Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA MUNANE

Ubatizo Ni Hatua Inayomuongoza Mutu Kwenye Uhusiano Muzuri Pamoja na Mungu

Ubatizo Ni Hatua Inayomuongoza Mutu Kwenye Uhusiano Muzuri Pamoja na Mungu
  • Ubatizo wa Kikristo unafanywa namna gani?

  • Ni hatua gani unazopaswa kufanya ili ustahili kubatizwa?

  • Ili mutu ajitoe kwa Mungu inaomba afanye nini?

  • Ubatizo unaonyesha kabisa nini?

1. Sababu gani yule Muetiopia aliomba kubatizwa?

“TAZAMA! Maji; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Muetiopia mumoja aliyekuwa na mamlaka katika makao ya kifalme ndiye aliyeuliza ulizo hilo wakati wa mitume. Mukristo aliyeitwa Filipo, alikuwa amemuonyesha wazi kama Yesu alikuwa ndiye Masiya aliyeahidiwa. Kwa sababu Muetiopia huyo aliguswa na mambo hayo, alichukua uamuzi. Alimuambia Filipo kama anapenda kubatizwa!​—Matendo 8:26-36.

2. Ni nini inayoonyesha kama unapaswa sasa kuwaza kwa uzito juu ya ubatizo?

2 Ikiwa umejifunza vizuri sura zilizotangulia pamoja na Shahidi fulani wa Yehova, labda wewe vilevile utapenda kuuliza, ‘Ni nini kinachonizuia mimi kubatizwa?’ Kufikia sasa umejifunza ahadi za Biblia juu ya uzima wa milele katika Paradiso. (Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4) Tena umejifunza juu ya hali ya watu waliokufa na tumaini la ufufuo. (Mhubiri 9:5; Yohana 5:28, 29) Labda unakusanyika na Mashahidi wa Yehova na umejionea mwenyewe kama wao wana dini ya kweli. (Yohana 13:35) Jambo la lazima zaidi, labda mambo unayofanya sasa yamekusaidia kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova Mungu.

3. (a) Yesu aliwapa wanafunzi wake amri gani? (b) Ubatizo wa maji unafanywa namna gani?

3 Namna gani unaweza kuonyesha kama unataka kumutumikia Mungu? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: ‘Nendeni mufanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mukiwabatiza.(Mathayo 28:19) Yesu mwenyewe alituwekea mufano alipobatizwa katika maji. Hawakumumwangia maji kidogo kwenye kichwa. (Mathayo 3:16) Neno “kubatiza” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kuzamisha.” Kwa hiyo, ubatizo wa Kikristo unamaanisha kuzamisha, ao kutumbukiza kabisa mutu ndani ya maji.

4. Unapobatizwa katika maji unaonyesha nini?

4 Kila mutu anayetaka kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova Mungu anapaswa kubatizwa katika maji. Unapobatizwa katika maji unaonyesha mbele ya watu kama unapenda kumutumikia Mungu. Tena, unaonyesha kama unapenda kufanya mapenzi yake. (Zaburi 40:7, 8) Hata hivyo, ili ustahili kubatizwa unapaswa kufanya hatua fulani.

INAOMBA UWE NA UJUZI NA IMANI

5. (a) Taja hatua ya kwanza ambayo mutu anapaswa kufanya ili astahili kubatizwa? (b) Sababu gani kuhuzuria mikutano ni kwa lazima sana?

5 Umekwisha kuanza kufanya hatua ya kwanza. Namna gani? Tayari unajifunza kumujua Yehova na Yesu Kristo, na labda unajifunza Biblia kwa ukawaida na shahidi fulani. (Yohana 17:3) Hata hivyo, ungali na mambo mengi ya kujifunza. Wakristo wanataka ‘wajazwe ujuzi sahihi wa mapenzi yake [Mungu].’ (Wakolosai 1:9) Ndiyo sababu kukusanyika na Mashahidi wa Yehova kutakusaidia sana ufikie jambo hilo. Ni lazima sana kuhuzuria mikutano hiyo. (Waebrania 10:24, 25) Kukusanyika kwa ukawaida kutakusaidia umujue Mungu vizuri zaidi.

Kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu ni hatua ya lazima ambayo mutu anapaswa kufanya ili astahili kubatizwa

6. Ni mafundisho gani ya musingi mutu anapaswa kujua mbele ya kustahili kubatizwa?

6 Ni kweli kama si lazima ujue Biblia yote ili ustahili kubatizwa. Yule Muetiopia alikuwa na kiasi fulani cha ujuzi, lakini iliomba asaidiwe ili kuelewa mambo mengine yaliyo katika Maandiko. (Matendo 8:30, 31) Vilevile, wewe pia ungali na mambo mengi ya kujifunza. Jua kama kujifunza juu ya Mungu hakuna mwisho. (Mhubiri 3:11) Hata hivyo, mbele ya kubatizwa unapaswa kujua na kukubali mafundisho ya musingi ya Biblia. (Waebrania 5:12) Kwa mufano unapaswa kujua na kukubali yale Biblia inafundisha juu ya hali ya watu waliokufa na tena kujua sababu gani jina la Mungu na Ufalme wake ni mambo ya lazima sana.

7. Kujifunza Biblia kunapaswa kukusaidia uamini nini?

7 Hata hivyo, kuwa tu na ujuzi hakutoshi, kwa maana ‘bila imani haiwezekani kamwe kumupendeza [Mungu] vema.’ (Waebrania 11:6) Biblia inatuambia kama watu fulani wa muji wa kale wa Korintho waliposikia habari iliyohubiriwa na Wakristo, ‘walianza kuamini na kubatizwa.’ (Matendo 18:8) Vilevile, kujifunza Biblia kunapaswa kukusaidia uamini kama Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. Kujifunza Biblia kunapaswa kukusaidia uamini ahadi za Mungu, na uamini kama zabihu ya Yesu inaweza kukuokoa.​—Yoshua 23:14; Matendo 4:12; 2 Timotheo 3:16, 17.

INAOMBA KUZUNGUMUZIA WENGINE KWELI YA BIBLIA

Imani inapaswa kukusukuma ili uzungumuzie wengine mambo ambayo umejifunza

8. Ni nini itakayokusukuma kuzungumuzia wengine mambo ambayo umejifunza?

8 Imani inapoendelea kukomaa katika moyo wako, hautakosa kuwaelezea wengine yale ambayo umejifunza. (Yeremia 20:9) Kwa hiyo, imani itakusukuma kabisa kuzungumuza na wengine juu ya Mungu na makusudi yake.​—2 Wakorintho 4:13.

9, 10. (a) Unaweza kuanza kuwahubiria nani kweli ya Biblia? (b) Unapaswa kufanya nini ikiwa unapenda kuhubiri pamoja na kutaniko la Mashahidi wa Yehova?

9 Unaweza kwanza kuelezea watu wa jamaa yako, marafiki, majirani na wafanyakazi wenzako kweli ya Biblia, lakini fanya hivyo kwa busara. Kisha, labda utapenda kuhubiri pamoja na kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Ikiwa ni hivyo, basi zungumuza jambo hilo na Shahidi unayejifunza naye Biblia. Ikiwa unastahili kuwa muhubiri, mipango itafanywa ili wazee wawili wa kutaniko wazungumuze pamoja nawe, ndugu ao dada unayejifunza naye Biblia atakuwa hapo pia.

10 Mazungumuzo hayo yatakusaidia uwajue vizuri wazee wa kutaniko walio na daraka la kuchunga kundi la Mungu. (Matendo 20:28; 1 Petro 5:2, 3) Wazee hao wakiona kama unaelewa na kuamini mafundisho ya musingi ya Biblia, unaishi kulingana na kanuni za Mungu, na ikiwa kwa kweli unapenda kuwa Shahidi wa Yehova, watakujulisha kama unastahili kuwa muhubiri asiyebatizwa, na kwa hiyo unaweza sasa kuanza kuhubiri habari njema pamoja na kutaniko.

11. Ni mabadiliko gani ambayo watu fulani wanapaswa kufanya kwanza ili wastahili kuhubiri pamoja na kutaniko?

11 Labda wazee hao wataona kama ungali na lazima ya kufanya mabadiliko fulani katika maisha yako na tabia zako ili ustahili kuhubiri pamoja na kutaniko. Labda inaomba kwanza uachane na mazoea fulani mabaya ambayo ulikuwa ukifanya kwa siri. Kwa hiyo, mbele ya kuomba kuwa muhubiri asiyebatizwa, ni lazima uachane kabisa na zambi nzito, kama vile mambo ya uasherati, ulevi na dawa za kulewesha.​—1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5:19-21.

INAOMBA KUTUBU NA KUGEUKA

12. Sababu gani kila mutu anapaswa kutubu?

12 Kuna hatua zingine ambazo inakuomba kufanya ili ustahili kubatizwa. Mutume Petro alisema: ‘Tubuni na mugeuke ili zambi zenu zipate kufutwa.’ (Matendo 3:19) Kutubu ni kusikitika kwelikweli kwa Sababu ya jambo fulani ulilofanya. Ikiwa mutu alikuwa anafanya mambo mabaya anapaswa kutubu; lakini hata ikiwa mutu hakuwa anafanya mambo mabaya anapaswa kutubu pia. Sababu gani? Kwa sababu wanadamu wote ni watenda zambi na kwa hiyo wana lazima ya musamaha wa Mungu. (Waroma 3:23; 5:12) Mbele ya kujifunza Biblia, haukujua mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo, haingewezekana uishi kulingana na mapenzi yake, sivyo? Basi, unapaswa kutubu.

13. Kugeuka kunamaanisha nini?

13 Kisha kutubu, unapaswa ‘kugeuka.’ Haitoshi tu kusikitika. Ili kuonyesha kama unageuka, unapaswa kukataa kabisa mambo uliyokuwa ukifanya zamani na kuazimia kabisa kuendelea kufanya yaliyo mema katika maisha yako yote. Kutubu na kugeuka ni hatua unazopaswa kufanya mbele ya kubatizwa.

INAOMBA KUJITOA KWA MUNGU

14. Ni hatua gani ya lazima sana unayopaswa kufanya mbele ya kubatizwa?

14 Mbele ya kubatizwa kuna hatua ingine ya lazima sana unayopaswa kufanya. Unapaswa kujitoa kwa Yehova Mungu.

Je, umejitoa kwa Mungu katika sala?

15, 16. Kujitoa kwa Mungu kunamaanisha nini, na ni nini inayopaswa kumusukuma mutu ajitoe kwa Mungu?

15 Mutu anajitoa mwenyewe kwa Yehova Mungu katika sala inayotoka moyoni, siku hiyo anamuahidi kama atashikamana na yeye tu milele na milele. (Kumbukumbu la Torati 6:15) Kwa hiyo, ni nini inayoweza kumusukuma mutu afanye ahadi kama hiyo? Tuchukue mufano: Kijana fulani anaanza kumuchumbia binti fulani. Kadiri anavyoendelea kuona sifa nzuri za binti huyo ndivyo anavyozidi kuvutiwa naye. Kisha wakati fulani, atamuambia kama anapenda waoane. Ni kweli, hata ikiwa ndoa inaongeza madaraka, atamuoa tu binti huyo kwa sababu anamupenda.

16 Kisha kumujua Yehova na kumupenda, utasukumwa kumutumikia bila kusita na kumuabudu kwa moyo wako wote. Kila mutu anayetaka kumufuata Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, lazima “ajikane mwenyewe.” (Marko 8:34) Mutu anayejikana mwenyewe hataacha tamaa yake na miradi yake vimuzuie kumutii Mungu kwa moyo wote. Kwa hiyo, mbele ya kubatizwa, muradi wako maishani unapaswa kuwa kufanya mapenzi ya Yehova Mungu.​—1 Petro 4:2.

USIOGOPE KUJITOA KWA MUNGU

17. Sababu gani watu fulani wanasita kujitoa kwa Mungu?

17 Watu fulani wanasita kujitoa kwa Yehova kwa sababu wanaona kuwa hatua hiyo si ya muchezo, na kwa hiyo wanaogopa. Wanaogopa kama wakiwa wenye kujitoa kwa Mungu, Mungu atawaomba hesabu ya mambo wanayofanya. Wanaogopa kama wakifanya makosa Yehova atahuzunika sana, kwa hiyo, wanaona ni afazali wasijitoe kwake.

18. Ni nini inayoweza kukusukuma ujitoe kwa Mungu?

18 Ikiwa unaendelea kujifunza kumupenda Yehova, utasukumwa kujitoa kwake na utajikaza sana kuishi kulingana na ahadi yako. (Mhubiri 5:4) Kisha kujitoa, utajikaza ‘kutembea kwa kumustahili Yehova kwa kusudi la kumupendeza yeye kikamili.’ (Wakolosai 1:10) Kwa kuwa sasa unamupenda Mungu, utaona si vigumu kabisa kufanya mapenzi yake. Kwa kweli, utakubaliana na mutume Yohana aliyeandika: ‘Kumupenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si muzigo muzito.’​—1 Yohana 5:3.

19. Sababu gani haupaswi kuogopa kujitoa kwa Mungu?

19 Haiombi uwe mukamilifu ili ujitoe kwa Mungu. Yehova anajua uwezo wako naye hatazamii hata kidogo ufanye mambo yanayoshinda uwezo wako. (Zaburi 103:14) Anataka utimize ahadi yako kwake, kwa hiyo, atakutegemeza na kukusaidia. (Isaya 41:10) Hakika, ukimutumainia Yehova kabisa, “atanyoosha mapito yako.”​—Methali 3:5, 6.

UBATIZO UNAONYESHA KUWA UMEJITOA KWA MUNGU

20. Sababu gani tendo la kujitoa kwa Yehova halipaswi kubaki siri kati yako na Yehova?

20 Kufikiri kwa uzito mambo ambayo tumezungumuzia kunaweza kukusaidia uchukue uamuzi wa kujitoa kwa Yehova katika sala. Kila mutu anayemupenda Mungu kwelikweli anapaswa pia ‘kufanya tangazo la hazarani kwa ajili ya wokovu.’ (Waroma 10:10) Mutu anafanya tangazo hilo namna gani?

Ubatizo unamaanisha kufa, ao kuachana kabisa na maisha ya zamani, na kuanza maisha mapya ili kufanya mapenzi ya Mungu

21, 22. Namna gani unaweza ‘kufanya tangazo la hazarani’ la imani yako?

21 Umujulishe muratibu wa baraza la wazee wa kutaniko lenu kama unapenda kubatizwa. Atafanya mipango ili wazee fulani wachunguze tena pamoja nawe maulizo fulani ya mafundisho ya musingi ya Biblia. Ikiwa wazee hao wanaona unastahili, watakujulisha kama utabatizwa kwenye mukusanyiko unaofuata. * Kwa kawaida hotuba inayoeleza maana ya ubatizo inatolewa kwenye mikusanyiko hiyo. Kisha musemaji anawaomba wote watakaobatizwa wajibu maulizo mawili mepesi, hilo linawatolea nafasi ya ‘kufanya tangazo la hazarani’ la imani yao.

22 Unapobatizwa, wakati huo ndipo unaonyesha mbele ya watu wote kama ulijitoa kwa Mungu na sasa wewe ni Shahidi wa Yehova. Watu wanaobatizwa wanazamishwa kabisa katika maji ili kuonyesha mbele ya watu wote kama wamekwisha kujitoa kwa Yehova.

MAANA YA UBATIZO WAKO

23. Kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu” inamaanisha nini?

23 Yesu alisema kama wanafunzi wake watabatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mathayo 28:19) Hilo linamaanisha kuwa mutu anayetaka kubatizwa anatambua mamlaka ya Yehova Mungu na ya Yesu Kristo. (Zaburi 83:18; Mathayo 28:18) Tena anatambua kazi ya roho takatifu, ambayo ni nguvu ya utendaji ya Mungu.​—Wagalatia 5:22, 23; 2 Petro 1:21.

24, 25. (a) Ubatizo ni alama ya jambo gani la maana sana? (b) Ni ulizo gani linaomba kujibiwa?

24 Hata hivyo, ubatizo si tu jambo la kumuzamisha mutu katika maji. Ni alama ya jambo fulani la lazima sana. Unapozamishwa katika maji unaonyesha kama umekufa, ao umeachana kabisa na maisha yako ya zamani. Unapoinuliwa kutoka katika maji unaonyesha kama sasa umeanza maisha mapya ili kufanya mapenzi ya Mungu. Kumbuka pia kama haukujitoa kwa kazi fulani, muradi fulani, mutu fulani, ao tengenezo fulani, lakini kwa Yehova Mungu mwenyewe. Kujitoa kwako na ubatizo wako ni mwanzo wa kuwa na uhusiano muzuri sana na wenye nguvu pamoja na Yehova.​—Zaburi 25:14.

25 Mutu hatapata wokovu kwa kuwa tu amebatizwa. Ndiyo sababu, mutume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” (Wafilipi 2:12) Ubatizo ni hatua ya kwanza tu inayoongoza kwenye wokovu. Sasa ulizo ni hili: Unaweza kufanya nini ili ubaki katika upendo wa Mungu? Sura ya mwisho inayofuata itajibu ulizo hilo.

^ fu. 21 Kwa kawaida, ubatizo unafanywa kwenye mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ya kila mwaka.