Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA SITA

Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya Kweli

Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya Kweli
  • Biblia inafundisha nini kuhusu kutumia mifano katika ibada?

  • Wakristo huzionaje sikukuu za kidini?

  • Unaweza kuwaelezaje wengine imani yako bila kuwaudhi?

1, 2. Baada ya kutoka katika dini ya uwongo, unapaswa kujiuliza swali gani, na kwa nini ni muhimu?

NAMNA gani ukipata habari kwamba eneo lenu lote limetiwa sumu? Mtu fulani amekuwa akitupa kisiri takataka zenye sumu katika eneo lenu na maisha ya watu yamo hatarini sasa. Utafanya nini? Bila shaka utahama ikiwezekana. Hata hivyo, baada ya kuhama, bado utafikiria swali hili kwa uzito, ‘Je, nimeathiriwa na sumu hiyo?’

2 Ndivyo ilivyo kuhusiana na dini za uwongo. Biblia inafundisha kwamba ibada kama hiyo imechafuliwa na mafundisho na mazoea machafu. (2 Wakorintho 6:17) Ndiyo sababu unapaswa kutoka katika “Babiloni Mkubwa,” ambayo ni milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. (Ufunuo 18:2, 4) Je, tayari umefanya hivyo? Ikiwa ndivyo, unastahili kupongezwa. Hata hivyo, kuna mambo mengi ambayo unahitaji kufanya mbali na kujitenga au kujiuzulu kutoka katika dini ya uwongo. Baada ya kutoka, unapaswa kujiuliza, ‘Je, bado mimi ninashikilia mambo fulani niliyozoea kufanya nilipokuwa katika dini ya uwongo?’ Fikiria mifano kadhaa.

KUABUDU SANAMU NA MABABU

3. (a) Biblia inasema nini kuhusu kutumia sanamu, na kwa nini huenda ikawa vigumu kwa wengine kukubali maoni ya Mungu? (b) Unapaswa kufanya nini ikiwa una vitu vinavyohusiana na ibada ya uwongo?

3 Watu fulani wamekuwa na sanamu au vihekalu katika nyumba zao kwa miaka mingi. Je, wewe ni mmoja wao? Ikiwa ndivyo, huenda ukaona kwamba ni vigumu au ni vibaya kusali kwa Mungu bila kutumia vitu vinavyoonekana. Huenda hata unavipenda sana baadhi ya vitu hivyo. Lakini Mungu ndiye anayesema jinsi anavyotaka aabudiwe, na Biblia inafundisha kwamba hataki tutumie sanamu. (Kutoka 20:4, 5; Zaburi 115:4-8; Isaya 42:8; 1 Yohana 5:21) Kwa hiyo, unaweza kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli kwa kuharibu vitu vyovyote ulivyo navyo ambavyo vinahusiana na ibada ya uwongo. Kwa vyovyote vile, vione vitu hivyo jinsi Yehova anavyoviona, yaani, ni ‘vitu vinavyochukiza.’—Kumbukumbu la Torati 27:15.

4. (a) Tunajuaje kwamba kuabudu mababu ni kazi bure? (b) Kwa nini Yehova aliwaonya watu wake wasiwasiliane na pepo kwa njia yoyote?

4 Katika dini nyingi za uwongo, mababu pia huabudiwa. Kabla ya kujifunza kweli ya Biblia, watu fulani waliamini kwamba wafu wanaishi katika makao yasiyoonekana ya roho na kwamba wanaweza kuwasaidia au kuwaumiza walio hai. Labda ulikuwa ukijitahidi sana kuwatuliza mababu zako waliokufa. Lakini kama ulivyojifunza katika Sura ya 6 ya kitabu hiki, wafu hawana fahamu wala hawaishi popote. Kwa hiyo, ni kazi bure kujaribu kuwasiliana nao. Ujumbe wowote ambao inasemekana unatoka kwa mpendwa aliyekufa, kwa kweli unatoka kwa roho waovu. Kwa hiyo, Yehova aliwaonya Waisraeli wasijaribu kuongea na wafu au kuwasiliana na pepo kwa njia yoyote ile.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

5. Unaweza kufanya nini ikiwa zamani ulikuwa ukitumia sanamu au kuabudu mababu?

5 Ikiwa zamani ulikuwa ukitumia sanamu au kuabudu mababu, unaweza kufanya nini? Soma na utafakari maandiko ya Biblia yanayoonyesha maoni ya Mungu. Sali kwa Yehova kila siku kuhusu tamaa yako ya kuchukua msimamo upande wa kweli, na umwombe akusaidie uwe na maoni kama yake.—Isaya 55:9.

KRISMASI HAIKUSHEREHEKEWA NA WAKRISTO WA ZAMANI

6, 7. (a) Krismasi inasemekana kuwa ukumbusho wa nini, na je, wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza waliisherehekea? (b) Wakati wa wanafunzi wa kwanza wa Yesu, sherehe za kuzaliwa zilihusianishwa na nini?

6 Ibada ya mtu inaweza kuchafuliwa na dini za uwongo kupitia sherehe zinazopendwa. Kwa mfano, fikiria Krismasi. Inasemekana kwamba Krismasi ni ukumbusho wa kuzaliwa kwa Yesu Kristo, na karibu dini zote zinazodai kuwa za Kikristo husherehekea Krismasi. Hata hivyo, hakuna lolote linalothibitisha kwamba wanafunzi wa Yesu walisherehekea sikukuu hiyo. Kitabu Sacred Origins of Profound Things kinasema: “Kwa miaka 200 tangu Kristo alipozaliwa, hakuna mtu aliyejua siku hususa ambayo alizaliwa, na ni watu wachache tu waliotaka kujua.”

7 Hata kama wanafunzi wa Yesu wangejua tarehe hususa ya kuzaliwa kwake, hawangeisherehekea. Kwa nini? Kwa sababu, kama vile kitabu The World Book Encyclopedia kinavyosema, Wakristo wa zamani “waliona kusherehekea sikukuu ya kuzaliwa kwa mtu yeyote kuwa desturi ya kipagani.” Sikukuu pekee za kuzaliwa zinazotajwa katika Biblia ni zile za watawala wawili ambao hawakumwabudu Yehova. (Mwanzo 40:20; Marko 6:21) Pia, sikukuu za kuzaliwa zilisherehekewa ili kuheshimu miungu ya kipagani. Kwa mfano, mnamo Mei 24, Waroma walisherehekea kuzaliwa kwa mungu wa kike aliyeitwa Diana. Siku iliyofuata, walisherehekea kuzaliwa kwa mungu-jua aliyeitwa Apollo. Hivyo, sherehe za kuzaliwa zilihusianishwa na upagani wala si Ukristo.

8. Kuna uhusiano gani kati ya sherehe za kuzaliwa na ushirikina?

8 Kuna sababu nyingine ambayo ingewafanya Wakristo wasisherehekee kuzaliwa kwa Yesu. Inaelekea wanafunzi wake walijua kwamba sherehe za kuzaliwa zilihusiana na ushirikina. Kwa mfano, Wagiriki na Waroma wengi wa kale waliamini kwamba roho fulani ilikuwapo wakati wa kuzaliwa kwa kila mwanadamu na ilimlinda maisha yake yote. Kitabu The Lore of Birthdays kinasema kwamba, “roho hiyo ilikuwa na uhusiano wa kichawi pamoja na mungu ambaye siku ya kuzaliwa kwake ililingana na siku ya kuzaliwa kwa mtu huyo.” Bila shaka, Yehova hawezi kufurahishwa na sherehe yoyote ambayo inamhusianisha Yesu na ushirikina. (Isaya 65:11, 12) Basi, watu wengi walianzaje kusherehekea Krismasi?

KRISMASI ILIANZIA WAPI?

9. Desemba 25 ilichaguliwaje kuwa siku ya kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu?

9 Watu walitenga Desemba 25 kuwa siku ya kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu mamia ya miaka baada ya yeye kuishi duniani. Lakini Yesu hakuzaliwa siku hiyo, inaonekana alizaliwa mwezi wa Oktoba. * Basi, kwa nini Desemba 25 ilichaguliwa? Inaelekea kwamba baadaye watu fulani waliodai kuwa Wakristo “walitaka tarehe hiyo ipatane na sherehe ya kipagani ya Waroma ya ‘kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa.’” (The New Encyclopædia Britannica) Wakati wa majira ya baridi kali, jua lilipoonekana kuwa hafifu zaidi, wapagani walifanya sherehe ili kulifanya jua lirudi na kuwaletea joto na nuru. Walidhani kwamba jua lilianza kurudi Desemba 25. Katika jitihada za kuwafanya wapagani wawe Wakristo, viongozi wa kidini waliikubali sherehe hiyo na kujaribu kuifanya ionekane kuwa ya “Kikristo.” *

10. Kwa nini watu fulani hawakusherehekea Krismasi nyakati zilizopita?

10 Tangu zamani imejulikana kwamba Krismasi ilitokana na wapagani. Kwa kuwa ilitokana na chanzo kisichopatana na Maandiko, Krismasi ilipigwa marufuku katika karne ya 17 nchini Uingereza na pia katika koloni kadhaa za Amerika. Yeyote ambaye hakwenda kazini siku ya Krismasi alitozwa faini. Hata hivyo, punde si punde, desturi hizo za kale zikarudi, na nyingine mpya zikaongezwa. Kwa mara nyingine tena Krismasi ikawa sikukuu kubwa, na hivyo ndivyo ilivyo leo hii katika nchi nyingi. Hata hivyo, kwa sababu Krismasi inahusianishwa na dini za uwongo, wale wanaotaka kumpendeza Mungu hawaisherehekei wala hawasherehekei sikukuu nyingine yoyote iliyotokana na ibada ya kipagani. *

JE, VYANZO VYA SIKUKUU NI MUHIMU?

11. Kwa nini watu fulani husherehekea sikukuu, hata hivyo, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kwetu?

11 Watu fulani hukubali kwamba sikukuu kama vile Krismasi zilianzishwa na wapagani, hata hivyo, wanahisi kwamba si vibaya kuzisherehekea. Kwani, watu wengi wanaposherehekea sikukuu hizo hawafikirii ibada ya uwongo. Pia, pindi hizo huwezesha familia kuwa pamoja. Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Ikiwa ndivyo, huenda sababu inayokufanya uone ugumu kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli ni upendo wako kwa familia wala si kwa dini ya uwongo. Uwe na hakika kwamba Yehova aliyeanzisha familia anataka uwe na uhusiano mzuri na watu wako wa ukoo. (Waefeso 3:14, 15) Hata hivyo, unaweza kuimarisha vifungo hivyo kwa njia ambayo Mungu anakubali. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu jambo lililo muhimu zaidi maishani mwetu: “Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.”—Waefeso 5:10.

Je, unaweza kula peremende ambayo imeokotwa katika mtaro?

12. Eleza ni kwa nini tunapaswa kuepuka desturi na sherehe zenye vyanzo visivyofaa.

12 Huenda unahisi kwamba leo watu hawaadhimishi sikukuu kwa sababu ya vyanzo vyake. Je, vyanzo vya sikukuu ni muhimu? Ndiyo! Kwa mfano: Tuseme umeona peremende kwenye mtaro. Je, utaiokota na kuila? Haiwezekani! Peremende hiyo ni chafu. Sawa na peremende hiyo, huenda sikukuu hizo zinaonekana kuwa zenye kuvutia, hata hivyo, zimeokotwa mahali pachafu. Ili kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli, tunapaswa kuwa na maoni kama ya nabii Isaya, aliyewaambia hivi waabudu wa kweli: “Msiguse kitu chochote kilicho najisi.”—Isaya 52:11.

TUMIA UTAMBUZI UNAPOSHUGHULIKA NA WENGINE

13. Ni magumu gani yanayoweza kutokea usiposherehekea sikukuu?

13 Magumu yanaweza kutokea unapoamua kutosherehekea sikukuu. Kwa mfano, huenda wafanyakazi wenzako wakataka kujua ni kwa nini husherehekei sikukuu fulani zinazofanywa kazini. Vipi ukipewa zawadi ya Krismasi? Je, ni vibaya kuikubali? Vipi ikiwa mwenzi wako wa ndoa ana imani tofauti? Unaweza kuhakikishaje kwamba watoto wako hawahisi kwamba wamekosa kitu fulani kwa kutosherehekea sikukuu hizo?

14, 15. Unaweza kufanya nini ukipewa salamu ya sikukuu au ikiwa mtu anataka kukupa zawadi?

14 Unahitaji utambuzi ili kushughulikia kila hali inayotokea. Mtu akikupa salamu za sikukuu, unaweza tu kumshukuru kwa kukutakia heri. Lakini vipi ikiwa wewe humwona au kufanya kazi na mtu huyo kila siku. Basi, huenda ukaamua kumweleza mengi zaidi. Vyovyote vile, tumia busara. Biblia inashauri: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Uwe mwangalifu usije ukawavunjia wengine heshima. Badala yake, waeleze msimamo wako kwa busara. Waeleze waziwazi kwamba hakuna ubaya wa kutoa au kupokea zawadi na kuwa na sherehe, hata hivyo ungependa kufanya mambo hayo wakati mwingine.

15 Vipi ikiwa mtu anataka kukupa zawadi? Inategemea hali mbalimbali. Huenda mwenye kukupa zawadi akasema: “Najua kwamba husherehekei sikukuu. Hata hivyo, ningependa kukupa zawadi hii.” Basi, huenda ukaamua kwamba kupokea zawadi hiyo si sawa na kushiriki katika sikukuu. Bila shaka, ikiwa mwenye kukupa zawadi hajui imani yako, unaweza kumtajia kwamba wewe husherehekei sikukuu hiyo. Hilo litamsaidia kuelewa ni kwa nini ingawa unakubali kupokea zawadi yake, hutampa zawadi yoyote. Kwa upande mwingine, huenda isifae kupokea zawadi ikiwa yule anayekupa zawadi hiyo anataka kuonyesha kwamba hushikamani na imani yako au kwamba unaweza kuvunja imani yako ili kupata vitu vya kimwili.

NAMNA GANI WASHIRIKI WA FAMILIA?

16. Unawezaje kutumia busara unaposhughulikia mambo yanayohusiana na sikukuu?

16 Namna gani ikiwa washiriki wa familia wana imani tofauti? Unapaswa kuwa na busara. Hakuna haja ya kubishania kila desturi au sherehe ambayo watu wako wa ukoo wanaamua kusherehekea. Badala yake, heshimu maoni yao, kama vile ungependa waheshimu maoni yako. (Mathayo 7:12) Epuka mambo yoyote ambayo yangefanya uonekane kwamba unasherehekea sikukuu. Lakini utumie busara katika mambo ambayo hayahusiani moja kwa moja na sherehe za sikukuu. Bila shaka, sikuzote unapaswa kutenda kwa njia itakayokuacha ukiwa na dhamiri njema.—1 Timotheo 1:18, 19.

17. Unawezaje kuwasaidia watoto wako wasihisi kwamba wanakosa kitu fulani wanapowaona wengine wakisherehekea sikukuu fulani?

17 Unaweza kufanya nini ili watoto wako wasihisi kwamba wamekosa kitu fulani kwa sababu ya kutosherehekea sikukuu isiyopatana na Maandiko? Inategemea sana mambo unayofanya nyakati nyingine. Wazazi fulani hutenga nyakati za kuwapa watoto wao zawadi. Mojawapo ya zawadi bora zaidi ambazo unaweza kuwapa watoto wako ni kuwa pamoja nao na kuwaonyesha upendo.

UNGA MKONO IBADA YA KWELI

Kuunga mkono ibada ya kweli huleta furaha ya kweli

18. Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunawezaje kukusaidia kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli?

18 Ili kumpendeza Mungu, lazima ukatae kushiriki ibada ya uwongo na kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli. Hilo linatia ndani nini? Biblia inasema hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Mikutano ya Kikristo ni pindi za furaha ambazo unaweza kumwabudu Mungu kwa njia anayokubali. (Zaburi 22:22; 122:1) Kwenye mikutano hiyo, kuna “ubadilishanaji wa kitia-moyo” kati ya Wakristo waaminifu.—Waroma 1:12.

19. Kwa nini ni muhimu kuzungumza na wengine kuhusu mambo uliyojifunza katika Biblia?

19 Njia nyingine ya kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli ni kuwaambia wengine mambo ambayo umejua baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, watu wengi ‘wanaugua na kulia’ kwa sababu ya uovu unaotendeka ulimwenguni leo. (Ezekieli 9:4) Huenda unajua watu fulani wanaohisi hivyo. Unaweza kuzungumza nao kuhusu tumaini lako la wakati ujao linalotegemea Biblia. Unaposhirikiana na Wakristo wa kweli na kuzungumza na wengine kuhusu kweli nzuri za Biblia ambazo umejifunza, utaona kwamba tamaa yoyote ya kushiriki desturi za dini ya uwongo ambayo huenda bado ikawa moyoni mwako itatoweka hatua kwa hatua. Uwe na hakika kwamba utakuwa na furaha sana na utapata baraka nyingi ukichukua msimamo upande wa ibada ya kweli.—Malaki 3:10.

^ fu. 9 Sherehe ya Saturnalia pia ilichangia kuchaguliwa kwa Desemba 25. Sherehe hiyo inayomheshimu mungu wa kilimo wa Waroma ilifanywa Desemba 17 hadi 24. Katika sherehe hiyo ya Saturnalia, watu walikula na kunywa, walijitumbuiza na kupeana zawadi.

^ fu. 10 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu maoni ya Wakristo wa kweli juu ya sikukuu nyingine zinazopendwa na watu wengi, katika Nyongeza “Je, Tusherehekee Sikukuu?