Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA MBILI

Kuishi Maisha Yanayompendeza Mungu

Kuishi Maisha Yanayompendeza Mungu
  • Unawezaje kuwa rafiki ya Mungu?

  • Dai la Shetani linakuhusuje?

  • Ni mwenendo gani unaomchukiza Yehova?

  • Unawezaje kuishi maisha yanayompendeza Mungu?

1, 2. Taja baadhi ya wanadamu ambao Yehova aliwaona kuwa rafiki zake wa karibu.

UNGEPENDA kuwa na rafiki wa aina gani? Yaelekea ungependa kushirikiana na mtu aliye na maoni, mapendezi, na viwango kama vyako. Nawe ungevutiwa na mtu mwenye sifa nzuri, kama vile unyoofu na fadhili.

2 Katika historia yote, Mungu aliwachagua wanadamu fulani wawe rafiki zake wa karibu. Kwa mfano, Yehova alimwita Abrahamu rafiki yake. (Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Mungu alimtaja Daudi kuwa “mtu anayekubalika kwa moyo wangu” kwa sababu alikuwa na utu unaompendeza Yehova. (Matendo 13:22) Pia, Yehova alimwona nabii Danieli kuwa “mtu mwenye kutamanika sana.”—Danieli 9:23.

3. Kwa nini Yehova huwachagua wanadamu fulani wawe rafiki zake?

3 Kwa nini Yehova aliwaona Abrahamu, Daudi, na Danieli kuwa rafiki zake? Alimwambia Abrahamu: “Umeisikiliza sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Kwa hiyo Yehova huwakaribia wale wanaofanya mapenzi yake kwa unyenyekevu. Aliwaambia Waisraeli: “Tiini sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu.” (Yeremia 7:23) Ukimtii Yehova, wewe pia unaweza kuwa rafiki yake!

YEHOVA HUWAIMARISHA RAFIKI ZAKE

4, 5. Yehova anaonyeshaje nguvu zake kwa ajili ya watu wake?

4 Hebu fikiria faida za kuwa rafiki ya Mungu. Biblia inasema kwamba Yehova anatafuta nafasi ili “aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Yehova anawezaje kuonyesha nguvu zake kwa ajili yako? Njia moja inatajwa katika Zaburi 32:8, ambapo tunasoma hivi: “[Mimi Yehova] nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”

5 Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yehova anakujali sana. Atakupa mwongozo unaohitaji na kukulinda unapoufuata. Mungu anataka kukusaidia ushinde majaribu. (Zaburi 55:22) Kwa hiyo, ikiwa unamtumikia Yehova kwa moyo kamili, unaweza kuwa na hakika kama mtunga-zaburi aliyesema: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.” (Zaburi 16:8; 63:8) Ndiyo, Yehova anaweza kukusaidia uishi maisha yanayompendeza. Lakini, kama unavyojua, kuna adui ya Mungu ambaye anataka kukuzuia usifanye hivyo.

DAI LA SHETANI

6. Shetani alidai nini kuhusu wanadamu?

6 Sura ya 11 ya kitabu hiki ilieleza jinsi Shetani Ibilisi alivyopinga haki ya Mungu ya kutawala. Shetani alidai kwamba Mungu ni mwongo na kudokeza kwamba Yehova alikuwa akiwakandamiza Adamu na Hawa kwa kuwanyima haki ya kujiamulia yaliyo mema na mabaya. Baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi na wazao wao walipoanza kujaa duniani, Shetani alitilia shaka nia ya wanadamu wote. Shetani alidai kwamba “Watu hawamtumikii Mungu kwa sababu wanampenda.” Ni kana kwamba alisema, “Nikiruhusiwa, ninaweza kumgeuza mtu yeyote aache kumtumikia Mungu.” Masimulizi kuhusu Ayubu yanaonyesha kwamba hivyo ndivyo Shetani alivyoamini. Ayubu alikuwa nani, naye alihusikaje katika dai la Shetani?

7, 8. (a) Ni nini kilichomfanya Ayubu awe mtu wa pekee kati ya wanadamu wa wakati huo? (b) Shetani alitiliaje shaka nia ya Ayubu?

7 Ayubu aliishi miaka 3,600 hivi iliyopita. Alikuwa mtu mzuri, kwa kuwa Yehova alisema: “Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani, mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.” (Ayubu 1:8) Ayubu alimpendeza Mungu.

8 Shetani alitilia shaka nia ya Ayubu kumtumikia Mungu. Ibilisi alimwambia Yehova: “Je, wewe hukuweka ukuta kumzunguka yeye [Ayubu] na kuzunguka nyumba yake na kuzunguka kila kitu alicho nacho pande zote? Umeibariki kazi ya mikono yake, na mifugo yake imeenea kotekote duniani. Lakini, ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kila kitu alicho nacho, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.”—Ayubu 1:10, 11.

9. Yehova alijibuje dai la Shetani, na kwa nini?

9 Hivyo, Shetani alidai kwamba Ayubu alikuwa akimtumikia Mungu kwa sababu ya vitu alivyokuwa akipata. Pia, Shetani alidai kwamba Ayubu angemwasi Mungu ikiwa angejaribiwa. Yehova alijibuje dai la Shetani? Kwa kuwa suala hilo lilihusisha nia ya Ayubu, Yehova alimruhusu Shetani amjaribu Ayubu. Hivyo, ingeonekana wazi ikiwa Ayubu anampenda Mungu au hampendi.

AYUBU AJARIBIWA

10. Ni majaribu gani yaliyompata Ayubu, naye alitendaje?

10 Punde si punde Shetani alianza kumjaribu Ayubu katika njia mbalimbali. Baadhi ya mifugo ya Ayubu iliibiwa na mingine kuuawa. Watumishi wake wengi waliuawa. Hilo lililimletea matatizo ya kiuchumi. Halafu alipata msiba watoto wake kumi walipokufa katika dhoruba. Licha ya matukio hayo yenye kuhuzunisha, “Ayubu hakutenda dhambi, wala kumhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa.”—Ayubu 1:22.

11. (a) Ni dai gani la pili ambalo Shetani alizusha kumhusu Ayubu, na Yehova aliitikiaje? (b) Ayubu alitendaje baada ya kupata ugonjwa wenye maumivu makali?

11 Shetani hakukata tamaa. Haikosi alifikiri kwamba ingawa Ayubu angeweza kustahimili kupoteza mali zake, watumishi wake, na watoto wake, angeacha kumtumikia Mungu ikiwa angekuwa mgonjwa. Yehova alimruhusu Shetani amshambulie Ayubu kwa ugonjwa wenye kuchukiza sana na wenye maumivu makali. Lakini hata hilo halikumfanya Ayubu aache kumwamini Mungu. Badala yake, alisema hivi kwa uthabiti: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.

Ayubu alipata thawabu kwa sababu ya uaminifu wake

12. Ayubu alijibuje dai la Ibilisi?

12 Ayubu hakujua kwamba Shetani ndiye aliyekuwa akisababisha matatizo yake. Kwa kuwa hakujua masuala yaliyozushwa na Ibilisi kuhusu haki ya Yehova ya kutawala, Ayubu alidhani kwamba Mungu ndiye aliyesababisha matatizo yake. (Ayubu 6:4; 16:11-14) Hata hivyo, alidumisha utimilifu wake kwa Yehova. Uaminifu wa Ayubu ulithibitisha kwamba dai la Shetani eti Ayubu alikuwa akimtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi, si la kweli!

13. Uaminifu wa Ayubu kwa Mungu ulikuwa na matokeo gani?

13 Uaminifu wa Ayubu ulimwezesha Yehova kujibu dai la Shetani lenye kuleta suto. Kwa kweli Ayubu alikuwa rafiki ya Yehova, na Mungu alimthawabisha kwa sababu ya uaminifu wake.—Ayubu 42:12-17.

JINSI UNAVYOHUSIKA

14, 15. Kwa nini tunaweza kusema kwamba dai la Shetani kumhusu Ayubu linawahusu wanadamu wote?

14 Suala la utimilifu kwa Mungu lililozushwa na Shetani halikumhusu Ayubu peke yake. Wewe pia unahusika. Hilo linaonyeshwa waziwazi katika Methali 27:11, ambapo Neno la Yehova linasema hivi: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” Maneno hayo, yaliyoandikwa mamia ya miaka baada ya Ayubu kufa, yanaonyesha kwamba bado Shetani anamdhihaki Mungu na kuwashtaki watumishi Wake. Tunapoishi maisha yanayompendeza Yehova, tunamsaidia kujibu mashtaka ya uwongo ya Shetani, na hivyo kuufanya moyo wa Mungu ushangilie. Unahisije kuhusu hilo? Je, si pendeleo kushiriki kujibu madai ya uwongo ya Ibilisi, hata ikiwa utahitaji kufanya mabadiliko fulani maishani mwako?

15 Ona kwamba Shetani alisema: “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” (Ayubu 2:4) Aliposema “mtu,” Shetani alionyesha waziwazi kwamba dai lake liliwahusu wanadamu wote wala si Ayubu tu. Hilo ni jambo muhimu sana. Shetani anatilia shaka utimilifu wako kwa Mungu. Ibilisi angependa kuona ukimwasi Mungu na kuacha kuishi maisha ya uadilifu matatizo yanapotokea. Huenda Shetani akajaribuje kutimiza hilo?

16. (a) Shetani hutumia njia gani kujaribu kuwageuza watu waache kumtumikia Mungu? (b) Ibilisi anawezaje kutumia njia hizo kukunasa?

16 Kama tulivyozungumzia katika Sura ya 10, Shetani hutumia njia mbalimbali kujaribu kuwageuza watu waache kumtumikia Mungu. Kwanza, yeye hushambulia “kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Hivyo, huenda uvutano wa Shetani ukaonekana wakati ambapo marafiki, watu wa ukoo, au wengine wanapopinga jitihada zako za kujifunza Biblia na kuishi kulingana na mambo unayojifunza. * (Yohana 15:19, 20) Pia, Shetani “huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Ibilisi anaweza kutumia hila kukupotosha na kukunasa uache kuishi maisha yanayompendeza Mungu. Anaweza pia kutumia mambo yanayovunja moyo, labda kwa kukufanya uhisi kwamba huwezi kumpendeza Mungu. (Methali 24:10) Iwe Shetani anatenda kama “simba anayenguruma” au anajifanya “malaika wa nuru,” dai lake ni lilelile: Anasema kwamba unapokabili majaribu au vishawishi, utaacha kumtumikia Mungu. Unaweza kujibuje dai lake na kuthibitisha utimilifu wako kwa Mungu, kama Ayubu alivyofanya?

KUTII AMRI ZA YEHOVA

17. Tuna sababu gani kuu ya kutii amri za Yehova?

17 Unaweza kujibu dai la Shetani kwa kuishi maisha yanayompendeza Mungu. Hilo linahusisha nini? Biblia inajibu hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Kadiri upendo wako kwa Mungu unavyoongezeka, ndivyo utakavyotamani hata zaidi kufanya mapenzi yake. Mtume Yohana aliandika: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.” Ukimpenda Yehova kwa moyo wako wote, utaona kwamba “amri zake si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

18, 19. (a) Taja baadhi ya amri za Yehova. (Ona sanduku lenye kichwa “ Epuka Mambo Yanayomchukiza Yehova.”) (b) Tunajuaje kwamba Mungu hatarajii tufanye mambo yanayopita uwezo wetu?

18 Amri za Yehova ni gani? Baadhi yake zinahusu mwenendo tunaopaswa kuepuka. Kwa mfano, ona sanduku lenye kichwa “ Epuka Mambo Yanayomchukiza Yehova.” Sanduku hilo lina orodha ya mambo ambayo Biblia inashutumu waziwazi. Huenda baadhi ya mazoea yanayotajwa yasionekane kuwa mabaya sana mwanzoni. Lakini baada ya kutafakari maandiko yaliyotajwa, yaelekea utaona hekima ya sheria za Yehova. Huenda kubadili mwenendo wako kukawa jambo gumu zaidi maishani mwako. Hata hivyo, kuishi maisha yanayompendeza Mungu huridhisha sana na kuleta furaha. (Isaya 48:17, 18) Huo ni mradi ambao wewe unaweza kuufikia. Tunajuaje hivyo?

19 Yehova hatarajii kamwe tufanye mambo yanayopita uwezo wetu. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Anajua uwezo wetu na udhaifu wetu kuliko hata tunavyojijua. (Zaburi 103:14) Isitoshe, Yehova anaweza kututia nguvu ili tumtii. Mtume Paulo aliandika: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.” (1 Wakorintho 10:13) Ili kukusaidia kuvumilia, Yehova hata anaweza kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Baada ya kuvumilia majaribu mengi, Paulo angeweza kusema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.

KUSITAWISHA SIFA ZINAZOMPENDEZA MUNGU

20. Ni sifa gani zinazompendeza Mungu unazopaswa kusitawisha, na kwa nini sifa hizo ni muhimu?

20 Bila shaka, kumpendeza Yehova kunahusisha mengi zaidi kuliko tu kuepuka mambo yanayomchukiza. Unahitaji pia kupenda mambo anayopenda. (Waroma 12:9) Je, huvutiwi na watu walio na maoni, mapendezi, na viwango kama vyako? Yehova huvutiwa na watu kama hao pia. Kwa hiyo, jifunze kupenda mambo ambayo Yehova anapenda. Baadhi ya mambo hayo yanatajwa katika Zaburi 15:1-5, ambapo tunasoma kuhusu watu ambao Yehova anawaona kuwa rafiki zake. Rafiki za Yehova huonyesha yale yanayoitwa na Biblia, “matunda ya roho.” Yanatia ndani sifa kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Wagalatia 5:22, 23.

21. Ni nini kitakachokusaidia kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu?

21 Kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida kutakusaidia kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu. Na kujifunza mapenzi ya Mungu kutakusaidia kupatanisha mawazo yako na mawazo ya Mungu. (Isaya 30:20, 21) Kadiri unavyozidisha upendo wako kwa Yehova, ndivyo utakavyotamani hata zaidi kuishi maisha yanayompendeza Mungu.

22. Utatimiza nini kwa kuishi maisha yanayompendeza Mungu?

22 Jitihada inahitajiwa ili kuishi maisha yanayompendeza Yehova. Biblia husema, kubadili maisha yako ni sawa na kuvua utu wako wa kale na kujivika utu mpya. (Wakolosai 3:9, 10) Lakini kuhusu maagizo ya Yehova, mtunga-zaburi aliandika hivi: “Katika kuyashika kuna thawabu kubwa.” (Zaburi 19:11) Wewe pia utaona kwamba kuishi maisha yanayompendeza Mungu kunaleta thawabu kwelikweli. Kwa kufanya hivyo, utajibu dai la Shetani na kuufanya moyo wa Yehova ushangilie!

^ fu. 16 Hilo halimaanishi kwamba wale wanaokupinga wanaongozwa moja kwa moja na Shetani. Lakini Shetani ndiye mungu wa mfumo huu wa mambo, na ulimwengu wote uko katika nguvu zake. (2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, tunaweza kutarajia kwamba wengi hawatafurahi kuona ukiishi maisha yanayompendeza Mungu, na baadhi yao watakupinga.