Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa Masihi

Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa Masihi

NABII Danieli aliishi zaidi ya miaka 500 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu. Hata hivyo, Yehova alimpa Danieli ujumbe ambao ungefanya iwezekane kujua wakati hususa ambapo Yesu angetiwa mafuta au kuwekwa rasmi kuwa Masihi au Kristo. Danieli aliambiwa hivi: “Ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.”—Danieli 9:25.

Ili kujua wakati ambapo Masihi angetokea, kwanza tunahitaji kujua mwanzo wa kile kipindi ambacho Masihi angetokea mwishoni mwake. Kulingana na unabii huo, kingeanza wakati ambapo ‘lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu lingetolewa.’ Neno hilo lilitolewa wakati gani? Kulingana na Nehemia, mwandishi wa Biblia, neno la kujenga upya kuta za Yerusalemu lilitolewa “katika mwaka wa 20 wa Mfalme Artashasta.” (Nehemia 2:1, 5-8) Wanahistoria wanathibitisha kwamba mwaka wa 474 K.W.K., ndio uliokuwa mwaka wa kwanza wa utawala wa Artashasta. Kwa hiyo, mwaka wa 20 wa utawala wake ni mwaka wa 455 K.W.K. Kwa hiyo, kile kipindi cha unabii wa Danieli kuhusu Masihi kingeanza mwaka wa 455 K.W.K.

Pili, Danieli anaonyesha urefu wa kipindi hicho ambacho “Masihi aliye Kiongozi” angetokea. Unabii huo unataja “majuma 7, pia majuma 62”—jumla ya majuma 69. Kipindi hicho kina urefu gani? Tafsiri kadhaa za Biblia zinaonyesha kwamba hayo si majuma ya siku saba, bali ya miaka. Yaani, kila juma linawakilisha miaka saba. Wayahudi wa kale walizoea kuhesabu majuma ya miaka, au vipindi vya miaka saba. Kwa mfano, kila mwaka wa saba ulikuwa mwaka wa Sabato. (Kutoka 23:10, 11) Kwa hiyo, yale majuma 69 ya unabii yalikuwa vipindi 69 vya miaka 7 kila kimoja, au jumla ya miaka 483.

Sasa tunachohitaji ni kupiga hesabu tu. Tukihesabu miaka 483 kuanzia mwaka wa 455 K.W.K., tutafika mwaka wa 29 W.K. Huo ndio mwaka hususa ambao Yesu alibatizwa na kuwa Masihi! * (Luka 3:1, 2, 21, 22) Je, huo si utimizo wenye kustaajabisha wa unabii wa Biblia?

^ fu. 2 Kuanzia mwaka wa 455 K.W.K. hadi mwaka wa 1 K.W.K. ni miaka 454. Kuanzia mwaka wa 1 K.W.K. hadi 1 W.K. ni mwaka mmoja (hakukuwa na mwaka sufuri). Na kuanzia mwaka wa 1 W.K. hadi mwaka wa 29 W.K. ni miaka 28. Tukijumlisha miaka hiyo tunapata jumla ya miaka 483. Yesu “alikatiliwa mbali” alipouawa mwaka wa 33 W.K., katika juma la 70 la miaka. (Danieli 9:24, 26) Unaweza kupata habari zaidi kuhusu unabii huo katika kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! sura ya 11, na Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 899-901 au Étude Perspicase, Buku la 2, ukurasa wa 995-997. Vitabu hivyo vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.