Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 8

Mungu Anawapenda Watu Walio Safi

Mungu Anawapenda Watu Walio Safi

“Kwa mtu anayebaki safi utakuwa safi.”—ZABURI 18:26.

1-3. (a) Kwa nini mama huhakikisha kwamba mwana wake ni nadhifu na safi? (b) Kwa nini Yehova anataka waabudu wake wawe safi, na ni nini kinachotuchochea tutake kuendelea kuwa safi?

MAMA anamtayarisha mwana wake ili waende mahali fulani. Anahakikisha ameoga na nguo zake ni nadhifu na safi. Anajua kwamba usafi ni wa maana ili mwana wake awe na afya nzuri. Pia, anatambua kwamba sura ya mwana wake inaweza kuwaletea wazazi wake sifa au aibu.

2 Yehova, Baba yetu wa mbinguni, anataka watumishi wake wawe safi. Neno lake linasema: “Kwa mtu anayebaki safi utakuwa safi.” * (Zaburi 18:26) Yehova anatupenda; anajua kwamba kuendelea kuwa safi ni kwa faida yetu. Pia, anataka sisi Mashahidi wake tumletee sifa kupitia mwenendo wetu. Ndiyo, badala ya kumletea suto, usafi na mwenendo wetu mzuri humletea utukufu Yehova na jina lake takatifu.—Ezekieli 36:22; 1 Petro 2:12.

3 Kujua kwamba Mungu anawapenda watu walio safi kunatuchochea kuendelea kuwa safi. Tunataka maisha yetu yamletee sifa kwa sababu tunampenda. Tunataka pia kukaa katika upendo wake. Basi, acheni tuchunguze kwa nini tunahitaji kuendelea kuwa safi, maana ya kuwa safi, na jinsi tunavyoweza kuendelea kuwa safi. Kufanya hivyo kunaweza kutusaidia kutambua ikiwa tunahitaji kufanya maendeleo.

KWA NINI TUNAHITAJI KUENDELEA KUWA SAFI?

4, 5. (a) Taja sababu kuu ya kuendelea kuwa safi. (b) Ni kwa njia gani uumbaji unaonyesha usafi wa Yehova?

4 Njia moja ambayo Yehova anatumia kutuongoza ni kupitia mfano wake. Hivyo, Neno lake linatusihi kuwa “waigaji wa Mungu.” (Waefeso 5:1) Sababu kuu ya kuendelea kuwa safi ni hii: Yehova, Mungu tunayemwabudu, ni safi na ni mtakatifu katika kila njia.—Mambo ya Walawi 11:44, 45.

5 Usafi wa Yehova, kama vile sifa zake na njia zake nyingi, unaonekana katika uumbaji. (Waroma 1:20) Dunia iliumbwa iwe makao safi ya wanadamu. Yehova ameweka mifumo ya asili inayosafisha hewa na maji. Vijidudu fulani hugeuza takataka kuwa vitu visivyo na madhara. Wanasayansi wametumia baadhi ya vijidudu hivyo kusafisha mafuta yaliyomwagika baharini na uchafu mwingine unaotokana na ubinafsi na pupa ya mwanadamu. Ni wazi kwamba “Mtengenezaji wa dunia” anaona usafi kuwa jambo la maana. (Yeremia 10:12) Tunapaswa kuwa na maoni hayo pia.

6, 7. Ni kwa njia gani Sheria ya Musa ilikazia kwamba wale wanaomwabudu Yehova wanapaswa kuwa safi?

6 Sababu nyingine ya kuendelea kuwa safi ni kwamba Yehova, Mtawala wetu, anataka waabudu wake wawe safi. Chini ya Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli, usafi ulihusianishwa sana na ibada. Sheria iliagiza kwamba katika Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu alipaswa kuoga si mara moja bali mara mbili. (Mambo ya Walawi 16:4, 23, 24) Makuhani waliotumikia walipaswa kunawa mikono na miguu kabla ya kumtolea Yehova dhabihu. (Kutoka 30:17-21; 2 Mambo ya Nyakati 4:6) Sheria ilitaja mambo 70 yaliyomfanya mtu asiwe safi kimwili au kwa ajili ya sherehe za kiibada. Wakati ambapo hakuwa safi, Mwisraeli hangeweza kushiriki katika ibada, na ikiwa angeshiriki, katika visa fulani hata angeuawa. (Mambo ya Walawi 15:31) Yeyote ambaye angekataa kufuata utaratibu uliowekwa wa kujitakasa, kutia ndani kuoga na kufua nguo, alipaswa ‘kukatiliwa mbali kutoka katikati ya kutaniko.’—Hesabu 19:17-20.

7 Ingawa hatuko chini ya Sheria ya Musa, sheria hiyo inatusaidia kuelewa maoni ya Mungu kuhusu mambo. Kwa wazi, Sheria ilikazia kwamba wale wanaomwabudu Mungu wanapaswa kuwa safi. Yehova habadiliki. (Malaki 3:6) Ibada yetu isipokuwa “safi na isiyotiwa unajisi,” hawezi kuikubali. (Yakobo 1:27) Hivyo basi, tunahitaji kujua yale ambayo anatazamia tufanye kuhusiana na jambo hilo.

KUWA SAFI MACHONI PA MUNGU KUNAMAANISHA NINI?

8. Yehova anataka tuwe safi katika njia gani?

8 Katika Biblia, usafi unatia ndani mengi zaidi ya usafi wa kimwili. Kuwa safi machoni pa Mungu kunahusisha sehemu zote za maisha yetu. Yehova anataka tuwe safi katika njia nne kuu—kiroho, kiadili, kiakili, na kimwili. Acheni tuzungumzie kila moja ya njia hizo.

9, 10. Inamaanisha nini kuendelea kuwa safi kiroho, na Wakristo wa kweli huepuka nini?

9 Usafi wa kiroho. Kwa ufupi, kuendelea kuwa safi kiroho kunamaanisha kuepuka kuchanganya ibada ya kweli na ya uwongo. Waisraeli walipoondoka Babiloni ili kurudi Yerusalemu, walipaswa kutii himizo hili lililoongozwa na roho: “Tokeni humo, msiguse kitu chochote kilicho najisi; . . . jiwekeni safi.” (Isaya 52:11) Waisraeli walikuwa wanarudi nyumbani ili hasa kuirudisha ibada ya Yehova. Ibada hiyo ilipaswa kuwa safi, isiyotiwa unajisi wowote kutokana na mafundisho, mazoea, au desturi zozote zinazomvunjia Mungu heshima zilizotokana na dini za Babiloni.

10 Leo, sisi Wakristo wa kweli tunapaswa kujihadhari tusitiwe unajisi na dini ya uwongo. (1 Wakorintho 10:21) Tunapaswa kuwa macho kwa sababu uvutano wa dini ya uwongo umeenea sana. Katika nchi nyingi, utamaduni, shughuli, na desturi nyingi zinahusianishwa na mafundisho ya dini za uwongo, kama vile maoni ya kwamba kitu fulani ndani yetu huendelea kuishi baada ya mwili kufa. (Mhubiri 9:5, 6, 10) Wakristo wa kweli huepuka desturi zinazohusisha imani ya dini za uwongo. * Hatutaruhusu wengine watulazimishe kuacha kufuata viwango vya Biblia vya ibada safi.—Matendo 5:29.

11. Usafi wa kiadili unatia ndani nini, na kwa nini ni muhimu kuendelea kuwa safi kwa njia hiyo?

11 Usafi wa kiadili. Kuendelea kuwa safi kiadili kunatia ndani kuepuka upotovu wowote wa kingono. (Waefeso 5:5) Ni muhimu kuwa safi kiadili. Kama tutakavyoona katika sura inayofuata ya kitabu hiki, ili tukae katika upendo wa Mungu, lazima ‘tuukimbie uasherati.’ Waasherati wasiotubu “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10, 18) Machoni pa Mungu, watu hao ni kati ya wale wenye “kuchukiza katika uchafu wao.” Wasipojisafisha kiadili, “fungu lao litakuwa . . . kifo cha pili.”—Ufunuo 21:8.

12, 13. Kuna uhusiano gani kati ya mawazo na matendo, na tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuwa safi kiakili?

12 Usafi wa kiakili. Mawazo huongoza kwenye matendo. Tukiruhusu mawazo mabaya yatie mizizi katika akili na mioyo yetu, muda si muda tunaweza kutenda mambo machafu. (Mathayo 5:28; 15:18-20) Lakini tukijaza akili zetu mambo yaliyo safi, tunaweza kuchochewa kuendelea kuwa na mwenendo safi. (Wafilipi 4:8) Tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuwa safi kiakili? Kwanza, tunahitaji kuepuka burudani zozote zinazoweza kuchafua fikira zetu. * Pia, tunaweza kujaza akili zetu mambo yaliyo safi kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida.—Zaburi 19:8, 9.

13 Ili tukae katika upendo wa Mungu, tunapaswa kuendelea kuwa safi kiroho, kiadili, na kiakili. Mambo hayo yanazungumziwa kwa mapana na marefu katika sura nyingine za kitabu hiki. Acheni sasa tukazie fikira jambo la nne kuhusiana na usafi, yaani, usafi wa kimwili.

JINSI YA KUENDELEA KUWA SAFI KIMWILI

14. Kwa nini usafi wa kimwili si jambo la kibinafsi tu?

14 Usafi wa kimwili unatia ndani kutunza mwili wetu na mazingira yakiwa safi. Je, usafi huo ni jambo la kibinafsi ambalo watu wengine hawapaswi kuingilia? Waabudu wa Yehova hawapaswi kuwa na maoni hayo. Kama ilivyokwisha kutajwa, usafi wa kimwili ni jambo la maana machoni pa Yehova si kwa sababu ni kwa faida yetu tu bali pia kwa sababu tunamwakilisha. Fikiria mfano uliotajwa mwanzoni. Unapomwona mtoto ambaye sikuzote ni mchafu, huenda ukajiuliza, ‘Kwani wazazi wake ni watu wa aina gani?’ Hatungependa jambo lolote kuhusu sura yetu au maisha yetu lichafue jina la Baba yetu wa mbinguni au kufanya ujumbe tunaohubiri udharauliwe. Neno la Mungu linasema: “Sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza kwa njia yoyote, ili huduma yetu isilaumiwe; bali katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu.” (2 Wakorintho 6:3, 4) Basi, tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa safi kimwili?

15, 16. Mazoea mazuri ya usafi yanatia ndani nini, na mavazi yetu yanapaswa kuwa katika hali gani?

15 Kutunza mwili na sura yetu. Ingawa desturi na hali zinatofautiana katika nchi mbalimbali, kwa ujumla, tunaweza kupata sabuni na maji ya kutosha ili kuoga kwa ukawaida na kuhakikisha kwamba sisi na watoto wetu ni safi. Mazoea mazuri ya usafi yanatia ndani kunawa mikono kwa maji na sabuni kabla ya kula au kutayarisha chakula, baada ya kutoka msalani, na baada ya kumwosha mtoto au kubadili nepi (kitambaa cha kuzuia choo cha mtoto). Kunawa kwa sabuni na maji kunaweza kuzuia ugonjwa na kuokoa uhai. Kunaweza kuzuia kuenea kwa viini hatari vinavyosababisha magonjwa, na hivyo kuwaepusha watu na magonjwa ya kuharisha. Katika maeneo ambayo hayana vyoo, takataka zinaweza kuzikwa kama ilivyokuwa katika Israeli la kale.—Kumbukumbu la Torati 23:12, 13.

16 Mavazi yetu pia yanapaswa kufuliwa kwa ukawaida ili yawe safi na yenye kupendeza. Si lazima nguo za Mkristo ziwe za bei ghali au za mtindo wa kisasa, lakini zinapaswa kuwa nadhifu, safi, na zenye kiasi. (1 Timotheo 2:9, 10) Popote tulipo, sura yetu inapaswa ‘kulipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.’—Tito 2:10.

17. Kwa nini makao na mazingira yetu yanapaswa kuwa safi na yenye kupendeza?

17 Makao na mazingira yetu. Huenda makao yetu yasiwe ya kifahari au ya anasa, lakini yanapaswa kuwa safi na yenye kupendeza kadiri hali zinavyoruhusu. Vivyo hivyo, ikiwa tunatumia gari kwenda kwenye mikutano na katika huduma ya shambani, tunaweza kufanya yote tuwezayo kuhakikisha kwamba liko safi, ndani na nje. Tusisahau kwamba makao na mazingira safi ni njia moja ya kutoa ushahidi. Nasi tunawafundisha watu kwamba Yehova ni Mungu safi, ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ na hivi karibuni Ufalme wake utaifanya dunia yetu kuwa paradiso. (Ufunuo 11:18; Luka 23:43) Kwa kweli, tunataka makao yetu na mali zetu ziwe ushuhuda kwa wengine kwamba hata sasa tunajizoeza usafi utakaohitajika katika ulimwengu mpya unaokuja.

Usafi wa kimwili unatia ndani kuhakikisha kwamba mwili wetu na mazingira yetu ni safi

18. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba tunaheshimu Jumba letu la Ufalme?

18 Mahali petu pa ibada. Kumpenda Yehova kunatuchochea kuheshimu Jumba letu la Ufalme, kituo cha ibada ya kweli katika eneo letu. Wapya wanapokuja kwenye jumba hilo, tunataka wavutiwe na mahali petu pa kukutania. Jumba hilo linahitaji kusafishwa na kutunzwa kwa ukawaida ili kuhakikisha kwamba linavutia na kupendeza nyakati zote. Tunaheshimu Jumba letu la Ufalme kwa kufanya yote tuwezayo ili kuhakikisha kwamba liko katika hali nzuri. Ni pendeleo kutumia wakati wetu kusaidia katika kusafisha, ‘kutengeneza, na kurekebisha’ mahali petu pa ibada. (2 Mambo ya Nyakati 34:10) Kanuni hizohizo zinatumika tunapokusanyika katika Jumba la Kusanyiko au mahali pengine panapotumika kwa ajili ya makusanyiko.

KUONDOLEA MBALI TABIA NA MAZOEA MACHAFU

19. Ili tuwe safi kimwili, tunapaswa kuepuka nini, na Biblia inatusaidia jinsi gani kufanya hivyo?

19 Ili tuwe safi kimwili, tunapaswa kuepuka tabia na mazoea machafu kama vile kuvuta sigara, kunywa pombe kupita kiasi, na kutumia dawa za kulevya au dawa zinazopumbaza akili kwa kusudi lisilo la kitiba. Biblia haina orodha ya tabia na mazoea yote machafu na yenye kuchukiza ambayo yameenea sana leo, lakini ina kanuni zinazotusaidia kufahamu maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo. Kwa sababu tunajua maoni ya Yehova, kumpenda kunatuchochea kutenda kwa njia inayompendeza. Acheni tuchunguze kanuni tano za Kimaandiko.

20, 21. Yehova anataka tuondolee mbali mazoea gani, na ni sababu gani nzuri inayotuchochea kutii?

20 “Wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Yehova anataka tuondolee mbali mazoea yanayochafua mwili na akili zetu. Hivyo, tunapaswa kuepuka mazoea yanayohatarisha afya ya kimwili na ya kiakili.

21 Biblia inatoa sababu nzuri inayotuchochea “tujisafishe wenyewe kila unajisi.” Andiko la 2 Wakorintho 7:1 linaanza kwa kusema: “Kwa kuwa tuna ahadi hizi.” Ahadi gani? Kama mistari inayotangulia inavyotaja, Yehova anaahidi hivi: “Nitawakaribisha ndani. Nami nitakuwa baba kwenu.” (2 Wakorintho 6:17, 18) Hebu wazia: Yehova anaahidi kukulinda na kukupenda kama baba anavyomlinda na kumpenda mwana au binti yake. Lakini Yehova atatimiza ahadi hizo ikiwa tu utaepuka unajisi wa “mwili na roho.” Basi, lingekuwa jambo la kipumbavu kama nini kuruhusu tabia au zoea lolote lenye kuchukiza likuzuie usiwe na uhusiano huo wa karibu na wenye thamani pamoja na Yehova!

22-25. Ni kanuni gani za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kuepuka tabia na mazoea machafu?

22 “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Yesu alisema kwamba hiyo ndiyo amri kubwa kuliko zote. (Mathayo 22:38) Yehova anastahili upendo huo. Ili kumpenda kwa moyo, nafsi, na akili yetu yote, ni lazima tuepuke mazoea yanayoweza kufupisha maisha yetu au kupunguza uwezo wetu wa kufikiri tuliopewa na Mungu.

23 [Yehova] huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:24, 25) Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Kwa kuwa tunampenda Mtoaji wa zawadi hiyo, tunapaswa kuiheshimu. Tunaepuka tabia au mazoea yoyote yanayoweza kuhatarisha afya yetu, kwa maana tunatambua kwamba mazoea hayo hayaheshimu hata kidogo zawadi ya uhai.—Zaburi 36:9.

24 “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Mara nyingi tabia na mazoea machafu huwa na matokeo mabaya si kwa yule tu anayeyafanya bali pia kwa wale walio karibu naye. Kwa mfano, moshi wa sigara unaweza kuwaathiri wengine ambao si wavutaji. Mtu anayewaumiza watu walio karibu naye anavunja amri ya Mungu inayosema kwamba tumpende jirani yetu. Pia, anaonyesha wazi kwamba hampendi Mungu.—1 Yohana 4:20, 21.

25 ‘Mjitiishe na kuzitii serikali na mamlaka zikiwa watawala.’ (Tito 3:1) Katika nchi nyingi, kuwa na dawa za kulevya au kuzitumia ni kinyume cha sheria. Kwa kuwa sisi ni Wakristo wa kweli, hatuwi na dawa za kulevya wala kuzitumia.—Waroma 13:1.

26. (a) Ili tukae katika upendo wa Mungu, tunahitaji kufanya nini? (b) Kwa nini kuendelea kuwa safi machoni pa Mungu ndiyo njia nzuri zaidi ya maisha?

26 Ili kukaa katika upendo wa Mungu, tunahitaji kuendelea kuwa safi, si katika jambo moja au mawili tu, bali katika mambo yote. Huenda isiwe rahisi kuacha na kuepuka tabia na mazoea machafu, lakini inawezekana. * Kwa kweli, hiyo ndiyo njia nzuri zaidi ya maisha, kwa kuwa sikuzote Yehova anatufundisha ili tujifaidi wenyewe. (Isaya 48:17) Zaidi ya yote, tunapoendelea kuwa safi tunaweza kupata uradhi kwa sababu tunajua kwamba tunamwakilisha vizuri Mungu tunayempenda, na hivyo kukaa katika upendo wake.

^ fu. 2 Mbali na kufafanua usafi wa kimwili, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “safi” linatia ndani pia usafi wa kiadili au wa kiroho.

^ fu. 12 Sura ya 6 ya kitabu hiki inaonyesha jinsi ya kuchagua burudani zinazofaa.

^ fu. 67 Jina limebadilishwa.