Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA KENDA

Baki Katika Upendo wa Mungu

Baki Katika Upendo wa Mungu
  • Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunamupenda Mungu?

  • Ni nini inayoweza kutusaidia tubaki katika upendo wa Mungu?

  • Ni zawadi gani Yehova atawapatia wale wote wanaobaki katika upendo wake?

Utamufanya Yehova awe kimbilio lako katika nyakati hizi za misukosuko?

1, 2. Ni wapi tunaweza kupata kimbilio la kweli leo?

WAZIA kama siku fulani unapotembea njiani, bila kutazamia, upepo mukali wa mvua unavuma. Mawingu yanakuwa meusi kabisa. Unaona umeme wa radi na unasikia mingurumo, kisha mvua kubwa inaanza kunyesha. Unatafuta haraka mahali pa kukimbilia ili kujikinga. Mara moja, kule pembeni ya njia unaona nyumba fulani. Nyumba hiyo iko nguvu, haivuye na inakupendeza. Hakika, utafurahia mahali hapo pa usalama, sivyo?

2 Tunaishi katika wakati wenye misukosuko. Hali ya dunia inaendelea kuharibika. Hata hivyo, tuna mahali pa usalama tunapoweza kukimbilia. Ni wapi hapo? Biblia inasema: ‘Nitamuambia Yehova: Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye ninamutegemea.’​—Zaburi 91:2.

3. Namna gani tunaweza kumufanya Yehova awe kimbilio letu?

3 Wazia jambo hili! Yehova, Muumbaji na Mutawala wa ulimwengu muzima, anaweza kuwa kimbilio letu. Anaweza kutulinda kwa sababu yeye ana nguvu nyingi kuliko mutu yeyote ao kitu chochote kinachoweza kuhatarisha maisha yetu. Hata tukipatwa na jambo lolote mbaya, Yehova anaweza kutengeneza hali yote mbaya iliyotupata. Namna gani tunaweza kumufanya Yehova kuwa kimbilio letu? Tunapaswa kumutumainia. Tena, Neno lake linatuomba ‘[Kubaki] katika upendo wa Mungu.’ (Yuda 21) Ndiyo, tunapaswa kubaki katika upendo wa Mungu, kushikamana na Baba yetu wa mbinguni na kumupenda wakati wote. Tukifanya hivyo, yeye atakuwa kabisa kimbilio letu. Lakini namna gani tunaweza kushikamana naye hivyo?

TAMBUA UPENDO WA MUNGU NA ONYESHA SHUKRANI

4, 5. Taja mambo fulani ambayo Yehova amefanya ili kutuonyesha upendo wake?

4 Ili kubaki katika upendo wa Mungu, ni lazima kuelewa kwanza yale Yehova amefanya ili kutuonyesha upendo wake. Kumbuka mafundisho fulani ya Biblia ambayo umejifunza katika kitabu hiki. Yehova, Muumbaji, ametupatia dunia iwe makao yetu yenye kupendeza. Ameijaza chakula na maji, utajiri mbalimbali, wanyama wenye kufurahisha macho, na maeneo yenye kuvutia. Kwa sababu ni yeye aliyeiandikisha Biblia, Mungu ametujulisha jina lake na sifa zake. Zaidi ya hayo, Neno lake linatuonyesha kama alimutuma Mwana wake mupendwa duniani na kumuacha ateseke na kufa kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Sababu gani zawadi hiyo ni ya lazima kwetu? Kwa sababu inatutolea tumaini la kuwa na maisha mazuri wakati ujao.

5 Tumaini letu la wakati ujao linategemea pia jambo fulani ambalo Mungu amefanya. Yehova amesimamisha serikali huko mbinguni, Ufalme wa Kimasiya. Karibuni serikali hiyo itamaliza mateso yote na kuifanya dunia kuwa paradiso. Wazia namna maisha yatakavyokuwa! Kuishi humo katika amani na furaha milele. (Zaburi 37:29) Kwa kungojea, Mungu ametupatia mashauri yanayotusaidia kuishi maisha bora zaidi kuanzia sasa. Tena ametupatia zawadi ya sala; tunaweza kuzungumuza naye wakati wowote. Hayo ni mambo fulani machache tu ambayo Yehova amefanyia watu wote na wewe kwa kipekee, ili kuonyesha upendo wake.

6. Namna gani unaweza kumushukuru Yehova kwa ajili ya upendo ambao amekuonyesha?

6 Ulizo la lazima sana ambalo unapaswa kujiuliza ni hili: Nitamushukuru Yehova namna gani kwa ajili ya upendo wake? Wengi watajibu, “Mimi pia ninapaswa kumupenda Yehova.” Wewe pia unawaza hivyo? Yesu alisema kama amri inayoshinda amri zote ni hii: ‘Lazima umupende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ (Mathayo 22:37) Hakika, una mambo mengi yanayopaswa kukusukuma umupende Yehova. Lakini, je, kusema tu kama una upendo huo kunatosha ili kuonyesha kama unamupenda Yehova kwa moyo, kwa nafsi, na kwa akili yako yote?

7. Kusema tu kama unamupenda Mungu kunatosha? Fasiria.

7 Kusema unamupenda Yehova hakutoshi; Biblia inaonyesha kama kusema hivyo ni mwanzo tu wa upendo wa kweli unaopaswa kuwa kati yako na Mungu. Ni kweli, mbegu ndio inayozaa muti wa matunda. Lakini, ikiwa unataka kula tunda fulani, je, utatosheka mutu akikupatia tu mbegu ya tunda hilo? Hapana! Vilevile, kusema tu kama unamupenda Mungu hakutoshi. Biblia inafundisha hivi: ‘Kumupenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si muzigo muzito.’ (1 Yohana 5:3) Ili tumupende Mungu kwelikweli, lazima tuzae matunda mazuri. Ni lazima tuonyeshe kwa matendo kama tunamupenda.​—Mathayo 7:16-20.

8, 9. Namna gani tunaweza kuonyesha upendo wetu na shukrani yetu kwa Mungu?

8 Tunapotii amri za Mungu na kufuata kanuni zake ndipo tunaonyesha kama tunamupenda Mungu. Si vigumu kufanya hivyo. Sheria za Yehova si nzito, yeye ametupatia sheria hizo ili zitusaidie kuishi maisha mazuri, yenye furaha, na yenye kutosheleza. (Isaya 48:17, 18) Tunapofuata mashauri ya Yehova katika maisha yetu, tunamuonyesha Baba yetu wa mbinguni kama tunashukuru kabisa juu ya yote ambayo ametufanyia. Inahuzunisha sana kuona kuwa ni watu wachache tu duniani ndio wenye kufanya hivyo. Hatutaki kukosa shukrani kama watu fulani wa wakati wa Yesu. Yesu aliwaponya watu kumi wenye ukoma, lakini ni mumoja tu aliyerudi kumushukuru. (Luka 17:12-17) Hakika, ni vizuri tuwe kama yule mutu mumoja, wala si kama wale kenda ambao hawakuwa na shukrani!

9 Basi, ni amri gani za Yehova tunazopaswa kutii? Tumejifunza amri fulani katika kitabu hiki, lakini acha turudilie amri chache kati ya amri hizo. Kutii amri za Mungu kutatusaidia tubaki katika upendo wake.

UMUKARIBIE YEHOVA SIKUZOTE

10. Fasiria sababu gani ni lazima kuendelea kujifunza juu ya Yehova Mungu.

10 Kujifunza mambo yanayomuhusu Yehova ni hatua ya lazima ili kumukaribia. Unapaswa kuendelea kufanya hivyo sikuzote. Kwa mufano, unaota moto wakati wa usiku wenye baridi, je, ungeuacha moto huo uendelee kupunguka polepole mupaka kuzimika? Hapana. Utaendelea kuongeza kuni ili kuuchochea zaidi. Usipofanya hivyo labda unaweza kufa na baridi! Kama vile kuni zinachochea moto, ndivyo ‘kumujua Mungu’ kunavyochochea upendo wetu kwa Yehova na kuufanya kuwa nguvu.​—Methali 2:1-5.

Moto unahitaji kuni ili uendelee kuwaka, upendo wako kwa Yehova unahitaji pia kuchochewa

11. Mafundisho ya Yesu yaliwafanya wanafunzi wake wajisikie namna gani?

11 Yesu alitaka wanafunzi wake waendelee kumupenda Yehova sana na Neno Lake. Ndiyo sababu, kisha kufufuliwa kwake, alielezea wanafunzi wake wawili namna alivyotimiza unabii fulani ulio katika Maandiko ya Kiebrania. Walijisikia namna gani? Mwishowe walisema: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?”​—Luka 24:32.

12, 13. (a) Leo, upendo wa watu wengi kwa Yehova na Biblia uko namna gani? (b) Tunaweza kufanya nini ili upendo wetu usipoe?

12 Ulipojifunza kwa mara ya kwanza mambo ambayo Biblia inafundisha kabisa, je, haukusikia furaha sana katika moyo wako, ukaanza kuwa na bidii, na upendo mwingi kwa Yehova? Ndiyo. Wengi walijisikia hivyo. Kazi kubwa sasa ni ya kuendelea kuchunga upendo huo; kuuchochea ili usipoe. Hatutaki kuuiga ulimwengu. Yesu alitabiri hivi: “Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Unaweza kufanya nini ili upendo wako kwa Yehova na upendo wako juu ya kweli ya Biblia usipoe?

13 Endelea kujifunza juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Tafakari ao waza sana juu ya mambo unayojifunza katika Neno la Mungu, na ujiulize: ‘Mambo haya ninayojifunza yananifundisha nini juu ya Yehova Mungu? Namna gani mambo hayo yananisaidia tena kumupenda Yehova kwa moyo wangu wote, kwa akili yangu yote, na kwa nafsi yangu yote?’ (1 Timotheo 4:15) Ukizoea kutafakari hivyo, utamupenda Yehova zaidi.

14. Namna gani sala inaweza kutusaidia ili upendo wetu kwa Yehova usipoe?

14 Jambo lingine la kufanya ili upendo wako kwa Yehova usipoe ni kusali kwa ukawaida. (1 Wathesalonike 5:17) Katika Sura ya 17, tulijifunza kama sala ni zawadi ya bei sana kutoka kwa Mungu. Urafiki kati ya watu wawili unakuwa muzuri na wenye nguvu ikiwa wana zoezi ya kuzungumuza na bila kufichana siri, vivyo hivyo urafiki wetu na Yehova utakuwa muzuri na wenye nguvu ikiwa tuna zoezi ya kusali. Hatupaswi kusali kidesturi tu, kurudilia-rudilia maneno yaleyale yasiyotoka moyoni na yasiyo na maana. Tunapaswa kuzungumuza na Yehova kama vile mutoto anavyozungumuza na baba yake anayemupenda. Hata hivyo, tutazungumuza naye kwa heshima, waziwazi, bila unafiki, na tutamuambia yale yanayotoka moyoni. (Zaburi 62:8) Kwa kweli, funzo la pekee la Biblia na sala inayotoka moyoni ni mambo ya lazima sana ya ibada yetu, na yanatusaidia kuendelea kubaki katika upendo wa Mungu.

UMUABUDU MUNGU KWA FURAHA

15, 16. Sababu gani tunapaswa kuona kazi ya kuhubiri Ufalme kuwa pendeleo na hazina?

15 Funzo la pekee la Biblia na sala ni matendo ya ibada yanayoweza kufanywa bila mutu mwingine kujua. Sasa acha tuchunguze sehemu nyingine ya ibada yetu inayoonekana na watu wengine, yaani, kuzungumuzia wengine mambo tunayoamini. Je, umewahi kuzungumuzia wengine mafundisho ya kweli ya Biblia? Ikiwa umefanya hivyo, basi umekuwa na pendeleo nzuri sana. (Luka 1:74) Tunapozungumuzia wengine mafundisho ya kweli ya Biblia ambayo tumejifunza juu ya Yehova Mungu, tunatimiza kazi ya lazima sana ambayo Wakristo wa kweli walipewa, yaani, kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.​—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

16 Mutume Paulo aliona kazi yake ya kuhubiri kuwa kitu fulani cha bei sana, aliita kuwa hazina. (2 Wakorintho 4:7) Kazi nzuri inayoshinda kazi zote ni ile ya kuzungumuzia watu juu ya Yehova Mungu na makusudi yake. Bwana wa kazi hiyo ni bwana muzuri kuliko mabwana wengine na kazi tunayofanya inaleta faida nyingi sana. Kupitia kazi hiyo, unawasaidia watu wenye mioyo mizuri wamukaribie Baba yetu wa mbinguni na waanze kutembea katika njia inayoongoza kwenye uzima wa milele! Kazi hiyo inaweza kumupatia mutu furaha kuliko kazi zingine zote, sivyo? Zaidi ya hiyo, kutoa ushahidi juu ya Yehova na Neno lake kunaongeza imani yako na kunafanya umupende Yehova zaidi. Na Yehova anafurahia sana bidii yako. (Waebrania 6:10) Kuendelea kufanya kazi hiyo kwa bidii kutakusaidia ubaki katika upendo wa Mungu.​—1 Wakorintho 15:58.

17. Sababu gani kazi ya kuhubiri ni ya haraka leo?

17 Tusisahau kama kazi ya kuhubiri Ufalme ni ya haraka sana. Biblia inasema hivi: “Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii.” (2 Timotheo 4:2) Sababu gani ni kazi ya haraka leo? Neno la Mungu linatuambia: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) Ndiyo, wakati ambao Yehova ataharibu ulimwengu huu muovu unakaribia sana. Watu wanapaswa kuonywa! Wanapaswa kujua kama huu ndio wakati wa kumuchagua Yehova kuwa Mutawala wao. Mwisho ‘hautachelewa.’​—Habakuki 2:3.

18. Sababu gani tunapaswa kumuabudu Yehova pamoja na Wakristo wa kweli?

18 Yehova anataka tumuabudu pamoja na Wakristo wa kweli. Ndiyo sababu Neno lake linasema: ‘Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri munavyoona siku ile kuwa inakaribia.’ (Waebrania 10:24, 25) Tunapokusanyika pamoja na ndugu wengine katika mikutano, tuna nafasi nzuri kabisa ya kumusifu na kumuabudu Mungu wetu wa upendo. Tena tunajengana na kutiana moyo.

19. Tunaweza kufanya nini ili upendo uongezeke katika kutaniko la Kikristo?

19 Tunapokusanyika pamoja na waabudu wa Yehova, upendo katika kutaniko unaongezeka, na urafiki unakuwa muzuri sana. Ni vizuri kuangalia sifa nzuri za wengine, kama vile Yehova anavyofanya. Usitazamie ndugu ao dada wawe wakamilifu. Usisahau kama maendeleo yao ya kiroho yanatofautiana na pia kila mumoja wetu anafanya makosa. (Wakolosai 3:13) Ujikaze kufanya urafiki na wale wanaomupenda Yehova sana, nawe utafanya maendeleo ya kiroho. Ndiyo, kumuabudu Yehova pamoja na wengine kutakusaidia ubaki katika upendo wa Mungu. Ni zawadi gani ambayo Yehova atawapa wale wanaomuabudu kwa uaminifu na kubaki katika upendo wake?

FANYA NGUVU ILI UPATE ULE “UZIMA ULIO WA KWELI”

20, 21. “Uzima ulio wa kweli” ni uzima gani, na sababu gani tumaini hilo ni nzuri kabisa?

20 Zawadi ambayo Yehova atawapa watumishi wake waaminifu ni uzima. Lakini uzima huo ni uzima wa namna gani? Unawazia uzima tulio nao leo ni uzima wa kweli? Wengi watajibu “Ndiyo.” Kwa kuwa tunapumua, tunakula, na tunakunywa, hilo linaonyesha kama tuna uzima. Na wakati tunapofurahi, tunaweza hata kusema eti, “Haya ndio maisha kabisa!” Lakini, Biblia inaonyesha kama, katika maana kamili ya uzima, hakuna mwanadamu ambaye ana uzima wa kweli leo.

Yehova anapenda upate ule “uzima ulio wa kweli.” Je, Utaupata?

21 Neno la Mungu linatushauri ‘tuushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Timotheo 6:19) Maneno hayo yanaonyesha kama tuna tumaini la kupata ule “uzima ulio wa kweli” wakati ujao. Ndiyo, tutakapokuwa wakamilifu, ndipo tutasema kama tuna uzima wa kweli, kwa maana wakati huo tutaishi kama vile Mungu alivyokusudia. Tutakapoishi katika paradiso duniani tutakuwa na afya nzuri kabisa, amani, na furaha. Wakati huo ndipo tutafurahia ule “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele. (1 Timotheo 6:12) Hilo ni tumaini nzuri kabisa, sivyo?

22. Namna gani unaweza ‘kushika imara ule uzima ulio wa kweli’?

22 Namna gani tunaweza ‘kushika imara ule uzima ulio wa kweli’? Paulo alipozungumuzia jambo hilo, aliwashauri Wakristo “wafanye mema” na “wawe matajiri katika matendo mazuri.” (1 Timotheo 6:18) Basi, tutafanya hivyo ikiwa tunatumia katika maisha yetu mambo tunayojifunza katika Biblia. Lakini, je, Paulo alitaka kusema kama “uzima ulio wa kweli” ni mushahara wa matendo mema tunayofanya? Hapana, kwa kuwa tuna tumaini hilo nzuri kwa sababu ya ‘fazili zisizostahiliwa’za Mungu. (Waroma 5:15) Hata hivyo, Yehova anapenda kuwapa zawadi wale wanaomutumikia kwa uaminifu. Anapenda upate ule “uzima ulio wa kweli.” Wale wanaobaki katika upendo wa Mungu ndio watakaopata uzima huo wa milele, uzima wa furaha na amani.

23. Sababu gani kubaki katika upendo wa Mungu ni jambo la lazima sana?

23 Kwa hiyo, kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, ninamuabudu Mungu kama vile Biblia inavyofundisha?’ Ikiwa tunamuabu Mungu hivyo kila siku, basi tunafuata njia inayofaa. Tunaweza kuwa hakika kama Yehova ni kimbilio letu. Atawalinda watu wake waaminifu katika siku hizi za mwisho zenye taabu za ulimwengu huu muovu. Pia, Yehova atatuokoa na kutuingiza katika dunia mupya yenye utukufu inayokaribia. Itakuwa furaha sana kuishi wakati huo! Tena tutakuwa na furaha sana kwa sababu tulichukua uamuzi muzuri katika siku hizi za mwisho! Ukichukua uamuzi huo sasa, utapata kwa umilele ule “uzima ulio wa kweli,” ambao Yehova Mungu alikusudia tangu mwanzo!