Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Babiloni Mukubwa’ Ni Nini?

‘Babiloni Mukubwa’ Ni Nini?

NYONGEZA

‘Babiloni Mukubwa’ Ni Nini?

KITABU cha Ufunuo kina majina ambayo yana maana ya mufano. (Ufunuo 1:1) Kwa mufano, kinamutaja mwanamuke fulani kahaba ao malaya ambaye jina ‘Babiloni Mukubwa’ limeandikwa kwenye uso wake. Kinasema kama mwanamuke huyo ameketi juu ya “umati na mataifa.” (Ufunuo 17:1, 5, 15) Kwa sababu hakuna mwanamuke wa kawaida anayeweza kufanya hivyo, basi Babiloni Mukubwa ni mwanamuke wa mufano. Kwa hiyo, mwanamuke huyo kahaba wa mufano anafananisha nini?

Kwenye Ufunuo 17:18, mwanamuke huyohuyo wa mufano anatajwa kuwa “lile jiji kubwa lililo na ufalme juu ya wafalme wa dunia.” Neno “jiji” linaonyesha kikundi cha watu. Kwa sababu ‘jiji hilo kubwa’ linaongoza “wafalme wa dunia,” lazima yule mwanamuke anayeitwa Babiloni Mukubwa iwe tengenezo fulani lenye nguvu kabisa duniani pote; tengenezo fulani la kidini. Ona namna maandiko mengine katika kitabu cha Ufunuo yanatusaidia kujua jambo hilo.

Tengenezo linaweza kuwa la kisiasa (politike), la kibiashara, ao la kidini. Mwanamuke anayeitwa Babiloni Mukubwa si tengenezo la kisiasa (politike) kwa sababu Neno la Mungu linasema kama “wafalme wa dunia,” ni kusema, watu wa politike wa dunia hii, “walifanya uasherati” naye. Uasherati wake ni mapatano ambayo amefanya na watawala wa dunia na ndio sababu anaitwa “kahaba mukubwa.”​—Ufunuo 17:1, 2; Yakobo 4:4.

Babiloni Mukubwa hawezi kuwa tengenezo la kibiashara kwa sababu “wanabiashara wa dunia,” watamulilia atakapoharibiwa. Tena, Biblia inasema kama wakati huo wafalme na wanabiashara watamuangalia Babiloni Mukubwa wakiwa “mbali.” (Ufunuo 18:3, 9, 10, 15-17) Kwa hiyo, ni wazi kama Babiloni Mukubwa, si tengenezo la politike wala la kibiashara, bali ni tengenezo la kidini.

Jambo lingine linaloonyesha kama Babiloni Mukubwa ni tengenezo la kidini ni vile Biblia inaonyesha kama anapotosha mataifa kwa ‘mazoea yake ya kuzungumuza na pepo’ ao mashetani. (Ufunuo 18:23) Kwa sababu mazoea yote ya mashetani ni ya kidini na yanatokana na roho wabaya, haishangazi kuona Biblia inamuita Babiloni Mukubwa “makao ya roho wabaya.” (Ufunuo 18:2; Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Tena, tengenezo hilo la dini ya uongo linapinga vikali dini ya kweli, linawatesa “manabii” na “watakatifu.” (Ufunuo 18:24) Kwa kweli, Babiloni Mukubwa anachukia sana dini ya kweli, ndio sababu anawatesa kinyama na hata kuwaua “mashahidi wa Yesu.” (Ufunuo 17:6) Basi, ni wazi kama mwanamuke huyo anayeitwa Babiloni Mukubwa anafananisha dini zote za uongo duniani pote zinazomupinga Yehova Mungu.