Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 12

Sema Lililo “Jema kwa Ajili ya Kujenga”

Sema Lililo “Jema kwa Ajili ya Kujenga”

“Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga.”—WAEFESO 4:29.

1-3. (a) Yehova ametupa zawadi gani, na ni kwa njia gani inaweza kutumiwa vibaya? (b) Ili tukae katika upendo wa Mungu, tunapaswa kutumia jinsi gani uwezo wetu wa kusema?

IKIWA ungempa mtu unayempenda zawadi, ungeonaje ikiwa angeitumia vibaya kimakusudi? Tuseme umempa gari, na baadaye usikie kwamba analiendesha ovyoovyo na kuwaumiza wengine. Ungevunjika moyo sana, sivyo?

2 Uwezo wa kusema kwa njia inayoeleweka ni zawadi kutoka kwa Yehova, Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yakobo 1:17) Zawadi hiyo hutofautisha wanadamu na wanyama, nayo inatuwezesha kuwaonyesha wengine jinsi tunavyofikiri na kuhisi. Hata hivyo, kama gari, uwezo wa kusema unaweza kutumiwa vibaya. Yehova huhuzunika sana uwezo wa kusema unapotumiwa ovyoovyo na kuwaumiza wengine!

3 Ili tukae katika upendo wa Mungu, tunahitaji kutumia uwezo wa kusema kwa njia ambayo Mpaji wa zawadi hiyo alikusudia. Yehova anataja waziwazi usemi unaompendeza. Neno lake linasema: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” (Waefeso 4:29) Acheni tuzungumzie kwa nini tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu yale tunayosema, usemi tunaopaswa kuepuka, na jinsi tunavyoweza kusema lililo “jema kwa ajili ya kujenga.”

KWA NINI TUNAPASWA KUWA WAANGALIFU KUHUSU YALE TUNAYOSEMA?

4, 5. Methali fulani za Biblia zinafafanua jinsi gani madhara ambayo yanaweza kusababishwa na maneno?

4 Sababu moja muhimu ya kuwa waangalifu kuhusu yale tunayosema ni kwamba maneno yana nguvu. Andiko la Methali 15:4 linasema: “Utulivu wa ulimi ni mti wa uzima, lakini upotovu wake humaanisha kuvunjika katika roho.” * Kama vile maji yanavyoupa uhai mti ulionyauka, ndivyo maneno yanayosemwa kwa utulivu yanavyoweza kuiburudisha roho ya wale wanaoyasikia. Kwa upande mwingine, maneno yaliyopotoka ya ulimi mpotovu yanaweza kuwafanya wengine wavunjike katika roho. Kwa kweli, maneno tunayosema yana nguvu za kuumiza au kuponya.—Methali 18:21.

5 Ikieleza waziwazi madhara ambayo yanaweza kusababishwa na maneno, methali nyingine inasema: “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma.” (Methali 12:18) Maneno yanayosemwa ovyo na bila kufikiri yanaweza kuumiza sana hisia na kuharibu mahusiano. Je, umewahi kuchomwa moyoni na maneno yaliyo makali kama upanga? Kwa upande mwingine, methali hiyo inasema jambo hili lenye kutia moyo: “Ulimi wa mwenye hekima huponya.” Maneno yenye ufikirio yanayosemwa na mtu mwenye hekima ya kimungu yanaweza kuponya moyo ulioumizwa na kujenga tena mahusiano. Je, unaweza kukumbuka wakati ambapo uliponywa na maneno yenye fadhili? (Methali 16:24) Tukitambua kwamba maneno tunayosema yanaweza kuwa na matokeo mazuri au mabaya kwa wengine, tutayatumia kuwaponya bali si kuwaumiza.

Maneno matulivu yanaburudisha

6. Kwa nini si rahisi kuudhibiti ulimi?

6 Hata tujaribu namna gani, hatuwezi kuuzuia ulimi wetu kabisa. Kwa hiyo, sababu ya pili ya kuwa waangalifu kuhusu yale tunayosema ni hii: Dhambi na kutokamilika hutuchochea kutumia vibaya ulimi wetu. Maneno hutoka moyoni, na “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya.” (Mwanzo 8:21; Luka 6:45) Hivyo, kuuongoza ulimi kwa lijamu si rahisi. (Yakobo 3:2-4) Ingawa hatuwezi kuudhibiti ulimi kabisa, tunaweza kuendelea kufanya maendeleo kuhusu jinsi tunavyoutumia. Kama vile mwogeleaji anayejaribu kuogelea dhidi ya mkondo, tunapaswa kuendelea kupambana na mwelekeo wenye dhambi wa kuutumia ulimi vibaya.

7, 8. Tunawajibika kadiri gani mbele za Yehova kwa sababu ya maneno yetu?

7 Sababu ya tatu ya kuwa waangalifu kuhusu yale tunayosema ni kwamba Yehova atatuhukumu kulingana na maneno yetu. Mbali na uhusiano wetu na wanadamu wenzetu, msimamo wetu mbele za Yehova pia unategemea jinsi tunavyoutumia ulimi wetu. Andiko la Yakobo 1:26 linasema: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.” * Kama tulivyoona katika sura inayotangulia, usemi wetu unahusiana sana na ibada yetu. Ikiwa hatuzuii ulimi wetu—tukiropoka maneno yenye kuumiza na yenye sumu—mambo yote tunayofanya ili kumpendeza Mungu, yanaweza kuwa bure machoni pake. Hilo ni jambo zito, sivyo?—Yakobo 3:8-10.

8 Ni wazi kwamba tuna sababu zenye nguvu za kuepuka kutumia vibaya uwezo wa kusema. Kabla ya kuzungumzia jinsi usemi wetu unavyoweza kuwa wenye kujenga, acheni tuzungumzie usemi ambao Mkristo wa kweli anapaswa kuepuka kabisa.

USEMI UNAOBOMOA

9, 10. (a) Ni maneno ya aina gani ambayo yameenea ulimwenguni leo? (b) Kwa nini tunapaswa kuepuka maneno machafu? (Ona pia maelezo ya chini.)

9 Maneno machafu. Matusi, makufuru, na maneno mengine machafu yameenea sana katika ulimwengu wa leo. Wengine hutumia maneno ya matusi ili kukazia mambo wanayozungumzia au wanapokosa neno la kutumia. Watumbuizaji hupenda kutumia maneno machafu yanayohusiana na ngono ili kuwachekesha watu. Hata hivyo, kutumia maneno machafu ni jambo zito. Miaka 2,000 hivi iliyopita, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kushauri kutaniko la Kolosai waondolee mbali “maneno machafu.” (Wakolosai 3:8) Alipoliandikia kutaniko la Efeso, Paulo alitaja “mizaha michafu” kati ya vitu ambavyo havikupaswa ‘kutajwa hata kidogo katikati’ ya Wakristo wa kweli.—Waefeso 5:3, 4.

10 Maneno machafu yanamchukiza Yehova. Yanawachukiza pia wale wanaompenda. Kwa hakika, kumpenda Yehova kunatuchochea kukataa maneno machafu. Anapoorodhesha “matendo ya mwili,” Paulo anataja “uchafu,” ambao unaweza kutia ndani usemi mchafu. (Wagalatia 5:19-21) Hilo ni jambo zito. Mtu anaweza kutengwa na ushirika wa kutaniko ikiwa baada ya kushauriwa tena na tena, bado anaendelea kutumia maneno machafu au mapotovu, yenye kushusha heshima, na matusi. *

11, 12. (a) Porojo ni nini, na ni kwa njia gani inaweza kuumiza? (b) Kwa nini waabudu wa Yehova wanapaswa kuepuka uchongezi?

11 Porojo yenye kuumiza, uchongezi. Porojo ni mazungumzo ya kupisha wakati kuhusu watu na maisha yao. Je, porojo zote ni mbaya? Hapana, ikiwa mazungumzo yetu si ya kuumiza, ambayo huenda yanahusu habari nzuri au za maana, kama vile mtu aliyebatizwa karibuni au anayehitaji kutiwa moyo. Wakristo wa karne ya kwanza walipendezwa sana na hali ya wengine nao walizungumzia habari zinazofaa kuhusu waamini wenzao. (Waefeso 6:21, 22; Wakolosai 4:8, 9) Hata hivyo, porojo inaweza kuumiza ikiwa inapotosha mambo au inaingilia mambo ya kibinafsi. Inaweza kuongoza kwenye uchongezi wenye kudhuru, jambo ambalo ni zito hata zaidi. Uchongezi ni “kusema mambo ya uwongo . . . ambayo yanamvunjia mtu heshima na kumharibia sifa.” Kwa mfano, Mafarisayo walitumia uchongezi wenye hila ili kumharibia Yesu sifa. (Mathayo 9:32-34; 12:22-24) Mara nyingi uchongezi husababisha ugomvi.—Methali 26:20.

12 Kutumia uwezo wa kusema kuwavunjia wengine heshima au kusababisha migawanyiko ni jambo zito machoni pa Yehova. Anachukia wale wanaotokeza “magomvi kati ya ndugu.” (Methali 6:16-19) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mchongezi” ni di·aʹbo·los, ambalo pia ni jina la Shetani. Yeye ndiye “Ibilisi,” yule mwovu anayemchongea Mungu. (Ufunuo 12:9, 10) Bila shaka, tunataka kuepuka usemi unaoweza kutufanya tuwe maibilisi. Uchongezi ambao unatokeza matendo ya mwili kama vile “magomvi” na “migawanyiko” haupaswi kuwepo katika kutaniko. (Wagalatia 5:19-21) Hivyo, kabla ya kuwaambia wengine habari fulani ulizosikia kuhusu mtu fulani, jiulize: ‘Habari hizo ni za kweli? Ni jambo la fadhili kuwaambia wengine? Je, inafaa au ni jambo la hekima kueneza habari hiyo?’—1 Wathesalonike 4:11.

13, 14. (a) Mtu anaweza kuhisi jinsi gani anapotukanwa? (b) Matukano ni nini, na kwa nini mtukanaji anajihatarisha?

13 Matukano. Kama ilivyotajwa tayari, maneno yanaweza kuumiza. Ni kweli kwamba nyakati nyingine kwa sababu ya kutokamilika, tunasema mambo ambayo baadaye tunajutia. Hata hivyo, Biblia inaonya kuhusu usemi ambao haupaswi kutumiwa katika nyumba ya Kikristo au kutanikoni. Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Tafsiri nyingine zinatafsiri neno “matukano” kuwa “maneno maovu,” “usemi wenye kuumiza,” na “matusi.” Matukano, yanayotia ndani matusi na kuchambua-chambua watu kwa ukali, yanaweza kuwashushia wengine heshima na kuwafanya wahisi kwamba hawafai. Kwa kuwa watoto wanaamini mambo haraka na ni wapole, wanaumia zaidi wanapotukanwa.—Wakolosai 3:21.

14 Biblia inashutumu vikali matukano, yaani, mazoea ya kuwavunjia wengine heshima kwa matusi, maneno ya dharau, au yenye kuaibisha. Mtu anayezoea kuwatukana wengine anajihatarisha, kwa kuwa mtukanaji anaweza kuondolewa kutanikoni asipobadilika baada ya kusaidiwa tena na tena. Asipobadili njia zake, anaweza pia kukosa baraka za Ufalme. (1 Wakorintho 5:11-13; 6:9, 10) Hivyo basi, hatuwezi kukaa katika upendo wa Mungu tukiwa na mazoea ya kusema mambo yasiyofaa, yasiyo ya kweli, au yenye kuumiza. Maneno ya aina hiyo yanabomoa.

MANENO AMBAYO NI ‘MEMA KWA AJILI YA KUJENGA’

15. Ni maneno gani yaliyo ‘mema kwa ajili ya kujenga’?

15 Ni kwa njia gani tunaweza kutumia uwezo wetu wa kusema kama vile Yehova alivyokusudia? Kumbuka kwamba Neno la Mungu linatuhimiza tuseme “neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga.” (Waefeso 4:29) Yehova anafurahi tunaposema maneno yanayojenga, yanayotia moyo, na yanayowaimarisha wengine. Ili kusema maneno yanayofaa tunahitaji kufikiri kwa makini. Biblia haitoi utaratibu fulani unaopaswa kutumika katika mazungumzo; wala haina orodha ya “maneno yenye afya” yanayokubalika. (Tito 2:8) Ili tuseme maneno yaliyo ‘mema kwa ajili ya kujenga,’ tunahitaji kukumbuka mambo matatu ya maana yanayofanya usemi uwe wenye kujenga: Usemi huo unapaswa kuwa wenye kufaa, wa kweli, na wenye fadhili. Tukiwa na hayo akilini, acheni tuchunguze mifano michache ya usemi unaojenga.—Ona sanduku “ Je, Usemi Wangu Unajenga?”.

16, 17. (a) Kwa nini tuwapongeze wengine? (b) Kuna nafasi gani za kuwapongeza wengine kutanikoni? katika familia?

16 Pongezi zinazotoka moyoni. Yehova na Yesu wanatambua uhitaji wa kutoa pongezi. (Mathayo 3:17; 25:19-23; Yohana 1:47) Tukiwa Wakristo, inafaa pia tuwapongeze wengine kwa unyoofu. Kwa nini? Andiko la Methali 15:23 linasema: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” Jiulize: ‘Mimi hujisikia namna gani ninapopongezwa kikweli? Bila shaka, ninachangamka na kuhisi nimetiwa moyo.’ Ndiyo, unapopongezwa kikweli unahisi kwamba mtu fulani anakutambua, anakujali, na kwamba jambo ulilofanya lilifaa. Uhakikisho huo unafanya ujiamini na kukuchochea ujitahidi hata zaidi wakati ujao. Kwa kuwa unathamini kupongezwa, je, haifai hata wewe ujitahidi sana kuwapongeza wengine?—Mathayo 7:12.

17 Jizoeze kuona sifa nzuri za wengine, kisha uwapongeze. Kutanikoni, huenda ukasikia hotuba nzuri, ukaona kijana anayejitahidi kufikia miradi ya kiroho, au ukamwona mtu mwenye umri mkubwa ambaye anahudhuria mikutano kwa uaminifu ingawa ana matatizo ya uzee. Watu hao wanapopongezwa kikweli wanaweza kuguswa moyo na kuimarishwa kiroho. Katika familia, waume na wake wanahitaji kusikia wakipongezwa kwa uchangamfu na kuthaminiwa na wenzi wao. (Methali 31:10, 28) Watoto hasa hufurahi wanapoona kwamba wanatambuliwa na kuthaminiwa. Kama vile mmea unavyositawi unapopata mwangaza wa jua na maji, ndivyo watoto wanavyositawi wanapopongezwa na kuthaminiwa. Wazazi, msikose kamwe kuwapongeza watoto wenu kwa ajili ya sifa zao nzuri na bidii yao. Pongezi kama hizo zinaweza kuwafanya watoto wenu wawe hodari na wajiamini na hivyo kuwachochea hata zaidi kutenda mema.

18, 19. Kwa nini tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuwafariji na kuwaliwaza waamini wenzetu, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

18 Kufariji na kuliwaza. Yehova anawajali sana “watu wa hali ya chini” na “wale wanaopondwa.” (Isaya 57:15) Neno lake linatuhimiza ‘tuendelee kufarijiana na kujengana’ na ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:11, 14) Tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba Mungu anatambua na anathamini jitihada zetu za kuwafariji na kuwaliwaza waamini wenzetu ambao wamelemewa na huzuni moyoni.

Yehova anafurahi tunaposema maneno yanayojenga wengine

19 Hata hivyo, unaweza kusema nini ili kumjenga Mkristo mwenzako aliyevunjika moyo au kushuka moyo? Usihisi kwamba ni lazima utatue tatizo lake. Mara nyingi, maneno machache ndiyo husaidia zaidi. Mhakikishie mtu huyo kwamba unamjali. Sali pamoja naye; unaweza kumsihi Yehova amsaidie kujua kwamba anapendwa sana na Mungu na vilevile wengine. (Yakobo 5:14, 15) Mhakikishie kwamba yeye ni mshiriki wa kutaniko ambaye anahitajiwa na kuthaminiwa sana. (1 Wakorintho 12:12-26) Msomee Andiko lenye kutia moyo ili kumhakikishia kwamba Yehova anamhangaikia kikweli. (Zaburi 34:18; Mathayo 10:29-31) Kutumia wakati wetu pamoja na mtu aliyeshuka moyo na kumwambia “neno lililo jema” kutafanya ahisi kwamba anapendwa na kuthaminiwa.—Methali 12:25.

20, 21. Ni mambo gani yanayofanya shauri liwe lenye matokeo mazuri?

20 Shauri lenye matokeo. Kwa kuwa hatujakamilika, sote tunahitaji shauri mara kwa mara. Biblia inatuhimiza hivi: “Sikiliza shauri na kukubali nidhamu, ili upate kuwa na hekima katika wakati wako ujao.” (Methali 19:20) Kutoa shauri si jukumu la wazee peke yao. Wazazi huwashauri watoto. (Waefeso 6:4) Huenda akina dada wakomavu wakahitaji kuwashauri wanawake vijana. (Tito 2:3-5) Kuwapenda wengine kunatuchochea kutoa shauri ambalo linaweza kukubaliwa bila kumuumiza anayeshauriwa. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutoa shauri kama hilo? Fikiria mambo matatu yanayofanya shauri liwe lenye na matokeo mazuri: mtazamo na nia ya mshauri, msingi wa shauri, na jinsi shauri linavyotolewa.

21 Shauri zuri linategemea mtazamo wa yule anayelitoa. Jiulize, ‘Ni wakati gani inapokuwa rahisi kwangu kukubali shauri?’ Unapojua kwamba yule anayekushauri anakujali na kwamba hazungumzi nawe kwa sababu amekasirika wala hana nia yoyote mbaya, inakuwa rahisi kukubali shauri. Kwa hiyo, unapowashauri wengine, je, hupaswi kuwa na mtazamo na nia hiyohiyo? Shauri zuri pia hutegemea Neno la Mungu. (2 Timotheo 3:16) Iwe tunanukuu Biblia moja kwa moja au hapana, shauri letu linapaswa kuwa na msingi wa Kimaandiko. Hivyo, wazee huwa waangalifu wasiwalazimishie wengine maoni yao wenyewe; wala hawapindi au kupotosha Maandiko, kwa kufanya ionekane kana kwamba Biblia inaunga mkono maoni yao ya kibinafsi. Shauri pia huwa na matokeo mazuri zaidi likitolewa kwa njia inayofaa. Shauri linapotolewa kwa fadhili, inakuwa rahisi zaidi kulikubali, nalo halimwaibishi mwenye kushauriwa.—Wakolosai 4:6.

22. Utaitumia jinsi gani zawadi yako ya usemi?

22 Kwa kweli, uwezo wa kusema ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Kumpenda Yehova kunapaswa kutuchochea tuitumie zawadi hiyo, bali si kuitumia vibaya. Na tukumbuke kwamba maneno tunayowaambia wengine yanaweza kujenga au kubomoa. Acheni basi tutumie zawadi hiyo kama Mpaji alivyokusudia, yaani, “kwa ajili ya kujenga.” Hivyo, usemi wetu utawaburudisha wale walio karibu nasi na utatuwezesha kukaa katika upendo wa Mungu.

^ fu. 4 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘potovu’ kwenye Methali 15:4 linaweza pia kumaanisha “kombo,” au “kaidi.”

^ fu. 7 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ubatili” linaweza pia kutafsiriwa “bure” na “-siozaa matunda.”—1 Wakorintho 15:17; 1 Petro 1:18.

^ fu. 10 Neno “uchafu” kama linavyotumiwa katika Maandiko ni neno pana na linaweza kutia ndani dhambi za aina mbalimbali. Ingawa si uchafu wa kila aina unaochukuliwa hatua ya kihukumu, mtu ambaye amezoea mwenendo mchafu sana anaweza kutengwa na ushirika wa kutaniko.—2 Wakorintho 12:21; Waefeso 4:19; ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2006.