Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 6

Jinsi ya Kuchagua Burudani Inayofaa

Jinsi ya Kuchagua Burudani Inayofaa

“Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 WAKORINTHO 10:31.

1, 2. Tunapaswa kufanya uamuzi gani kuhusu burudani?

WAZIA kwamba unakula matunda. Unachukua tunda moja linaloonekana kuwa tamu wee! Kabla tu ya kuliuma, unagundua kwamba sehemu fulani imeoza. Utafanya nini? Unaweza kula tunda lote, kutia ndani sehemu iliyooza; unaweza kulitupa lote, pamoja na sehemu iliyooza; au unaweza kukata sehemu iliyooza na ufurahie kula sehemu nzuri. Utafanya nini?

2 Kwa njia fulani, burudani ni kama tunda hilo. Nyakati nyingine, unataka kujiburudisha, lakini unatambua kwamba burudani nyingi zilizopo leo ni mbovu kiadili, na hata zimeoza. Basi, utafanya nini? Huenda wengine wakapuuza kilicho kiovu na kumeza burudani yoyote ile inayopatikana ulimwenguni. Huenda wengine wakaepuka burudani zote ili kuhakikisha kwamba hawaathiriwi na zile zenye madhara. Na huenda wengine wakaepuka burudani zenye madhara, lakini mara kwa mara wanafurahia burudani zinazofaa kwa kiasi fulani. Unapaswa kufanya uamuzi gani ili uendelee kujitunza katika upendo wa Mungu?

3. Tutachunguza nini sasa?

3 Wengi wetu wangechagua jambo la tatu. Tunatambua uhitaji wa kuwa na burudani lakini tunaweka mipaka ili tusijihusishe katika burudani isiyofaa. Kwa hiyo, tunahitaji kufikiria jinsi tunavyoweza kutambua burudani inayofaa na isiyofaa. Hata hivyo, kwanza, acheni tuzungumzie jinsi burudani tunayochagua inavyoweza kuathiri ibada tunayomtolea Yehova.

“FANYENI MAMBO YOTE KWA UTUKUFU WA MUNGU”

4. Wakfu wetu unaweza kutuongoza jinsi gani tunapochagua burudani?

4 Wakati fulani uliopita, Shahidi mmoja aliyebatizwa mwaka wa 1946, alisema: “Nimehakikisha kwamba ninakuwapo wakati wa kila hotuba ya ubatizo na kusikiliza kwa makini kana kwamba ni mimi ninayebatizwa.” Kwa nini? Alisema hivi: “Kuendelea kufikiria wakfu wangu kumenisaidia kubaki mwaminifu.” Hapana shaka kwamba utakubaliana na maneno hayo. Kujikumbusha kwamba ulimwahidi Yehova kuwa utatumia maisha yako yote kumtumikia kunakuchochea kuvumilia. (Mhubiri 5:4; Waebrania 10:7) Kwa hakika, kutafakari kuhusu wakfu wako kutakuwa na uvutano juu ya maoni yako kuhusu huduma ya Kikristo na vilevile shughuli nyingine maishani mwako, kutia ndani burudani. Mtume Paulo alikazia jambo hilo alipowaandikia Wakristo wa siku zake: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

5. Andiko la Mambo ya Walawi 22:18-20 linatusaidia jinsi gani kuelewa Waroma 12:1?

5 Kila kitu unachofanya maishani kinahusiana na ibada yako kwa Yehova. Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alitumia maneno yenye nguvu ili kukazia jambo hilo kwa waamini wenzake. Aliwasihi: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.” (Waroma 12:1) Mwili wako unatia ndani akili yako, moyo wako, na nguvu zako. Unatumia vitu vyote hivyo unapomtumikia Mungu. (Marko 12:30) Paulo anataja utumishi huo wa nafsi yote kuwa dhabihu. Anapotumia neno “dhabihu,” anatoa onyo lisilo la moja kwa moja. Chini ya Sheria ya Musa, Mungu alikataa dhabihu yoyote yenye kasoro. (Mambo ya Walawi 22:18-20) Vivyo hivyo, dhabihu ya kiroho ya Mkristo ikiwa na kasoro fulani, Mungu ataikataa. Hilo linawezekanaje?

6, 7. Mkristo anaweza kuchafua mwili wake jinsi gani, na matokeo yanaweza kuwa nini?

6 Paulo aliwashauri hivi Wakristo huko Roma: “Msiendelee kuvitoa viungo vyenu [“hata sehemu moja ya miili yenu,” Biblia Habari Njema] kwa dhambi.” Pia, Paulo aliwaambia ‘waue mazoea ya mwili.’ (Waroma 6:12-14; 8:13) Mapema katika barua yake, alikuwa ametoa mifano kuhusu “mazoea [hayo] ya mwili.” Tunasoma hivi kuhusu wanadamu wenye dhambi: “Kinywa chao kimejaa kulaani.” “Miguu yao inaharakisha kwenda kumwaga damu.” “Hakuna kumwogopa Mungu mbele ya macho yao.” (Waroma 3:13-18) Mkristo atatia doa mwili wake ikiwa atatumia “viungo” vyake, au sehemu za mwili, kutenda dhambi. Kwa mfano, Mkristo akitazama kimakusudi mambo machafu kama ponografia (picha au habari za ngono) au kutazama jeuri yenye ukatili, ‘anayatoa macho yake kwa dhambi’ na hivyo anachafua mwili wake wote. Ibada yoyote anayotoa si dhabihu takatifu na haikubaliki machoni pa Mungu. (Kumbukumbu la Torati 15:21; 1 Petro 1:14-16; 2 Petro 3:11) Hayo ni matokeo mabaya kama nini ya kuchagua burudani isiyofaa!

7 Ni wazi kwamba kuchagua burudani ni jambo zito kwa Mkristo. Basi, kwa hakika tunataka kuchagua burudani itakayoboresha dhabihu tunayomtolea Mungu badala ya kuitia kasoro. Acheni sasa tuzungumzie jinsi tunavyoweza kutambua burudani inayofaa na isiyofaa.

“CHUKIENI MAOVU”

8, 9. (a) Kwa ujumla, kuna aina gani mbili za burudani? (b) Sisi hukataa burudani gani, na kwa nini?

8 Kwa ujumla, kuna aina mbili za burudani. Aina moja ni burudani ambazo Wakristo wanapaswa kuepuka; aina ya pili ni burudani ambazo huenda Wakristo wakahitaji kujifanyia uamuzi. Acheni kwanza tuzungumzie aina ya kwanza, yaani, burudani ambazo Wakristo wanaepuka.

9 Kama ilivyotajwa katika Sura ya 1, burudani fulani hutia ndani mambo ambayo Biblia inashutumu waziwazi. Kwa mfano, fikiria vituo vya Intaneti, sinema, programu za televisheni, na muziki, na burudani nyingine kama hizo zinazotia ndani ukatili, mambo ya kishetani, ponografia, au mazoea mengine mapotovu na yenye kuchukiza. Kwa kuwa burudani hizo zinaonyesha mambo ambayo hayapatani na kanuni au sheria za Biblia kuwa yenye kufurahisha, Wakristo wa kweli wanapaswa kuziepuka. (Matendo 15:28, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Kwa kukataa burudani hizo zisizofaa, unamwonyesha Yehova kwamba kwa kweli ‘unachukia maovu’ na kwamba sikuzote ‘unageuka kutoka katika yaliyo mabaya.’ Kwa kufanya hivyo, unaonyesha kwamba una “imani bila unafiki.”—Waroma 12:9; Zaburi 34:14; 1 Timotheo 1:5.

10. Ni maoni gani kuhusu burudani ambayo ni hatari, na kwa nini?

10 Hata hivyo, huenda wengine wakafikiri kwamba hakuna madhara yoyote yanayoweza kutokea kwa kutazama burudani zinazoonyesha waziwazi mambo mapotovu. Huenda wakasema hivi, ‘Mimi hutazama tu mambo hayo katika sinema au televisheni, lakini siwezi kamwe kuyafanya.’ Kuwa na maoni kama hayo ni kujidanganya na ni hatari. (Yeremia 17:9) Ikiwa tunafurahia kutazama mambo ambayo Yehova anashutumu, je, kweli ‘tunachukia maovu’? Kuzoea kutazama mambo maovu kunaweza kufanya fahamu zetu zife ganzi. (Zaburi 119:70; 1 Timotheo 4:1, 2) Mazoea hayo yanaweza kuathiri matendo yetu au jinsi tunavyoona mwenendo wenye dhambi wa wengine.

11. Maneno ya Wagalatia 6:7 yamethibitika kuwa kweli jinsi gani kuhusiana na burudani?

11 Kwa kweli, wengine wamejikuta katika hali kama hiyo. Wakristo fulani wametenda mambo yaliyopotoka kwa sababu waliathiriwa na burudani waliyozoea kutazama. Wamejionea ukweli wa maneno haya: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Wagalatia 6:7) Lakini majuto hayo yanaweza kuepukwa. Ukipanda mambo yaliyo safi katika akili yako, utavuna kwa shangwe mambo mazuri katika maisha yako.—Ona sanduku “ Ni Burudani Gani Inayofaa?

MAAMUZI YA KIBINAFSI YANAYOTEGEMEA KANUNI ZA BIBLIA

12. Andiko la Wagalatia 6:5 linaweza kutumiwa namna gani kuhusu burudani, nasi tuna mwongozo gani unaoweza kutusaidia kufanya maamuzi ya kibinafsi?

12 Acheni sasa tuzungumzie aina ya pili—burudani zinazoonyesha mambo ambayo Neno la Mungu halishutumu moja kwa moja wala kuyakubali waziwazi. Anapochagua burudani za aina hiyo, kila Mkristo anapaswa kujiamulia kile anachoona kuwa kinafaa. (Wagalatia 6:5) Hata hivyo, tuna mwongozo unaotusaidia kufanya uamuzi huo. Biblia ina kanuni au kweli za msingi zinazotusaidia kufahamu maoni ya Yehova. Kufikiria kanuni hizo kutatuwezesha kufahamu “yale yaliyo mapenzi ya Yehova” katika mambo yote, kutia ndani burudani tunayochagua.—Waefeso 5:17.

13. Ni nini kitakachotuchochea kuepuka burudani zinazoweza kumchukiza Yehova?

13 Bila shaka, si Wakristo wote ambao wamesitawisha kwa kiwango kilekile utambuzi au uwezo wa kufanya maamuzi yanayohusu maadili. (Wafilipi 1:9) Pia, Wakristo wanatambua kwamba mapendezi yao ya burudani yanatofautiana. Kwa hiyo, haitazamiwi kwamba Wakristo wote watafanya maamuzi yaleyale. Hata hivyo, kadiri tunavyoruhusu kanuni za Mungu ziongoze akili na mioyo yetu, ndivyo tutakavyotaka zaidi kuepuka burudani zozote zinazoweza kumchukiza Yehova.—Zaburi 119:11, 129; 1 Petro 2:16.

14. (a) Tunapaswa kufikiria jambo gani tunapochagua burudani? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kutanguliza mambo ya Ufalme maishani?

14 Unapochagua burudani, kuna jambo lingine la maana ambalo unahitaji kufikiria: wakati wako. Aina ya burudani unayochagua huonyesha kile unachoona kuwa kinafaa, nao wakati unaotumia katika burudani hiyo unaonyesha kile unachoona kuwa cha maana. Kwa Wakristo, mambo ya kiroho ndiyo ya maana zaidi. (Mathayo 6:33) Basi, unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba unatanguliza mambo ya Ufalme maishani? Mtume Paulo alisema: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa.” (Waefeso 5:15, 16) Kwa kweli, kuamua muda hususa unaoweza kutumia katika burudani kutakusaidia kuwa na wakati kwa ajili ya “mambo yaliyo ya maana zaidi”—mambo yatakayokujenga kiroho.—Wafilipi 1:10.

15. Tunapochagua burudani, kwa nini ni jambo la hekima kutoacha nafasi yoyote kwa ajili ya burudani isiyofaa?

15 Tunapochagua burudani, ni jambo la hekima pia kuhakikisha kwamba hatujaacha nafasi yoyote kwa ajili ya burudani isiyofaa. Hiyo inamaanisha nini? Fikiria tena ule mfano wa tunda. Ili kuepuka kula bila kujua sehemu iliyooza, hutakata sehemu iliyooza tu bali pia sehemu fulani inayoizunguka. Vivyo hivyo, ni jambo la hekima kuhakikisha kwamba hatuachi nafasi yoyote kwa ajili ya burudani isiyofaa. Mkristo mwenye hekima haepuki tu burudani ambazo zinavunja waziwazi kanuni za Biblia bali anaepuka pia zile zenye kutilika shaka au zile ambazo huenda zikawa na mambo yanayoweza kuharibu uhusiano wake pamoja na Yehova. (Methali 4:25-27) Kufuata kwa ukaribu mashauri ya Neno la Mungu kutakusaidia kufanya hivyo.

“MAMBO YOYOTE YALIYO SAFI KIADILI”

Kutumia kanuni za Mungu tunapochagua burudani hutulinda kutokana na hatari ya kiroho

16. (a) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuna maoni kama ya Yehova kuhusu maadili? (b) Ni nini ambacho kitakuchochea kutumia kanuni za Biblia kila siku maishani?

16 Wanapochagua burudani, Wakristo wa kweli hufikiria maoni ya Yehova kwanza. Biblia inaonyesha maoni na viwango vya Yehova. Kwa mfano, Mfalme Sulemani anataja vitu ambavyo Yehova anachukia, kama vile “ulimi wa uwongo, na mikono inayomwaga damu isiyo na hatia, moyo unaotunga hila zenye kuumiza, miguu iliyo myepesi kukimbilia ubaya.” (Methali 6:16-19) Maoni ya Yehova yanapaswa kukuchochea kufanya nini? Mtunga-zaburi anatuhimiza: “Enyi mnaompenda Yehova, chukieni yaliyo mabaya.” (Zaburi 97:10) Burudani unazochagua zinapaswa kuonyesha kwamba kwa kweli unachukia vitu ambavyo Yehova anachukia. (Wagalatia 5:19-21) Pia, kumbuka kwamba si mambo unayofanya ukiwa mbele za watu, bali yale unayofanya ukiwa peke yako ndiyo yanayoonyesha wewe ni mtu wa aina gani. (Zaburi 11:4; 16:8) Hivyo, ikiwa unatamani kutoka moyoni kuongozwa na maoni ya Yehova kuhusu mambo ya kiadili katika sehemu zote za maisha yako, sikuzote utafanya maamuzi yanayopatana na kanuni za Biblia. Hiyo itakuwa njia yako ya maisha.—2 Wakorintho 3:18.

17. Kabla ya kuchagua burudani, tunapaswa kujiuliza nini?

17 Ni mambo gani mengine unayoweza kufanya ili kuhakikisha kwamba unatenda kulingana na maoni ya Yehova unapochagua burudani? Jiulize, ‘Jambo hili linaweza kuwa na matokeo gani juu yangu na juu ya msimamo wangu pamoja na Mungu?’ Kwa mfano, kabla ya kuamua kutazama sinema fulani, jiulize, ‘Mambo yanayoonyeshwa katika sinema hii yatakuwa na matokeo gani kwa dhamiri yangu?’ Acheni tufikirie kanuni zinazohusika.

18, 19. (a) Kanuni ya Wafilipi 4:8 inaweza kutusaidia jinsi gani kuamua ikiwa burudani yetu inafaa? (b) Ni kanuni gani nyingine zinazoweza kukusaidia kuchagua burudani inayofaa? (Ona maelezo ya chini.)

18 Kanuni moja ya maana inapatikana katika Wafilipi 4:8, ambayo inasema: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.” Ni kweli kwamba Paulo hakuwa akizungumzia burudani, bali kutafakari kwa moyo ambako kunapaswa kupatana na mapenzi ya Mungu. (Zaburi 19:14) Hata hivyo, maneno ya Paulo yanaweza kutupa kanuni ambayo tunaweza kutumia kuhusiana na burudani. Jinsi gani?

19 Jiulize, ‘Je, sinema, michezo ya video, miziki, au burudani nyinginezo ninazochagua zinajaza akili yangu “mambo yoyote yaliyo safi kiadili”?’ Kwa mfano, baada ya kutazama sinema, unabaki na picha gani akilini? Ikiwa zinapendeza, ni safi, na zinaburudisha akili, basi utajua kwamba burudani uliyochagua inafaa. Hata hivyo, ikiwa sinema uliyotazama inakufanya ufikirie mambo yasiyo safi kiadili, basi burudani uliyochagua haikufaa na ni hatari. (Mathayo 12:33; Marko 7:20-23) Kwa nini? Kwa sababu kufikiria mambo yasiyo safi kiadili kunavuruga amani yako ya akili, kunachafua dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia, na kunaweza kuharibu uhusiano wako pamoja na Mungu. (Waefeso 5:5; 1 Timotheo 1:5, 19) Kwa kuwa burudani kama hiyo inakuhatarisha wewe binafsi, azimia kuiepuka. * (Waroma 12:2) Uwe kama mtunga-zaburi aliyemwomba Yehova: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.”—Zaburi 119:37.

TAFUTA FAIDA ZA WENGINE

20, 21. Andiko la 1 Wakorintho 10:23, 24 linahusika jinsi gani katika kuchagua burudani zinazofaa?

20 Paulo alitaja kanuni muhimu ya Biblia inayopaswa kufikiriwa tunapofanya maamuzi kuhusu mambo ya kibinafsi. Alisema: “Mambo yote ni halali; lakini si mambo yote yanayojenga. Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:23, 24) Kanuni hiyo inahusika jinsi gani katika kuchagua burudani inayofaa? Unahitaji kujiuliza, ‘Burudani ninayochagua inaweza kuwaathiri wengine jinsi gani?’

21 Huenda dhamiri yako ikakuruhusu ufurahie burudani fulani unazoona kuwa “halali” au zenye kukubalika. Hata hivyo, ukitambua kwamba waamini wengine wana dhamiri ambazo haziwaruhusu kufurahia burudani kama hizo, unaweza kuamua kuiepuka. Kwa nini? Kwa sababu hungependa ‘kutenda dhambi juu ya ndugu zako’—au hata ‘kumtendea dhambi Kristo,’ kama Paulo alivyosema—kwa kufanya iwe vigumu kwa waamini wenzako kudumisha uaminifu kwa Mungu. Unatii himizo hili: “Epukeni kuwa vikwazo.” (1 Wakorintho 8:12; 10:32) Wakristo wa kweli leo wanatii shauri la Paulo lenye upendo na busara kwa kuepuka burudani ambazo ‘hazijengi’ ingawa huenda zikawa “halali.”—Waroma 14:1; 15:1.

22. Kwa nini Wakristo hawawalazimishi wengine wafuate maoni yao katika mambo ya kibinafsi?

22 Hata hivyo, kuna jambo lingine linalohusika katika kutafuta faida za wengine. Mkristo ambaye dhamiri yake haimruhusu kufanya mambo fulani hapaswi kusisitiza kwamba wote katika kutaniko la Kikristo wafuate maoni yake kuhusu burudani inayofaa. Ikiwa atafanya hivyo, atakuwa kama dereva anayesisitiza madereva wengine wote wanaotumia barabara ileile anayotumia waendeshe gari kwa mwendo anaotaka. Hayo si maoni yenye usawaziko. Upendo wa Kikristo utamchochea mtu ambaye dhamiri yake haimruhusu kushiriki katika mambo fulani, kuwaheshimu waamini wenzake ambao maoni yao kuhusu burudani ni tofauti kwa kadiri fulani ingawa hayavunji kanuni za Kikristo. Kwa kufanya hivyo, anaacha ‘usawaziko wake ujulikane kwa watu wote.’—Wafilipi 4:5; Mhubiri 7:16.

23. Unaweza kufanya nini ili kuhakikisha unachagua burudani inayofaa?

23 Kwa ufupi, unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba unachagua burudani inayofaa? Kataa katakata burudani yoyote inayotia ndani mambo mapotovu ambayo Neno la Mungu linayashutumu waziwazi. Fuata kanuni za Biblia zinazoweza kutumika kuhusiana na burudani ambazo hazitajwi moja kwa moja katika Biblia. Epuka burudani inayochafua dhamiri yako na uwe tayari kuacha burudani zote zinazoweza kusumbua dhamiri za wengine, hasa waamini wenzako. Azimio lako thabiti la kufanya hivyo na limletee Mungu utukufu na kukutunza wewe na familia yako katika upendo wake.

^ fu. 19 Kanuni nyingine zinazohusu burudani zinapatikana katika Methali 3:31; 13:20; Waefeso 5:3, 4; na Wakolosai 3:5, 8, 20.