani, Adamu, na Hawa waliutumia vibaya uhuru wao wa kuchagua. Walimkataa Yehova Mungu. Wewe utafanya nini?

21 Unaweza kuitumia vizuri zaidi zawadi hiyo yenye thamani ya uhuru wa kuchagua. Unaweza kujiunga na mamilioni ya watu ambao wamechukua msimamo upande wa Yehova. Wanamfanya Mungu ashangilie kwa sababu wanashiriki kwa bidii kumthibitisha Shetani kuwa mwongo na mtawala asiyefaa. (Methali 27:11) Wewe pia unaweza kuchagua kuishi maisha yanayofaa. Hilo litafafanuliwa katika sura inayofuata.