Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Nafsi” na “Roho”​—Ni Nini Kabisa?

“Nafsi” na “Roho”​—Ni Nini Kabisa?

NYONGEZA

“Nafsi” na “Roho”​—Ni Nini Kabisa?

UNAPOSIKIA maneno “nafsi” na “roho,” wewe unawaza kuwa ni nini? Wengi wanaamini kama maneno hayo yanamaanisha kitu fulani kilicho ndani ya mutu, na kitu hicho hakiwezi kufa wala hakionekani. Wanawaza kama mutu anapokufa kitu hicho kisichoonekana kinauacha mwili na kuendelea kuishi mahali fulani. Kwa kuwa fundisho hilo limeenea sana, watu wengi wanashangaa wanapovumbua kama si fundisho la Biblia. Kwa hiyo, Neno la Mungu linafundisha kuwa nafsi ni nini na roho ni nini?

YALE BIBLIA INAFUNDISHA JUU YA “NAFSI”

Kwanza, acha tuzungumuzie nafsi. Labda ungali unakumbuka kama Biblia iliandikwa mwanzoni hasa katika Kiebrania na Kigiriki. Waandikaji wa Biblia, walipoandika juu ya nafsi walitumia neno la Kiebrania nèphèsh ao neno la Kigiriki psukhê. Maneno hayo mawili yanapatikana zaidi ya mara 800 katika Maandiko, na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inayatafsiri yote kuwa “nafsi.” Unapochunguza jinsi neno “nafsi” linavyotumiwa katika Biblia, utaona wazi kama neno hilo linamaanisha (1) watu, (2) wanyama, ao (3) uzima wa mutu ao wa nyama. Basi, acha tuzungumuzie Maandiko fulani yanayoonyesha maana hiyo tatu.

Watu. “Katika siku za Noa . . . watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Ni wazi kwamba katika andiko hilo, neno “nafsi” linamaanisha watu, yaani, Noa, bibi yake, watoto wake watatu, na bibi zao. Andiko la Kutoka 16:16 linaonyesha maagizo ya kuokota mana ambayo Waisraeli walipokea. Waliambiwa hivi: ‘Okoteni kiasi chake kulingana na hesabu ya nafsi ambazo kila mumoja wenu anazo katika hema lake.’ Kwa hiyo, kila mutu alipaswa kuokota mana kulingana na hesabu ya watu wa familia yake. Katika Biblia, utakuta Maandiko mengine yanayotumia neno “nafsi” ili kumaanisha “mutu” ao “watu,” kwenye Mwanzo 46:18; Yoshua 11:11; Matendo 27:37; na Waroma 13:1.

Wanyama. Katika masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji, tunasoma hivi: ‘Mungu akaendelea kusema: Maji na yajawe na nafsi hai na viumbe vinavyoruka viruke juu ya dunia kwenye uso wa anga la mbingu. Mungu akaendelea kusema: Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake, munyama wa kufugwa na munyama anayetambaa na munyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake. Ikawa hivyo.’ (Mwanzo 1:20, 24) Katika andiko hilo, samaki, wanyama wa kufugwa, na wanyama-mwitu wote wanaitwa kwa neno lilelile, yaani, “nafsi.” Ndege na wanyama wengine wanaitwa nafsi kwenye Mwanzo 9:10; Walawi 11:46; na Hesabu 31:28.

Uzima wa mutu. Kuna wakati neno “nafsi” linamaanisha uzima wa mutu. Yehova alimuambia Musa hivi: “Watu wote waliokuwa wakiiwinda nafsi yako wamekufa.” (Kutoka 4:19) Adui za Musa walikuwa wakitafuta nini? Uzima wake, yaani, walitafuta kumuua Musa. Wakati Raheli alipokuwa anamuzaa mutoto wake Benyamini, Biblia inasema kama ‘nafsi yake ilitoka (kwa sababu alikufa).’ (Mwanzo 35:16-19) Wakati huo, Raheli alipoteza uzima wake. Waza tena juu ya yale Yesu alisema: ‘Mimi ndiye muchungaji mwema; muchungaji mwema huitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.’ (Yohana 10:11) Yesu alitoa nafsi yake ao uzima wake kwa ajili ya wanadamu. Katika Maandiko hayo yote, ni wazi kama neno “nafsi” linamaanisha uzima wa mutu. Utapata mifano mingine yenye maana hiyo ya neno “nafsi” kwenye 1 Wafalme 17:17-23; Mathayo 10:39; Yohana 15:13; na Matendo 20:10.

Unapoendelea kujifunza Neno la Mungu utaona kama hakuna andiko katika Biblia ambalo linaonyesha “kutoweza kufa” kwa nafsi ao “kuishi milele” kwa nafsi. Maandiko yanasema wazi kama nafsi inaweza kufa. (Ezekieli 18:4, 20) Ndiyo sababu, katika Biblia mutu ambaye amekufa anaitwa “nafsi iliyokufa.”​—Walawi 21:11.

“ROHO” NI NINI?

Sasa, acha tuchunguze yale Biblia inasema juu ya “roho.” Watu fulani wanawaza kama “roho” ni neno lingine linalomaanisha tu “nafsi.” Lakini, si hivyo. Biblia inaonyesha wazi kama “roho” na “nafsi” ni mambo mawili tofauti. Kuna tofauti gani?

Waandikaji wa Biblia walipoandika juu ya “roho” walitumia neno la Kiebrania ruʹach ao la Kigiriki pneuʹma. Maandiko yenyewe yanaonyesha maana ya maneno hayo. Kwa mufano, andiko la Zaburi 104:29 linasema: ‘[Yehova] ukiiondoa roho [ruʹach] yao, wanakata pumuzi, na kurudi katika mavumbi yao.’ Na andiko la Yakobo 2:26 linasema kama “mwili bila roho [pneuʹma] umekufa.” Katika Maandiko hayo, “roho” inamaanisha kile ambacho kinafanya mwili uishi. Bila roho, mwili unakufa. Kwa hiyo, katika Biblia neno ruʹach halitafsiriwi tu “roho” bali pia “nguvu” ao nguvu ya uzima. Kwa mufano, juu ya Garika ya siku za Noa, Mungu alisema hivi: ‘Ninaleta garika ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili walio na nguvu [ruʹach] ya uhai ndani yao.’ (Mwanzo 6:17; 7:15, 22) Kwa hiyo, “roho” ni nguvu isiyoonekana, inayotendesha viumbe vyote vinavyoishi ao vilivyo na uzima.

Nafsi inatofautiana na roho. Mwili una lazima ya roho kama vile radio ina lazima ya mawe (pile) ao umeme ili ifanye kazi. Kwa mufano, unapotia pile katika radio na kuifungua, nguvu zilizo katika pile zinafanya radio iseme. Bila nguvu hiyo, radio haiwezi kufanya lolote. Vilevile radio ikiondolewa kwenye umeme, haiwezi kufanya lolote. Roho pia ni nguvu inayofanya mwili wetu utende. Kama umeme ao nguvu zinazopatikana katika pile ya radio, roho haiwezi kusikia furaha ao huzuni, wala kuwaza. Ni nguvu isiyokuwa na umbo lolote. Lakini bila roho ao nguvu ya uzima ‘tunakata pumuzi na kurudi katika mavumbi’ kama mutunga-zaburi alivyosema.

Andiko la Mhubiri 12:7 linazungumuzia kifo cha mwanadamu, linasema hivi: ‘Mavumbi [mwili wake] huirudia inchi kama yalivyokuwa, nayo roho yenyewe humurudia Mungu wa kweli aliyeitoa.’ Wakati roho, ao nguvu ya uzima, inapouacha mwili, mwili unakufa na kurudi ulipotoka, ni kusema kwenye udongo. Na nguvu ya uzima inarudi mahali ilipotoka, ni kusema kwa Mungu. (Ayubu 34:14, 15; Zaburi 36:9) Hiyo haimanishi kama nguvu ya uzima inaenda moja kwa moja mbinguni. Lakini, inamaanisha kama mutu anapokufa, ni Yehova Mungu ndiye anayeweza kumufanya mutu huyo aishi tena. Ni kama vile uzima wake uko katika mikono ya Mungu. Ni kwa nguvu ya Mungu tu ndipo roho ao nguvu ya uzima inaweza kurudishwa ili mutu aweze kuishi tena.

Kwa kweli inatuliza moyo kujua kama hivyo ndivyo Mungu atatendea wote wanaopumuzika ndani ya “makaburi ya ukumbusho”! (Yohana 5:28, 29) Wakati Yehova atawafufua watu, atamufanyizia kila mumoja wao mwili mupya na kutia roho ao nguvu ya uzima ndani ya mwili huo ili uanze kutenda tena. Itakuwa siku ya furaha kabisa!

Ili kupata maelezo zaidi ya Biblia juu ya “nafsi” na “roho,” soma broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa? na kitabu Kutoa sababu kwa Kutumia Maandiko, ukurasa wa 221-226; 242-246, chapa ya 2004, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.