Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA SABA

Mkaribie Mungu Katika Sala

Mkaribie Mungu Katika Sala
  • Kwa nini tunapaswa kusali kwa Mungu?

  • Ni lazima tufanye nini ili Mungu asikilize sala zetu?

  • Mungu hujibuje sala zetu?

“Mtengenezaji wa mbingu na dunia” yuko tayari kusikiliza sala zetu

1, 2. Kwa nini tunapaswa kuiona sala kuwa pendeleo kubwa, na kwa nini ni muhimu tujue mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu sala?

DUNIA ni ndogo sana inapolinganishwa na ulimwengu wote mzima. Kwa kweli, Yehova, “Mtengenezaji wa mbingu na dunia,” anayaona mataifa ya wanadamu kuwa kama tone dogo la maji katika ndoo. (Zaburi 115:15; Isaya 40:15) Hata hivyo, Biblia inasema: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli. Atawatimizia wale wanaomwogopa tamaa yao, naye atakisikia kilio chao cha kuomba msaada.” (Zaburi 145:18, 19) Hebu wazia! Muumba mweza-yote yuko karibu nasi naye atatusikiliza ‘tukimwitia yeye katika ukweli.’ Tuna pendeleo lililoje la kumkaribia Mungu katika sala!

2 Hata hivyo, ikiwa tungependa Yehova asikilize sala zetu, ni lazima tusali kulingana na mapenzi yake. Hatuwezi kufanya hivyo tusipojua mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu sala. Ni muhimu tujue yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu hilo kwa sababu sala inatusaidia kumkaribia Yehova.

KWA NINI TUSALI KWA YEHOVA?

3. Taja sababu moja muhimu inayotufanya tusali kwa Yehova.

3 Sababu moja muhimu inayotufanya tusali kwa Yehova ni kwamba anatuhimiza tufanye hivyo. Neno lake linatutia moyo: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kwa kweli, hatupaswi kupuuza uandalizi huo wenye fadhili kutoka kwa Mtawala Mkuu wa ulimwengu!

4. Kusali kwa ukawaida kunawezaje kuimarisha uhusiano wetu na Yehova?

4 Sababu nyingine ni kwamba tunaposali kwa ukawaida, uhusiano wetu na Yehova unaimarika. Marafiki wa kweli hawawasiliani tu wanapohitaji kitu fulani. Badala yake, marafiki wazuri huhangaikiana, na urafiki wao huimarika wanapozungumza kwa uhuru kuhusu maoni yao, kueleza hisia zao, na mahangaiko yao. Kwa njia fulani, ndivyo uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu ulivyo. Kitabu hiki kimekusaidia kujua mambo mengi ambayo Biblia inafundisha kumhusu Yehova, utu wake, na makusudi yake. Umejua kwamba yeye ni Mungu halisi. Sala hukuwezesha kumueleza Baba yako wa mbinguni mawazo na hisia zako za moyoni. Unapofanya hivyo, unamkaribia zaidi Yehova.​—Yakobo 4:8.

TUNAPASWA KUTIMIZA MATAKWA GANI?

5. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hasikilizi sala zote?

5 Je, Yehova husikiliza sala zote? Fikiria yale aliyowaambia Waisraeli waasi katika siku za nabii Isaya: “Hata mjapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa umwagaji wa damu.” (Isaya 1:15) Kwa hiyo, matendo fulani yanaweza kumfanya Mungu asisikilize sala zetu. Basi, ili sala zetu zisikilizwe na Mungu, ni lazima tutimize matakwa fulani muhimu.

6. Ili Mungu asikilize sala zetu, tunapaswa kutimiza takwa gani muhimu, na tunawezaje kufanya hivyo?

6 Takwa moja muhimu ni kuwa na imani. (Marko 11:24) Mtume Paulo aliandika: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Mbali na kuamini kwamba kuna Mungu anayesikiliza na kujibu sala, mengi yanahitajiwa ili kuwa na imani ya kweli. Imani huthibitika kwa matendo yetu. Maisha yetu ya kila siku yanapaswa kuthibitisha kwamba tuna imani.​—Yakobo 2:26.

7. (a) Kwa nini tunapaswa kuonyesha heshima tunapozungumza na Yehova katika sala? (b) Tunawezaje kuonyesha unyenyekevu na unyoofu tunaposali kwa Mungu?

7 Pia Yehova anataka wale wanaosali, wafanye hivyo kwa unyenyekevu na unyoofu. Tuna kila sababu ya kuwa wanyenyekevu tunapozungumza na Yehova, sivyo? Kwa kawaida, watu huzungumza na mfalme au rais, kwa heshima, wakitambua cheo chake cha juu. Basi, tunapaswa kumheshimu Yehova hata zaidi tunapozungumza naye. (Zaburi 138:6) Kwa kweli, yeye ni “Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Tunaposali kwa Mungu, tunapaswa kumfikia kwa njia inayoonyesha kwamba tunatambua kwa unyenyekevu hali yetu mbele zake. Unyenyekevu huo utatuchochea kusali kwa unyoofu kutoka moyoni mwetu, na kuepuka sala za kidesturi au za kurudia-rudia.​—Mathayo 6:7, 8.

8. Tunawezaje kutenda kulingana na sala zetu?

8 Ikiwa tunataka Mungu atusikilize, tunapaswa kutenda kulingana na sala zetu. Yehova anatarajia tujitahidi kadiri ya uwezo wetu kutenda kulingana na sala zetu. Kwa mfano, tukisali “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii,” ni lazima tufanye kwa bidii kazi yoyote tunayoweza kufanya. (Mathayo 6:11; 2 Wathesalonike 3:10) Tukisali atusaidie kushinda udhaifu fulani wa kimwili, ni lazima tuwe waangalifu na kuepuka mambo au hali zinazoweza kututia majaribuni. (Wakolosai 3:5) Mbali na matakwa hayo muhimu, kuna maswali kuhusu sala ambayo tungependa kujibiwa.

KUJIBU MASWALI FULANI KUHUSU SALA

9. Tunapaswa kusali kwa nani, na kupitia nani?

9 Tunapaswa kusali kwa nani? Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kwa ‘Baba yetu aliye mbinguni.’ (Mathayo 6:9) Hivyo, sala zetu zinapaswa kuelekezwa kwa Yehova Mungu peke yake. Hata hivyo, Yehova anataka tutambue cheo cha Mwana wake mzaliwa wa pekee, Yesu Kristo. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 5, Yesu alitumwa duniani ili awe fidia na kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo. (Yohana 3:16; Waroma 5:12) Yeye ndiye Kuhani Mkuu na Hakimu aliyewekwa rasmi. (Yohana 5:22; Waebrania 6:20) Hivyo, Maandiko yanatuagiza tutoe sala zetu kupitia Yesu. Yeye mwenyewe alisema: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Ili sala zetu zisikiwe, ni lazima tusali kwa Yehova tu kupitia Mwanaye.

10. Kwa nini hatuhitaji kuwa katika hali fulani hususa tunaposali?

10 Je, ni lazima tuwe katika hali fulani hususa tunaposali? Hapana. Yehova hahitaji tufanye jambo fulani hususa tunaposali. Biblia inafundisha kwamba tunaweza kusali tukiwa katika hali mbalimbali. Tunaweza kusali tukiwa tumeketi, tumeinama, tumepiga magoti, na tukiwa tumesimama. (1 Mambo ya Nyakati 17:16; Nehemia 8:6; Danieli 6:10; Marko 11:25) Jambo muhimu si kukaa katika hali fulani hususa ili tuonwe na wengine, bali ni kuwa na mwelekeo unaofaa. Isitoshe, tunapokuwa katika shughuli zetu za kila siku au tunapokabili hali ya dharura, tunaweza kusali kimyakimya popote tulipo. Yehova husikiliza sala kama hizo hata ingawa hazisikiwi na watu walio karibu nasi.​—Nehemia 2:1-6.

11. Ni mahangaiko gani ya kibinafsi tunayoweza kusali juu yake?

11 Tunaweza kusali kuhusu nini? Biblia inaeleza: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye [Yehova] hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Basi tunaweza kuomba chochote kulingana na mapenzi ya Mungu. Je, ni mapenzi yake tusali kuhusu mahangaiko yetu? Ndiyo, bila shaka! Kusali kwa Yehova ni kama kuongea na rafiki wa karibu. Tunaweza kuongea waziwazi, ‘tukimimina moyo wetu’ mbele za Mungu. (Zaburi 62:8) Tunapaswa kuomba roho takatifu, kwa sababu itatusaidia kufanya mambo yanayofaa. (Luka 11:13) Tunaweza pia kuomba mwongozo wa kufanya maamuzi ya hekima na nguvu za kukabiliana na magumu. (Yakobo 1:5) Tunapofanya dhambi, tunapaswa kuomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Kristo. (Waefeso 1:3, 7) Lakini hatupaswi kusali tu kuhusu mambo ya kibinafsi. Tunapaswa kusali kwa niaba ya watu wengine kama vile familia yetu na pia waabudu wenzetu.​—Matendo 12:5; Wakolosai 4:12.

12. Tunawezaje kumtanguliza Baba yetu wa mbinguni katika sala zetu?

12 Katika sala zetu, tunapaswa kutanguliza mambo yanayomhusu Yehova Mungu. Bila shaka tuna kila sababu ya kumsifu na kumshukuru kutoka moyoni kwa sababu ya wema wake wote. (1 Mambo ya Nyakati 29:10-13) Katika sala ya kielelezo iliyo kwenye Mathayo 6:9-13, Yesu alitufundisha tusali jina la Mungu litakaswe, yaani, lionwe kuwa takatifu. Kisha tusali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Baada ya kuzungumzia mambo hayo muhimu kumhusu Yehova ndipo Yesu alipotaja mambo ya kibinafsi. Sisi pia tunapomtanguliza Mungu katika sala zetu, tunaonyesha kwamba hatuhangaikii tu mambo yetu wenyewe.

13. Maandiko yanasema nini kuhusu urefu wa sala zinazokubalika?

13 Sala zetu zinapaswa kuwa na urefu gani? Biblia haisemi sala zinazotolewa faraghani au hadharani zinapaswa kuwa na urefu gani. Tunaweza kutoa sala fupi kabla ya kula au sala ndefu faraghani tunapomweleza Yehova mambo yaliyo moyoni mwetu. (1 Samweli 1:12, 15) Hata hivyo, Yesu aliwashutumu watu waliojiona kuwa waadilifu ambao walitoa sala ndefu ili waonekane na watu. (Luka 20:46, 47) Sala za aina hiyo hazimpendezi Yehova. Jambo muhimu ni kusali kutoka moyoni. Hivyo, sala zinazokubalika zinaweza kuwa na urefu mbalimbali ikitegemea hali na mahitaji.

Mungu anaweza kusikia sala zako wakati wowote

14. Biblia inamaanisha nini inapotuhimiza ‘tusali sikuzote,’ na kwa nini hilo linatufariji?

14 Tunapaswa kusali mara ngapi? Biblia inatutia moyo ‘tusali sikuzote,’ ‘tudumu katika sala,’ na ‘tusali bila kuacha.’ (Mathayo 26:41; Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 5:17) Bila shaka, maandiko hayo hayamaanishi kwamba tunapaswa kusali kwa Yehova kila dakika. Badala yake, Biblia inatuhimiza tusali kwa ukawaida na kumshukuru Yehova daima kwa sababu ya wema wake kwetu na kumwomba atuongoze, atufariji, na kutuimarisha. Je, haitii moyo kujua kwamba Yehova haweki mipaka kuhusu urefu au mara ambazo tunaweza kuzungumza naye katika sala? Ikiwa tunathamini kikweli pendeleo la sala, tutapata nafasi nyingi za kusali kwa Baba yetu wa mbinguni.

15. Kwa nini tunapaswa kusema “Amina” mwishoni mwa sala za kibinafsi na za hadharani?

15 Kwa nini tunapaswa kusema “Amina” mwishoni mwa sala? Neno “amina” humaanisha “bila shaka,” au “iwe hivyo.” Mifano ya kimaandiko inaonyesha kwamba tunapaswa kusema “Amina” mwishoni mwa sala za kibinafsi na za hadharani. (1 Mambo ya Nyakati 16:36; Zaburi 41:13) Tunaposema “Amina” mwishoni mwa sala zetu, tunaonyesha kwamba maneno yetu yanatoka moyoni. Tunaposema “Amina” kimyakimya au kwa sauti baada ya mtu fulani kutoa sala hadharani, tunaonyesha kwamba tunakubaliana na sala hiyo.​—1 Wakorintho 14:16.

JINSI MUNGU ANAVYOJIBU SALA ZETU

16. Tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu sala zetu?

16 Je, kweli Yehova hujibu sala? Bila shaka! Tuna sababu thabiti ya kuamini kwamba “Msikiaji wa sala” hujibu sala zinazotolewa na mamilioni ya wanadamu wanyoofu. (Zaburi 65:2) Yehova anaweza kujibu sala zetu kwa njia mbalimbali.

17. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mungu hutumia malaika na watumishi wake duniani kujibu sala zetu?

17 Yehova hutumia malaika wake na watumishi wake duniani kujibu sala. (Waebrania 1:13, 14) Kuna watu wengi ambao walisali kwa Mungu ili wapate msaada wa kuielewa Biblia na muda si muda wakatembelewa na mmoja wa watumishi wa Yehova. Mambo kama hayo yanaonyesha kwamba malaika wanaongoza kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme. (Ufunuo 14:6) Yehova anaweza kumchochea Mkristo mwenzetu atusaidie tunaposali wakati wa uhitaji mkubwa.​—Methali 12:25; Yakobo 2:16.

Yehova anaweza kujibu sala zetu kwa kumchochea Mkristo mwenzetu atusaidie

18. Yehova hutumiaje roho yake takatifu na Neno lake kujibu sala za watumishi wake?

18 Yehova Mungu pia hutumia roho yake takatifu na Neno lake, Biblia, kujibu sala za watumishi wake. Tunapoomba msaada wa kukabiliana na majaribu, anaweza kutujibu kwa kutuongoza na kutuimarisha kwa roho yake takatifu. (2 Wakorintho 4:7) Mara nyingi Biblia hujibu sala zetu za kuomba mwongozo. Yehova hutusaidia kufanya maamuzi ya hekima kupitia Biblia. Tunapojifunza Biblia kibinafsi na tunaposoma vichapo vya Kikristo kama kitabu hiki, tunaweza kupata maandiko yanayoweza kutusaidia. Tunaweza kukumbushwa habari za kimaandiko kwenye mikutano ya Kikristo au na mzee wa kutaniko anayetuhangaikia.​—Wagalatia 6:1.

19. Tunapaswa kukumbuka nini tunapohisi kwamba sala zetu hazijibiwi nyakati nyingine?

19 Tukihisi kwamba Yehova anachelewa kujibu sala zetu, haimaanishi kwamba hawezi kujibu. Badala yake, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hujibu sala kupatana na mapenzi yake na kwa wakati wake. Anajua mahitaji yetu na jinsi ya kuyatimiza kuliko tuwezavyo. Mara nyingi yeye huturuhusu ‘tuendelee kuomba, kutafuta, na kupiga hodi.’ (Luka 11:5-10) Tunapoendelea kufanya hivyo, tunamwonyesha Mungu kwamba tunatamani sana jambo tunaloomba na tuna imani ya kweli. Isitoshe, Yehova anaweza kujibu sala zetu kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Kwa mfano, anaweza kujibu sala yetu kuhusiana na jaribu fulani kwa kutupa nguvu za kuvumilia badala ya kuliondoa jaribu hilo.​—Wafilipi 4:13.

20. Kwa nini tunapaswa kutumia kikamili pendeleo lenye thamani la sala?

20 Tunapaswa kushukuru kwamba Muumba wa ulimwengu huu mkubwa yuko karibu na wote wanaomwitia kwa njia inayofaa katika sala. (Zaburi 145:18) Na tutumie kikamili pendeleo lenye thamani la sala. Tukifanya hivyo, tutapata shangwe ya kumkaribia zaidi Yehova, ambaye ni Msikiaji wa sala.