Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Jina la Mungu​—Je, Inafaa Tulitumie? Maana ya Jina Hilo Ni Nini

Jina la Mungu​—Je, Inafaa Tulitumie? Maana ya Jina Hilo Ni Nini

NYONGEZA

Jina la Mungu​—Je, Inafaa Tulitumie? Maana ya Jina Hilo Ni Nini?

KATIKA Biblia yako, andiko la Zaburi 83:18 (83:19 katika tafsiri fulani) linatafsiriwa namna gani? Katika Biblia Takatifu​Tafsiri ya Ulimwengu Mpya andiko hilo linatafsiriwa hivi: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Katika Biblia zingine andiko hilo limetafsiriwa hivyo pia. Lakini katika Biblia nyingi jina Yehova limeondolewa, na nafasi hiyo utakuta majina ya cheo ao ya heshima kama vile “Bwana” ao “Mwenyezi.” Ni jina gani lilipaswa kutumiwa katika andiko hilo? Jina la cheo ao jina Yehova?

Andiko hilo linazungumuzia jina la pekee. Katika Kiebrania cha mwanzo-mwanzo ambacho kilitumiwa kuandika sehemu kubwa ya Biblia, ni jina la pekee ndilo linapatikana katika andiko hilo. Katika herufi za Kiebrania linaandikwa hivi יהוה (YHWH). Katika Kiswahili, mara nyingi jina hilo linatafsiriwa “Yehova.” Je, jina hilo linapatikana katika andiko moja tu la Biblia? Hapana. Katika Maandiko ya mwanzo-mwanzo ya Kiebrania, jina hilo linapatikana karibu mara 7 000!

Je, jina la Mungu ni la lazima? Wazia ile sala ya mufano ambayo Yesu Kristo alifundisha. Inaanza hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kisha, Yesu alisali kwa Mungu hivi: “Baba, litukuze jina lako.” Mungu alijibu hivi kutoka mbinguni: “Nimelitukuza na pia nitalitukuza tena.” (Yohana 12:28) Hilo linaonyesha wazi kama jina la Mungu ni la lazima sana. Kwa nini basi watafsiri wengine wameliondoa jina hilo katika Biblia walizotafsiri na kutumia majina ya cheo ao ya heshima?

Inaonekana kuna sababu mbili kubwa zilizowasukuma kufanya hivyo. Ya kwanza, wengi wao wanasema kama jina hilo halipaswi kutumiwa kwa sababu hakuna mutu leo anayejua vizuri namna walivyokuwa wakilitamuka hapo zamani. Kiebrania zamani kiliandikwa bila herufi za sauti kama hizi: a, e, i, o, u. Kwa hiyo, hakuna mutu leo anayeweza kujua kwa uhakika namna watu zamani walivyotamuka jina YHWH. Lakini tujiulize, hiyo ndio sababu inayopaswa kutuzuia kutumia jina la Mungu? Tuchukue mufano, wakati wa zamani, jina Yesu lingepaswa kutamukwa Yeshua ao hata Yehoshua​—hakuna mutu leo anayejua kwa uhakika namna watu walivyokuwa wakilitamuka. Hata hivyo, leo watu duniani pote wanatumia namna mbalimbali za jina Yesu, kila mutu analitamuka namna linavyotamukwa kwa ukawaida katika luga yake. Hawasiti kulitumia jina hilo hata ikiwa hawajui namna lilivyokuwa likitamukwa wakati huo wa zamani. Ni hivyo pia leo, ukisafiri na kwenda inchi nyingine, labda utasikia watu wakitamuka jina lako tofauti katika luga yao. Kwa hiyo, hata ikiwa hatujuwi vizuri namna watu walivyokuwa wakitamuka jina la Mungu wakati wa zamani, hiyo si sababu ya kuacha kulitumia.

Sababu ya pili ambayo mara nyingi wanatoa iliyowasukuma kuondoa jina la Mungu katika Biblia inatokana na mawazo yasiyo ya kweli ambayo Wayahudi wengi waliamini; wao waliamini kama jina la Mungu halipaswi kamwe kutajwa. Inaonekana kama wazo hilo linatokana na matumizi mabaya ya sheria ya Biblia inayosema: ‘Usilitumie jina la Yehova Mungu wako kwa njia isiyofaa, kwa maana Yehova hatamuacha bila kuazibiwa yule anayelitumia jina lake kwa njia isiyofaa.’​—Kutoka 20:7.

Je, sheria hiyo inakataza kulitumia jina la Mungu kwa njia inayofaa ao kwa heshima? Hapana. Waandikaji wote wa Maandiko ya Kiebrania (“Agano la Kale”) walikuwa wanaume waaminifu waliotii Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale. Wao walizoea kulitumia jina la Mungu. Kwa mufano, walilitia katika zaburi nyingi zilizotumiwa na watu wengi waliokuwa wakiimba wakati wa ibada. Kwanza, Yehova Mungu mwenyewe aliwaomba waabudu wake waliitie jina lake, na wale waliokuwa waaminifu walifanya hivyo. (Yoeli 2:32; Matendo 2:21) Kwa hiyo, Wakristo leo hawasiti kulitumia jina la Mungu kwa njia inayofaa, kama vile Yesu alivyofanya.​—Yohana 17:26.

Watafsiri hao wa Biblia wanapotumia majina ya cheo mahali pa jina la Mungu wanafanya kosa kubwa sana. Wanafanya watu wawaze kama Mungu si mutu kabisa na kama hawawezi kumukaribia. Lakini Biblia inawatia watu moyo kuwa na “urafiki wa karibu pamoja na Yehova.” (Zaburi 25:14) Wazia kidogo jambo hili, ikiwa ungekuwa na rafiki ambaye haumujui jina, je, tunaweza kusema kweli kama huyo ni rafiki yako? Vilevile, watu wanapofichwa jina la Mungu, Yehova, namna gani wanaweza kumukaribia? Tena, ikiwa watu hawalitumii jina la Mungu, hawatajua pia maana ya ajabu ya jina hilo. Basi, jina hilo la Mungu linamaanisha nini?

Mungu mwenyewe alifasiria mutumishi wake mwaminifu Musa maana ya jina lake. Musa alipomuuliza Mungu jina lake, Yehova alimuambia hivi: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Biblia ya Rotherham inatafsiri maneno hayo hivi: “Nitakuwa chochote nipendacho kuwa.” Kwa hiyo, Yehova anaweza kuwa namna yote anayopenda kuwa ili kutimiza mapenzi yake.

Wazia kama una uwezo wa kuwa namna yote unayopenda kuwa. Ungewafanyia marafiki wako mambo mengi, sivyo? Tuseme mumoja wao anakuwa mugonjwa sana, kwa kuwa una uwezo wa kuwa munganga, ungekuwa hivyo ili kumuponyesha. Ikiwa mwingine anakosewa na feza, kwa kuwa una uwezo wa kuwa tajiri, ungekuwa hivyo ili kumusaidia. Lakini, ukweli ni kama wewe hauna uwezo wa kuwa namna yote unayopenda kuwa. Sisi wote hatuna uwezo huo. Ukiendelea kujifunza Biblia utashangaa kuona namna Yehova anavyokuwa namna yote anayopenda kuwa ili kutimiza ahadi zake. Naye anapenda kutumia nguvu zake kwa faida ya wale wanaomupenda. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Wale wasiojua jina la Yehova hawawezi kuona sifa hizo nzuri za utu wa Yehova, yaani, uwezo wake wa kuwa namna yote anayopenda kuwa.

Kwa hiyo, ni wazi kama jina Yehova linapaswa kuwa katika Biblia. Kujua maana yake na kulitumia bila woga katika ibada yetu kunaweza kutusaidia sana kumukaribia Yehova, Baba yetu wa mbinguni. *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Ili kupata maelezo zaidi juu ya jina la Mungu, maana ya jina hilo, na kwa nini linapaswa kutumiwa katika ibada, soma broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.