Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sheoli na Hadesi Ni Nini?

Sheoli na Hadesi Ni Nini?

NYONGEZA

Sheoli na Hadesi Ni Nini?

KATIKA luga zilizotumiwa kuandika Biblia hapo mwanzoni, walitumia neno la Kiebrania sheʼohlʹ na neno la Kigiriki haiʹdes zaidi ya mara 70. Maneno hayo mawili yanazungumuzia kifo. Biblia fulani zinatafsiri maneno hayo kuwa “kaburi,” “kuzimu,” ao “shimo.” Lakini, luga nyingi zinakosa maneno yanayoweza kutoa maana kamili ya maneno hayo ya Kiebrania na Kigiriki. Biblia Takatifu​Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia maneno “Sheoli” na “Hadesi” katika maelezo ya chini. Maneno hayo mawili yanamaanisha nini kabisa? Acha tuone namna yanavyotumiwa katika maandiko mbalimbali ya Biblia.

Andiko la Mhubiri 9:10 linasema hivi: “Hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi [“Sheoli,”], mahali unapokwenda.” Je, hiyo inamaanisha kama Sheoli ni kaburi fulani ambamo labda tumemuzika mutu fulani tuliyemupenda? Hapana. Biblia inapozungumuzia kaburi fulani inatumia maneno mengine ya Kiebrania na Kigiriki, wala si sheʼohlʹ na haiʹdes. (Mwanzo 23:7-9; Mathayo 28:1) Tena, Biblia haitumii neno “Sheoli” ili kuzungumuzia kaburi ambamo watu wengi wamezikwa pamoja, kama vile kaburi la familia.​—Mwanzo 49:30, 31.

Kwa hiyo, basi, “Sheoli” ni mahali pa namna gani? Neno la Mungu linaonyesha kama maneno “Sheoli” na “Hadesi” hayamaanishe kaburi kubwa la watu wengi. Kwa mufano, andiko la Isaya 5:14 linasema kama Sheoli ‘imepanua sana nafsi yake nayo imepanua kinywa chake kupita mipaka.’ Ingawa Sheoli imekwisha kumeza watu wengi waliokufa, nyakati zote inaonekana kama haiwezi kushiba. (Methali 30:15, 16) ‘Sheoli haitosheki’ wala kujaa. (Methali 27:20) Sheoli haiwezi kujaa na haina mipaka. Kwa hiyo, Sheoli ao Hadesi, si mahali fulani panapoweza kuonekana. Lakini ni kaburi ao mahali pa mufano ambapo watu walio wengi wanalala usingizi katika kifo.

Fundisho la Biblia juu ya ufufuo linatusaidia kuelewa vizuri zaidi maana ya “Sheoli” na “Hadesi.” Neno la Mungu linapozungumuza juu ya ufufuo linatumia maneno Sheoli na Hadesi. * (Ayubu 14:13; Matendo 2:31; Ufunuo 20:13) Linaonyesha pia kama si wale tu waliomutumikia Mungu ndio walio katika Sheoli ao Hadesi, lakini pia wengi ambao hawakumutumikia. (Mwanzo 37:35; Zaburi 55:15) Ndiyo sababu Biblia inafundisha kama kutakuwa na “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”​—Matendo 24:15.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Tofauti na hilo Biblia inafundisha kama watu waliokufa ambao hawatafufuliwa wako katika “Gehena” wala si katika Sheoli, ao Hadesi. (Mathayo 5:30; 10:28; 23:33) Gehena pia ni mahali pa mufano, kama vile Sheoli na Hadesi ni mahali pa mufano.