Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA TATU

Mawazo ya Mungu juu ya Uzima

Mawazo ya Mungu juu ya Uzima
  • Mungu anauona uzima namna gani?

  • Mawazo ya Mungu ni nini juu ya kutoa mimba?

  • Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunaheshimu uzima?

1. Ni nani aliyeumba kila kitu kilicho na uzima?

NABII Yeremia alisema: “Kwa kweli Yehova ni Mungu. Yeye ndiye Mungu aliye hai.” (Yeremia 10:10) Tena, Yehova Mungu ndiye Muumbaji wa kila kitu kilicho na uzima. Kule mbinguni viumbe vya kiroho walimuambia hivi: ‘Uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vikawako navyo vikaumbwa.’ (Ufunuo 4:11) Mufalme Daudi alimuimbia Mungu wimbo wa sifa, na katika wimbo huo alisema hivi: ‘Kwako wewe iko chemchemi ya uzima.’ (Zaburi 36:9) Kwa hiyo, uzima ni zawadi ambayo Mungu ametupatia.

2. Mungu anafanya nini ili tuendelee kuwa wazima?

2 Tena, Yehova ndiye anayefanya tuendelee kuwa wazima. (Matendo 17:28) Anatutolea chakula, maji, hewa, pia alifanya dunia mahali tunapoishi. (Matendo 14:15-17) Namna Yehova alivyofanya vitu hivyo inafanya mutu afurahie maisha. Lakini, ili tufurahie maisha kabisa, tunapaswa kujifunza sheria za Mungu na kuzitii.​—Isaya 48:17, 18.

TUHESHIMU UZIMA

3. Kaini alipomuua Abeli, Mungu alifanya nini?

3 Mungu anapenda tuheshimu uzima wetu na ule wa watu wengine. Kwa mufano, katika siku za Adamu na Eva, mwana wao Kaini alimukasirikia sana ndugu yake mudogo Abeli. Yehova alimuonya Kaini kama hasira yake inaweza kumufanya atende zambi nzito. Kaini hakupenda kusikia onyo hilo. ‘Alimushambulia Abeli ndugu yake, akamuua.’ (Mwanzo 4:3-8) Yehova alimuazibu Kaini kwa sababu alimuua ndugu yake.​—Mwanzo 4:9-11.

4. Katika Sheria ya Musa, namna gani Mungu alionyesha mawazo ambayo tunapaswa kuwa nayo juu ya uzima?

4 Kisha miaka 2 400 hivi, Yehova aliwapa Waisraeli sheria ili kuwasaidia wamutumikie namna anavyopenda. Wakati mwingine sheria hizo zinaitwa Sheria ya Musa, kwa sababu Mungu aliwapatia sheria hizo kupitia nabii Musa. Moja kati ya sheria hizo ilisema: “Usiue.” (Kumbukumbu la Torati 5:17) Hilo lilionyesha Waisraeli kama Mungu anaona uzima wa mwanadamu kuwa kitu cha bei sana na kama wanadamu wanapaswa kuona uzima wa wengine hivyo.

5. Namna gani tunapaswa kuona jambo la kutoa mimba?

5 Tuseme nini juu ya uzima wa mutoto ambaye hajazaliwa? Sheria ya Musa ilikataza kuua mutoto aliyekuwa angali katika tumbo la mama yake. Kwa kweli, hata uzima wa mutoto huyo Yehova anauona kuwa kitu cha bei sana. (Kutoka 21:22, 23; Zaburi 127:3) Hilo linaonyesha kama kutoa mimba ni vibaya kabisa.

6. Sababu gani hatupaswi kuwachukia wanadamu wenzetu?

6 Ili kuheshimu uzima inaomba pia kuwa na maoni mazuri juu ya wanadamu wenzetu. Biblia inasema hivi: ‘Kila mutu anayemuchukia ndugu yake ni muuaji, nanyi munajua kwamba hakuna muuaji aliye na uzima wa milele ukikaa ndani yake.’ (1 Yohana 3:15) Ikiwa tunataka kabisa kupata uzima wa milele, tunapaswa kuacha kabisa kuwachukia wanadamu wenzetu, kwa sababu mara nyingi chuki inaleta jeuri. (1 Yohana 3:11, 12) Tunapaswa kujifunza kupendana.

7. Taja mazoea fulani yanayoonyesha kama mutu anakosa kuheshimu uzima.

7 Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunauheshimu uzima wetu wenyewe? Kwa kawaida hakuna mutu anayependa kufa, lakini watu fulani wanahatarisha uzima wao kwa kujifurahisha tu. Kwa mufano, wanavuta tumbako, ao bangi na wengine wanatumia dawa ao vitu vingine vya kulewesha kwa kujifurahisha. Vitu hivyo vinaharibu mwili na mara nyingi vinaua wale wanaovitumia. Kama mutu ana mazoea ya kutumia vitu hivyo, hilo litaonyesha kama haoni uzima kuwa kitu kitakatifu. Mungu anaona mazoea hayo kuwa ni uchafu. (Waroma 6:19; 12:1; 2 Wakorintho 7:1) Ili Mungu akubali mutu amutumikie, mutu anapaswa kuachana kabisa na mazoea hayo. Hata ikiwa wakati mwingine inaweza kuwa vigumu sana kuachana na mazoea hayo, Yehova anaweza kutusaidia ili tuyashinde. Na anafurahi anapoona kuwa tunajikaza kuona uzima wetu kuwa zawadi yenye bei aliyotupatia.

8. Sababu gani tunapaswa kuepuka mambo yanayoweza kuhatarisha uzima?

8 Ikiwa tunaheshimu uzima, tutaepuka mambo yanayoweza kuhatarisha uzima. Tutakuwa wangalifu juu ya mambo tunayofanya ili tusihatarishe uzima wetu kwa kujifurahisha tu. Hatutatembeza motokari, pikipiki ao kinga ovyoovyo na hatutashiriki katika michezo ya jeuri na yenye kuhatarisha uzima. (Zaburi 11:5) Sheria ambayo Mungu aliwapatia Waisraeli zamani ilisema hivi: ‘Ikiwa utajenga nyumba mupya [yenye paa tambarare], pia utafanya ukuta wa ukingoni kwa ajili ya dari lako, ili usiletee nyumba yako hatia ya damu kwa sababu mutu anaweza kuanguka kutoka hapo.’ (Kumbukumbu la Torati 22:8) Kupatana na kanuni ya sheria hiyo, nafasi kama vile mwingilio wa nyumba inapaswa kuwa katika hali nzuri ili mutu asijikwae, aanguke, na kuumia vibaya. Ikiwa una motokari, pikipiki ao kinga uwe hakika kama haitatokeza musiba wakati unapoitembeza; uwe mwangalifu ili vitu hivyo visihatarishe uzima wako na uzima wa watu wengine.

9. Ikiwa tunaheshimu uzima, namna gani tutawatendea wanyama?

9 Tuseme nini juu ya uzima wa wanyama? Huo pia ni kitu kitakatifu machoni pa Muumbaji. Mungu anakubali tuue wanyama ili tupate chakula na mavazi ao ikiwa munyama anaweza kuhatarisha maisha ya watu. (Mwanzo 3:21; 9:3; Kutoka 21:28) Lakini, kutesa wanyama ao kuwaua kwa sababu ya kujifurahisha tu ni vibaya; kufanya hivyo ni kukosa kuheshimu utakatifu wa uzima.​—Methali 12:10.

TUHESHIMU DAMU

10. Namna gani Mungu alionyesha kama damu na uzima ni vitu viwili vinavyotembea pamoja?

10 Kaini alipokwisha kumuua ndugu yake Abeli, Yehova alimuambia hivi: “Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo.” (Mwanzo 4:10) Mungu alipotaja damu ya Abeli, alikuwa akisemea uzima wa Abeli. Kaini alipaswa kuazibiwa kwa sababu alikatiza uzima wa Abeli. Ni kama vile damu ya Abeli, ao uzima wake, ilikuwa ikimulilia Yehova ili akate jambo hilo. Kisha Garika ya siku za Noa, Yehova alionyesha tena kama damu na uzima ni vitu viwili vinavyotembea pamoja. Mbele ya Garika hiyo, watu walikuwa wanakula tu matunda, mboga, na vitu kama mihindi ao kalanga. Kisha Garika, Yehova alimuambia Noa na wana wake hivi: ‘Kila munyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu. Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapa ninyi hao wote.’ Hata hivyo, Mungu aliwaambia hivi: ‘Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi yake [ao, uzima]​—damu yake—​musikule.’ (Mwanzo 1:29; 9:3, 4) Yehova alionyesha wazi kama damu na uzima ni vitu viwili vinavyotembea pamoja.

11. Mungu alikataza nini juu ya damu tokea siku za Noa?

11 Ikiwa tunakataa kula damu, hilo linaonyesha kama tunaiheshimu. Katika Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli, aliwaamuru hivi: ‘Na mutu yeyote ambaye katika kuwinda anamukamata munyama wa mwitu ao ndege anayeweza kuliwa, basi ataimwaga damu yake na kuifunika kwa mavumbi. Niliwaambia wana wa Israeli: Hamutakula damu ya mwili wa namna yoyote.’ (Walawi 17:13, 14) Amri ambayo Mungu alimupatia Noa, kulikuwa kumekwisha kupita miaka 800, iliyomukataza kula damu ya munyama ilikuwa ingali inatumika. Yehova alionyesha wazi kama watumishi wake wangeweza kula nyama ya munyama lakini hawakupaswa kula damu. Walipaswa kumwanga damu chini, ili kuonyesha kama wanamurudishia Mungu uzima wa kiumbe hicho.

12. Wakati wa mitume, ni amri gani juu ya damu iliyotolewa na roho takatifu inayoendelea kutumika mupaka leo?

12 Wakristo pia wanapaswa kufuata amri hiyo. Wakati wa mitume, mitume na wanaume wengine waliokuwa wanaongoza Wakristo wengine walikutana ili kuamua ni amri gani zilizopaswa kufuatwa katika kutaniko la Kikristo. Walifikia uamuzi huu: ‘Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiwaongezee ninyi muzigo zaidi, ila mambo haya ya lazima, kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa zabihu kwa sanamu na damu na vitu vilivyonyongwa [bila kutoa damu] na uasherati.’ (Matendo 15:28, 29; 21:25) Kwa hiyo, tunapaswa ‘kujiepusha na damu.’ Machoni pa Mungu, kujiepusha na damu ni kwa lazima sana kama vile kujiepusha na ibada ya sanamu na uasherati.

Ikiwa muganga anakuambia ujiepushe na pombe, je, utakubali iingizwe katika mwili wako kwa njia ya mishipa?

13. Toa mufano unaoonyesha kama amri ya kujiepusha na damu inaangalia pia kutiwa damu katika mwili.

13 Je, amri ya kujiepusha na damu inaangalia pia kutiwa damu katika mwili? Ndiyo. Tuchukue mufano: Tuseme muganga anakuambia ujiepushe na pombe. Je, hilo linamaanisha kama anakuambia haupaswi kunywa pombe lakini unaweza kuiingiza katika mwili wako kwa njia ya mishipa? Hapana! Kujiepusha na damu kunamaanisha pia kukataa kuiingiza katika mwili kwa njia yoyote. Kwa hiyo, amri ya kujiepusha na damu inamaanisha kama hatukubali mutu yeyote atuingize damu katika mwili.

14, 15. Muganga akisema Mukristo anapaswa kutiwa damu, Mukristo atafanya nini, na sababu gani?

14 Tutafanya nini ikiwa Mukristo anaumia vikali ao inaomba afanyiwe upasuaji mukubwa? Labda muganga anaweza kusema kama ikiwa Mukristo huyo anakataa damu basi atakufa. Ni kweli kama Mukristo huyo hatapenda kufa. Atafanya yote awezayo ili kulinda uzima ambao ni zawadi ya Mungu yenye bei, kwa hiyo atakubali matunzo ya aina yote ambayo hayataomba kutiwa damu. Kwa hiyo, atakubali namna hiyo ya kutunzwa ikiwa inapatikana, na atakubali dawa zinazoweza kutumiwa lakini zisizo na damu.

15 Mukristo atavunja sheria ya Mungu ili ajaribu kurefusha kidogo maisha yake katika dunia hii? Yesu alisema hivi: “Kwa maana yeyote yule anayetaka kuikoa nafsi yake [ao uzima] ataipoteza; lakini yeyote yule anayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataipata.” (Mathayo 16:25) Hakuna mutu anayependa kufa. Lakini tukijaribu kuokoa uzima wetu wa sasa kwa kuvunja sheria ya Mungu, tutakuwa katika hatari ya kupoteza uzima wa milele. Basi ni jambo la hekima kutumaini sheria ya Mungu. Tuwe hakika kama tukikufa kwa sababu fulani, Yeye aliyetupatia uzima atatukumbuka wakati wa ufufuo na ataturudishia uzima ambao ni zawadi yenye bei.​—Yohana 5:28, 29; Waebrania 11:6.

16. Watumishi wa Mungu wameazimia nini kabisa juu ya damu?

16 Leo, watumishi waaminifu wa Mungu wameazimia kabisa kufuata amri ya Mungu juu ya damu. Hawawezi kula damu kwa njia yoyote. Wala hawawezi kukubali damu ili kuponyeshwa magonjwa fulani. * Wanaamini kabisa kama Mungu, aliyeumba damu, anajua ni nini inayowafaa zaidi. Wewe pia, unaamini jambo hilo?

NJIA MOJA TU ILIYOKUBALIWA ILI KUTUMIA DAMU

17. Katika Israeli, ni njia gani moja tu ya kutumia damu iliyokubaliwa na Yehova Mungu?

17 Sheria ya Musa ilionyesha njia moja tu iliyokubaliwa ili kutumia damu. Juu ya mambo ya ibada, Yehova aliamuru Waisraeli wa zamani hivi: ‘Nafsi [ao uzima] ya mwili iko katika damu, nami mwenyewe nimeiweka juu ya mazabahu ili ninyi mufanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu, kwa sababu damu ndiyo inayofanya upatanisho.’ (Walawi 17:11) Waisraeli walipofanya zambi, wangeweza kusamehewa kwa kutoa zabihu ya munyama na kwa kutia kiasi fulani cha damu yake kwenye mazabahu, ambayo hapo zamani ilipatikana katika hema, na baadaye kwenye hekalu. Hiyo ndio njia moja tu iliyokubaliwa ili kutumia damu.

18. Kwa sababu damu ya Yesu ilimwangika tunaweza kupata faida gani?

18 Wakristo wa kweli hawako chini ya Sheria ya Musa na kwa hiyo hawatowi zabihu za wanyama na kutia damu ya wanyama kwenye mazabahu. (Waebrania 10:1) Hata hivyo, damu ambayo Waisraeli walikuwa wakitia kwenye mazabahu, ilionyesha zabihu ya bei sana ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 5, Yesu alitoa uzima wa kibinadamu kwa ajili yetu kwa kukubali damu yake imwangwe ili iwe zabihu. Kisha alienda mbinguni na huko alimutolea Mungu kwa milele bei ya damu iliyomwangwa. (Waebrania 9:11, 12) Kwa hivyo, aliweka musingi wa kusamehewa kwa zambi zetu na kutufungulia njia ya kupata uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Njia hiyo ya kutumia damu imekuwa ya lazima sana! (1 Petro 1:18, 19) Tunaweza kupata wokovu ikiwa tu tunaamini bei ya damu ya Yesu iliyomwangika.

Namna gani unaweza kuonyesha kama unaheshimu uzima na damu?

19. Tunapaswa kufanya nini ili tusiwe na deni ya damu ya watu?

19 Tunapaswa kumushukuru Yehova Mungu kwa sababu ya zawadi ya uzima aliyotupatia kwa upendo! Je, hilo halipaswi kutuchochea tuwaambie wengine kama wao pia wanaweza kupata uzima wa milele ikiwa wanaamini zabihu ya Yesu? Ikiwa tunaona uzima wa wanadamu wenzetu kuwa kitu cha bei kama vile Mungu anavyouona, basi, tutawahubiria kwa furaha na kwa bidii. (Ezekieli 3:17-21) Tukitimiza kazi hiyo kwa bidii, tunaweza kusema kama mutume Paulo alivyosema: “Mimi ni safi kutokana na damu ya watu wote, kwa maana sikuepuka kuwaambia ninyi mashauri yote ya Mungu.” (Matendo 20:26, 27) Kuwahubiria watu juu ya Mungu na makusudi yake ndiyo njia nzuri zaidi ya kuonyesha kama tunaheshimu kabisa uzima na damu.

^ fu. 16 Ukipenda kujua zaidi juu ya dawa ao matunzo yasiyoomba kutiwa damu, soma ukurasa wa 13-17 wa broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.