Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA TATU

Maoni ya Mungu Kuhusu Uhai

Maoni ya Mungu Kuhusu Uhai
  • Mungu anauonaje uhai?

  • Mungu huonaje kutoa mimba?

  • Tunawezaje kuonyesha kwamba tunauheshimu uhai?

1. Ni nani aliyeumba vitu vyote vilivyo hai?

NABII Yeremia alisema hivi: “Kwa kweli Yehova ni Mungu. Yeye ndiye Mungu aliye hai.” (Yeremia 10:10) Isitoshe, Yehova Mungu ndiye Muumba wa vitu vyote vilivyo hai. Viumbe walio mbinguni walimwambia hivi: “Uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Alipokuwa akimwimbia Mungu wimbo wa sifa, Mfalme Daudi alisema hivi: “Kwako wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Kwa hiyo, uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu.

2. Mungu hufanya nini ili kuutegemeza uhai wetu?

2 Pia, Yehova huutegemeza uhai wetu. (Matendo 17:28) Yeye hutuandalia chakula, maji, hewa, na mahali pa kuishi. (Matendo 14:15-17) Yehova amefanya hilo kwa njia inayofanya maisha yawe yenye kufurahisha sana. Lakini, ili tufurahie maisha kikamili, tunahitaji kujifunza sheria za Mungu na kuzitii.—Isaya 48:17, 18.

KUUHESHIMU UHAI

3. Yehova alionaje kuuawa kwa Abeli?

3 Mungu anataka tuuheshimu uhai wetu wenyewe na wa wengine. Kwa mfano, katika siku za Adamu na Hawa, mwana wao Kaini alimkasirikia sana Abeli, ndugu yake mdogo. Yehova alimwonya Kaini kwamba hasira yake ingeweza kumfanya atende dhambi nzito. Kaini alipuuza onyo hilo. ‘Alimshambulia Abeli ndugu yake, akamuua.’ (Mwanzo 4:3-8) Yehova alimwadhibu Kaini kwa kumuua ndugu yake.—Mwanzo 4:9-11.

4. Katika Sheria ya Musa, Mungu alikaziaje maoni yanayofaa kuhusu uhai?

4 Maelfu ya miaka baadaye, Yehova aliwapa watu wa Israeli sheria zilizowasaidia kumtumikia kwa njia inayompendeza. Kwa sababu sheria hizo zilitolewa kupitia nabii Musa, nyakati nyingine zinaitwa Sheria ya Musa. Mojawapo ya sheria hizo inasema: “Usiue.” (Kumbukumbu la Torati 5:17) Hilo liliwaonyesha Waisraeli kwamba Mungu anathamini uhai wa wanadamu na kwamba wanadamu wanapaswa kuuthamini uhai wa wengine.

5. Tuoneje kutoa mimba?

5 Namna gani uhai wa mtoto ambaye hajazaliwa? Kulingana na Sheria ya Musa, ilikuwa kosa kumuua mtoto aliye katika tumbo la mama yake. Ndiyo, hata uhai wa mtoto huyo ni wenye thamani kwa Yehova. (Kutoka 21:22, 23; Zaburi 127:3) Hilo linamaanisha kwamba ni kosa kutoa mimba.

6. Kwa nini hatupaswi kuwachukia wanadamu wenzetu?

6 Kuuheshimu uhai kunatia ndani kuwa na maoni yanayofaa kuelekea wanadamu wenzetu. Biblia inasema: “Kila mtu anayemchukia ndugu yake ni muuaji, nanyi mnajua kwamba hakuna muuaji aliye na uzima wa milele ukikaa ndani yake.” (1 Yohana 3:15) Ikiwa tunataka kupata uzima wa milele, tunapaswa kuacha kabisa kuwachukia wanadamu wenzetu, kwa sababu mara nyingi chuki husababisha jeuri. (1 Yohana 3:11, 12) Tunapaswa kujifunza kupendana.

7. Taja baadhi ya mazoea yanayoonyesha kwamba mtu haheshimu uhai.

7 Namna gani kuuheshimu uhai wetu wenyewe? Kwa kawaida watu hawapendi kufa, lakini watu fulani huhatarisha uhai wao ili kujifurahisha. Kwa mfano, watu wengi huvuta sigara, hutafuna miraa, au kutumia dawa za kulevya ili kujisisimua. Vitu hivyo huudhuru mwili na mara nyingi husababisha kifo. Mtu mwenye mazoea ya kutumia vitu hivyo hauoni uhai kuwa mtakatifu. Mazoea hayo ni machafu machoni pa Mungu. (Waroma 6:19; 12:1; 2 Wakorintho 7:1) Ili kumtumikia Mungu kwa njia inayompendeza, lazima tuache mazoea hayo. Ingawa huenda ikawa vigumu sana kuacha mazoea hayo, Yehova anaweza kutupa msaada tunaohitaji. Naye huthamini tunapojitahidi kuuona uhai wetu kuwa zawadi yenye thamani kutoka kwake.

8. Kwa nini tunapaswa kuzingatia usalama?

8 Ikiwa tunauheshimu uhai, tutazingatia usalama. Hatutakuwa wazembe wala kuhatarisha uhai ili kupata raha au msisimuko tu. Tutaepuka kuendesha magari ovyovyo na kushiriki katika michezo yenye jeuri au hatari. (Zaburi 11:5) Sheria ya Mungu aliyowapa Waisraeli wa kale ilisema: “Ikiwa utajenga nyumba mpya [yenye paa tambarare], pia utafanya ukuta wa ukingoni kwa ajili ya dari lako, ili usiletee nyumba yako hatia ya damu kwa sababu mtu anaweza kuanguka kutoka hapo.” (Kumbukumbu la Torati 22:8) Kupatana na kanuni ya sheria hiyo, ngazi za nyumba zinapaswa kuwa katika hali nzuri ili mtu asijikwae, aanguke, na kuumia vibaya. Ikiwa una gari, hakikisha kwamba ni salama kuliendesha. Makao yako au gari lako lisihatarishe kamwe uhai wako au wa wengine.

9. Ikiwa tunauheshimu uhai, tutawatendeaje wanyama?

9 Namna gani uhai wa wanyama? Huo pia ni mtakatifu kwa Muumba. Mungu anaruhusu kuua wanyama kwa ajili ya chakula na mavazi au ili kuwalinda watu wasipatwe na madhara. (Mwanzo 3:21; 9:3; Kutoka 21:28) Hata hivyo, kuwa mkatili kwa wanyama au kuwaua kwa ajili ya kujifurahisha tu ni kosa na ni kutoheshimu hata kidogo utakatifu wa uhai.—Methali 12:10.

KUHESHIMU DAMU

10. Mungu ameonyeshaje kwamba kuna uhusiano kati ya uhai na damu?

10 Baada ya Kaini kumuua Abeli ndugu yake, Yehova alimwambia Kaini: “Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo.” (Mwanzo 4:10) Mungu alipotaja damu ya Abeli, alikuwa akizungumzia uhai wa Abeli. Kaini alikuwa amekomesha uhai wa Abeli, na sasa ilikuwa lazima Kaini aadhibiwe. Ilikuwa kana kwamba damu ya Abeli, au uhai wake, ulikuwa ukimlilia Yehova ili haki itekelezwe. Uhusiano kati ya uhai na damu ulionyeshwa tena baada ya Mafuriko ya siku ya Noa. Kabla ya Mafuriko hayo, wanadamu walikuwa wakila matunda, mboga, nafaka, na kokwa tu. Baada ya Mafuriko, Yehova alimwambia Noa na wanawe: “Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu. Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapeni hao wote.” Hata hivyo, Mungu alitoa amri hii: “Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi yake [au, uhai wake]—damu yake—msile.” (Mwanzo 1:29; 9:3, 4) Ni wazi kwamba Yehova anahusianisha uhai na damu ya kiumbe.

11. Mungu alitoa amri gani kuhusu damu tangu siku za Noa?

11 Tunaonyesha kwamba tunaheshimu damu kwa kutoila. Katika Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli, aliamuru hivi: “Na mtu yeyote . . . ambaye katika kuwinda anamkamata mnyama-mwitu au ndege anayeweza kuliwa, basi ataimwaga damu yake na kuifunika kwa mavumbi. . . . Niliwaambia wana wa Israeli: ‘Hamtakula damu ya mwili wa namna yoyote.’” (Mambo ya Walawi 17:13, 14) Amri ambayo Mungu alimpa Noa karibu miaka 800 mapema kuhusu kutokula damu ya mnyama bado ilikuwa ikitumika. Maoni ya Yehova yalikuwa wazi: Watumishi wake wangeweza kula nyama ya mnyama lakini si damu yake. Walipaswa kuimwaga chini na hivyo kuurudisha uhai wa kiumbe huyo kwa Mungu.

12. Ni amri gani kuhusu damu iliyotolewa na roho takatifu katika karne ya kwanza ambayo ingali inatumika leo?

12 Wakristo pia wanapaswa kufuata amri hiyo. Mitume na wanaume wengine waliokuwa wakiongoza kati ya wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walikutana ili kuamua ni amri gani zilizopaswa kufuatwa katika kutaniko la Kikristo. Waliamua hivi: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi, ila mambo haya ya lazima, kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu na damu na vitu vilivyonyongwa [bila kutoa damu] na uasherati.” (Matendo 15:28, 29; 21:25) Kwa hiyo, lazima ‘tuendelee kujiepusha na damu.’ Machoni pa Mungu, kujiepusha na damu ni muhimu kama kujiepusha na ibada ya sanamu na uasherati.

Ikiwa daktari angekwambia ujiepushe na pombe, je, ungekubali itiwe mishipani mwako?

13. Toa mfano unaoonyesha kwamba amri ya kujiepusha na damu inahusu kutiwa damu mishipani.

13 Je, amri kuhusu kujiepusha na damu inahusu kutiwa damu mishipani? Ndiyo. Kwa mfano: Tuseme daktari angekuambia ujiepushe na pombe. Je, hilo lingemaanisha kwamba hupaswi kunywa pombe lakini unaweza kutiwa pombe mishipani mwako? Bila shaka hapana! Vivyo hivyo, kujiepusha na damu kunamaanisha kutoitia mwilini kwa njia yoyote ile. Kwa hiyo, amri ya kujiepusha na damu inamaanisha kwamba hatutamruhusu mtu yeyote atutie damu mishipani.

14, 15. Ikiwa madaktari wanasema kwamba Mkristo anapaswa kutiwa damu mishipani, afanyeje, na kwa nini?

14 Namna gani ikiwa Mkristo amejeruhiwa vibaya au anahitaji kufanyiwa upasuaji mkubwa? Huenda madaktari wakasema kwamba anapaswa kutiwa damu mishipani, la sivyo atakufa. Bila shaka, Mkristo hangependa kufa. Atajitahidi kuulinda uhai ambao ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu kwa kukubali matibabu ya aina nyingine ambayo hayahusishi matumizi yasiyofaa ya damu. Hivyo, atatafuta matibabu ya aina hiyo ikiwezekana na kukubali njia nyingine za tiba zisizotia ndani damu.

15 Je, Mkristo avunje sheria ya Mungu ili aishi muda mrefu kidogo katika mfumo huu wa mambo? Yesu alisema: “Kwa maana yeyote yule anayetaka kuiokoa nafsi yake [au uhai] ataipoteza; lakini yeyote yule anayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataipata.” (Mathayo 16:25) Hatutaki kufa. Lakini tukijaribu kuokoa uhai wetu wa sasa kwa kuvunja sheria ya Mungu, tutakuwa katika hatari ya kupoteza uzima wa milele. Basi ni jambo la hekima kutumaini sheria ya Mungu ya uadilifu, tukiwa na hakika kwamba ikiwa tutakufa kwa sababu yoyote ile, Mpaji-Uhai wetu atatukumbuka katika ufufuo na kuturudishia uhai ambao ni zawadi yenye thamani.—Yohana 5:28, 29; Waebrania 11:6.

16. Watumishi wa Mungu huazimia nini kwa uthabiti kuhusu damu?

16 Watumishi waaminifu wa Mungu leo, huazimia kwa uthabiti kufuata amri ya Mungu kuhusu damu. Hawawezi kula damu kwa njia yoyote ile. Wala hawawezi kukubali damu kwa sababu za matibabu. * Wana hakika kwamba Mungu, aliyeumba damu anajua kinachowafaa. Je, unaamini kwamba anajua?

MATUMIZI PEKEE YANAYOFAA YA DAMU

17. Yehova Mungu alikubali damu itumiwe kwa njia gani ya pekee katika Israeli la kale?

17 Sheria ya Musa ilikazia njia moja tu inayofaa ya kutumia damu. Kuhusu ibada ya Waisraeli wa kale, Yehova aliamuru hivi: “Nafsi ya [au, uhai wa] mwili iko katika damu, nami mwenyewe nimeiweka juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu, kwa sababu damu ndiyo hufanya upatanisho.” (Mambo ya Walawi 17:11) Waisraeli walipofanya dhambi, walipata msamaha kwa kutoa dhabihu ya mnyama na kiasi fulani cha damu yake kilitiwa kwenye madhabahu katika maskani au baadaye kwenye hekalu la Mungu. Njia pekee iliyofaa ya kutumia damu ilikuwa kwa ajili ya dhabihu kama hizo.

18. Tunaweza kupata baraka gani kupitia kwa damu ya Yesu iliyomwagwa?

18 Wakristo wa kweli hawako chini ya Sheria ya Musa na hivyo hawatoi dhabihu za wanyama na kuweka damu kwenye madhabahu. (Waebrania 10:1) Hata hivyo, kutumiwa kwa damu kwenye madhabahu katika Israeli la kale kuliwakilisha dhabihu ya mwisho na yenye thamani sana ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 5 ya kitabu hiki, Yesu alitoa uhai wake wa kibinadamu kwa ajili yetu kwa kuruhusu damu yake imwagwe ikiwa dhabihu. Kisha alienda mbinguni na kumtolea Mungu mara moja kwa wakati wote thamani ya damu yake iliyomwagwa. (Waebrania 9:11, 12) Kwa kufanya hivyo, aliweka msingi wa msamaha wa dhambi zetu na kutufungulia njia ya kupata uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Njia hiyo ya kutumia damu imethibitika kuwa muhimu sana! (1 Petro 1:18, 19) Tunaweza tu kupata wokovu kwa kuthamini damu ya Yesu iliyomwagwa.

Unaweza kuonyeshaje kwamba unathamini uhai na damu?

19. Ni lazima tufanye nini ili tuwe “safi kutokana na damu ya watu wote”?

19 Tunapaswa kumshukuru Yehova Mungu sana kwa sababu ya kutupa zawadi ya uhai kwa upendo! Je, hilo halipaswi kutuchochea kuwaambia wengine kuhusu pendeleo la kupata uzima wa milele kwa msingi wa imani katika dhabihu ya Yesu? Ikiwa tunathamini uhai wa wanadamu wenzetu kama Mungu anavyouthamini, tutachochewa kuwahubiria kwa hamu na bidii. (Ezekieli 3:17-21) Tukitimiza jukumu hilo kwa bidii, tutaweza kusema kama mtume Paulo alivyosema: “Mimi ni safi kutokana na damu ya watu wote, kwa maana sikuepuka kuwaambia ninyi mashauri yote ya Mungu.” (Matendo 20:26, 27) Kuwahubiria watu kumhusu Mungu na makusudi yake ni njia bora ya kuonyesha kwamba tunathamini sana uhai na damu.

^ fu. 16 Unaweza kupata habari kuhusu matibabu yasiyohusisha kutiwa damu mishipani kwenye sura yenye kichwa “Matibabu Mengine Bora Badala ya Damu” katika broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.