Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Yule Malaika Mkuu Mikaeli Ni Nani?

Yule Malaika Mkuu Mikaeli Ni Nani?

KIUMBE wa roho anayeitwa Mikaeli hatajwi mara nyingi katika Biblia. Hata hivyo, kila mara anatajwa akitenda jambo fulani. Katika kitabu cha Danieli, Mikaeli anapigana na malaika waovu; katika barua ya Yuda, anabishana na Shetani; na katika Ufunuo, anapigana na Ibilisi na malaika wake waovu. Anapoutetea utawala wa Yehova na kupigana na adui za Mungu, Mikaeli anatenda kupatana na maana ya jina lake—“Ni Nani Aliye Kama Mungu?” Lakini Mikaeli ni nani?

Nyakati nyingine, watu huitwa majina mbalimbali. Kwa mfano, mzee wa ukoo Yakobo aliitwa pia Israeli, na mtume Petro aliitwa Simoni. (Mwanzo 49:1, 2; Mathayo 10:2) Vivyo hivyo, Biblia inaonyesha kwamba Mikaeli ni jina lingine la Yesu Kristo, kabla na baada ya maisha yake duniani. Hebu tuone sababu za Kimaandiko zinazotufanya tukate kauli hiyo.

Malaika Mkuu. Neno la Mungu linamwita Mikaeli “yule malaika mkuu.” (Yuda 9) Ona kwamba Mikaeli anaitwa yule malaika mkuu. Hilo linaonyesha kwamba kuna malaika mmoja tu aliye mkuu. Isitoshe katika Biblia, jina “malaika mkuu” linatumiwa katika hali ya umoja tu, wala si kwa wingi. Zaidi ya hayo, Yesu anahusianishwa na wadhifa wa malaika mkuu. Kuhusu Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa, andiko la 1 Wathesalonike 4:16 linasema: “Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, kwa sauti ya malaika mkuu.” Kwa hiyo sauti ya Yesu inafafanuliwa kuwa sauti ya malaika mkuu. Basi, andiko hilo linadokeza kwamba Yesu mwenyewe ndiye Mikaeli yule malaika mkuu.

Kiongozi wa Jeshi. Biblia inasema kwamba ‘Mikaeli na malaika zake walipigana na yule joka mkubwa na malaika zake.’ (Ufunuo 12:7) Kwa hiyo, Mikaeli ni Kiongozi wa jeshi la malaika waaminifu. Pia kitabu cha Ufunuo kinamtaja Yesu akiwa Kiongozi wa jeshi la malaika waaminifu. (Ufunuo 19:14-16) Naye mtume Paulo anamtaja kihususa “Bwana Yesu” na “malaika zake wenye nguvu.” (2 Wathesalonike 1:7) Kwa hiyo, Biblia inataja Mikaeli na “malaika zake” na Yesu na “malaika zake.” (Mathayo 13:41; 16:27; 24:31; 1 Petro 3:22) Kwa kuwa Neno la Mungu halionyeshi popote kwamba kuna majeshi mawili ya malaika waaminifu mbinguni—moja likiongozwa na Mikaeli na lingine likiongozwa na Yesu—ni wazi kwamba Mikaeli si mwingine ila ni Yesu Kristo akiwa katika wadhifa wake mbinguni. *

^ fu. 1 Unaweza kupata habari zaidi zinazoonyesha kwamba jina Mikaeli linamhusu Mwana wa Mungu katika Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 393-394 au Étude Perspicase, Buku la 2, ukurasa wa 280-281, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.