Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yale Unayopaswa Kujua Juu ya Baba, Mwana, na Roho Takatifu

Yale Unayopaswa Kujua Juu ya Baba, Mwana, na Roho Takatifu

NYONGEZA

Yale Unayopaswa Kujua juu ya Baba, Mwana, na Roho Takatifu

WATU wanaoamini fundisho la Utatu wanasema kama katika Mungu mumoja kuna nafsi tatu​—Baba, Mwana, na Roho Mutakatifu. Wanasema kama kati ya hao wote watatu hakuna mwenye kushinda mwingine, ni wenye nguvu zote, na wote hawana mwanzo. Kwa hiyo, fundisho la Utatu linasema kama Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Mutakatifu ni Mungu, hata hivyo, kuna Mungu mumoja tu.

Watu wengi wanaoamini Utatu wanasema kama fundisho hilo ni fumbo, yaani, haliwezi kufasiriwa. Hata hivyo, labda wanawaza kama hilo ni fundisho la Biblia. Ni vizuri ujue kama katika Biblia hakuna mahali utaona neno “Utatu.” Lakini, je, wazo lenyewe la utatu linapatikana katika Biblia? Ili kujibu ulizo hilo, acha tuchunguze andiko ambalo wale wanaotetea Utatu wanatumia mara nyingi.

“NENO ALIKUWA MUNGU”

Andiko la Yohana 1:1 linasema hivi: “Katika mwanzo alikuwa Neno, na Neno alikuwa pamoja na Mungu, na Neno alikuwa Mungu.” (La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo) Kisha katika sura hiyohiyo, mutume Yohana anaonyesha waziwazi kama “Neno” ni Yesu. (Yohana 1:14) Basi, kwa sababu Neno anaitwa Mungu, watu fulani wanawaza mara moja kama Mwana na Baba ni Mungu yuleyule.

Jambo unalopaswa kujua ni kama sehemu hiyo ya Biblia iliandikwa mwanzoni katika Kigiriki. Kisha, mustari huo wa Kigiriki ulitafsiriwa katika luga zingine. Lakini, watafsiri wengi wa Biblia hawakutumia maneno “Neno alikuwa Mungu.” Kwa sababu gani? Kufuatana na ujuzi wao wa luga ya Kigiriki iliyotumiwa kuandika Biblia, watafsiri hao waliona kama maneno “Neno alikuwa Mungu” hayakupaswa kutafsiriwa hivyo. Basi, wamesema yalipaswa kutafsiriwa namna gani? Kuna mifano fulani hapa: “Logos [Neno] alikuwa na sifa za kimungu.” (A New Translation of the Bible) “Neno alikuwa mungu.” (The New Testament in an Improved Version; Traduction du monde nouveau) “Neno alikuwa pamoja na Mungu na alikuwa na utu kama wake.” (The Translator’s New Testament) “Neno alikuwa wa kimungu.” (La Bible du Centenaire) Tafsiri hizo zinaonyesha kama Neno si Mungu mwenyewe. * Lakini, kwa sababu ya ukubwa wake kati ya viumbe wa Yehova, Neno anaitwa “mungu.” Hapa, neno “mungu” linamaanisha “mwenye nguvu.”

TAFUTA MAELEZO MENGINE

Watu wengi hawajui Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia. Basi, namna gani unaweza kujua kile mutume Yohana alipenda kusema? Wazia mufano huu: Mwalimu anawafundisha wanafunzi jambo fulani. Kisha, kila mwanafunzi anaelewa jambo hilo tofauti na wengine. Namna gani wanafunzi hao wanaweza kumaliza ubishi wao? Ni vizuri wamuulize mwalimu wao awape maelezo zaidi. Hakika, maelezo mengine ambayo atawatolea yanaweza kuwasaidia kujua vizuri jambo hilo. Ni hivyo pia, ikiwa unapenda kujua maana ya Yohana 1:1, unaweza kutafuta maelezo mengine juu ya cheo cha Yesu katika Injili ya Yohana. Maelezo hayo yatakusaidia ili ujue vizuri ukweli wa jambo hilo.

Kwa mufano, angalia sasa yale Yohana aliandika katika sura ya 1, mustari wa 18: ‘Hakuna mutu aliyeona Mungu [Mweza-Yote] wakati wowote.’ Lakini, wanadamu wamemuona Mwana, yaani, Yesu kwa sababu Yohana alikuwa amesema: “Neno [Yesu] alifanyika mwili, akakaa kwetu, tukatazama utukufu wake.” (Yohana 1:14La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo) Kwa hiyo, namna gani Mwana angekuwa pia Mungu Mwenza-Yote? Yohana anasema pia kama Neno alikuwa “pamoja na Mungu.” Basi, namna gani mutu anaweza kuwa pamoja na mutu mwingine na wakati huohuo awe ndiye mutu huyo? Tena, katika Yohana 17:3, Yesu anaonyesha waziwazi kama kuna tofauti kati yake na Baba yake wa mbinguni. Anamuita Baba yake “Mungu wa pekee wa kweli.” Kisha Yohana anasema kwa kifupi mwishoni mwa Injili yake hivi: ‘Haya yameandikwa ili mupate kuamini kwamba Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu.’ (Yohana 20:31) Unaona kama Yesu anaitwa, Mwana wa Mungu, wala si Mungu. Maelezo hayo mengine ambayo yanatolewa na Injili ya Yohana yanatusaidia kuelewa vizuri andiko la Yohana 1:1. Yesu, yule Neno, ni “mungu” katika maana ya kama ana cheo cha juu kuliko viumbe vingine vyote, lakini yeye si Mungu Mweza-Yote.

IKIWA BADO KUNA MASHAKA

Wazia tena ule mufano wa mwalimu na wanafunzi. Tuseme kama wanafunzi fulani wangali na mashaka, hata kisha kusikiliza yale maelezo mengine ya mwalimu wao. Kwa hiyo, wanaweza kufanya nini? Wanaweza kumuendea mwalimu mwingine ili awape maelezo zaidi juu ya jambo hilo. Ikiwa mwalimu huyo wa pili anaunga mukono maelezo ya yule wa kwanza, bila shaka ubishi wa wanafunzi wengi unaweza kumalizika. Ni hivyo pia, ikiwa ungali na mashaka juu ya yale Yohana alipenda kusema alipoandika juu ya uhusiano kati ya Yesu na Mungu Mweza-Yote, unaweza kupata maelezo zaidi kutoka kwa mwandikaji mwingine wa Biblia. Kwa mufano, wazia yale ambayo Mathayo aliandika juu ya Yesu. Mathayo anaandika yale Yesu mwenyewe alisema juu ya mwisho wa ulimwengu huu muovu: ‘Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mutu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.’ (Mathayo 24:36) Namna gani maneno hayo yanaonyesha wazi kama Yesu si Mungu Mweza-Yote?

Yesu anasema kama Baba yake anajua mambo mengi kuliko yeye. Ikiwa Yesu ni Mungu Mweza-Yote, basi, angejua mambo yote ambayo Baba yake anajua. Kwa hiyo, basi, Mwana na Baba yake hawalingani. Hata hivyo, wengine watasema: ‘Yesu ni Mungu na ni mwanadamu, na hapa anazungumuza kama mwanadamu.’ Na hata kama hilo lingekuwa kweli, sababu gani hasemi kama roho takatifu inajua mambo ambayo Baba anajua, kwa kuwa inasemekana kuwa hiyo pia ni Mungu yuleyule ambaye ndiye Baba?

Ukiendelea kujifunza Biblia, utaona maandiko mengine mengi yanayozungumuzia jambo hilo. Yanaonyesha wazi yale tunayopaswa kujua juu ya Baba, Mwana, na roho takatifu.​—Zaburi 90:2; Matendo 7:55; Wakolosai 1:15.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Ili kupata maelezo zaidi juu ya Yohana 1:1, soma Mnara wa Mlinzi wa tarehe 1 mwezi wa 11, 2008, uliochapishwa na Mashahidi wa Yehova.