Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 9

“Ukimbieni Uasherati”

“Ukimbieni Uasherati”

“Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”—WAKOLOSAI 3:5.

1, 2. Balaamu alitunga hila gani ili kuwadhuru watu wa Yehova?

MVUVI anaenda mahali ambapo amezoea kuvua samaki. Leo anataka kuvua samaki wa aina fulani. Anachagua chambo na kutupa ndoana ndani ya maji. Muda mfupi baadaye, ndoana inakazika, ufito wa kuvulia unapindika, naye aanza kuvuta windo lake. Anafurahi kwa kuwa anajua kwamba ametumia chambo kinachofaa.

2 Mwaka wa 1473 K.W.K., mwanamume mmoja anayeitwa Balaamu alifikiria sana chambo au mtego ambao angetumia. Kusudi lake lilikuwa kuwanasa watu wa Mungu waliokuwa wamepiga kambi katika Nchi Tambarare za Moabu, kwenye mpaka wa Nchi ya Ahadi. Balaamu alidai kwamba yeye ni nabii wa Yehova, lakini kwa kweli alikuwa mtu mwenye pupa aliyekuwa ameahidiwa malipo ili awalaani Waisraeli. Hata hivyo, Yehova aliingilia kati na kumfanya Balaamu abariki Israeli. Akiwa ameazimia kupokea malipo yake, Balaamu alifikiri kwamba huenda anaweza kumchochea Mungu awalaani watu wake mwenyewe, ikiwa tu wangeshawishiwa kutenda dhambi nzito. Akiwa na lengo hilo akilini, Balaamu akaweka chambo kwenye ndoana yake. Chambo hicho kilikuwa wasichana wa Moabu wenye ushawishi.—Hesabu 22:1-7; 31:15, 16; Ufunuo 2:14.

3. Mbinu ya Balaamu ilifanikiwa kwa kadiri gani?

3 Je, mbinu yake ilifanikiwa? Ndiyo, kwa kadiri fulani. Maelfu ya wanaume Waisraeli walinaswa na chambo hicho kwa “kufanya uasherati na binti za Moabu.” Hata walianza kuabudu miungu ya Moabu, kutia ndani Baali wa Peori mwenye kuchukiza, mungu wa uwezo wa kuzaa, au ngono. Matokeo yakawa kwamba Waisraeli 24,000 waliangamia wakiwa ukingoni mwa Nchi ya Ahadi. Huo ulikuwa msiba mkubwa kama nini!—Hesabu 25:1-9.

4. Kwa nini maelfu ya Waisraeli walinaswa na mtego wa uasherati?

4 Ni nini kilichosababisha msiba huo? Watu wengi walikuwa wamesitawisha moyo mwovu kwa kujiondoa kwa Yehova, Mungu yuleyule aliyewakomboa kutoka Misri, akawalisha nyikani, na kuwaongoza salama mpaka nchi ya ahadi. (Waebrania 3:12) Akizungumzia kisa hicho, mtume Paulo aliandika: “Wala tusifanye uasherati, kama baadhi yao walivyofanya uasherati, na kuanguka, 23,000 kati yao katika siku moja.” *1 Wakorintho 10:8.

5, 6. Kwa nini masimulizi kuhusu dhambi ya Waisraeli katika Nchi Tambarare za Moabu yanaweza kutufaidi sana leo?

5 Watu wa Mungu leo wanaokaribia kuingia katika nchi ya ahadi iliyo bora hata zaidi, wanaweza kujifunza mambo mengi muhimu kutokana na masimulizi ya kitabu cha Hesabu. (1 Wakorintho 10:11) Kwa mfano, pupa ya ngono kama ile ya Wamoabu wa kale inaonekana katika ulimwengu wa leo kwa kiwango kikubwa hata zaidi. Kwa kuongezea, kila mwaka maelfu ya Wakristo hunaswa na uasherati—mtego uleule uliowanasa Waisraeli. (2 Wakorintho 2:11) Na kwa kumwiga Zimri, aliyemleta kwa ukaidi mwanamke Mmidiani katika kambi ya Waisraeli na kumwingiza katika hema lake, watu fulani wanaoshirikiana na watu wa Mungu leo wamewapotosha wengine katika kutaniko la Kikristo.—Hesabu 25:6, 14; Yuda 4.

6 Je, unajiona ukiwa kwenye Nchi Tambarare za Moabu? Je, unaona kwamba uko karibu kupokea thawabu yako, yaani, ulimwengu mpya ambao umengojewa kwa muda mrefu? Ikiwa ndivyo, basi fanya yote uwezayo kukaa katika upendo wa Mungu kwa kutii amri hii: “Ukimbieni uasherati.”—1 Wakorintho 6:18.

Kutazama Nchi Tambarare za Moabu

UASHERATI NI NINI?

7, 8. “Uasherati” ni nini, na ni kwa njia gani wale walio na mazoea ya kufanya uasherati huvuna kile wanachopanda?

7 Katika Biblia, neno “uasherati” (Kigiriki, por·neiʹa) linahusu mahusiano haramu ya ngono nje ya ndoa ya Kimaandiko. Linatia ndani uzinzi, ukahaba, ngono kati ya watu ambao hawajaoana, ngono ya kinywa, ufiraji au ulawiti, na kusisimua kingono viungo vya uzazi vya mtu mwingine ambaye si mwenzi wako wa ndoa. Pia linatia ndani mazoea kama hayo kati ya watu wa jinsia moja au kati ya mtu na mnyama. *

8 Maandiko yanataja waziwazi: Walio na mazoea ya kufanya uasherati hawawezi kuendelea kuwa katika kutaniko la Kikristo na hawatapata uzima wa milele. (1 Wakorintho 6:9; Ufunuo 22:15) Pia, wanajiletea wenyewe madhara makubwa hata sasa. Wanakuwa watu wasiotumainika, wanajidharau, wanakuwa na mizozo katika ndoa zao, wanakuwa na dhamiri chafu, wanapata mimba zisizotakikana, magonjwa, na hata kifo. (Wagalatia 6:7, 8) Kwa nini uanze kutembea katika barabara hiyo yenye hatari nyingi? Inasikitisha kwamba wengi hawafikirii madhara yanayoweza kutokea kabla ya kuchukua hatua ya kwanza isiyofaa, ambayo mara nyingi hutia ndani ponografia.

PONOGRAFIA—HATUA YA KWANZA

9. Je, ni kweli kwamba ponografia haina madhara yoyote kama wengine wanavyodai? Eleza.

9 Katika nchi nyingi, ponografia hupatikana katika magazeti, muziki, televisheni, na imejaa katika Intaneti. * Je, ni kweli kwamba haina madhara yoyote kama wengine wanavyodai? Sivyo hata kidogo! Mara nyingi wale wanaotazama ponografia husitawisha mazoea ya kupiga punyeto na kukuza “hamu za ngono yenye kufedhehesha,” mambo ambayo yanaweza kusababisha pupa ya ngono, tamaa potovu, matatizo mazito katika ndoa, na hata talaka. * (Waroma 1:24-27; Waefeso 4:19) Mchunguzi fulani analinganisha pupa ya ngono na ugonjwa wa kansa. Anasema: “Hukua na kuenea daima. Uwezekano wa kupungua ni mdogo sana nayo haitibiki wala kupona kwa urahisi.”

Katika familia, ni jambo la hekima kuhakikisha kwamba Intaneti inatumiwa tu mahali palipo wazi

10. Tunaweza kutumia jinsi gani kanuni iliyo katika Yakobo 1:14, 15? (Ona pia sanduku “ Nilivyopata Nguvu za Kuwa Safi Kiadili.”.)

10 Fikiria maneno haya yaliyo katika andiko la Yakobo 1:14, 15: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” Kwa hiyo tamaa mbaya ikiingia akilini mwako, iondolee mbali mara moja! Kwa mfano, ukiona bila kukusudia picha zenye kuamsha hamu ya ngono, angalia kando haraka, au uzime kompyuta, au ubadili stesheni ya televisheni. Fanya yote unayoweza ili kuepuka kulemewa na tamaa zilizopotoka kabla hazijaenea sana na kupita mipaka!—Mathayo 5:29, 30.

11. Tunaposhindana na tamaa mbaya, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamtegemea Yehova?

11 Kwa sababu nzuri, Yule anayetujua vizuri kuliko tunavyojijua anatuhimiza hivi: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.” (Wakolosai 3:5) Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Lakini kumbuka, tuna Baba wa mbinguni mwenye upendo na subira tunayeweza kumtegemea. (Zaburi 68:19) Kwa hiyo, mawazo yasiyofaa yanapoingia katika akili yako, zungumza naye papo hapo. Sali upate “nguvu zinazopita zile za kawaida,” na ulazimishe akili yako kukazia fikira mambo tofauti.—2 Wakorintho 4:7; 1 Wakorintho 9:27; ona sanduku  “Ninaweza Kufanya Nini ili Kuacha Mazoea Mabaya?” katika ukurasa wa 104.

12. “Moyo” wetu ni nini, na kwa nini tunapaswa kuulinda?

12 Yule mwanamume mwenye hekima, Sulemani, aliandika: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) “Moyo” wetu unawakilisha utu wetu, jinsi tulivyo kikweli machoni pa Mungu. Zaidi ya hilo, kupata au kutopata uzima wa milele kunategemea jinsi Mungu anavyouona “moyo” wetu, bali si vile wengine wanavyotuona. Hilo ni jambo rahisi. Lakini, ni jambo zito pia. Mwanamume mwaminifu Ayubu alifanya agano, au mapatano rasmi, pamoja na macho yake ili asimtazame mwanamke kwa njia isiyofaa. (Ayubu 31:1) Huo ni mfano mzuri kama nini kwetu! Mtunga-zaburi pia alikuwa na maoni kama hayo aliposali: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.”—Zaburi 119:37.

DINA AFANYA UAMUZI MBAYA

13. Dina alikuwa nani, na kwa nini uchaguzi wake wa marafiki haukuwa wa hekima?

13 Kama tulivyoona katika Sura ya 3, marafiki wetu wanaweza kuwa na uvutano mzuri au mbaya juu yetu. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Fikiria mfano wa Dina, binti ya Yakobo. (Mwanzo 34:1) Ingawa alipata malezi mazuri nyumbani, Dina hakutenda kwa hekima alipofanya urafiki na wasichana Wakanaani. Kama Wamoabu, maadili ya Wakanaani yalikuwa yamepotoka sana. (Mambo ya Walawi 18:6-25) Dina alionekana kuwa windo rahisi machoni pa wanaume Wakanaani, kutia ndani Shekemu, aliyekuwa “mwenye kuheshimika zaidi” katika nyumba ya baba yake.—Mwanzo 34:18, 19.

14. Ni kwa njia gani uchaguzi wa Dina wa marafiki ulisababisha msiba?

14 Huenda Dina hakufikiri kuhusu ngono alipomwona Shekemu. Hata hivyo, Shekemu alifanya kile ambacho kwa kawaida Wakanaani wengi wangefanya waliposisimka kingono. Hakuna chochote ambacho Dina angeweza kufanya dakika ya mwisho, kwa kuwa Shekemu ‘alimchukua’ na ‘kumnajisi.’ Inaonekana kwamba baadaye, Shekemu ‘alimpenda’ Dina, hata hivyo hilo halikubadili jambo alilokuwa amemfanyia. (Mwanzo 34:1-4) Na si Dina tu aliyeumia. Uchaguzi wake wa marafiki ulianzisha matukio yaliyoleta aibu na suto kwa familia yao yote.—Mwanzo 34:7, 25-31; Wagalatia 6:7, 8.

15, 16. Tunaweza kupata hekima ya kweli jinsi gani? (Ona pia sanduku “ Maandiko ya Kutafakari.”)

15 Ikiwa Dina alipata somo lolote, basi ilikuwa baada ya kufunzwa na ulimwengu. Wale wanaompenda na kumtii Yehova hawahitaji kufunzwa na ulimwengu. Kwa sababu wanamsikiliza Mungu, wanachagua ‘kutembea na watu wenye hekima.’ (Methali 13:20a) Hivyo wanapata kuelewa “njia yote ya yaliyo mema” na kuepuka matatizo na maumivu yasiyo ya lazima. —Methali 2:6-9; Zaburi 1:1-3.

16 Mungu humpa hekima Yake yeyote yule anayeitamani na anayesali daima na kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu na habari zinazoandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu. (Mathayo 24:45; Yakobo 1:5) Jambo lingine la maana ni unyenyekevu, ambao unaonekana kwa kuwa tayari kutii shauri la Maandiko. (2 Wafalme 22:18, 19) Kwa mfano, huenda Mkristo anajua kanuni ya kwamba moyo ni wenye hila na ni hatari. (Yeremia 17:9) Hata hivyo, anapotenda kwa kutotumia hekima, je, yuko tayari kujinyenyekeza na kukubali msaada na shauri lenye upendo?

17. Eleza hali inayoweza kutokea katika familia, na jinsi baba anavyoweza kumsaidia binti yake kuhusiana na jambo hilo.

17 Fikiria hali hii. Baba hamruhusu binti yake aende matembezi pamoja na kijana Mkristo wakiwa peke yao. Msichana huyo anasema: “Baba, kwani huniamini? Hatutafanya chochote!” Huenda anampenda Yehova na hana nia mbaya, hata hivyo, je, kweli ‘anatembea katika hekima’ inayotoka kwa Mungu? Je, ‘anaukimbia uasherati’? Au ‘anautegemea moyo wake’ kwa ujinga? (Methali 28:26) Huenda unaweza kufikiria kanuni nyingine zinazoweza kumsaidia baba huyo na binti yake katika jambo hilo.—Ona Methali 22:3; Mathayo 6:13; 26:41.

YOSEFU ALIUKIMBIA UASHERATI

18, 19. Yosefu alishawishiwa jinsi gani, naye alifanya nini?

18 Yosefu, ndugu-nusu ya Dina, aliyekuwa kijana mzuri aliyempenda Mungu, aliukimbia uasherati. (Mwanzo 30:20-24) Alipokuwa mtoto, Yosefu aliona matokeo mabaya ya upumbavu wa dada yake. Inaonekana kukumbuka mambo hayo, na vilevile kutamani kukaa katika upendo wa Mungu, kulimlinda Yosefu miaka mingi baadaye huko Misri wakati mke wa bwana wake alipokuwa akijaribu kumshawishi “siku baada ya siku.” Bila shaka, kwa sababu Yosefu alikuwa mtumwa, hangeweza kuacha kazi na kuondoka! Ilimbidi ashughulikie hali hiyo kwa hekima na uhodari. Alifanya hivyo kwa kukataa tena na tena vishawishi vya mke wa Potifa, na mwishowe, kwa kumkimbia.—Mwanzo 39:7-12.

19 Fikiria hili: Ikiwa Yosefu angetumia muda mwingi akiwaza kuhusu mwanamke huyo au kuwaza-waza juu ya ngono, je, angeendelea kuwa mtimilifu? Haielekei angeweza. Badala ya kuwazia daima mambo yasiyofaa, Yosefu alithamini uhusiano wake pamoja na Yehova, jambo ambalo lilionekana wazi katika maneno ambayo alimwambia mke wa Potifa. Alisema: “Bwana wangu  . . . hakunizuilia chochote ila wewe, kwa sababu wewe ni mke wake. Basi ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”—Mwanzo 39:8, 9.

20. Yehova alielekeza mambo jinsi gani katika kisa cha Yosefu?

20 Wazia shangwe ambayo Yehova alikuwa nayo alipomwona kijana Yosefu akiendelea kuwa mtimilifu siku baada ya siku, ingawa alikuwa mbali na familia yao. (Methali 27:11) Baadaye Yehova alielekeza mambo ili Yosefu afunguliwe kutoka gerezani na vilevile kuwa waziri mkuu wa Misri na msimamizi wa chakula! (Mwanzo 41:39-49) Jinsi yalivyo kweli maneno haya ya Zaburi 97:10: “Enyi mnaompenda Yehova, chukieni yaliyo mabaya. Yeye anazilinda nafsi za washikamanifu wake; huwakomboa kutoka katika mkono wa waovu”!

21. Ndugu mmoja kijana katika nchi fulani ya Afrika alitetea maadili yake kwa uhodari jinsi gani?

21 Vivyo hivyo leo, watumishi wengi wa Mungu wanaonyesha kwamba ‘wanachukia yaliyo mabaya, na kupenda yaliyo mema.’ (Amosi 5:15) Ndugu mmoja kijana katika nchi fulani ya Afrika anakumbuka kwamba wakati fulani msichana mmoja katika darasa lao, hata bila haya yoyote, alikuwa tayari kulala naye ikiwa angemsaidia katika mtihani wa hesabu. “Nilikataa papo hapo,” anasema ndugu huyo. “Kuendelea kuwa mtimilifu kumeniwezesha kuheshimiwa na kujiheshimu, mambo ambayo ni yenye thamani sana kuliko dhahabu na fedha.” Ni kweli kwamba mtu anaweza “kufurahia dhambi kwa muda,” lakini mara nyingi raha hizo za muda mfupi huleta maumivu mengi. (Waebrania 11:25) Zaidi ya hilo, raha hizo hazina thamani yoyote zinapolinganishwa na furaha ya kudumu inayotokana na kumtii Yehova.—Methali 10:22.

KUBALI MSAADA KUTOKA KWA MUNGU WA REHEMA

22, 23. (a) Mkristo akitenda dhambi nzito, kwa nini hilo halimaanishi kwamba hana tumaini? (b) Mtenda-dhambi anaweza kupata msaada gani?

22 Kwa sababu ya kutokuwa wakamilifu, sote tunahitaji kujitahidi sana ili kudhibiti tamaa za mwili na kufanya yaliyo sawa machoni pa Mungu. (Waroma 7:21-25) Yehova anatambua hilo, “akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Hata hivyo, nyakati nyingine huenda Mkristo akatenda dhambi nzito. Je, hilo linamaanisha kwamba hana tumaini? Sivyo hata kidogo! Ni kweli kwamba mtenda-dhambi huyo anaweza kuvuna mabaya, kama Mfalme Daudi. Lakini, sikuzote Mungu ‘yuko tayari kuwasamehe’ wale ambao ni wanyoofu na ‘wanaoungama waziwazi’ dhambi zao.—Zaburi 86:5; Yakobo 5:16; Methali 28:13.

23 Pia, kwa fadhili Mungu ameandalia kutaniko la Kikristo “zawadi katika wanadamu”—wachungaji wa kiroho waliokomaa, wanaostahili, na walio tayari kusaidia. (Waefeso 4:8, 12; Yakobo 5:14, 15) Kusudi lao ni kumsaidia mtenda-dhambi arudie uhusiano wake pamoja na Mungu na kama vile yule mwanamume mwenye hekima alivyosema, wanamsaidia ‘kujipatia utambuzi wa moyo’ ili asirudie dhambi.—Methali 15:32.

‘JIPATIE MOYO’

24, 25. (a) Kijana anayetajwa katika Methali 7:6-23 alionyesha jinsi gani kwamba “amepungukiwa moyoni”? (b) Tunaweza ‘kujipatia moyo’ jinsi gani?

24 Biblia inataja watu ambao ‘wamepungukiwa moyoni’ na wale ambao ‘wanajipatia moyo.’ (Methali 7:7) Kwa sababu ya kutokomaa kiroho na kutokuwa na uzoefu katika utumishi wa Mungu, mtu ambaye “amepungukiwa moyoni” anaweza kukosa utambuzi na busara. Kama yule kijana anayetajwa katika Methali 7:6-23, mtu huyo anaweza kutumbukia katika dhambi nzito kwa urahisi. Hata hivyo, mtu “anayejipatia moyo” anahangaikia sana utu wake kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kwa kusali. Na kwa kadiri anavyoweza akiwa mwanadamu asiye mkamilifu, anapatanisha mawazo, tamaa, hisia, na miradi yake maishani na mambo ambayo Mungu anakubali. Hivyo, “anapenda nafsi yake mwenyewe” au anajibariki, na “atapata mema.”—Methali 19:8.

25 Jiulize: ‘Je, ninasadiki kabisa kwamba viwango vya Mungu vinafaa? Je, ninaamini kabisa kwamba kuvifuata hutokeza furaha nyingi?’ (Zaburi 19:7-10; Isaya 48:17, 18) Ukiwa na shaka hata kidogo, chukua hatua. Tafakari kuhusu matokeo ya kupuuza sheria za Mungu. Pia, ‘onja uone ya kuwa Yehova ni mwema’ kwa kuishi kupatana na kweli na kujaza mawazo yanayofaa katika akili yako—mambo yaliyo ya kweli, ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, yaliyo ya kupendeka, na yaliyo mema kiadili. (Zaburi 34:8; Wafilipi 4:8, 9) Unaweza kuwa na hakika kwamba kadiri unavyoendelea kufanya hivyo, ndivyo unavyopata kumpenda Mungu zaidi, kupenda mambo anayopenda, na kuchukia mambo anayochukia. Yosefu hakuwa malaika. Hata hivyo, ‘aliukimbia uasherati’ kwa sababu alimruhusu Yehova amfinyange kwa miaka mingi, na kumsaidia atamani kumpendeza. Na iwe hivyo kwako.—Isaya 64:8.

26. Ni jambo gani la maana litakalozungumziwa?

26 Muumba wetu hakuumba viungo vyetu vya uzazi ili vichezewe-chezewe, bali ili vipitishe uhai na kutuwezesha kufurahia uhusiano wa karibu katika ndoa. (Methali 5:18) Maoni ya Mungu kuhusu ndoa yatazungumziwa katika sura mbili zinazofuata.

^ fu. 4 Inaonekana kwamba idadi inayotajwa katika kitabu cha Hesabu inatia ndani idadi ya “walio vichwa vya watu.” Baadhi yao, ambao huenda hesabu yao ilikuwa watu 1,000, waliuawa na waamuzi, na wengine wakauawa moja kwa moja na Yehova.—Hesabu 25:4, 5.

^ fu. 7 Unaweza kupata maelezo zaidi kuhusu uchafu na mwenendo mpotovu katika “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2006 (15/7/2006), kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Neno “ponografia” linatumiwa hapa kufafanua maneno, maandishi, au picha zinazokusudiwa kuamsha hamu ya ngono. Ponografia inaweza kuwa picha ya mtu ambayo inakusudiwa kuamsha hamu ya ngono au hata picha zinazoonyesha matendo machafu sana ya kingono kati ya watu wawili au zaidi.

^ fu. 9 Kupiga punyeto kunazungumziwa katika nyongeza “Shinda Zoea la Kupiga Punyeto.”