Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Kwa Nini Wakristo wa Kweli Hawatumii Msalaba Katika Ibada?

Kwa Nini Wakristo wa Kweli Hawatumii Msalaba Katika Ibada?

MSALABA unapendwa na kuheshimiwa na mamilioni ya watu. Kitabu The Encyclopædia Britannica kinasema kwamba msalaba ni “ishara kuu ya dini ya Kikristo.” Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawatumii msalaba katika ibada. Kwa nini?

Sababu kuu ni kwamba Yesu Kristo hakufa kwenye msalaba. Kwa kawaida neno la Kigiriki linalotafsiriwa “msalaba” ni stau·rosʹ. Neno hilo linamaanisha “mti au nguzo iliyo wima.” The Companion Bible inasema hivi: “[Neno stau·rosʹ] halimaanishi kamwe vipande viwili vya mbao vilivyokingamana kwa njia yoyote ile . . . Hakuna jambo lolote katika [Agano Jipya] lugha ya Kigiriki linalodokeza vipande viwili vya mbao.”

Katika maandiko kadhaa, waandishi wa Biblia wanatumia neno lingine kurejelea kifaa ambacho Yesu alifia juu yake. Ni neno xyʹlon la Kigiriki. (Matendo 5:30; 10:39; 13:29; Wagalatia 3:13; 1 Petro 2:24) Neno hilo linamaanisha “mbao” au “kijiti, rungu, au mti.”

Kikieleza kwa nini ni mti tu wa kawaida uliotumiwa mara nyingi kuwatundikia waliohukumiwa kifo, kitabu kimoja kinasema: “Miti haikupatikana kila mahali ambapo palichaguliwa kuwatundikia watu waliohukumiwa kifo. Kwa hiyo, nguzo zilisimamishwa ardhini. Mara nyingi wahalifu walitundikwa kwenye nguzo hizo, mikono yao ikiwa imeinuliwa juu na mara nyingi miguu yao ikiwa imefungwa au kupigiliwa misumari.”—Kitabu Das Kreuz und die Kreuzigung, kilichoandikwa na Hermann Fulda.

Hata hivyo, Neno la Mungu linatoa uthibitisho wenye kusadikisha zaidi. Mtume Paulo alisema: “Kristo kwa kutununua alituachilia huru kutoka katika laana ya Sheria kwa yeye kuwa laana badala yetu, kwa sababu imeandikwa: ‘Amelaaniwa kila mtu aliyetundikwa juu ya mti.’” (Wagalatia 3:13) Hapa Paulo ananukuu andiko la Kumbukumbu la Torati 21:22, 23, ambalo kwa wazi linarejelea mti wala si msalaba. Kwa kuwa watu waliouawa kwa njia hiyo walionwa kuwa “laana,” haifai Wakristo kupamba nyumba zao kwa sanamu za Kristo akiwa ametundikwa.

Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba wale waliodai kuwa Wakristo walitumia msalaba katika ibada kwa muda wa miaka 300 baada ya Kristo kufa. Hata hivyo, katika karne ya nne, Maliki mpagani Konstantino alijiunga na Wakristo waasi-imani na kuutetea msalaba kuwa ishara yao. Hata Konstantino awe alikuwa na nia gani, msalaba haukuwa na uhusiano wowote na Yesu Kristo. Kwa kweli, msalaba ulibuniwa na wapagani. Kitabu New Catholic Encyclopedia kinakiri hivi: “Msalaba ulitumiwa na watu walioishi kabla ya enzi za Ukristo na wale ambao hawakuwa Wakristo.” Watu fulani maarufu wamesema kwamba msalaba unahusiana na ibada ya viumbe na desturi za kipagani za ngono.

Kwa nini basi ishara hiyo ya kipagani ilienezwa? Yaelekea ilienezwa ili kufanya iwe rahisi kwa wapagani kukubali “Ukristo.” Hata hivyo, Biblia inashutumu waziwazi matumizi ya ishara yoyote ya kipagani. (2 Wakorintho 6:14-18) Biblia inakataza pia kila namna ya ibada ya sanamu. (Kutoka 20:4, 5; 1 Wakorintho 10:14) Hivyo basi, Wakristo wa kweli wana sababu nzuri za kutotumia msalaba katika ibada yao. *

^ fu. 4 Ili kupata habari zaidi kuhusu msalaba, ona ukurasa wa 211-215 wa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Chapa ya 2004, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.