Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 3

Wapende Wale Ambao Mungu Anawapenda

Wapende Wale Ambao Mungu Anawapenda

“Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”—METHALI 13:20.

1-3. (a) Biblia inataja ukweli gani ulio wazi? (b) Tunaweza kuchagua jinsi gani marafiki ambao watatuchochea kutenda mema?

INAWEZA kusemwa kwamba watu ni kama sifongo; wanafyonza chochote kilicho karibu nao. Hata bila kujua, ni rahisi sana kuiga mitazamo, viwango, na nyutu za watu tunaoshirikiana nao kwa ukaribu.

2 Biblia inataja ukweli huu ulio wazi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Methali hiyo haizungumzi kuhusu kukutana na watu mara kwa mara tu. Maneno ‘kutembea na’ yanaonyesha urafiki unaoendelea. * Kitabu kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi kuhusu mstari huo: “Kutembea na mtu kunahusisha kumpenda na kushikamana naye.” Je, hukubali kwamba tuna mwelekeo wa kuwaiga watu tunaowapenda? Kwa kweli, kwa sababu tunashikamana sana na watu tunaowapenda, wanaweza kuwa na uvutano juu yetu—mzuri au mbaya.

3 Ili tukae katika upendo wa Mungu, tunapaswa kutafuta marafiki ambao watatuchochea kutenda mema. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwa ufupi, ni kwa kuwapenda wale ambao Mungu anawapenda, yaani, marafiki wake wawe marafiki wetu. Fikiria jambo hili. Je, kweli tunaweza kupata marafiki bora kuliko marafiki wa Yehova ambao wana sifa anazopenda? Basi acheni tuchunguze aina ya watu ambao Mungu anapenda. Kuelewa waziwazi maoni ya Yehova kutatusaidia kuchagua marafiki wanaofaa.

WALE AMBAO MUNGU ANAWAPENDA

4. Kwa nini Yehova ana haki ya kuchagua marafiki kwa uangalifu, na kwa nini Yehova alimwita Abrahamu “rafiki yangu”?

4 Yehova anachagua marafiki kwa uangalifu. Bila shaka ana haki ya kufanya hivyo. Yeye ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, na kuwa rafiki yake ndilo pendeleo kubwa zaidi. Basi, yeye anachagua marafiki wa aina gani? Yehova anawakaribia wale wanaomtegemea na kumwamini kabisa. Kwa mfano, mfikirie mzee wa ukoo, Abrahamu, anayejulikana kwa imani yake ya pekee. Kumwomba baba amtoe mwana wake kuwa dhabihu ni jaribu kali sana la imani. * Hata hivyo, ‘ni kana kwamba Abrahamu alimtoa Isaka’ akiwa na imani kamili kwamba “Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua hata kutoka kwa wafu.” (Waebrania 11:17-19) Kwa kuwa Abrahamu alionyesha imani na utii, kwa upendo Yehova alimwita “rafiki yangu.”—Isaya 41:8; Yakobo 2:21-23.

5. Yehova ana maoni gani kuhusu wale wanaomtii kwa ushikamanifu?

5 Yehova anathamini sana utii mshikamanifu. Anawapenda wale walio tayari kutanguliza ushikamanifu wao kwake. (2 Samweli 22:26) Kama tulivyoona katika Sura ya 1 ya kitabu hiki, Yehova anapendezwa sana na wale wanaochagua kumtii kwa sababu wanampenda. Andiko la Methali 3:32 linasema kwamba “urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.” Wale wanaotimiza matakwa ya Mungu kwa ushikamanifu wanapata mwaliko wenye fadhili kutoka kwa Yehova: Wanaweza kuwa wageni katika “hema” lake—wakiwa wamealikwa kumwabudu na kumkaribia kwa uhuru katika sala.—Zaburi 15:1-5.

6. Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yesu, na Yehova ana maoni gani kuhusu wale wanaompenda Mwana wake?

6 Yehova anawapenda wale wanaompenda Yesu, Mwana wake mzaliwa-pekee. Yesu alisema: “Ikiwa yeyote ananipenda, atalishika neno langu, na Baba yangu atampenda, nasi hakika tutakuja kwake na kukaa pamoja naye.” (Yohana 14:23) Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yesu? Kwa kuzishika amri zake, kutia ndani amri ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20; Yohana 14:15, 21) Pia, tunaonyesha kwamba tunampenda Yesu ‘tunapofuata hatua zake kwa ukaribu,’ kwa kumwiga kwa maneno na matendo kadiri tunavyoweza tukiwa wanadamu wasio wakamilifu. (1 Petro 2:21) Moyo wa Yehova hushangilia anapoona jitihada za wale ambao kwa sababu wanampenda Mwana wake wanachochewa kumwiga Kristo.

7. Kwa nini ni jambo la hekima kufanya urafiki na marafiki wa Yehova?

7 Imani, ushikamanifu, utii, na kumpenda Yesu na viwango vyake, ni kati ya sifa ambazo Yehova anataka marafiki Wake wawe nazo. Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Je, marafiki wangu wa karibu wana sifa na viwango kama hivyo? Je, nimefanya urafiki na marafiki wa Yehova?’ Ni jambo la hekima kufanya hivyo. Watu wanaositawisha sifa kama za Mungu na wanaohubiri habari njema ya Ufalme kwa bidii wanaweza kutuchochea kuishi kupatana na azimio letu la kumpendeza Mungu.—Ona sanduku lenye kichwa “ Ni Nani Aliye Rafiki Mzuri?

KUJIFUNZA KUTOKANA NA MIFANO ILIYO KATIKA BIBLIA

8. Ni nini kinachokuvutia kuhusu urafiki kati ya (a) Naomi na Ruthu? (b) wale vijana watatu Waebrania? (c) Paulo na Timotheo?

8 Maandiko yana mifano mingi ya watu waliofaidika kwa kuchagua marafiki wanaofaa. Unaweza kusoma kuhusu urafiki kati ya Naomi na binti-mkwe wake, Ruthu, kati ya wale vijana watatu Waebrania ambao waliendelea kuwa marafiki wakiwa Babiloni, na kati ya Paulo na Timotheo. (Ruthu 1:16; Danieli 3:17, 18; 1 Wakorintho 4:17; Wafilipi 2:20-22) Hata hivyo, acheni tuzungumzie mfano mwingine wa pekee: urafiki kati ya Daudi na Yonathani.

9, 10. Urafiki kati ya Daudi na Yonathani ulitegemea nini?

9 Biblia inasema kwamba baada ya Daudi kumuua Goliathi, “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi, na Yonathani akaanza kumpenda kama nafsi yake mwenyewe.” (1 Samweli 18:1) Hivyo, urafiki ulio imara ukasitawi ijapokuwa umri wao ulitofautiana sana, na urafiki huo ukaendelea mpaka Yonathani alipokufa vitani. * (2 Samweli 1:26) Urafiki wa karibu kati ya Daudi na Yonathani ulitegemea nini?

10 Daudi na Yonathani walikuwa marafiki wakubwa kwa sababu walimpenda Mungu na walitamani sana kuendelea kuwa waaminifu kwake. Wote wawili walitaka kumpendeza Mungu. Kila mmoja wao alikuwa na sifa zilizomvutia mwenzake. Bila shaka, Yonathani alivutiwa na uhodari na bidii ya kijana huyo ambaye alitetea jina la Yehova bila woga. Naye Daudi alimheshimu mwanamume huyo aliyekuwa na umri mkubwa kuliko yeye na ambaye aliunga mkono kwa ushikamanifu mipango ya Yehova na kutanguliza mapendezi ya Daudi bila ubinafsi. Kwa mfano, fikiria kilichotukia wakati Daudi alipovunjika moyo akiwa amekimbilia nyikani ili kuhepa ghadhabu ya Mfalme Sauli mwovu, baba ya Yonathani. Yonathani alionyesha ushikamanifu wa pekee alipoamua ‘kwenda kwa Daudi ili autie nguvu mkono wake kuhusiana na Mungu.’ (1 Samweli 23:16) Wazia jinsi Daudi alivyohisi rafiki yake mpendwa alipofika na kumtegemeza na kumtia moyo! *

11. Unajifunza nini kuhusu urafiki kutokana na mfano wa Yonathani na Daudi?

11 Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yonathani na Daudi? Jambo kuu tunalojifunza ni kwamba urafiki kati ya watu unapaswa kutegemea hasa urafiki wao pamoja na Mungu. Tunapositawisha urafiki pamoja na wale walio na imani kama yetu, maadili kama yetu, na tamaa kama yetu ya kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu, tunaweza kuzungumza pamoja nao kuhusu maoni, hisia, na mambo yanayotutia moyo na kutujenga. (Waroma 1:11, 12) Tunapata marafiki wa aina hiyo kati ya waabudu wenzetu. Je, hiyo inamaanisha kwamba kila mtu anayehudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme ni rafiki mzuri? Hapana, haiwi hivyo nyakati zote.

KUCHAGUA MARAFIKI WA KARIBU

12, 13. (a) Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu tunapochagua marafiki hata kati ya Wakristo wenzetu? (b) Ni tatizo gani lililotokea katika makutaniko ya karne ya kwanza, naye Paulo alitoa maonyo gani makali?

12 Hata katika kutaniko, ni lazima tuwe waangalifu ili tuchague marafiki ambao watatujenga kiroho. Je, hilo litushangaze? Hapana. Wakristo fulani katika kutaniko wanaweza kuchukua muda mrefu kufikia ukomavu wa kiroho kama vile matunda fulani kwenye mti yanavyoweza kuchukua muda mrefu kuiva. Kwa hiyo, katika kutaniko lolote lile, kuna Wakristo walio katika hatua mbalimbali za ukuzi wa kiroho. (Waebrania 5:12–6:3) Bila shaka, tunaonyesha uvumilivu na upendo kwa wapya au walio dhaifu, kwa kuwa tunataka kuwasaidia wakomae kiroho.—Waroma 14:1; 15:1.

13 Mara kwa mara huenda hali ikatokea katika kutaniko ambayo inahitaji tuwe waangalifu kuhusu wale tunaoshirikiana nao. Huenda watu fulani wakajiendesha isivyofaa. Wengine wanaweza kusitawisha roho ya kulalamika. Hali kama hiyo ilitokea katika makutaniko ya karne ya kwanza W.K. Ingawa washiriki wengi wa makutaniko hayo walikuwa waaminifu, wengine hawakujiendesha kwa njia inayofaa. Kwa kuwa watu fulani katika kutaniko la Korintho hawakufuata mafundisho fulani ya Kikristo, mtume Paulo alilionya kutaniko hilo: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:12, 33) Paulo alimwonya Timotheo kwamba hata kati ya Wakristo wenzake, huenda kukawa na watu wanaojiendesha kwa njia isiyofaa. Timotheo aliambiwa ajiepushe kabisa na watu kama hao, asifanye urafiki wa karibu pamoja nao.—2 Timotheo 2:20-22.

14. Ni kwa njia gani tunaweza kutumia kanuni iliyo katika maonyo ambayo Paulo alitoa kuhusu mashirika?

14 Ni kwa njia gani tunaweza kutumia kanuni inayopatikana katika maonyo ya Paulo? Kwa kuepuka kushirikiana kwa ukaribu na mtu yeyote—ndani au nje ya kutaniko—ambaye anaweza kutupotosha. (2 Wathesalonike 3:6, 7, 14) Lazima tulinde hali yetu ya kiroho. Kumbuka kwamba kama sifongo, tunafyonza mitazamo na viwango vya marafiki wetu wa karibu. Kama vile hatuwezi kuitumbukiza sifongo ndani ya siki na kutazamia ijae maji, hatuwezi kushirikiana na watu waliopotoka na kutazamia watuchochee kutenda mema.—1 Wakorintho 5:6.

Unaweza kupata marafiki wanaofaa kati ya waabudu wenzako

15. Unaweza kufanya nini ili upate marafiki kutanikoni ambao wanahangaikia mambo ya kiroho?

15 Tunafurahi kwamba kuna uwezekano mkubwa sana wa kupata marafiki wanaofaa kati ya waabudu wenzetu. (Zaburi 133:1) Unaweza kufanya nini ili upate marafiki kutanikoni ambao wanahangaikia mambo ya kiroho? Kadiri unavyositawisha sifa na viwango vya Kikristo, wengine walio na sifa kama hizo watavutiwa nawe. Wakati huohuo, huenda ukahitaji kuchukua hatua ya kutafuta marafiki wapya. (Ona sanduku lenye kichwa “ Jinsi Tulivyopata Marafiki Wazuri.”) Tafuta wale walio na sifa ambazo ungependa kuwa nazo. Tii shauri la Biblia la ‘kupanuka,’ kwa kujitahidi kuanzisha urafiki pamoja na waamini wenzako hata wale wa jamii, taifa, au utamaduni tofauti. (2 Wakorintho 6:13; 1 Petro 2:17) Usitafute marafiki wa umri wako tu. Kumbuka kwamba Yonathani alikuwa na umri mkubwa sana kuliko Daudi. Watu wenye umri mkubwa wanaweza kuchangia hekima na uzoefu wao katika urafiki.

MATATIZO YANAPOTOKEA

16, 17. Mwabudu mwenzetu akiumiza hisia zetu, kwa nini hatupaswi kuacha kushirikiana na kutaniko?

16 Kwa kuwa kutanikoni kuna watu wenye nyutu na hali mbalimbali maishani, matatizo yanaweza kutokea mara kwa mara. Huenda mwamini mwenzetu akasema au kufanya jambo linaloumiza hisia zetu. (Methali 12:18) Nyakati nyingine matatizo yanatokea kwa sababu ya tofauti za nyutu, kutoelewana, au maoni yanayotofautiana. Je, tutakwazwa na matatizo hayo na kuacha kushirikiana na kutaniko? Hatuwezi kufanya hivyo ikiwa tunampenda Yehova kikweli na kuwapenda wale anaowapenda.

17 Akiwa Muumba wetu na Mtegemezaji wa uhai, Yehova anastahili upendo wetu na ujitoaji wetu kamili. (Ufunuo 4:11) Zaidi ya hilo, tunapaswa kuwa washikamanifu kwa kutaniko ambalo amechagua kulitumia. (Waebrania 13:17) Kwa hiyo, mwabudu mwenzetu akiumiza hisia zetu au kutuvunja moyo, hatutaacha kushirikiana na kutaniko ili kuonyesha kwamba tumekasirika. Ni jambo lisilowazika. Si Yehova aliyetukasirisha. Kwa kuwa tunampenda Yehova, hatuwezi kamwe kumgeuzia mgongo, yeye na watu wake!—Zaburi 119:165.

18. (a) Tunaweza kufanya nini ili kuendeleza amani katika kutaniko? (b) Tunapata faida gani tunapoamua kusamehe kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo?

18 Kuwapenda waabudu wenzetu kunatuchochea kuendeleza amani katika kutaniko. Yehova hadai ukamilifu kutoka kwa wale wanaompenda, nasi hatupaswi kufanya hivyo. Upendo unatuwezesha kuachilia makosa madogo-madogo, tukikumbuka kwamba sisi sote si wakamilifu na tunakosea. (Methali 17:9; 1 Petro 4:8) Upendo unatusaidia kuendelea “kusameheana kwa hiari.” (Wakolosai 3:13) Mara nyingi si rahisi kufuata shauri hilo. Tukiruhusu tushindwe na hisia zisizofaa, tunaweza kuweka kinyongo, labda tukifikiri kwamba hasira yetu inamwadhibu mkosaji kwa njia fulani. Hata hivyo, ukweli ni kwamba tunapoweka kinyongo tunajiumiza sisi wenyewe. Tunapata faida nyingi tunapoamua kusamehe kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. (Luka 17:3, 4) Tunapata amani ya akilini na ya moyoni, tunaendeleza amani katika kutaniko, na zaidi ya yote tunatunza uhusiano wetu pamoja na Yehova.—Mathayo 6:14, 15; Waroma 14:19.

WAKATI WA KUACHA KUSHIRIKIANA NA MTU FULANI

19. Ni wakati gani ambapo inaweza kuwa lazima tuache kushirikiana na mtu fulani?

19 Wakati mwingine tunaagizwa tuache kushirikiana na mshiriki fulani wa kutaniko. Hilo linatokea wakati mtu fulani aliyevunja sheria ya Mungu bila kutubu anapotengwa na ushirika au wakati mtu anapoikana imani kwa kufundisha uwongo au kujitenga na kutaniko. Neno la Mungu linatueleza waziwazi ‘tuache kuchangamana katika ushirika’ na watu kama hao. * (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Inaweza kuwa vigumu kumwepuka mtu wa ukoo au mtu ambaye alikuwa rafiki yetu. Je, tutasimama imara, na hivyo kuonyesha kwamba tunauona ushikamanifu wetu kwa Yehova na sheria zake za uadilifu kuwa wa maana zaidi? Kumbuka kwamba Yehova anaona ushikamanifu na utii kuwa wa maana sana.

20, 21. (a) Kwa nini kutenga na ushirika ni mpango wenye upendo? (b) Kwa nini tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa hekima?

20 Kwa hakika, mpango wa kutenga na ushirika ni mpango wenye upendo wa Yehova. Kwa nini? Kumwondoa mtenda-dhambi asiyetubu kunaonyesha kwamba tunampenda Yehova, jina lake takatifu, na viwango vyake. (1 Petro 1:15, 16) Mpango wa kutenga na ushirika unalinda kutaniko. Washiriki waaminifu wanalindwa kutokana na uvutano wa watu wanaotenda dhambi kimakusudi na wanaweza kuendelea na ibada yao wakijua kwamba kutaniko ni mahali salama katika ulimwengu huu mbovu. (1 Wakorintho 5:7; Waebrania 12:15, 16) Nidhamu hiyo ni wonyesho wa upendo kwa mkosaji. Pengine hilo ndilo jambo linaloweza kumwamsha arudiwe na fahamu na kuchukua hatua zinazohitajiwa ili kumrudia Yehova.—Waebrania 12:11.

21 Bila shaka, marafiki wetu wa karibu wana uvutano wenye nguvu juu yetu. Basi, tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa hekima. Kwa kufanya urafiki pamoja na marafiki wa Yehova, yaani, ikiwa tutawapenda wale ambao Mungu anawapenda, tutakuwa na marafiki bora zaidi. Mambo tunayofyonza kutoka kwao yatatusaidia kutimiza azimio letu la kumpendeza Yehova.

^ fu. 2 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘kushirikiana na’ linaweza pia kutafsiriwa ‘kuwa mwenzi wa,’ au ‘kufanya urafiki.’—Waamuzi 14:20; Methali 22:24, Verbum Bible.

^ fu. 4 Kwa kumwomba Abrahamu afanye hivyo, Yehova alitangulia kuonyesha dhabihu ambayo yeye mwenyewe angeandaa kwa kumtoa Mwana wake mzaliwa-pekee. (Yohana 3:16) Katika kisa cha Abrahamu, Yehova aliingilia kati na kuandaa kondoo-dume ambaye angetolewa badala ya Isaka.—Mwanzo 22:1, 2, 9-13.

^ fu. 9 Daudi alikuwa kijana—“mvulana tu”—alipomuua Goliathi, na alikuwa na umri wa miaka 30 hivi Yonathani alipokufa. (1 Samweli 17:33; 31:2; 2 Samweli 5:4) Yonathani, ambaye alikuwa na umri wa miaka 60 hivi alipokufa, alikuwa amemzidi Daudi kwa miaka 30 hivi.

^ fu. 10 Kama inavyoonyeshwa katika 1 Samweli 23:17, Yonathani alisema mambo matano ili kumtia moyo Daudi: (1) Alimsihi Daudi asiogope. (2) Alimhakikishia Daudi kwamba Sauli hangefanikiwa. (3) Alimkumbusha Daudi kwamba atapokea ufalme, kama Mungu alivyoahidi. (4) Aliahidi kwamba atakuwa mshikamanifu kwa Daudi. (5) Alimwambia Daudi kwamba hata Sauli anajua kwamba yeye ni mshikamanifu kwa Daudi.

^ fu. 19 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu jinsi ya kuwatendea watu waliotengwa au waliojitenga na ushirika, katika nyongeza “Jinsi ya Kushughulika na Mtu Aliyetengwa na Ushirika.”