Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA MBILI

Mwenendo Unaomupendeza Mungu

Mwenendo Unaomupendeza Mungu
  • Unaweza kufanya nini ili uwe rafiki ya Mungu?

  • Katika mashitaka ya Shetani, ni nini alitilia mashaka juu yako?

  • Ni mwenendo wa namna gani unaomuchukiza Yehova?

  • Unaweza kufanya nini ili uwe na mwenendo unaomupendeza Mungu?

1, 2. Taja wanadamu fulani ambao Yehova alichagua wawe marafiki wake.

NI MUTU wa namna gani ungechagua awe rafiki yako? Hakika, utapenda kufanya urafiki na mutu anayeona mambo kama wewe, anayependa mambo unayopenda, na aliye na kanuni za maisha kama zako. Tena ungevutiwa na mutu mwenye sifa nzuri, kama vile mutu asiyedanganya, na aliye na moyo mwema.

2 Tangu zamani, Mungu amechagua wanadamu fulani ili wawe marafiki wake. Kwa mufano, Yehova alimuita Abrahamu: “rafiki yangu.” (Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Mungu alisema Daudi ni ‘mutu anayekubalika kwa moyo [wake]’ kwa sababu alikuwa na sifa za watu ambao Yehova anapenda. (Matendo 13:22) Tena, Yehova alimuona Danieli kuwa ‘mutu mwenye kutamanika sana.’​—Danieli 9:23.

3. Sababu gani Yehova aliwachagua wanadamu fulani ili wawe marafiki wake?

3 Sababu gani Yehova alikubali Abrahamu, Daudi, na Danieli wawe marafiki wake? Sikia namna alimuambia Abrahamu: “Umesikiliza sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Hilo linaonyesha kama Yehova anawakaribia wale ambao kwa unyenyekevu wanakubali kufanya yale anayowaambia. Aliwaambia Waisraeli hivi: ‘Mutii sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mutakuwa watu wangu.’ (Yeremia 7:23) Wewe pia ukimutii Yehova, unaweza kuwa rafiki yake!

YEHOVA ANAPATIA MARAFIKI WAKE NGUVU

4, 5. Namna gani Yehova anaonyesha nguvu zake kwa ajili ya watu wake?

4 Wazia kwanza mambo mazuri ambayo utapata ukiwa rafiki ya Mungu! Biblia inasema kama Yehova anatafuta nafasi ili ‘aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mukamilifu kumuelekea yeye.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Namna gani Yehova anaweza kuonyesha nguvu zake kwa ajili yako? Zaburi 32:8, inataja namna moja, inasema hivi: “[Mimi Yehova] nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”

5 Maneno hayo yanaonyesha kama Yehova anakuhangaikia sana! Atakupa shauri unalohitaji na kukulinda unapolitumia. Mungu anapenda kabisa kukusaidia ili ushinde majaribu unayokutana nayo. (Zaburi 55:22) Basi, ukimutumikia Yehova kwa moyo wote, unaweza kuwa na uhakika kama mutunga zaburi aliyesema: ‘Nimemuweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mukono wangu wa kuume, sitatikiswa.’ (Zaburi 16:8; 63:8) Kwa kweli, Yehova anaweza kukusaidia ili uwe na mwenendo unaomupendeza. Lakini, kama unavyojua, Mungu ana adui ambaye hataki uwe na mwenendo muzuri.

MASHAKA YA SHETANI

6. Shetani alishakia nini juu ya wanadamu?

6 Katika Sura ya 11 tulijifunza namna Shetani alivyopinga haki ya Mungu ya kutawala. Shetani alimushitaki Mungu kuwa muongo; maneno yake yalionyesha tena kama Mungu alikuwa anawagandamiza Adamu na Eva kwa sababu hakuwaacha wajichagulie wao wenyewe yaliyo mema na yaliyo mabaya. Kisha Adamu na Eva kufanya zambi, na watoto wao walipoanza kujaa duniani, Shetani alishakia mawazo yanayowachochea wanadamu kumutumikia Mungu. Shetani alisema kama “watu hawamutumikii Mungu kwa sababu wanamupenda.” Ni kama vile alisema, “Nikiruhusiwa, ninaweza kumufanya kila mutu amuache Mungu.” Habari ya Biblia juu ya Ayubu inaonyesha kama hivyo ndivyo Shetani alivyowaza. Ayubu alikuwa nani, na namna gani Shetani alitilia mawazo yake mashaka?

7, 8. (a) Ni nini iliyomufanya Ayubu awe tofauti sana na watu wa wakati wake? (b) Shetani alisema nini ili kuonyesha kama alishakia mawazo yaliyomuchochea Ayubu kumutumikia Mungu?

7 Ayubu aliishi kumekwisha kupita miaka 3 600 hivi. Alikuwa mutu muzuri, kwa sababu Yehova alisema juu yake hivi: ‘Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani, mutu asiye na lawama na munyoofu, mwenye kumuogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.’ (Ayubu 1:8) Ayubu alikuwa anamupendeza Mungu.

8 Shetani alitilia mashaka mawazo yaliyomuchochea Ayubu kumutumikia Mungu. Ibilisi alimuambia Yehova: ‘Je, wewe hukuweka ukuta kumuzunguka yeye [Ayubu] na kuzunguka nyumba yake na kuzunguka kila kitu alicho nacho pande zote? Umeibariki kazi ya mikono yake, na mifugo yake imeenea kotekote duniani. Lakini, ili kuwe na badiliko, tafazali nyoosha mukono wako, uguse kila kitu alicho nacho, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.’​—Ayubu 1:10, 11.

9. Yehova alifanya nini ili kumujibu Shetani, na sababu gani alifanya hivyo?

9 Kwa hiyo, ni kama vile Shetani alisema hivi: Ikiwa Ayubu anamutumikia Mungu ni kwa sababu Mungu alimupatia vitu vingi. Ibilisi akasema tena ikiwa Ayubu anajaribiwa, atamuacha Mungu. Namna gani Yehova alijibu mashitaka hayo ya Shetani? Kwa sababu Shetani alitilia shaka mawazo ya Ayubu, basi Yehova alimuacha amujaribu Ayubu. Hilo lingesaidia kuonyesha wazi mawazo ya Ayubu, ikiwa anamupenda Mungu ao hapana.

AYUBU ANAJARIBIWA

10. Ayubu alipatwa na majaribu gani, naye alifanya nini?

10 Shetani akaanza mara moja kumujaribu Ayubu; alitumia njia mbalimbali. Wanyama aliokuwa akifuga, wengine waliibwa na wengine waliuawa. Watumishi wake wengi waliuawa. Jaribu hilo lilimutia katika hali ya umasikini. Zaidi ya hilo, alipatwa na musiba wakati upepo mukali uliwaua watoto wake kumi. Ijapokuwa alipatwa na mambo hayo yenye kuhuzunisha, ‘Ayubu hakutenda zambi, wala hakumuhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa.’​—Ayubu 1:22.

11. (a) Ni shaka gani lingine Shetani alitokeza juu ya Ayubu, na Yehova alifanya nini? (b) Ayubu alifanya nini alipopatwa na ugonjwa mubaya sana?

11 Shetani hakurudi nyuma. Labda aliwaza hivi: ‘Hata ikiwa Ayubu alivumilia kupoteza mali zake, watumishi wake, watoto wake, lakini akipatwa na ugonjwa atamuacha Mungu.’ Yehova alimuacha Shetani amushambulie Ayubu kwa ugonjwa mubaya sana na wenye kuchukiza sana. Lakini hata jaribu hilo halikumufanya Ayubu amuache Mungu. Badala yake, alisema hivi kwa ushikamanifu: ‘Mupaka nitakapokata pumuzi, sitajiondolea utimilifu wangu!’​—Ayubu 27:5.

Ayubu alipata baraka nyingi kwa sababu alibaki mwaminifu kwa Mungu

12. Namna gani Ayubu alionyesha kama mashitaka ya Shetani ni ya uongo?

12 Ayubu hakujua kama Shetani ndiye aliyekuwa akimuletea matatizo hayo. Kwa sababu hakujua yale yaliyokuwa yakipita kati ya Mungu na Shetani, yaani, shitaka la Ibilisi juu ya haki ya Yehova ya kutawala, Ayubu aliwaza kama ni Mungu aliyemuletea mateso yake. (Ayubu 6:4; 16:11-14) Hata hivyo, aliendelea kushikamana na Yehova. Kwa kuwa Ayubu alibaki mwaminifu kwa Mungu, alionyesha kama Shetani alisema uongo kwa kuwaza kama yeye alikuwa akimutumikia Mungu kwa sababu ya faida zake mwenyewe!

13. Uaminifu wa Ayubu ulimupatia Mungu nafasi ya kufanya nini?

13 Kwa sababu Ayubu alibaki mwaminifu, Yehova alipata nafasi ya kujibu mashitaka ya Shetani yaliyomuchafua Yehova. Kwa kweli Ayubu alikuwa rafiki ya Yehova, naye alimubariki sana kwa sababu ya uaminifu wake.​—Ayubu 42:12-17.

SHETANI ANATILIA PIA UAMINIFU WAKO MASHAKA

14, 15. Shetani alitilia mashaka uaminifu wa Ayubu, nini inayoonyesha kama alitilia pia mashaka uaminifu wa wanadamu wote?

14 Shetani alitilia uaminifu wa Ayubu mashaka. Lakini jua kama alitilia pia uaminifu wako mashaka. Wazo hilo linaonyeshwa waziwazi katika andiko la Methali 27:11, hapo Neno la Yehova linasema hivi: ‘Uwe na hekima mwana wangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumujibu anayenizihaki.’ Maneno hayo, yaliyoandikwa mamia ya miaka kisha Ayubu kufa, yanaonyesha kama mupaka leo Shetani anaendelea kumuzihaki ao kumuchokoza Mungu na kuwashitaki watumishi Wake. Tunapokuwa na mwenendo unaomupendeza Yehova, tunamupatia nafasi ya kujibu mashitaka ya uongo ya Shetani, na kwa kufanya hivyo tunaufurahisha moyo wa Mungu. Unawaza nini? Je, hauoni kama ni pendeleo kabisa kumupatia Mungu nafasi ya kujibu mashitaka ya uongo ya Ibilisi, hata ikiwa jambo hilo litakuomba ufanye mabadiliko fulani katika maisha yako?

15 Sikia yale Shetani alisema: ‘Kila kitu alicho nacho mutu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.’ (Ayubu 2:4) Alipotumia neno ‘mutu,’ Shetani alionyesha waziwazi kama hakumushitaki Ayubu tu lakini alishitaki pia wanadamu wote. Hilo ni jambo la lazima sana kujua. Linaonyesha kama Shetani alitilia mashaka uaminifu wako kwa Mungu. Kwa hiyo, Ibilisi atafurahi ikiwa unakosa kumutii Mungu na ukiacha kuwa mwaminifu unapokutana na magumu. Shetani atafanya namna gani ili afikie kusudi hilo?

16. (a) Shetani anatumia njia gani mbalimbali ili ajaribu kuwafanya watu wamuache Mungu? (b) Namna gani Ibilisi anaweza kutumia njia hizo ili akupate?

16 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 10, Shetani anatumia njia mbalimbali ili ajaribu kuwafanya watu wamuache Mungu. Kwanza, yeye anashambulia ‘kama simba anayenguruma, akitafuta kumumeza mutu.’ (1 Petro 5:8) Kwa hiyo, labda Shetani atatumia marafiki, watu wa jamaa, ao watu wengine ili kukupinga unapojikaza kujifunza Biblia na kutumikisha yale unayojifunza katika maisha yako. * (Yohana 15:19, 20) Tena, Shetani ‘anaendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.’ (2 Wakorintho 11:14) Ibilisi anaweza kutumia mayele fulani ili kukudanganya na kukuvuta uache kuwa na mwenendo unaomupendeza Mungu. Anaweza pia kutumia mambo yanayoweza kukuvunja moyo, labda kwa kukufanya ujisikie kuwa hauwezi kumupendeza Mungu. (Methali 24:10) Iwe Shetani anatenda kama “simba anayenguruma” ao anajifanya kuwa “malaika wa nuru,” shitaka lake ni lilelile: Anasema kama ukipatwa na majaribu ao ukishawishiwa, wewe hautamutumikia Mungu. Namna gani wewe unaweza kuonyesha kama Shetani ni muongo na kuonyesha uaminifu wako kwa Mungu, kama Ayubu?

KUTII AMRI ZA MUNGU

17. Ni sababu gani kubwa inayotuchochea kutii amri za Yehova?

17 Unaweza kuonyesha kama Shetani ni muongo ikiwa una mwenendo unaomupendeza Mungu. Kwa hiyo, inakuomba kufanya nini? Biblia inajibu hivi: ‘Lazima umupende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.’ (Kumbukumbu la Torati 6:5) Kadiri upendo wako kwa Mungu unavyoongezeka, ndivyo utakavyokuwa na tamaa zaidi ya kufanya mapenzi yake. Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Kumupenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.’ Ikiwa unamupenda Yehova kwa moyo wako wote, utaona kama ‘amri zake si muzigo muzito.’​—1 Yohana 5:3.

18, 19. (a) Taja amri fulani za Yehova? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 122.) (b) Namna gani tunajua kama Mungu hatuombi tufanye mambo yanayopita uwezo wetu?

18 Amri hizo za Yehova ni gani? Amri fulani zinatuonyesha mwenendo tunaopaswa kuepuka. Kwa mufano, angalia  kisanduku ‘Chukia Kabisa Mambo Ambayo Yehova Anachukia,’ kwenye ukurasa wa 122. Katika kisanduku hicho utaona mambo ambayo Biblia inakataza waziwazi. Utakaposoma mambo hayo, labda kijuujuu utaona kama si mambo mabaya sana. Lakini kisha kuwaza sana juu ya maandiko yanayotajwa hapo, labda utafikia kuona kama sheria za Yehova ni za hekima. Ni kweli kama kubadilisha mwenendo wako ndilo linaweza kuwa jambo ngumu zaidi maishani mwako. Lakini, jua kama kuwa na mwenendo unaomupendeza Mungu kunamufanya mutu atosheke sana na awe mwenye furaha. (Isaya 48:17, 18) Wewe pia unaweza kuwa na furaha ya namna hiyo. Sababu gani tunasema hivyo?

19 Yehova hatuombi hata kidogo tufanye mambo yanayopita uwezo wetu. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Yeye anajua uwezo na uzaifu wetu kuliko namna sisi wenyewe tunavyojijua. (Zaburi 103:14) Tena, Yehova anaweza kutupatia nguvu ili tumutii. Mutume Paulo aliandika: ‘Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mujaribiwe kupita munavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi muweze kulivumilia.’ (1 Wakorintho 10:13) Ili kukusaidia kuvumilia, Yehova anaweza hata kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Kisha kuvumilia majaribu mengi, Paulo alisema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”​—Wafilipi 4:13.

ONYESHA SIFA ZINAZOMUPENDEZA MUNGU

20. Unapaswa kuonyesha sifa gani zinazomupendeza Mungu, na kwa nini sifa hizo ni za lazima?

20 Kwa kweli, ili kumupendeza Yehova mutu hapaswi tu kuepuka mambo ambayo Mungu anachukia. Anapaswa pia kupenda mambo ambayo Mungu anapenda. (Waroma 12:9) Utapenda kuwa na rafiki anayeona mambo kama wewe, anayependa mambo unayopenda, na aliye na kanuni za maisha kama zako, sivyo? Yehova pia anapenda hivyo. Kwa hiyo, jifunze kupenda mambo ambayo Yehova anapenda. Mambo fulani kati ya hayo yanatajwa katika Zaburi 15:1-5, mahali tunasoma juu ya wale ambao Yehova anakubali wawe marafiki wake. Marafiki wa Yehova wanaonyesha ‘tunda la roho’ katika maisha yao; tunda hilo lina sifa kama ‘upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fazili, wema, imani, upole, kujiweza.’​—Wagalatia 5:22, 23.

21. Ni nini itakayokusaidia uwe na sifa zinazomupendeza Mungu?

21 Kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida kutakusaidia uwe na sifa zinazomupendeza Mungu. Na kujifunza mambo ambayo Mungu anataka kutakusaidia upatanishe mawazo yako na mawazo yake. (Isaya 30:20, 21) Kadiri unavyomupenda Yehova sana, ndivyo utakuwa na tamaa sana ya kuwa na mwenendo unaomupendeza.

22. Ukiwa na mwenendo unaomupendeza Mungu, jambo hilo litakutolea nafasi ya kufanya nini?

22 Inaomba kufanya nguvu ili kuwa na mwenendo unaomupendeza Yehova. Biblia inasema kama kubadilisha maisha yako ni sawa na kuvua utu wako wa zamani na kujivika utu mupya. (Wakolosai 3:9, 10) Lakini juu ya amri za Yehova, mutunga zaburi aliandika hivi: “Katika kuzishika kuna [faida] kubwa.” (Zaburi 19:11) Wewe pia utaona kama kuwa na mwenendo unaomupendeza Mungu kunaleta faida nyingi sana. Kwa kufanya hivyo, utajibu mashitaka ya Shetani na utaufurahisha moyo wa Yehova!

^ fu. 16 Hilo halimaanishi kama kila mutu anayekupinga anatumwa moja kwa moja na Shetani. Lakini Shetani ndiye mungu wa ulimwengu huu muovu, na dunia yote iko katika nguvu zake. (2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, ni lazima kujua kama wengi hawatafurahia mwenendo wako unaomupendeza Mungu, na wengine hata watakupinga.