Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna Nabii Danieli Alivyotabiri Kutokea Kwa Masiya

Namna Nabii Danieli Alivyotabiri Kutokea Kwa Masiya

NYONGEZA

Namna Nabii Danieli Alivyotabiri Kutokea kwa Masiya

NABII Danieli aliishi zaidi ya miaka 500 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu ao kabla ya wakati wetu (K.W.W.) Yehova alimufunulia habari iliyosaidia kujua wakati kamili ambapo Yesu angetiwa mafuta kwa roho takatifu, ao kufanywa kuwa Masiya ao Kristo. Danieli aliambiwa hivi: ‘Ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mupaka Masiya aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.’​—Danieli 9:25.

Ili kujua wakati Masiya angetokea, tunapaswa kwanza kujua ni wakati gani kipindi hicho kilichotabiriwa kilianza. Kulingana na unabii huo, kipindi hicho kingeanza wakati ambapo “lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu” lingetolewa. Ni wakati gani “lile neno” lilitolewa? Nehemia, mumoja kati ya waandikaji wa Biblia, alisema kama lile neno la kujenga upya kuta za Yerusalemu lilitolewa ‘katika mwaka wa 20 wa Mufalme Artashasta.’ (Nehemia 2:1, 5-8) Wanahistoria wanahakikisha kama mwaka wa 474 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, ndio ulikuwa mwaka wa kwanza wa utawala wa Artashasta (Artaxerxes). Kwa hiyo, mwaka wa 20 wa utawala wake ni mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Sasa tunajua kama mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu ndio mwanzo wa kipindi hicho kilichotabiriwa katika unabii wa Danieli unaozungumuzia kutokea kwa Masiya.

Jambo lingine ni hili: Nabii Danieli anaonyesha ni miaka ngapi ingepita ili ‘Masiya aliye Kiongozi’ atokee. Unabii huo unazungumuzia “majuma 7, pia majuma 62,” yaani, jumla ya majuma 69. Kipindi hicho kina urefu gani? Biblia nyingi zinaonyesha kama majuma hayo si majuma ya kawaida ya siku saba, lakini majuma ya miaka. Kila juma linaonyesha miaka saba. Wayahudi wa zamani walijua vizuri wazo la kuhesabu majuma ya miaka, ao vipindi vya miaka saba kila kimoja. Kwa mufano, kila mwaka wa saba ulikuwa mwaka wa Sabato. (Kutoka 23:10, 11) Kwa hiyo, yale majuma 69 ya unabii ni vipindi 69 vya miaka 7 kila kimoja, ao jumla ya miaka 483.

Sasa tunaweza kuhesabu miaka hiyo. Tukihesabu miaka 483 kuanzia mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, tutafikia mwaka wa 29 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Huo ndio mwaka ambao Yesu alibatizwa na kuwa Masiya! * (Luka 3:1, 2, 21, 22) Kwa sababu unabii huo wa Biblia ulitimia hivyo bila kukosea, hilo ni jambo la ajabu, sivyo?

[Maelezo ya chini]

^ fu. 2 Kuanzia mwaka wa 455 kabla ya wakati wetu mupaka mwaka wa 1 kabla ya wakati wetu tunapata miaka 454. Kuanzia mwaka wa 1 kabla ya wakati wetu mupaka mwaka wa 1 wakati wetu tunapata mwaka moja (hakuna mwaka zero). Na kuanzia mwaka huo wa 1 mupaka mwaka wa 29, ni miaka 28. Tukijumulisha 454+1+28 tunapata jumla ya miaka 483. Yesu “alikatiliwa mbali” alipouawa mwaka wa 33, katika juma la 70 la miaka. (Danieli 9:24, 26) Ili kupata habari zaidi soma kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! sura ya 11, na kitabu Étude perspicace des Écritures, buku la 2, ukurasa wa 995-997. Vitabu hivyo vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.