Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 11

“Ndoa na Iheshimiwe””

“Ndoa na Iheshimiwe””

“Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako.”—METHALI 5:18.

1, 2. Tutazungumzia swali gani, na kwa nini?

JE, UMEFUNGA ndoa? Ikiwa ndivyo, je, unapata furaha katika ndoa yako au kuna matatizo mazito? Je, pengo kati yako na mwenzi wako linazidi kuongezeka? Je, unavumilia maisha ya ndoa badala ya kuyafurahia? Ikiwa ndivyo, inaelekea unasikitika kwamba upendo uliokuwapo mwanzoni katika ndoa yako umepoa. Ukiwa Mkristo, ni wazi kwamba ungependa ndoa yako imletee utukufu Yehova, Mungu unayempenda. Hivyo, huenda hali ya ndoa yako sasa inakuhangaisha na kukuvunja moyo sana. Hata hivyo, tafadhali usikate kauli kwamba ndoa yako imegonga mwamba.

2 Leo, kuna wenzi wa ndoa Wakristo ambao ndoa zao zilikuwa katika hali mahututi wakati fulani. Hata hivyo, walipata njia ya kuimarisha uhusiano wao. Wewe pia unaweza kupata furaha katika ndoa. Jinsi gani?

KUMKARIBIA MUNGU NA MWENZI WAKO

3, 4. Toa mfano unaoonyesha kwa nini wenzi wa ndoa wanaweza kukaribiana wakijitahidi kumkaribia Mungu.

3 Wewe na mwenzi wako mtazidi kuwa na uhusiano wa karibu ikiwa mtajitahidi kumkaribia Mungu. Kwa nini? Hebu fikiria mfano huu: Wazia mlima ulio mpana chini na ambao umechongoka juu. Tuseme kwamba mwanamume amesimama chini ya mlima huo upande wa kaskazini huku mwanamke akiwa amesimama chini ya mlima huo upande wa kusini. Wote wawili wanaanza kuupanda. Mwanzoni wanatenganishwa na sehemu pana ya mlima. Lakini kadiri wanavyoendelea kupanda juu zaidi na zaidi kuelekea kilele cha mlima huo, ndivyo wanavyozidi kukaribiana. Je, unaona jambo lenye kutia moyo katika mfano huo?

4 Jitihada zako za kumtumikia Yehova kikamili zinaweza kulinganishwa na jitihada za kupanda mlima. Kwa kuwa unampenda Yehova, tayari unajitahidi sana kuupanda mlima huo wa mfano. Lakini, ikiwa kuna pengo kati yako na mwenzi wako, huenda mko pande tofauti za mlima. Hata hivyo, ni nini kinachotukia mnapozidi kuupanda? Ni kweli kwamba mwanzoni kila mmoja yuko mbali sana na mwingine. Hata hivyo, kadiri mnavyotia bidii kumkaribia Mungu, yaani, kuzidi kuupanda mlima huo wa mfano, ndivyo wewe na mwenzi wako mnavyozidi kukaribiana. Kwa kweli, kumkaribia Mungu ndiyo siri ya kumkaribia mwenzi wako. Lakini unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Ujuzi wa Biblia unapotumiwa, unaweza kuimarisha ndoa yenu

5. (a) Taja njia moja ya kumkaribia Yehova na mwenzi wa ndoa. (b) Yehova ana maoni gani kuhusu ndoa?

5 Njia moja muhimu ambayo wewe na mwenzi wako mnaweza kuupanda mlima huo wa mfano ni kwa kutii shauri la Neno la Mungu kuhusu ndoa. (Zaburi 25:4; Isaya 48:17, 18) Hivyo basi, fikiria shauri hususa ambalo mtume Paulo alitoa. Alisema: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote.” (Waebrania 13:4) Hilo linamaanisha nini? Neno “iheshimiwe” linadokeza wazo la kuona kitu kuwa cha maana sana na chenye thamani. Na hivyo ndivyo Yehova anavyoiona ndoa—anaiona kuwa yenye thamani kubwa.

KUMPENDA YEHOVA NA KUKUCHOCHEE

6. Muktadha wa shauri la Paulo kuhusu ndoa unaonyesha nini, na kwa nini hilo ni jambo la maana kukumbuka?

6 Bila shaka, kwa kuwa wewe na mwenzi wako ni watumishi wa Mungu, tayari mnajua kwamba ndoa ni yenye thamani na takatifu. Yehova mwenyewe ndiye aliyeanzisha mpango wa ndoa. (Mathayo 19:4-6) Hata hivyo, ikiwa kwa sasa una matatizo katika ndoa, kujua tu kwamba ndoa inaheshimika hakutoshi kukuchochea wewe na mwenzi wako kupendana na kuheshimiana. Ni nini basi kitakachowachochea? Ona jinsi Paulo alivyozungumzia suala la kuonyesha heshima katika ndoa. Hakusema, “ndoa inaheshimiwa”; badala yake alisema, “ndoa na iheshimiwe.” Paulo hakuwa akisema jinsi mambo yalivyo; bali alikuwa akitoa himizo. * Kukumbuka jambo hilo kunaweza kukuchochea hata zaidi kuanza tena kumthamini mwenzi wako. Kwa nini?

7. (a) Ni amri gani za Kimaandiko tunazotii, na kwa nini? (b) Ni matokeo gani mazuri yanayotokana na utii?

7 Hebu fikiria jinsi unavyoona amri nyingine za Kimaandiko, kama vile utume wa kufanya wanafunzi au shauri la kukutana pamoja ili kuabudu. (Mathayo 28:19; Waebrania 10:24, 25) Ni kweli kwamba nyakati nyingine si rahisi kutimiza amri hizo. Watu unaowahubiria wanaweza kukupinga, au unaweza kuchoka sana kwa sababu ya kazi ya kimwili unayofanya hivi kwamba inakuwa vigumu sana kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, unaendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme, na unaendelea kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hakuna mtu anayeweza kukuzuia—hata Shetani! Kwa nini? Kwa sababu kumpenda Yehova kutoka moyoni kunakuchochea kutii amri zake. (1 Yohana 5:3) Kufanya hivyo kuna matokeo gani mazuri? Kuhubiri na kuhudhuria mikutano kunakuwezesha kuwa na amani ya akili na shangwe moyoni kwa sababu unajua kwamba unafanya mapenzi ya Mungu. Na unapohisi hivyo, unapata nguvu mpya. (Nehemia 8:10) Tunajifunza nini?

8, 9. (a) Ni nini kinachoweza kutuchochea kutii himizo la kuiheshimu ndoa, na kwa nini? (b) Tutazungumzia hoja gani mbili?

8 Kama vile kumpenda Mungu sana kunavyokuchochea kutii amri ya kuhubiri na kukutanika pamoja hata kunapokuwa na vizuizi, ndivyo kumpenda Yehova kunavyoweza pia kukuchochea kutii himizo la Biblia la kuifanya ‘ndoa yako iheshimiwe,’ hata inapoonekana kuwa vigumu. (Waebrania 13:4; Zaburi 18:29; Mhubiri 5:4) Pia, kama vile Mungu anavyobariki sana jitihada zako za kuhubiri na kuhudhuria mikutano, ndivyo anavyoona na kubariki jitihada zako za kuiheshimu ndoa yako.—1 Wathesalonike 1:3; Waebrania 6:10.

9 Basi, unaweza kufanya nini ili ndoa yako iheshimiwe? Unahitaji kuepuka mwenendo ambao utaharibu mpango wa ndoa. Vilevile, unahitaji kuchukua hatua ambazo zitaimarisha kifungo cha ndoa.

EPUKA USEMI NA MWENENDO UNAOFANYA NDOA ISIHESHIMIKE

10, 11. (a) Ni mwenendo gani unaofanya ndoa isiheshimike? (b) Tunaweza kumuuliza nini mwenzi wa ndoa?

10 Wakati fulani, mke mmoja Mkristo alisema: “Mimi husali kwa Yehova anipe nguvu za kuvumilia.” Kuvumilia nini? Alieleza hivi: “Mume wangu hunishambulia kwa maneno. Sina majeraha mwilini, lakini maneno yake yenye kuchoma anayosema kila wakati, kama vile ‘Umenichosha!’ na ‘Wewe ni bure kabisa!’ yananiumiza sana moyoni.” Mke huyo anataja jambo zito sana—maneno yenye kuumiza katika ndoa.

11 Ni jambo lenye kusikitisha kama nini wakati wenzi wa ndoa Wakristo wanaporushiana maneno yenye kuchoma na kusababisha maumivu ya kihisia ambayo si rahisi kupona! Bila shaka, wenzi wa ndoa wanapotumia usemi wenye kuumiza, ndoa yao haiheshimiki. Je, hivyo ndivyo ndoa yako ilivyo? Unaweza kujua kwa kumuuliza mwenzi wako kwa unyenyekevu, “Je, maneno yangu yanakuumiza?” Ikiwa mwenzi wako anahisi kwamba mara kwa mara maneno yako yanamuumiza kihisia, unapaswa kuwa tayari kufanya marekebisho.—Wagalatia 5:15; Waefeso 4:31.

12. Ni nini kinachoweza kufanya ibada ya mtu iwe ubatili machoni pa Mungu?

12 Usisahau kamwe kwamba uhusiano wako pamoja na Yehova unaweza kuwa mzuri au mbaya ikitegemea jinsi unavyoutumia ulimi wako katika ndoa. Biblia inasema: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.” (Yakobo 1:26) Maneno yako yanahusiana sana na ibada yako. Biblia haiungi mkono maoni ya kwamba chochote kinachotendeka nyumbani si neno mradi mtu anadai kumtumikia Mungu. Tafadhali usijidanganye. Hilo ni jambo zito. (1 Petro 3:7) Unaweza kuwa mtu mwenye vipawa na bidii nyingi, lakini ikiwa unamuumiza mwenzi wako kwa maneno yanayomkatakata, unakosa kuuheshimu mpango wa ndoa na huenda Mungu akaiona ibada yako kuwa ubatili mtupu.

13. Mwenzi wa ndoa anaweza kusababisha maumivu ya moyoni jinsi gani?

13 Wenzi wa ndoa wanapaswa pia kuwa waangalifu wasisababishe maumivu ya moyoni kwa njia nyingine zisizo za moja kwa moja. Fikiria mifano miwili: Mama asiye na mwenzi anampigia simu kwa ukawaida mwanamume Mkristo katika kutaniko lao ambaye amefunga ndoa ili kumwomba mashauri, nao wanazungumza kwa muda mrefu; ndugu Mkristo aliye mseja anahubiri kwa muda mrefu kila juma pamoja na dada Mkristo aliyeolewa. Katika mifano hiyo, huenda watu hao waliofunga ndoa hawana nia mbaya; hata hivyo, mwenendo wao unawafanya wenzi wao wa ndoa wajisikie namna gani? Mke aliyekuwa katika hali kama hiyo alisema: “Ninaumia ninapoona mume wangu akitumia muda mwingi sana ili kumhangaikia dada mwingine kutanikoni. Hilo hunifanya nihisi kwamba sifai.”

14. (a) Ni wajibu gani wa ndoa unaokaziwa katika Mwanzo 2:24? (b) Tunapaswa kujiuliza nini?

14 Mwenzi huyo na wenzi wengine wa ndoa walio katika hali kama hiyo wanaumia kihisia kwa sababu wenzi wao wanapuuza agizo hili la msingi ambalo Mungu alitoa kuhusiana na ndoa: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mwanzo 2:24) Bila shaka, wale wanaofunga ndoa bado wanawaheshimu wazazi wao; hata hivyo, kulingana na mpango wa Mungu wajibu wao mkuu ni kuelekea mwenzi wao wa ndoa. Vivyo hivyo, Wakristo wanawapenda sana waamini wenzao; lakini daraka lao kuu ni kuelekea mwenzi wao wa ndoa. Hivyo, Wakristo waliofunga ndoa wanapotumia wakati mwingi mno au kuzoeana kupita kiasi na waamini wenzao, hasa wa jinsia tofauti, wanafanya ndoa iwe na mikazo. Je, inawezekana kwamba jambo hilo linasababisha mkazo katika ndoa yako? Jiulize, ‘Je, kweli ninatumia wakati pamoja na mwenzi wangu wa ndoa, ninamhangaikia, na kumwonyesha upendo anavyostahili?’

15. Kulingana na Mathayo 5:28, kwa nini Wakristo waliofunga ndoa wanapaswa kuepuka kumhangaikia isivyofaa mtu wa jinsia tofauti?

15 Zaidi ya hilo, Wakristo waliofunga ndoa wanacheza na moto wanapowahangaikia isivyofaa watu wa jinsia tofauti ambao si wenzi wao wa ndoa. Inasikitisha kwamba Wakristo fulani waliofunga ndoa wameanza kuwa na hisia za kimapenzi kuelekea watu ambao wamezoeana nao kupita kiasi. (Mathayo 5:28) Hisia hizo zimewatumbukiza katika mwenendo unaofanya ndoa isiheshimike hata zaidi. Fikiria yale ambayo mtume Paulo alisema kuhusu jambo hilo.

“KITANDA CHA NDOA KIWE BILA UNAJISI”

16. Ni amri gani ambayo Paulo anatoa kuhusu ndoa?

16 Baada tu ya Paulo kutoa himizo la kwamba “ndoa na iheshimiwe,” alitoa onyo hili: “Kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Paulo alitumia maneno “kitanda cha ndoa” kurejelea mahusiano ya ngono. Mahusiano hayo hayana “unajisi,” nayo ni safi kiadili, yakiwa tu kati ya watu waliofunga ndoa. Kwa hiyo, Wakristo wanatii maneno haya yaliyoongozwa na roho: “Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako.”—Methali 5:18.

17. (a) Kwa nini Wakristo hawaongozwi na maoni ya ulimwengu kuhusu uzinzi? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kufuata mfano wa Ayubu?

17 Wale wanaofanya ngono na mtu ambaye si mwenzi wao wa ndoa wanaonyesha kwamba hawaheshimu hata kidogo sheria za Mungu za maadili. Ni kweli kwamba watu wengi leo wanaona uzinzi kuwa jambo la kawaida. Lakini, hata wanadamu wengine wawe na maoni gani kuhusu uzinzi, maoni yao hayapaswi kubadili maoni ya Wakristo kuhusu jambo hilo. Wanatambua kwamba mwishowe, si mwanadamu, bali ‘Mungu ndiye atakayewahukumu waasherati na wazinzi.’ (Waebrania 10:31; 12:29) Hivyo, Wakristo wa kweli hushikamana sana na maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. (Waroma 12:9) Kumbuka kwamba Ayubu alisema: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu.” (Ayubu 31:1) Ndiyo, ili kuepuka hata hatua ya kwanza ambayo inaweza kuelekeza kwenye uzinzi, Wakristo wa kweli huzuia macho yao, nao hawamtazami hata kidogo kwa tamaa mtu wa jinsia tofauti ambaye si mwenzi wao wa ndoa.—Ona nyongeza “Maoni ya Biblia Kuhusu Talaka na Kutengana.”

18. (a) Uzinzi ni jambo zito kadiri gani machoni pa Yehova? (b) Kuna ulinganifu gani kati ya uzinzi na ibada ya sanamu?

18 Uzinzi ni jambo zito kadiri gani machoni pa Yehova? Sheria ya Musa inatusaidia kuelewa maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. Katika Israeli, uzinzi na ibada ya sanamu ni kati ya dhambi zilizostahili adhabu ya kifo. (Mambo ya Walawi 20:2, 10) Je, unaona ulinganifu kati ya mambo hayo mawili? Mwisraeli aliyeabudu sanamu alivunja agano kati yake na Yehova. Vivyo hivyo, Mwisraeli aliyefanya uzinzi alivunja agano kati yake na mwenzi wake wa ndoa. Wote wawili walitenda kwa hila. (Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 5:9; Malaki 2:14) Kwa hiyo, wote wawili walikuwa na hatia mbele za Yehova, Mungu mwaminifu na mwenye kuaminika.—Zaburi 33:4.

19. Ni nini kinachoweza kumchochea mtu aazimie hata zaidi kuepuka uzinzi, na kwa nini?

19 Ni kweli kwamba Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. Hata hivyo, kukumbuka kwamba katika Israeli la kale uzinzi ulionwa kuwa dhambi nzito kunaweza kuwachochea Wakristo waazimie hata zaidi kutotenda dhambi hiyo. Kwa nini? Fikiria ulinganifu huu: Je, unaweza kuingia kanisani, upige magoti, na kusali mbele ya sanamu? ‘Siwezi hata kidogo!’ ndivyo utakavyosema. Lakini je, unaweza kushawishiwa kufanya hivyo ukipewa pesa nyingi? ‘Haiwezekani!’ utasema. Bila shaka, wazo lenyewe la kumsaliti Yehova kwa kuabudu sanamu linamchukiza Mkristo wa kweli. Vivyo hivyo, Wakristo wanapaswa kuchukizwa na wazo la kumsaliti Mungu wao Yehova na mwenzi wao wa ndoa kwa kufanya uzinzi—hata washawishiwe na jambo gani kutenda dhambi hiyo. (Zaburi 51:1, 4; Wakolosai 3:5) Hatungependa kamwe kutenda jambo ambalo litamfanya Shetani ashangilie na kumvunjia heshima Yehova na mpango mtakatifu wa ndoa.

JINSI YA KUIMARISHA KIFUNGO CHA NDOA

20. Ndoa fulani zimepatwa na nini? Toa mfano.

20 Mbali na kuepuka mwenendo unaofanya ndoa isiheshimike, ni hatua gani unazoweza kuchukua ili uanze tena kumheshimu mwenzi wako wa ndoa? Tunaweza kupata jibu la swali hilo kwa kulinganisha mpango wa ndoa na nyumba. Kisha, maneno ya fadhili, matendo mazuri, na mambo mengine ambayo wenzi wa ndoa hutendeana ili kuonyeshana heshima yanaweza kulinganishwa na vitu vinavyoipamba nyumba. Ikiwa mnahisi kwamba mna uhusiano wa karibu, basi ndoa yenu ni kama nyumba iliyo na mapambo yanayoifanya iwe maridadi na yenye kupendeza. Upendo wenu ukipungua, mapambo hayo yanatoweka pole kwa pole, na kufanya ndoa isivutie tena kama nyumba isiyo na mapambo yoyote. Kwa kuwa unataka kutii amri ya Mungu ya kuifanya ‘ndoa iheshimike,’ utachochewa kurekebisha hali hiyo. Kwa kweli, kitu chenye thamani na chenye kuheshimika kinastahili kurekebishwa. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Neno la Mungu linasema: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi itasimamishwa imara. Na kwa ujuzi vyumba vya ndani vitajazwa vitu vyote vyenye thamani na vyenye kupendeza.” (Methali 24:3, 4) Fikiria jinsi maneno hayo yanavyoweza kutumiwa kuhusu ndoa.

21. Ni kwa njia gani tunaweza kuimarisha ndoa yetu hatua kwa hatua? (Ona pia sanduku“ Ninaweza Kufanya Nini Ili Kuimarisha Ndoa Yangu?”)

21 ‘Vitu vyenye thamani’ vinavyoijaza nyumba yenye furaha vinatia ndani sifa kama vile upendo wa kweli, kumwogopa Mungu, na imani yenye nguvu. (Methali 15:16, 17; 1 Petro 1:7) Sifa hizo zinaifanya ndoa iwe imara. Lakini je, ulitambua jinsi vyumba vinavyotajwa katika methali hiyo vimejazwa vitu vyenye thamani? “Kwa ujuzi.” Ndiyo, ujuzi wa Biblia unapotumiwa, unaweza kubadili maoni ya watu na kuamsha tena upendo wao. (Waroma 12:2; Wafilipi 1:9) Hivyo, wakati wowote ambapo wewe na mwenzi wako mnaketi pamoja na kuchunguza kwa utulivu andiko fulani la Biblia, kama vile andiko la siku, au makala inayozungumzia ndoa kwa kutegemea Biblia katika gazeti la Mnara wa Mlinzi au Amkeni!, ni kana kwamba mnatazama pambo linaloweza kurembesha nyumba yenu. Kumpenda Yehova kunapowachochea kutumia shauri hilo katika ndoa yenu, ni kana kwamba mnaingiza pambo hilo katika “vyumba vya ndani.” Kwa njia hiyo, huenda upendo na uchangamfu ambao ulikuwepo katika ndoa yenu ukarudi.

22. Ni uradhi gani ambao tunaweza kupata tukijikakamua kufanya sehemu yetu katika kuimarisha ndoa yetu?

22 Ni kweli kwamba inaweza kuchukua muda na kazi nyingi kurudisha pambo moja baada ya lingine. Hata hivyo, ukijikakamua kufanya sehemu yako, utapata uradhi mwingi kwa kujua kwamba unatii amri hii ya Biblia: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10; Zaburi 147:11) Zaidi ya hilo, jitihada zako za kuiheshimu ndoa yako zitakusaidia kukaa katika upendo wa Mungu.

^ fu. 6 Muktadha unaonyesha kwamba Paulo alitoa shauri hilo kuhusu ndoa pamoja na mahimizo mengine mengi.—Waebrania 13:1-5.