Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Je, Tusherehekee Sikukuu?

Je, Tusherehekee Sikukuu?

SIKUKUU za kidini na sikukuu nyingine zinazopendwa na watu wengi ambazo husherehekewa sehemu nyingi za ulimwengu leo, hazikutokana na Biblia. Basi, sikukuu hizo zilianzia wapi? Ikiwa unaweza kufanya utafiti katika maktaba, unaweza kujifunza mengi kuhusu sikukuu zinazopendwa na wengi katika eneo lenu. Fikiria mifano michache.

Ista. “Katika Agano Jipya, hakuna lolote linaloonyesha kwamba Ista ilisherehekewa,” yasema The Encyclopædia Britannica. Ista ilianzaje? Ilitokana na ibada ya kipagani. Ingawa inasemekana kwamba sikukuu hiyo ni ukumbusho wa kufufuka kwa Yesu, desturi zinazohusiana na sikukuu ya Ista si za Kikristo. Kwa mfano, The Catholic Encyclopedia inasema hivi kuhusu yule “sungura wa Ista”: “Sungura huyo ni mfano wa kipagani na sikuzote huwakilisha nguvu za uzazi.”

Sherehe za Mwaka Mpya. Tarehe na desturi zinazohusiana na sherehe za Mwaka Mpya hutofautiana katika nchi mbalimbali. Kuhusu chanzo cha sikukuu hiyo, The World Book Encyclopedia inasema: “Mtawala Mroma Kaisari Yulio aliteua Januari 1 kuwa Siku ya Mwaka Mpya katika mwaka wa 46 W.K. Waroma walitenga siku hiyo kwa ajili ya Yanu, mungu wa malango, milango, na mianzo. Mwezi wa Januari ulipata jina lake kutoka kwa Yanu, aliyekuwa na nyuso mbili—mmoja ukiangalia mbele na mwingine ukiangalia nyuma.” Kwa hiyo, sherehe za Mwaka Mpya zinatokana na mapokeo ya kipagani.

Mkesha wa Siku ya Watakatifu Wote (“Halloween”). The Encyclopedia Americana inasema: “Desturi fulani-fulani zinazohusiana na Mkesha wa Siku ya Watakatifu Wote zilitokana na sherehe za kidini za Kiselti za kabla ya enzi za Ukristo. Waselti walikuwa na sikukuu kwa ajili ya miungu wawili wakuu—mungu-jua na mungu wa wafu . . . , ambaye sikukuu yake ilikuwa Novemba 1, mwanzo wa Mwaka Mpya wa Kiselti. Pole kwa pole, sikukuu hiyo ya wafu ikaingizwa katika desturi za Kikristo.”

Sikukuu Nyingine. Haiwezekani kuzungumzia sikukuu zote ulimwenguni. Hata hivyo, sikukuu zinazowatukuza wanadamu au mashirika ya kibinadamu hazimpendezi Yehova. (Yeremia 17:5-7; Matendo 10:25, 26) Pia, kumbuka kwamba Mungu hupendezwa au kuchukizwa na sikukuu za kidini ikitegemea vyanzo vyake. (Isaya 52:11; Ufunuo 18:4) Kanuni za Biblia zilizotajwa katika Sura ya 16 ya kitabu hiki zitakusaidia kujua maoni ya Mungu kuhusu sikukuu zisizo za kidini.