Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Ukweli Kuhusu Baba, Mwana, na Roho Takatifu

Ukweli Kuhusu Baba, Mwana, na Roho Takatifu

WATU wanaoamini Utatu husema kwamba kuna Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu. Wote wanasemekana kuwa sawa, wenye nguvu zote, na hawana mwanzo. Kwa hiyo, kulingana na fundisho la Utatu, Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Mtakatifu ni Mungu, hata hivyo, Mungu ni mmoja tu.

Wengi wanaoamini fundisho la Utatu hukubali kwamba hawawezi kulieleza. Lakini, huenda wakafikiri kwamba hilo ni fundisho la Biblia. Ni muhimu kutambua kwamba neno “Utatu” halipatikani kamwe katika Biblia. Lakini je, wazo lenyewe linapatikana katika Biblia? Ili kujibu swali hilo, hebu tuchunguze andiko ambalo wanaounga mkono fundisho hilo hutumia kutetea Utatu.

“NENO ALIKUWA MUNGU”

Andiko la Yohana 1:1 linasema: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu.” (Union Version) Baadaye, katika sura hiyohiyo, mtume Yohana anaonyesha waziwazi kwamba “Neno” ni Yesu. (Yohana 1:14) Hata hivyo, kwa kuwa Neno anaitwa Mungu, watu fulani hukata kauli kwamba Mwana na Baba ni Mungu yuleyule.

Kumbuka kwamba mwanzoni sehemu hiyo ya Biblia iliandikwa katika Kigiriki. Baadaye, mstari huo wa Kigiriki ulitafsiriwa katika lugha nyingine. Hata hivyo, watafsiri fulani wa Biblia hawakusema “Neno alikuwa Mungu.” Kwa nini? Kulingana na ufahamu wao wa lugha ya Kigiriki iliyotumiwa kuandika Biblia, watafsiri hao walikata kauli kwamba maneno “Neno alikuwa Mungu” yalipaswa kutafsiriwa tofauti. Jinsi gani? Kuna mifano michache hapa: “Logos [Neno] alikuwa na sifa za kimungu.” (A New Translation of the Bible) “Neno alikuwa mungu.” (The New Testament in an Improved Version) “Neno alikuwa pamoja na Mungu na alikuwa na utu kama wake.” (The Translator’s New Testament) Kulingana na tafsiri hizo, Neno si Mungu mwenyewe. * Badala yake, kwa sababu ya ukuu wake miongoni mwa viumbe wa Yehova, Neno anaitwa “mungu.” Hapa, jina “mungu” linamaanisha “mwenye nguvu.”

PATA HABARI ZAIDI

Watu wengi hawajui Kigiriki kilichotumiwa kuiandika Biblia. Basi unawezaje kujua alichomaanisha mtume Yohana? Fikiria mfano huu: Mwalimu anawafundisha wanafunzi jambo fulani. Baadaye, wanafunzi wanakuwa na maoni tofauti kuhusu jambo walilofundishwa. Wanafunzi hao wanaweza kutatuaje tofauti zao? Wanaweza kumwomba mwalimu awape habari zaidi. Bila shaka, kupata habari zaidi kutawasaidia kuelewa jambo hilo vizuri zaidi. Vivyo hivyo, ili kuelewa maana ya Yohana 1:1, unaweza kutafuta habari zaidi kuhusu cheo cha Yesu katika Injili ya Yohana. Kupata habari zaidi kutakusaidia kujua ukweli.

Kwa mfano, fikiria yale ambayo Yohana aliandika katika sura ya 1, mstari wa 18: “Hakuna mwanadamu amemwona Mungu [Mweza-Yote] wakati wowote.” Hata hivyo, wanadamu wamemwona Mwana, yaani, Yesu kwa kuwa Yohana alisema: “Neno [Yesu] alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake.” (Yohana 1:14, UV) Basi, Mwana angewezaje kuwa ndiye Mungu Mweza-Yote? Yohana anasema pia kwamba Neno alikuwa “pamoja na Mungu.” Basi, mtu anawezaje kuwa pamoja na mtu mwingine na wakati huohuo awe ndiye mtu huyo? Isitoshe, katika Yohana 17:3, Yesu anaonyesha waziwazi tofauti iliyopo kati yake na Baba yake wa mbinguni. Anamwita Baba yake “Mungu wa pekee wa kweli.” Kisha Yohana anasema hivi mwishoni-mwishoni mwa Injili yake: “Haya yameandikwa ili mpate kuamini kwamba Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu.” (Yohana 20:31) Ona kwamba Yesu anaitwa, Mwana wa Mungu, wala haitwi Mungu. Habari hiyo ya ziada iliyo katika Injili ya Yohana inatusaidia kuelewa andiko la Yohana 1:1. Yesu, yule Neno, ni “mungu” katika maana ya kwamba ana cheo cha juu lakini siye Mungu Mweza-Yote.

CHANGANUA UTHIBITISHO

Ufikirie tena ule mfano wa mwalimu na wanafunzi. Wazia kwamba baadhi ya wanafunzi wangali na shaka, hata baada ya kusikiliza maelezo ya ziada ya mwalimu wao. Wafanye nini? Wanaweza kumwomba mwalimu mwingine awape habari zaidi kuhusu suala hilo. Mwalimu huyo wa pili akiunga mkono maelezo ya yule wa kwanza, wanafunzi wengi wataridhika. Vivyo hivyo, ikiwa huna uhakika kuhusu alichomaanisha mwandishi wa Biblia Yohana alipoandika kuhusu uhusiano kati ya Yesu na Mungu Mweza-Yote, unaweza kupata habari zaidi kutoka kwa mwandishi mwingine wa Biblia. Kwa mfano, hebu fikiria aliyoandika Mathayo. Kuhusu mwisho wa ulimwengu huu, anamnukuu Yesu akisema: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Maneno hayo yanathibitishaje kwamba Yesu si Mungu Mweza-Yote?

Yesu anasema kwamba Baba anajua mambo mengi kuliko Mwana. Hata hivyo, ikiwa Yesu angekuwa ndiye Mungu Mweza-Yote, angejua mambo yote anayojua Baba yake. Kwa hiyo, basi, Mwana na Baba hawalingani. Hata hivyo, wengine wanadai: ‘Yesu ana nyutu mbili. Hapa anazungumza akiwa mwanadamu.’ Na hata kama hilo lingekuwa kweli, namna gani roho takatifu? Ikiwa hiyo pia ni Mungu yuleyule ambaye ndiye Baba, mbona Yesu hasemi kwamba roho hiyo inajua mambo anayojua Baba?

Unapoendelea kujifunza Biblia, utaona maandiko mengine mengi ya Biblia yanayohusiana na habari hii. Yanathibitisha ukweli kumhusu Baba, Mwana, na roho takatifu.—Zaburi 90:2; Matendo 7:55; Wakolosai 1:15.

^ fu. 3 Kwa habari zaidi kuhusu Yohana 1:1, ona makala “Je, Neno alikuwa ‘Mungu’ au ‘mungu’?” inayopatikana kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2008, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.