Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Jina la Mungu—Maana na Matumizi

Jina la Mungu—Maana na Matumizi

ANDIKO la Zaburi 83:18 limetafsiriwaje katika Biblia yako? Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya husema hivi: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Biblia nyingine hutumia maneno yanayofanana na hayo. Hata hivyo, tafsiri nyingi hazitumii jina Yehova, badala yake zinatumia majina ya heshima kama vile “Bwana” au “Mwenyezi.” Ni jina gani linalopaswa kutumiwa katika mstari huo? Jina la heshima au jina halisi Yehova?

Jina la Mungu katika herufi za Kiebrania

Mstari huo unazungumzia jina halisi. Katika Kiebrania cha awali ambacho kilitumiwa kuandika sehemu kubwa ya Biblia, jina halisi la pekee linatumiwa katika mstari huo. Linaandikwa hivi katika herufi za Kiebrania יהוה )YHWH(. Katika Kiswahili, mara nyingi jina hilo hutafsiriwa “Yehova.” Je, jina hilo hupatikana katika mstari mmoja tu wa Biblia? Hapana. Linapatikana katika maandishi ya awali ya Maandiko ya Kiebrania karibu mara 7,000!

Jina la Mungu ni muhimu kadiri gani? Fikiria ile sala ya mfano ambayo Yesu Kristo aliwafundisha wanafunzi wake. Inaanza kwa kusema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Baadaye, Yesu alisali hivi kwa Mungu: “Baba, litukuze jina lako.” Mungu akajibu kutoka mbinguni, akisema “Nimelitukuza na pia nitalitukuza tena.” (Yohana 12:28) Ni wazi kwamba jina la Mungu ni muhimu sana. Kwa nini basi watafsiri fulani wameliondoa jina hilo katika Biblia wanapotafsiri na kutumia majina ya heshima badala yake?

Inaonekana kuna sababu mbili kuu. Kwanza, wengi wao hudai kwamba jina hilo halipaswi kutumiwa kwa sababu hakuna yeyote leo anayejua jinsi lilivyokuwa likitamkwa zamani. Kiebrania cha awali hakikuandikwa kwa kutumia irabu—kama vile a, e, i, o, u. Kwa hiyo, hakuna yeyote leo anayeweza kusema kwa uhakika jinsi watu wa nyakati za Biblia walivyotamka jina YHWH. Hata hivyo, je, hilo lituzuie tusitumie jina la Mungu? Katika nyakati za Biblia, huenda jina Yesu lilikuwa likitamkwa Yeshua au hata Yehoshua—hakuna yeyote anayejua kwa hakika. Hata hivyo, leo watu ulimwenguni pote wanatumia namna mbalimbali za jina Yesu, wakilitamka jinsi linavyotamkwa kwa ukawaida katika lugha yao. Hawasiti kulitumia jina hilo eti kwa sababu hawajui jinsi lilivyokuwa likitamkwa katika karne ya kwanza. Pia, ikiwa ungesafiri kwenda nchi nyingine, huenda ukaona kwamba jina lako mwenyewe linatamkwa kwa njia tofauti kabisa katika lugha nyingine. Kwa hiyo, kutojua jinsi jina la Mungu lilivyokuwa likitamkwa zamani si sababu ya kutolitumia.

Sababu ya pili ambayo hutolewa mara nyingi inayowafanya watafsiri fulani waliondoe jina la Mungu katika Biblia inahusisha mapokeo ya kale ya Wayahudi. Wengi wao huamini kwamba jina la Mungu halipaswi kutajwa. Inaonekana imani hiyo inatokana na kutoelewa vizuri sheria ya Biblia inayosema: “Usilitumie jina la Yehova Mungu wako kwa njia isiyofaa, kwa maana Yehova hatamwacha bila kuadhibiwa yule anayelitumia jina lake kwa njia isiyofaa.”—Kutoka 20:7.

Sheria hiyo inakataza kulitumia jina la Mungu kwa njia isiyofaa. Lakini je, inakataza kulitumia jina lake kwa heshima? Hapana. Waandikaji wote wa Maandiko ya Kiebrania (“Agano la Kale”) walikuwa wanaume waaminifu waliotii Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale. Hata hivyo, walilitumia jina la Mungu kwa ukawaida. Kwa mfano, walilitia katika zaburi nyingi zilizoimbwa na umati wa waabudu kwa sauti. Yehova Mungu hata aliwaagiza waabudu wake waliitie jina lake, na wale waliokuwa waaminifu walifanya hivyo. (Yoeli 2:32; Matendo 2:21) Kwa hiyo, Wakristo leo hawasiti kulitumia jina la Mungu kwa heshima, kama Yesu alivyofanya.—Yohana 17:26.

Wanapoliondoa jina la Mungu na kutumia majina ya heshima badala yake, watafsiri wa Biblia hufanya kosa kubwa. Wanamfanya Mungu asijulikane, na hali Biblia inawahimiza wanadamu wasitawishe “urafiki wa karibu pamoja na Yehova.” (Zaburi 25:14) Ikiwa ungekuwa na rafiki ambaye hujui jina lake, uhusiano wenu ungekuwa wa karibu kadiri gani? Vivyo hivyo, watu wasipojulishwa jina la Mungu, Yehova, wanawezaje kumkaribia? Isitoshe, watu wasipolitumia jina la Mungu, hawawezi kuelewa maana muhimu ya jina hilo. Jina la Mungu linamaanisha nini?

Mungu mwenyewe alimweleza mtumishi wake mwaminifu Musa maana ya jina lake. Musa alipomwuliza Mungu jina lake, Yehova alimjibu: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Tafsiri ya Rotherham inatafsiri hivi maneno hayo: “Nitakuwa chochote Nipendacho kuwa.” Kwa hiyo, Yehova anaweza kuwa chochote kinachohitajika ili kutimiza makusudi yake.

Hebu wazia kwamba ungeweza kuwa chochote ambacho ungependa kuwa. Ungewafanyia nini rafiki zako? Ikiwa mmoja wao angekuwa mgonjwa sana, ungeweza kuwa daktari stadi na kumtibu. Ikiwa mwingine angefilisika, ungeweza kuwa tajiri na kumsaidia. Hata hivyo, ukweli ni kwamba wewe huna uwezo wa kuwa chochote ambacho ungependa kuwa. Hakuna yeyote kati yetu aliye na uwezo huo. Unapoendelea kujifunza Biblia, utafurahi kuona jinsi Yehova huwa chochote kinachohitajika ili kutimiza makusudi yake. Naye anapenda kutumia nguvu zake kwa niaba ya wale wanaompenda. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Wale wasiojua jina la Yehova hawawezi kuuona uwezo wake wa kuwa chochote anachopenda kuwa.

Ni wazi kwamba, jina Yehova linapaswa kuwa katika Biblia. Kujua maana yake na kulitumia kwa uhuru katika ibada yetu kunaweza kutusaidia sana kumkaribia Baba yetu wa mbinguni Yehova. *

^ fu. 3 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu jina la Mungu, maana yake, na sababu za kulitumia katika ibada kwenye broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.