Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 14

Uwe Mnyoofu Katika Mambo Yote

Uwe Mnyoofu Katika Mambo Yote

“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—WAEBRANIA 13:18.

1, 2. Kwa nini Yehova anafurahi anapoona tukijitahidi kuwa wanyoofu? Toa mfano.

MAMA na mwana wake mdogo wanatoka dukani. Ghafula, mtoto huyo anashtuka na kusimama. Mkononi mwake, ana kitu cha kuchezea ambacho alichukua dukani. Alisahau kukirudisha au kumwomba mama yake amnunulie. Akiwa na wasiwasi, anamuuliza mama yake afanye nini. Mama anamtuliza na kuandamana pamoja naye mpaka dukani ili arudishe kitu hicho na kuomba msamaha. Mama anafurahi sana na kujivunia mtoto wake. Kwa nini?

2 Wazazi hufurahi sana wanapoona watoto wao wakijifunza faida za kuwa wanyoofu. Ndivyo pia anavyohisi Baba yetu wa mbinguni, “Mungu wa ukweli.” (Zaburi 31:5) Anapotutazama tukiendelea kukua ili kufikia ukomavu wa kiroho, anafurahi kuona tunajitahidi kuwa wanyoofu. Kwa kuwa tunataka kumpendeza na kukaa katika upendo wake, tunakubaliana na maneno haya ya mtume Paulo: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Acheni tuchunguze sehemu nne kuu za maisha yetu ambazo huenda nyakati nyingine ikawa vigumu kuwa wanyoofu. Kisha tutazungumzia baraka fulani zinazotokana na kufanya hivyo.

KUJICHUNGUZA KWA UNYOOFU

3-5. (a) Neno la Mungu linatupa maonyo gani kuhusu hatari za kujidanganya? (b) Ni nini kitakachotusaidia kujichunguza kwa unyoofu?

3 Kwanza tunahitaji kujifunza jinsi ya kujichunguza kwa unyoofu. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, ni rahisi sana kujidanganya. Kwa mfano, Yesu aliwaambia Wakristo wa Laodikia kwamba wamejidanganya kwa kufikiri kwamba wao ni matajiri, ingawa kwa kweli, wao ni “maskini na kipofu na uchi” kiroho—hali yenye kusikitisha kwelikweli. (Ufunuo 3:17) Kujidanganya kulifanya wawe hatarini.

4 Huenda pia ukakumbuka kwamba mwanafunzi Yakobo alionya hivi: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.” (Yakobo 1:26) Tukifikiri kwamba tunaweza kutumia ulimi wetu vibaya na bado Yehova aikubali ibada yetu, tunajidanganya. Ibada yetu kwa Yehova itakuwa bure—hasara tupu. Ni nini kinachoweza kutuepusha na hali hiyo yenye kusikitisha?

5 Katika sura hiyohiyo, Yakobo analinganisha kweli ya neno la Mungu na kioo. Anatushauri tuchunguze sheria kamilifu ya Mungu na kufanya marekebisho yanayohitajiwa. (Yakobo 1:23-25) Biblia inaweza kutusaidia kujichunguza kwa unyoofu na kutambua mambo tunayohitaji kurekebisha. (Maombolezo 3:40; Hagai 1:5) Pia, tunaweza kusali kwa Yehova na kumwomba atuchunguze, na kutusaidia kutambua na kushughulikia udhaifu wowote mkubwa tulio nao. (Zaburi 139:23, 24) Kutokuwa mnyoofu ni udhaifu usiotambulika kwa urahisi, nasi tunahitaji kuwa na maoni ya Baba yetu wa mbinguni kuhusu jambo hilo. Andiko la Methali 3:32 linasema: “Mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.” Yehova anaweza kutusaidia kuwa na maoni kama yake na kujichunguza kama vile anavyotuchunguza. Kumbuka kwamba Paulo alisema: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” Hatuwezi kuwa wakamilifu sasa, lakini kwa kweli tunataka na tunajitahidi juu chini kuwa wanyoofu.

UNYOOFU KATIKA FAMILIA

Kuwa wanyoofu hutusaidia kuepuka kufanya mambo ambayo hayafai, hata tunapokuwa peke yetu

6. Kwa nini wenzi wa ndoa wanapaswa kutendeana kwa unyoofu, na wanaepuka hatari gani wanapofanya hivyo?

6 Familia ya Kikristo inapaswa kutambuliwa kwa unyoofu. Kwa hiyo, mume na mke wanapaswa kusema mambo waziwazi na kwa unyoofu. Wenzi wa ndoa Wakristo hawapaswi kufanya mambo machafu na yenye kuumiza kama vile kuchezeana kimapenzi na watu walio nje ya ndoa, kuwa na uhusiano wa siri katika Intaneti, au kutumia ponografia ya aina yoyote ile. Wenzi fulani wa ndoa wamejihusisha na mwenendo mbaya kama huo na kuwaficha wenzi wao mambo hayo. Huo si unyoofu. Ona maneno haya ya Mfalme Daudi mwaminifu: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zaburi 26:4) Ikiwa umefunga ndoa, usijihusishe kamwe na mwenendo ambao unaweza kukushawishi kumficha mwenzi wako jinsi ulivyo!

7, 8. Ni mifano gani ya Biblia inayoweza kuwasaidia watoto kujifunza faida za kuwa wanyoofu?

7 Wazazi wanapowafundisha watoto wao faida za kuwa wanyoofu, inafaa watumie mifano ya Biblia. Masimulizi ya watu ambao hawakuwa wanyoofu yanatia ndani yale ya Akani, ambaye aliiba na kujaribu kuficha tendo hilo; Gehazi, ambaye alidanganya ili ajifaidi kifedha; na Yuda, aliyeiba na kumchongea Yesu kwa chuki ili auawe.—Yoshua 6:17-19; 7:11-25; 2 Wafalme 5:14-16, 20-27; Mathayo 26:14, 15; Yohana 12:6.

8 Masimulizi ya watu waliokuwa wanyoofu yanatia ndani yale ya Yakobo, ambaye aliwahimiza wana wake warudishe pesa ambazo walipata katika mifuko yao kwa sababu alihisi kwamba huenda ziliwekwa humo kimakosa; masimulizi kuhusu Yeftha na binti yake, ambao walitimiza nadhiri ya Yeftha kwa kujidhabihu sana; na masimulizi kuhusu Yesu, ambaye alijitambulisha kwa uhodari mbele ya umati wenye fujo ili kutimiza unabii na kuwalinda marafiki wake. (Mwanzo 43:12; Waamuzi 11:30-40; Yohana 18:3-11) Mifano hiyo michache ni kati ya hazina nyingi zilizo katika Neno la Mungu ambazo zinaweza kuwasaidia wazazi kuwafundisha watoto wao kupenda na kuthamini unyoofu.

9. Wazazi wanapaswa kuepuka nini ikiwa wanataka kuwawekea watoto wao mfano wa kuwa wanyoofu, na kwa nini mfano wao ni wa maana?

9 Mafundisho hayo yanawapa wazazi wajibu fulani wa maana. Mtume Paulo aliuliza: “Hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba?” (Waroma 2:21) Wazazi fulani huwachanganya watoto wao kwa kuwafundisha kuhusu unyoofu hali wao wenyewe si wanyoofu. Wanapoiba vitu vidogo-vidogo na kusema uwongo, huenda wakatoa visingizio ili kujitetea, labda kwa kusema “Ah, wakubwa hawajali hata tukichukua vitu hivi” au “Huo ni uwongo mdogo tu.” Lakini, kusema kweli, wizi ni wizi, haidhuru kitu kilichoibwa kina thamani gani, na uwongo ni uwongo, haidhuru mazungumzo ni juu ya nini au uwongo wenyewe ni mkubwa kadiri gani. * (Luka 16:10) Ni rahisi kwa watoto kutambua unafiki, na wanaweza kuathiriwa vibaya sana. (Waefeso 6:4) Hata hivyo, wakijifunza kuwa wanyoofu kwa kuiga mifano ya wazazi wao, huenda siku moja wakawa watu wazima wanaomtukuza Yehova katika ulimwengu huu usio na unyoofu.—Methali 22:6.

UNYOOFU KUTANIKONI

10. Tunapojitahidi kuzungumza kwa unyoofu pamoja na waamini wenzetu, tunahitaji kuwa waangalifu kuhusiana na mambo gani?

10 Tunaposhirikiana na Wakristo wenzetu tunapata nafasi nyingi za kuonyesha unyoofu. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 12, tunahitaji kuwa waangalifu kuhusiana na jinsi tunavyotumia zawadi ya usemi, hasa tunapokuwa na ndugu na dada zetu wa kiroho. Mazungumzo ya kawaida yanaweza kugeuka kuwa porojo yenye kudhuru, na hata uchongezi! Tukiwaambia wengine jambo ambalo halijathibitishwa, huenda tukachangia kueneza uwongo, hivyo ni afadhali kuzuia midomo yetu. (Methali 10:19) Kwa upande mwingine, tunaweza kujua kwamba jambo fulani ni la kweli, lakini si lazima tuliseme. Kwa mfano, huenda jambo hilo halituhusu ndewe wala sikio, au huenda isiwe jambo la fadhili kulitaja. (1 Wathesalonike 4:11) Watu fulani hutetea ukaidi wao wakidai kwamba wanasema mambo kwa unyoofu, lakini sikuzote maneno yetu yanapaswa kuwa yenye neema na yenye fadhili.—Wakolosai 4:6.

11, 12. (a) Watu fulani wanaofanya dhambi nzito huzidisha tatizo lao kwa njia gani? (b) Ni uwongo gani unaoenezwa na Shetani kuhusu dhambi nzito, nasi tunaweza kuupinga jinsi gani? (c) Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba sisi ni wanyoofu kwa tengenezo la Yehova?

11 Ni muhimu tuwe wanyoofu hasa tunaposhughulika na wale wanaoongoza kutanikoni. Watu fulani wanaofanya dhambi nzito huzidisha tatizo lao kwa kujaribu kuficha dhambi yao na kudanganya wakati wazee wa kutaniko wanapowauliza. Watu hao hata huanza kuishi maisha ya unafiki, kwa upande mmoja wanajifanya wanamtumikia Yehova na wakati huohuo wanaendelea kutenda dhambi nzito. Hivyo, inaweza kusemwa kwamba watu hao wanaishi maisha ya uwongo. (Zaburi 12:2) Wengine wanawaambia wazee ukweli kwa kadiri fulani huku wakificha habari muhimu. (Matendo 5:1-11) Mara nyingi udanganyifu kama huo unatokana na kuamini uwongo ambao Shetani anaeneza.—Ona sanduku “ Uwongo Ambao Shetani Anaeneza Kuhusu Dhambi Nzito.”

12 Tunapaswa pia kuwa wanyoofu kwa tengenezo la Yehova tunapojaza habari fulani zinazohitajiwa. Kwa mfano, tunaporipoti utendaji wetu katika huduma, tunakuwa waangalifu tusidanganye. Vivyo hivyo, tunapojaza fomu ya ombi la pendeleo fulani la utumishi, hatupaswi kamwe kujaza habari zisizo za kweli kuhusu afya yetu au mambo mengine yoyote yanayotuhusu.—Methali 6:16-19.

13. Ni kwa njia gani tunaweza kuendelea kuwa wanyoofu tunapokuwa na uhusiano wa kikazi pamoja na mwamini mwenzetu?

13 Tunashughulika kwa unyoofu na waamini wenzetu katika mambo ya kibiashara pia. Nyakati nyingine, huenda akina ndugu na dada Wakristo wakashirikiana kufanya biashara. Wanapaswa kuwa waangalifu wasichanganye mambo hayo na ibada yao katika Jumba la Ufalme au katika huduma. Huenda uhusiano wao wa kikazi ukawa ule wa tajiri na mfanyakazi. Tukiwaajiri akina ndugu au dada, tuhakikishe kwamba tunawatendea kwa unyoofu, tunawalipa kwa wakati, tunawalipa mshahara ambao tumekubaliana, na kuwatimizia mambo mengine ambayo wafanyakazi wanastahili kulingana na sheria za nchi. (1 Timotheo 5:18; Yakobo 5:1-4) Kwa upande mwingine, ikiwa tumeajiriwa na ndugu au dada, tutafanya kikamili kazi tunayolipwa kufanya. (2 Wathesalonike 3:10) Hatutazamii kutendewa kwa njia ya pekee eti kwa sababu ya uhusiano wetu wa kiroho, kana kwamba tajiri wetu anawajibika kutupa likizo au marupurupu mengine ambayo wafanyakazi wengine hawapewi.—Waefeso 6:5-8.

14. Wakristo wanapofanya biashara ya pamoja, wanapaswa kuchukua hatua gani ya hekima, na kwa nini?

14 Namna gani ikiwa biashara ya pamoja inahusisha rasilimali fulani au mkopo? Biblia inatoa kanuni muhimu inayoweza kutumika: Andikianeni mambo yote! Kwa mfano, Yeremia aliponunua shamba, alitayarisha nakala mbili za hati, kukiwa na mashahidi, naye akazihifadhi mahali salama ili ziweze kurejelewa siku za baadaye. (Yeremia 32:9-12; ona pia Mwanzo 23:16-20.) Tunapofanya biashara pamoja na waamini wenzetu, kuandika habari zote katika hati iliyotayarishwa vizuri, ikatiwa sahihi, na kushuhudiwa na mashahidi hakumaanishi hatuwaamini. Badala yake, kufanya hivyo kunazuia hali ya kutoelewana, kuvunjwa moyo, na hata mizozo inayoweza kusababisha migawanyiko. Wakristo wowote wanaofanya biashara na waamini wenzao wanapaswa kukumbuka kwamba biashara yoyote ile haipaswi kuhatarisha umoja na amani ya kutaniko. *1 Wakorintho 6:1-8.

UNYOOFU KATIKA SHUGHULI ZA KIMWILI

15. Yehova ana maoni gani kuhusu mazoea ya kibiashara yenye udanganyifu, na Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mazoea hayo yaliyoenea sana?

15 Mkristo anapaswa kuwa mnyoofu hata nje ya kutaniko. Paulo alisema: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Muumba wetu anatazamia tuwe wanyoofu katika shughuli za kibiashara. Katika kitabu cha Methali peke yake, mizani ya udanganyifu inazungumziwa katika mistari minne. (Methali 11:1; 16:11; 20:10, 23) Zamani za kale, kwa kawaida watu walitumia mizani na mawe ya mizani katika shughuli za kibiashara ili kupima uzito wa bidhaa zilizonunuliwa na pesa zilizotumiwa kuzilipia. Wanabiashara wasio wanyoofu walitumia mizani yenye kasoro na aina mbili za mawe ya mizani ili kuwadanganya na kuwaibia wateja wao. * Yehova anachukia matendo kama hayo! Ili kukaa katika upendo wake, tunapaswa kuepuka kabisa mazoea yote ya kibiashara yenye udanganyifu.

16, 17. Watu wengi ulimwenguni leo wanajihusisha na mazoea gani ya udanganyifu, na Wakristo wa kweli wameazimia kufanya nini?

16 Kwa kuwa Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu, haishangazi kwamba ukosefu wa unyoofu umeenea ulimwenguni pote. Kila siku huenda tukashawishiwa kutokuwa wanyoofu. Watu wanaotafuta kazi wanapoandika ripoti kuhusu sifa zao za kustahili kazi hiyo, mara nyingi wao hudanganya na kutia chumvi kuhusu kiwango cha elimu yao na uzoefu walio nao. Watu wanapojaza fomu za uhamiaji, kodi, bima, na kadhalika, mara nyingi wanatoa majibu yasiyo ya kweli ili kupata wanachotaka. Wanafunzi wengi huiba mtihani au kutumia habari za Intaneti kwa njia isiyo halali wanapoandika ripoti za shule na hivyo kudanganya kwamba walitumia akili zao na kumbe walitegemea jasho la mwingine. Na watu wanaposhughulika na maofisa wafisadi, mara nyingi wao huwapa “kitu kidogo” ili wapate wanachotaka. Mambo hayo hayatushangazi kwa kuwa watu wengi sana katika ulimwengu ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiopenda wema.”—2 Timotheo 3:1-5.

17 Wakristo wa kweli wameazimia kutojihusisha na mazoea hayo. Jambo ambalo linafanya iwe vigumu nyakati nyingine kuwa wanyoofu ni kwamba watu wanaojihusisha katika matendo yasiyo ya unyoofu huonekana kuwa wamefanikiwa na hata kupiga hatua katika ulimwengu wa leo. (Zaburi 73:1-8) Wakati huohuo, huenda Wakristo wakapata hasara kwa sababu wanataka kuendelea kuwa wanyoofu “katika mambo yote.” Basi, je, kweli kuna haja ya kujikakamua kuwa mnyoofu? Hakika! Kwa nini? Unyoofu huleta baraka gani?

BARAKA ZA KUWA WANYOOFU

18. Kwa nini kujulikana kuwa mnyoofu ni jambo lenye thamani sana?

18 Kati ya mambo machache yenye thamani sana maishani ni kujulikana kuwa mtu mnyoofu anayeaminika. (Ona sanduku “ Mimi Ni Mnyoofu Kadiri Gani?”) Amini usiamini, mtu yeyote anaweza kuwa na sifa hiyo! Haitegemei kipawa, mali, sura, cheo, au hali nyingine yoyote inayopita uwezo wako. Hata hivyo, watu wengi hushindwa kuwa na sifa hiyo iliyo kama hazina yenye thamani. Ni sifa ya wachache. (Mika 7:2) Huenda wengine wakakudhihaki kwa kuwa mnyoofu, lakini wengine watakuthamini, watakuheshimu, na kukuamini. Hata Mashahidi wengi wa Yehova wamefaidika kifedha kwa sababu ya kuwa wanyoofu. Wamedumisha kazi zao wakati ambapo wafanyakazi wenzao wamepigwa kalamu, nao wamepata kazi wakati ambapo wafanyakazi wanyoofu wametakikana sana.

19. Kuwa wanyoofu nyakati zote kunaweza kuwa na matokeo gani kwa dhamiri yetu na uhusiano wetu pamoja na Yehova?

19 Iwe umepata au hujapata baraka hizo, utaona kwamba unyoofu huleta baraka nyingi hata zaidi. Utapata baraka ya kuwa na dhamiri safi. Paulo aliandika: “Tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu.” (Waebrania 13:18) Zaidi ya hilo, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo hakosi kamwe kutambua jina lako jema, naye anawapenda watu wanyoofu. (Zaburi 15:1, 2; Methali 22:1) Ndiyo, kuwa mnyoofu kunakusaidia kukaa katika upendo wa Mungu, na hiyo ndiyo thawabu kubwa zaidi tunayoipigania. Acheni sasa tufikirie jambo lingine linalohusiana na mambo ambayo tumezungumzia: Maoni ya Yehova kuhusu kazi.

^ fu. 9 Katika kutaniko, mtu anapozoea kusema uwongo kimakusudi ili kuwaumiza wengine, huenda wazee wakahitaji kumchukulia hatua ya kihukumu.

^ fu. 14 Ili ujue yale unayoweza kufanya matatizo yanapotokea katika mapatano ya kibiashara, chunguza nyongeza “Kutatua Mizozo ya Kibiashara.”

^ fu. 15 Walitumia aina moja ya mawe ya mizani waliponunua vitu na ile nyingine walipouza vitu, na katika visa vyote viwili walijifaidi wenyewe tu. Pia, nyakati nyingine walitumia mizani ambayo upande wake mmoja ulikuwa mrefu zaidi au mzito zaidi ya ule mwingine ili kumdanganya mteja wakati wowote ule.