Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA MOJA

Sababu Gani Mungu Anawaacha Watu Wateseke?

Sababu Gani Mungu Anawaacha Watu Wateseke?
  • Mungu ndiye anayeleta mateso yaliyo duniani?

  • Ni nini ilipingwa katika bustani ya Edeni?

  • Namna gani Mungu atamaliza mateso ya wanadamu?

1, 2. Ni mateso gani yanayowapata watu leo, na hilo linafanya watu wajiulize maulizo gani?

VITA kali ilitokea katika inchi moja inayosumbuliwa na vita, maelfu ya wanawake na watoto waliuawa na kuzikwa katika kaburi moja lililozungukwa na misalaba. Kwenye kila musalaba, ulizo hili liliandikwa: “Juu ya nini?” Wakati fulani, watu wanajiuliza ulizo hilo ili kuonyesha huzuni yao. Wanajiuliza hivyo wakati mambo kama vile vita, misiba, magonjwa, ao mambo mengine mabaya yanaua watu wa jamaa zao ao marafiki, yanaharibu nyumba zao, ao kuwaletea mateso katika njia mbalimbali. Wanataka kujua sababu gani wamepatwa na mambo hayo mabaya.

2 Sababu gani Mungu anawaacha watu wateseke? Ikiwa Yehova Mungu ni mweza-yote, mwenye upendo, hekima, na haki, sababu gani dunia inajaa chuki na ukosefu wa haki? Umekwisha kujiuliza maulizo hayo?

3, 4. (a) Ni nini inayoonyesha kama si vibaya kuuliza sababu gani Mungu anawaacha watu wateseke? (b) Namna gani Yehova anaona mateso na mambo mengine mabaya?

3 Je, ni vibaya kuuliza sababu gani Mungu anawaacha watu wateseke? Watu fulani wanaogopa kuuliza ulizo hilo, wanawaza kama wakiuliza ulizo hilo itaonekana hawana imani ao hawamuheshimu Mungu. Lakini, unaposoma Biblia, utaona kama watu waaminifu na wenye kumuogopa Mungu waliuliza maulizo kama hayo. Kwa mufano, nabii Habakuki alimuuliza Yehova hivi: ‘Kwa nini unanionyesha jambo lenye kuzuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana kunatokea, kwa nini muzozo huendelezwa?’​—Habakuki 1:3.

Yehova atamaliza mateso yote

4 Je, Yehova alimukaripia nabii mwaminifu Habakuki kwa sababu aliuliza maulizo hayo? Hapana. Kuliko kumukaripia, Mungu aliandikisha maneno hayo ya nabii Habakuki katika Biblia, kitabu kilichoongozwa na roho yake. Tena, Mungu alimusaidia aelewe mambo vizuri na awe na imani yenye nguvu zaidi. Yehova anataka kukusaidia vilevile. Kumbuka, Biblia inasema kama anakuhangaikia. (1 Petro 5:7) Mungu anachukia uovu sana na mateso yanayoletwa na uovu huo kuliko mwanadamu yeyote. (Isaya 55:8, 9) Basi, sababu gani kuna mateso mengi duniani?

SABABU GANI KUNA MATESO MENGI SANA DUNIANI?

5. Wakati fulani, viongozi wa dini mbalimbali wanasema nini ili kueleza sababu gani watu wanateseka, lakini Biblia inafundisha nini?

5 Watu wa dini mbalimbali wameendea viongozi nawalimu wao ili kuwauliza sababu gani watu wanateseka sana. Mara nyingi, wanawajibu kama ikiwa watu wanateswa ni mapenzi ya Mungu. Wanasema pia kama ni Mungu aliyepanga mbele ya wakati kila jambo linalotokea, na matukio yote yenye kuhuzunisha sana. Wengi wanaambiwa kama mambo ya Mungu ni fumbo na ikiwa watu wanakufa, hata watoto, ni sababu Mungu anawachukua ili waende kuishi naye mbinguni. Lakini, kama ulivyojifunza, Yehova Mungu hawezi kuleta mambo mabaya hata kidogo ili kuwatesa watu. Biblia inasema: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu, na Mweza-Yote kutenda isivyo haki!”​—Ayubu 34:10.

6. Sababu gani watu wengi wanakosea kwa kumulaumu Mungu na kusema ni yeye anayeleta mateso yaliyo duniani?

6 Je, unajua sababu gani watu wanakosea kwa kumulaumu Mungu na kusema ni yeye anayeleta mateso yote yaliyo duniani? Mara nyingi, wanamulaumu Mungu Mweza-Yote kwa sababu wanawaza kama yeye ndiye anayetawala dunia hii. Wanasema hivyo kwa sababu hawajui fundisho fulani la Biblia lililo rahisi lakini la lazima. Ulijifunza fundisho hilo katika Sura ya 3. Shetani Ibilisi ndiye mutawala wa dunia hii.

7, 8. (a) Watu wengi wanaonyesha tabia gani za mutawala wa dunia hii? (b) Namna gani kutokamilika kwa wanadamu na “wakati na tukio lisilotazamiwa” vinafanya kuwe mateso duniani?

7 Biblia inasema waziwazi hivi: ‘Ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’ (1 Yohana 5:19) Maneno hayo ni ya kweli kabisa, sivyo? Watu wa dunia wanaonyesha kabisa tabia za kiumbe huyo asiyeonekana “anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Kwa sababu Shetani mutawala wa dunia hii ni mwenye chuki, muongo, na muovu, watu wengi duniani wanaonyesha pia tabia hizo mbaya. Hiyo ndiyo sababu ya kwanza inayofanya kuwe mateso mengi duniani.

8 Kama tulivyoona katika Sura ya 3, sababu ya pili ni hii: Tangu uasi ulipoanza katika Edeni, wanadamu wamepoteza ukamilifu nao wamekuwa watenda-zambi. Wanadamu wenye zambi wana mwelekeo wa kufanya yote wawezayo ili kuwatawala wengine, na hilo linatokeza vita, mateso, na kuwaonea wengine. (Mhubiri 4:1; 8:9) Sababu ya tatu ni hii: “Wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Kwa sababu Yehova hatawali wala kulinda dunia hii, watu wanaweza kuteseka kwa sababu tu wako mahali pasipofaa na wakati usiofaa.

9. Sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kama Yehova ana sababu inayomufanya awaache wanadamu waendelee kuteseka?

9 Moyo wetu unatulia sana kujua kama si Mungu anayeleta mateso. Si yeye anayetokeza vita, mambo mabaya, uonevu, ao hata misiba inayofanya watu wateseke. Hata hivyo, ni lazima tujiulize: Sababu gani Yehova anaacha watu wateseke sana hivi? Ikiwa yeye ni Mweza-yote, ana uwezo wa kumaliza mateso; basi, sababu gani hafanyi jambo lolote? Kwa sababu tunajua kama Mungu ni mwenye upendo, anapaswa kuwa na sababu inayomufanya aache watu wateseke.​—1 Yohana 4:8.

MUNGU ANAPINGWA

10. Shetani alipinga nini, na namna gani?

10 Ili tujue sababu gani Mungu anaacha watu wateseke, ni lazima tukumbuke namna mateso yalivyoanza. Shetani alimushitaki Mungu alipowashawishi Adamu na Eva wasimutii Yehova. Shetani hakupinga nguvu za Yehova. Yeye pia anajua kama Yehova ana nguvu nyingi sana. Lakini alipinga haki ya Yehova ya kutawala. Shetani alimushitaki Yehova kuwa mutawala mubaya aliposema kama yeye ni muongo na anawaima watu wake mambo mazuri. (Mwanzo 3:2-5) Shetani alimaanisha kama wanadamu wangekuwa na maisha mazuri ikiwa wanaishi bila kutawaliwa na Mungu. Kwa kufanya hivyo, alishambulia enzi kubwa ya Yehova, ao haki yake ya kutawala.

11. Sababu gani Yehova hakuharibu mara moja waasi hao katika bustani ya Edeni?

11 Adamu na Eva walimuasi Yehova. Ni kama vile walisema: ‘Hatuna lazima ya kutawaliwa na Yehova. Sisi wenyewe tunaweza kujichagulia yaliyo mema na mabaya.’ Namna gani Yehova angekata maneno hayo? Namna gani angeonyesha wanadamu na malaika kama waasi hao walikosea na kuwa njia yake ya kutawala ndio iliyo nzuri zaidi? Mutu fulani anaweza kusema kama angewaharibu waasi hao na kuumba watu wengine. Lakini tusisahau kama hapo mwanzo Yehova alitaka watoto wa Adamu na Eva waijaze dunia, na kuishi katika paradiso duniani. (Mwanzo 1:28) Sikuzote, Yehova anatimiza makusudi yake. (Isaya 55:10, 11) Pia, kuua waasi hao hakungemaliza upinzani ambao Shetani alitokeza katika Edeni juu ya haki ya Yehova ya kutawala.

12, 13. Toa mufano unaoonyesha sababu gani Yehova amemuacha Shetani atawale dunia na sababu gani amewaacha wanadamu wajitawale wenyewe.

12 Tuchukue mufano. Wazia mwalimu anayewafundisha wanafunzi wake namna ya kupata jibu la hesabu fulani ngumu. Mwanafunzi fulani mwenye akili lakini muasi anasema kama njia ya mwalimu ya kutafuta jibu si nzuri. Ili kuonyesha kama mwalimu anakosea, mwanafunzi huyo anasema kama anajua njia nzuri ya kupata jibu. Wanafunzi fulani wanawaza kama anasema kweli, na wanajiunga naye. Mwalimu atafanya nini? Ikiwa anawafukuza wanafunzi hao waasi, wanafunzi wengine watawaza nini? Watawaza kama mwanafunzi mwenzao na wale waliojiunga naye walisema kweli, sivyo? Labda wanafunzi wengine wote wanaweza kupoteza heshima kwa mwalimu wao, wakiwaza kama anaogopa wale waasi wasionyeshe kosa lake. Lakini wazia kama mwalimu huyo anamuacha yule mwanafunzi muasi awaonyeshe wengine njia ya kupata jibu anayowazia kuwa nzuri.

Je, mwanafunzi huyu anajua mengi zaidi kuliko mwalimu wake?

13 Yehova amefanya kama mwalimu huyo. Kumbuka kama, zaidi ya Adamu na Eva, kulikuwa na malaika wengi waliosikia namna Shetani alivyomushitaki Mungu. Maelfu ya malaika hao walikuwa pia wakitazama. (Ayubu 38:7; Danieli 7:10) Namna Yehova angejibu shitaka hilo ingetolea malaika na wanadamu wote nafasi ya kuamua kukubali ao kukataa utawala wa Mungu. Basi, namna gani Yehova alijibu shitaka hilo? Amemuacha Shetani aonyeshe njia anayowazia kuwa nzuri ya kutawala wanadamu. Tena, Mungu amewaacha wanadamu wajitawale wenyewe wakiongozwa na Shetani.

14. Uamuzi wa Yehova wa kuwaacha wanadamu wajitawale wenyewe utaleta faida gani?

14 Katika mufano wetu, mwalimu anajua kama mwanafunzi muasi na wengine wanaojiunga naye watashindwa. Lakini anajua pia kama kuwaacha waonyeshe mawazo yao kutasaidia somo nzima. Waasi wanaposhindwa, wanafunzi wazuri wote wataona kama ni mwalimu tu ndiye anayestahili kuwafundisha. Mwishowe, mwalimu akifukuza somoni kila mwanafunzi anayeasi, wataelewa sababu gani anafanya hivyo. Vilevile, Yehova anajua kama wanadamu na malaika wote wema watafaidika kwa kuona namna Shetani na waasi waliojiunga naye wameshindwa na namna wanadamu hawana uwezo wa kujitawala wenyewe. Kama Yeremia, nabii wa zamani, watajifunza kweli hii ya lazima: ‘Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mutu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.’​—Yeremia 10:23.

SABABU GANI MUNGU ANAWAACHA WATU WATESEKE KWA MUDA MUREFU HIVI?

15, 16. (a) Sababu gani Yehova ameacha mateso kwa muda murefu hivi? (b) Na sababu gani Yehova hazuii mambo mabaya kutendeka?

15 Basi, sababu gani Yehova ameacha mateso yaendelee kwa muda murefu? Na sababu gani hazuii mambo mabaya kutendeka? Wazia mambo mawili ambayo mwalimu katika mufano wetu hawezi kufanya. Jambo la kwanza, hawezi kumuzuia mwanafunzi muasi kuonyesha njia yake ya kupata jibu. Jambo la pili, hawezi kumusaidia muasi huyo anapofasiria wengine njia yake ya kupata jibu. Vilevile, wazia sasa mambo mawili ambayo Yehova ameamua kutofanya. Jambo la kwanza, Yehova hawezi kumuzuia Shetani na wale wanaomuunga mukono wajaribu kuonyesha kama njia yao ya kutawala ndiyo nzuri. Ndio sababu Mungu amewaachia wakati wa kutosha. Kwa maelefu ya miaka, wanadamu wamejaribu kila aina ya utawala, ao serikali za wanadamu. Wamefanya maendeleo fulani katika sayansi na mambo mengine, lakini ukosefu wa haki, umaskini, mambo mabaya, na vita vinaendelea kuongezeka sana. Sasa, imeonekana kama utawala wa wanadamu umeshindwa kabisa.

16 Jambo la pili, Yehova hawezi kumusaidia Shetani kutawala dunia hii. Kwa mufano, ikiwa angezuia mambo mabaya kutendeka, hilo lingeonyesha kama waasi wamesema kweli, sivyo? Labda watu wangewaza kama wanadamu wanaweza kujitawala wenyewe bila matatizo, sivyo? Yehova angefanya hivyo, angeunga mukono uongo wa Shetani. Japo, ‘Mungu hawezi kamwe kusema uongo.’​—Waebrania 6:18.

17, 18. Yehova atafanya nini juu ya mambo mabaya ambayo yameletwa na utawala wa wanadamu na uongozi wa Shetani?

17 Basi, tuseme nini juu ya maovu ambayo yametendeka kwa muda murefu ambao watu wamemuasi Mungu? Ni vizuri tukumbuke kama Yehova ni mweza-yote. Kwa hiyo, ana uwezo na nia ya kumaliza mateso yanayowapata wanadamu. Kama tulivyojifunza, watu hawataiharibu tena dunia; dunia nzima itakuwa Paradiso. Matokeo ya zambi yataondolewa kwa kuamini zabihu ya ukombozi ya Yesu, na matokeo ya kifo yataondolewa kwa njia ya ufufuo. Mungu atamutumia Yesu “ili azivunje kazi za Ibilisi.” (1 Yohana 3:8) Atatimiza mambo hayo yote kwa wakati unaofaa. Tunaweza kufurahi kwa sababu ameacha wakati murefu upite, na uvumilivu wake umetufanya tujifunze kweli na kumutumikia. (2 Petro 3:9, 10) Kwa kungojea wakati huo, Mungu anaendelea kuwatafuta kwa bidii waabudu wenye mioyo ya haki na kuwasaidia wavumilie mateso yote yanayoweza kuwapata katika dunia hii mbovu.​—Yohana 4:23; 1 Wakorintho 10:13.

18 Watu fulani wanaweza kujiuliza hivi: “Ikiwa Mungu angeumba Adamu na Eva kwa namna ambayo ingefanya wasiweze kumuasi, je, mateso haya yote hayangezuiwa?” Ili kujibu ulizo hilo, ni lazima ukumbuke zawadi ya maana sana ambayo Yehova amekutolea.

NAMNA GANI UTATUMIA UHURU WA KUCHAGUA ULIOPEWA NA MUNGU?

Mungu atakusaidia kuvumilia mateso

19. Yehova ametupatia zawadi gani ya lazima sana, na sababu gani tunapaswa kuifurahia?

19 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 5, wanadamu waliumbwa wakiwa na uhuru wa kuchagua. Je, unauona uhuru huo kuwa zawadi ya lazima sana? Mungu ameumba wanyama wengi sana, nao wanaongozwa na silika (tabia inayoongoza wanyama). (Methali 30:24) Wanadamu wametengeneza mashini zinazotumika bila kuwaza. Tungekuwa na furaha ikiwa Mungu angetuumba kama mashini? Hapana, tunafurahia uhuru tulio nao wa kuchagua kuwa kama tunavyotaka, njia yetu ya maisha, marafiki wetu, na kazalika. Tunafurahia kuwa na uhuru kwa kadiri fulani, na Mungu anataka tuwe hivyo.

20, 21. Namna gani tunaweza kutumia vizuri zaidi uhuru wetu wa kuchagua, na sababu gani tunapaswa kufanya hivyo?

20 Yehova hapendi tumutumikie kwa kulazimishwa. (2 Wakorintho 9:7) Kwa mufano: Muzazi anaweza kufurahia nini zaidi​—mutoto amuambie “Ninakupenda” kwa sababu mutu mwingine anamuambia aseme hivyo ao maneno hayo yatoke moyoni mwa mutoto? Kwa hiyo, ni jambo la lazima ujue namna utatumia uhuru wa kuchagua uliopewa na Yehova. Shetani, Adamu, na Eva walitumia vibaya zaidi uhuru huo. Walimukataa Yehova Mungu. Wewe utatumia namna gani uhuru huo?

21 Una nafasi ya kutumia vizuri zaidi zawadi hiyo ya lazima sana. Unaweza kujiunga na mamilioni ya watu ambao wamejitia upande wa Yehova. Wanamufurahisha Mungu kwa kuonyesha kama Shetani ni muongo na mutawala asiyefaa. (Methali 27:11) Wewe pia unaweza kufanya hivyo kwa kuwa na mwenendo unaomupendeza Mungu. Sura inayofuata itazungumuzia jambo hilo.