Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Je, Yesu Alizaliwa Desemba?

Je, Yesu Alizaliwa Desemba?

BIBLIA haisemi Yesu alizaliwa wakati gani. Hata hivyo, inatupa sababu za kutosha kukata kauli kwamba hakuzaliwa Desemba.

Fikiria hali ya hewa wakati huo wa mwaka huko Bethlehemu, ambako Yesu alizaliwa. Mwezi wa Kislevu katika kalenda ya Kiyahudi (unaolingana na miezi ya Novemba/Desemba) ulikuwa mwezi wa baridi na mvua. Mwezi unaofuata ulikuwa mwezi wa Tebethi (Desemba/Januari). Huo ndio mwezi uliokuwa na baridi kali zaidi, mara kwa mara kukiwa na theluji katika nyanda za juu. Hebu tuone Biblia inasema nini kuhusu hali ya hewa ya eneo hilo.

Mwandishi wa Biblia Ezra anaonyesha kwamba Kislevu ulikuwa mwezi wenye baridi na mvua nyingi. Baada ya kueleza kwamba umati ulikuwa umekusanyika Yerusalemu “katika mwezi wa 9 [Kislevu] siku ya 20 ya mwezi huo,” Ezra anasema kwamba watu walikuwa “wakitetemeka . . . kwa sababu ya manyunyu ya mvua.” Kuhusu hali za hewa wakati huo wa mwaka, watu waliokuwa wamekusanyika walisema: “Haya ni majira ya manyunyu ya mvua, wala haiwezekani kusimama nje.” (Ezra 10:9, 13; Yeremia 36:22) Basi, haishangazi kwamba wachungaji walioishi karibu na Bethlehemu walihakikisha kwamba wao wenyewe na mifugo yao hawakuwa nje malishoni mwezi wa Desemba ulipofika!

Hata hivyo, Biblia inasema kwamba wachungaji walikuwa malishoni wakilisha makundi yao usiku ambao Yesu alizaliwa. Isitoshe, mwandishi wa Biblia, Luka anaonyesha kwamba wakati huo wachungaji walikuwa “wakiishi nje, wakichunga makundi yao usiku” karibu na Bethlehemu. (Luka 2:8-12) Ona kwamba wachungaji hao walikuwa wakiishi nje, si kwamba walikuwa wakitembea-tembea nje wakati wa mchana. Walikuwa na makundi yao malishoni usiku. Je, wangeweza kuishi nje wakati wa baridi na mvua huko Bethlehemu mwezi wa Desemba? Hapana. Kwa hiyo, matukio hayo ya wakati wa kuzaliwa kwa Yesu yanaonyesha kwamba hakuzaliwa Desemba. *

Neno la Mungu linatuambia waziwazi wakati ambapo Yesu alikufa, lakini halielezi mengi kuhusu wakati ambapo alizaliwa. Hilo linatukumbusha maneno ya Mfalme Sulemani: “Jina ni bora kuliko mafuta mazuri, na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa kwa mtu.” (Mhubiri 7:1) Basi, haishangazi kwamba Biblia ina habari nyingi kuhusu huduma na kifo cha Yesu lakini inataja mambo machache tu kuhusu wakati wa kuzaliwa kwake.

Yesu alipozaliwa, wachungaji na makundi yao walikuwa malishoni wakati wa usiku

^ fu. 1 Unaweza kupata habari zaidi kwenye ukurasa wa 275-279 wa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Chapa ya 2004, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.