Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 16

Mpinge Ibilisi na Hila Zake

Mpinge Ibilisi na Hila Zake

‘Mpingeni Ibilisi, naye atakimbia.’—YAKOBO 4:7.

1, 2. Ni nani wanaofurahia pindi za ubatizo?

IKIWA umekuwa ukimtumikia Yehova kwa miaka mingi, bila shaka umesikia hotuba nyingi za ubatizo katika makusanyiko yetu. Hata hivyo, hata uwe umehudhuria pindi hizo mara nyingi kadiri gani, huenda bado unasisimuka kila mara unapowaona wale walioketi kwenye viti vya mbele wakisimama ili kujitoa kwa ajili ya ubatizo. Wakati huo, wote waliohudhuria husisimuka kwelikweli, na kupiga makofi kwa uchangamfu. Huenda ukalengwalengwa na machozi unapotazama kwa mara nyingine tena kikundi cha watu wenye thamani ambao wamechukua msimamo upande wa Yehova. Tunafurahi kama nini katika pindi kama hizo!

2 Ingawa tunajionea ubatizo mara chache kwa mwaka katika maeneo yetu, malaika wana pendeleo la kuona ubatizo mara nyingi zaidi. Hebu wazia ‘shangwe inayokuwa mbinguni,’ wanapoona maelfu ya watu ulimwenguni pote wakijiunga na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova kila juma! (Luka 15:7, 10) Bila shaka, malaika husisimuka sana kuona ongezeko hilo!—Hagai 2:7.

IBILISI “ANATEMBEA HUKU NA HUKU KAMA SIMBA ANAYENGURUMA”

3. Kwa nini Shetani anatembea huku na huku “kama simba anayenguruma,” naye anataka kufanya nini?

3 Kwa upande mwingine, kuna viumbe wengine wa roho ambao huwaka hasira katika pindi hizo za ubatizo. Shetani na roho wake waovu hukasirika sana wanapoona maelfu ya watu wakiukataa katakata ulimwengu huu wenye ufisadi. Sababu ni kwamba Shetani alidai kwa majivuno eti hakuna mwanadamu anayeweza kumtumikia Yehova akichochewa na upendo wa kweli na eti hakuna yeyote anayeweza kuendelea kuwa mwaminifu anapojaribiwa vikali. (Ayubu 2:4, 5) Kila mara mtu anapoamua kujiweka wakfu kwa Yehova, Shetani anathibitishwa kuwa mwongo. Ni kana kwamba Shetani anazabwa maelfu ya makofi kila juma. Ndiyo sababu haishangazi kwamba “anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu”! (1 Petro 5:8) “Simba” huyo anatamani kutumeza kiroho na kuharibu au hata kuvunja uhusiano wetu pamoja na Mungu.—Zaburi 7:1, 2; 2 Timotheo 3:12.

Kila mara mtu anapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, Shetani anathibitishwa kuwa mwongo

4, 5. (a) Yehova ameuwekea vizuizi uwezo wa Shetani katika njia gani mbili? (b) Mkristo wa kweli anaweza kuwa na uhakika gani?

4 Ingawa tuna adui mkali, hakuna haja ya kuogopa. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ameuwekea vizuizi uwezo wa ‘simba huyo anayenguruma’ katika njia mbili kuu. Njia gani? Kwanza, Yehova ametabiri kwamba “umati mkubwa” wa Wakristo wa kweli utaokoka “dhiki kuu” inayokuja. (Ufunuo 7:9, 14) Unabii wa Mungu hauwezi kukosa kutimia. Hivyo basi, hata Shetani mwenyewe anajua kwamba hawezi kuwashinda watu wote wa Mungu wakiwa kikundi.

5 Njia ya pili inaonekana katika maneno yaliyosemwa na mmoja kati ya watu wa kale waliokuwa waaminifu kwa Mungu. Nabii Azaria alimwambia hivi Mfalme Asa: “Yehova yuko pamoja nanyi ikiwa ninyi mko pamoja naye.” (2 Mambo ya Nyakati 15:2; 1 Wakorintho 10:13) Mifano mingi ya kale iliyoandikwa inaonyesha kwamba hakuna wakati ambapo Shetani alifaulu kummeza mtumishi yeyote wa Mungu mwenye uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. (Waebrania 11:4-40) Leo, Mkristo anayeendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, atafaulu kumpinga na hata kumshinda Ibilisi. Kwa hakika, Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yakobo 4:7.

“TUNA KUSHINDANA MWELEKA . . . JUU YA MAJESHI YA ROHO WAOVU”

6. Shetani anapigana jinsi gani na Mkristo mmoja-mmoja?

6 Katika vita hivyo vya mfano, Shetani hawezi kuwashinda watu wa Yehova wakiwa kikundi, hata hivyo, sisi mmoja-mmoja tunaweza kushindwa tusipokaa macho. Shetani anajua kwamba anaweza kutumeza akidhoofisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Shetani anatumia njia gani ili kufanya hivyo? Kwa kutushambulia vikali, moja kwa moja, na kwa kutumia hila. Acheni tuzungumzie njia hizo kuu ambazo Shetani anatumia.

7. Kwa nini Shetani amezidisha mashambulizi yake juu ya watu wa Yehova?

7 Mashambulizi makali. Mtume Yohana alisema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Maneno hayo yana onyo kwa Wakristo wote wa kweli. Kwa kuwa tayari Shetani amemeza ulimwengu mzima wa wanadamu wasiomwogopa Mungu, sasa anaweza kuzidisha mashambulizi yake na kukaza fikira juu ya wale ambao wamemponyoka, yaani, watu wa Yehova. (Mika 4:1; Yohana 15:19; Ufunuo 12:12, 17) Ana hasira kali kwa sababu anajua ana muda mfupi. Kwa hiyo amezidisha jitihada zake. Leo, anajitahidi kufa na kupona kutushambulia kikatili na kutuangamiza. Kwa hiyo, sasa kuliko wakati mwingine wowote, tunahitaji ‘kutambua nyakati ili kujua yale ambayo tunapaswa kufanya.’—1 Mambo ya Nyakati 12:32.

8. Mtume Paulo anamaanisha nini anaposema tuna kushindana “mweleka” juu ya roho waovu?

8 Kushindana mweleka. Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wenzake hivi: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Kwa nini Paulo alitumia neno “mweleka”? Kwa sababu neno hilo lina wazo la kumenyana mkono kwa mkono na kupambana karibu-karibu. Kwa hiyo, Paulo alitumia neno hilo kukazia kwamba kila mmoja wetu anapigana kibinafsi na roho waovu. Iwe tunaishi katika nchi ambako kuna itikadi nyingi kuhusu roho waovu au sivyo, tusisahau hata kidogo kwamba tulipojiweka wakfu kwa Yehova, ni kana kwamba tuliingia katika jukwaa la mweleka. Angalau kuanzia wakati anapojiweka wakfu, kila Mkristo anaingia vitani. Ndiyo sababu Paulo aliona uhitaji wa kuwahimiza mara tatu Wakristo waliokuwa katika jiji la Efeso ‘wasimame imara’!—Waefeso 6:11, 13, 14.

9. (a) Kwa nini Shetani na roho wake waovu wanatumia “hila” mbalimbali? (b) Kwa nini Shetani hujaribu kuchafua akili zetu, na tunaweza kufanya nini ili kupinga jitihada zake? (Ona sanduku “ Jihadhari Na Ujanja Wa Shetani!”) (c) Tutazungumzia hila gani?

9 Mbinu zenye hila. Paulo anawahimiza Wakristo wasimame imara ili kuzipinga “hila za” Shetani. (Waefeso 6:11) Ona kwamba Paulo hasemi “hila ya” bali “hila za.” Roho waovu hawatumii hila moja tu bali wana hila nyingi—na wana sababu ya kufanya hivyo. Kadiri muda unavyopita, waamini fulani ambao wamesimama imara na kupinga aina moja ya jaribu wameshindwa baada ya kujaribiwa kwa njia nyingine. Hivyo, Ibilisi na roho wake waovu wanachunguza kwa makini mazoea ya kila mmoja wetu ili wapate kujua udhaifu wetu mkubwa zaidi. Kisha wanalenga udhaifu wowote wa kiroho ambao huenda tukawa nao. Hata hivyo, jambo la kupendeza ni kwamba tunaweza kutambua njia nyingi ambazo Ibilisi anatumia kwa kuwa zinatajwa katika Biblia. (2 Wakorintho 2:11) Mapema katika kitabu hiki tulizungumzia mbinu kama vile tamaa ya vitu vya kimwili, mashirika mabaya, na upotovu katika ngono. Sasa, acheni tuzungumzie hila nyingine ya Shetani—kuwasiliana na pepo.

KUWASILIANA NA PEPO NI USALITI

10. (a) Kuwasiliana na pepo ni nini? (b) Yehova ana maoni gani kuhusu mazoea ya kuwasiliana na pepo, na wewe una maoni gani?

10 Mtu anapowasiliana na pepo, au roho waovu, anakuwa na uhusiano wa moja kwa moja na roho waovu. Uaguzi, ulozi, uchawi, na kuuliza habari kutoka kwa wafu ni njia mbalimbali za kuwasiliana na pepo. Kama tunavyojua, kuwasiliana na pepo ni “chukizo” machoni pa Yehova. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ufunuo 21:8) Kwa kuwa sisi pia tunapaswa ‘kuchukia maovu,’ hatuwezi hata kidogo kujaribu kushirikiana na roho waovu. (Waroma 12:9) Kufanya hivyo ni usaliti mbaya kama nini kwa Baba yetu wa mbinguni, Yehova!

11. Shetani akifaulu kutushawishi kuwasiliana na pepo, kwa nini huo unaweza kuwa ushindi mkubwa? Toa mfano.

11 Hata hivyo, kwa sababu kuwasiliana na pepo ni usaliti mkubwa kwa Yehova, Shetani ameazimia kufanya wengine kati yetu wajihusishe katika mazoea hayo. Kila mara Shetani anapomshawishi Mkristo ajihusishe katika mazoea ya kuwasiliana na pepo, ni ushindi mkubwa kwelikweli kwake. Kwa nini? Fikiria mfano huu: Ikiwa askari-jeshi angeshawishiwa kujitenga na kusaliti kikosi chao cha jeshi na kujiunga na jeshi la adui, jemadari wa jeshi adui angefurahi sana. Anaweza hata kumsimamisha msaliti huyo mbele ya wengine na kujivuna akimdhihaki jemadari wa jeshi lile lingine. Vivyo hivyo, Mkristo akiwasiliana na pepo, atakuwa akijitenga na Yehova kimakusudi na kujiunga waziwazi na upande wa Shetani. Wazia jinsi Shetani anavyoweza kufurahi akimtumia msaliti huyo ili kujivunia ushindi wake! Je, yeyote kati yetu angetaka kumpa Shetani ushindi kama huo? Hapana hata kidogo! Sisi si wasaliti.

MASWALI YANAYOTOKEZA SHAKA

12. Shetani anatumia mbinu gani ili kubadili maoni yetu kuhusu mazoea ya kuwasiliana na pepo?

12 Maadamu tunachukizwa kabisa na mazoea ya kuwasiliana na pepo, Shetani hataweza kutushinda kwa kutumia mbinu hiyo. Hivyo, anatambua kwamba lazima abadili maoni yetu. Jinsi gani? Anatafuta njia za kuvuruga akili za Wakristo ili wengine kati yao wafikiri kwamba “wema ni ubaya na ubaya ni wema.” (Isaya 5:20) Ili kufanya hivyo, mara nyingi Shetani hutumia moja kati ya mbinu ambazo ametumia kwa muda mrefu, yaani, maswali yanayotokeza shaka.

13. Ni kwa njia gani Shetani ametumia maswali yanayotokeza shaka?

13 Ona jinsi Shetani alivyotumia mbinu hiyo zamani. Katika Edeni alimuuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Katika siku za Ayubu, kulipokuwa na mkutano wa malaika mbinguni, Shetani aliuliza hivi: “Je, Ayubu amemwogopa Mungu bure?” Na mwanzoni mwa huduma ya Yesu duniani, Shetani alimjaribu Kristo kwa kusema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mikate.” Hebu wazia, katika kisa cha Yesu, Shetani alithubutu kumdhihaki Yehova akitumia maneno yaleyale ambayo Yehova mwenyewe alikuwa amesema majuma sita mapema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali”! —Mwanzo 3:1; Ayubu 1:9; Mathayo 3:17; 4:3.

14. (a) Shetani anatumia jinsi gani mbinu yake ya kutokeza shaka kuhusu kuwasiliana na pepo? (b) Tutazungumzia nini sasa?

14 Leo, Ibilisi anatumia mbinu kama hiyo ili kutokeza mashaka kuhusu ubaya wa kuwasiliana na pepo. Inasikitisha kwamba amefaulu kutokeza shaka katika akili za waamini fulani. Wameanza kutilia shaka ikiwa kweli aina fulani za kuwasiliana na pepo ni mbaya. Ni kana kwamba wanajiuliza, ‘Je, ni kweli?’ (2 Wakorintho 11:3) Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia watu hao wabadili maoni yao? Tunaweza kufanya nini ili tusishindwe na hila hiyo ya Shetani? Ili kujibu, acheni tuchunguze sehemu mbili za maisha ambazo Shetani ameingiza kwa ujanja mambo yanayohusiana na kuwasiliana na pepo. Sehemu hizo ni burudani na matibabu.

KUTUMIA KWA UJANJA TAMAA NA MAHITAJI YETU

15. (a) Watu wengi katika nchi za Ulaya na Amerika wana maoni gani kuhusu kuwasiliana na pepo? (b) Wakristo fulani wameathiriwa jinsi gani na maoni ya ulimwengu kuhusu kuwasiliana na pepo?

15 Hasa katika nchi za Ulaya na Amerika, nguvu za uchawi pamoja na njia nyingine za kuwasiliana na pepo huonwa kuwa mambo ya kawaida tu. Sinema, vitabu, vipindi vya televisheni, na michezo ya kompyuta inazidi kufanya mazoea ya kuwasiliana na pepo yaonekane kuwa yenye kufurahisha, ya ustadi, na yasiyo na hatari zozote. Watu wengi sana wanapenda sinema na vitabu fulani kuhusu uchawi hivi kwamba wapenzi wa hadithi hizo wameanzisha vikundi vyao vya kujadiliana na kusimuliana mambo hayo. Ni wazi kwamba roho waovu wamefaulu kuwafumba watu macho wasione hatari za uchawi. Je, Wakristo wameathiriwa na maoni hayo ya kwamba kuwasiliana na pepo si jambo zito? Wengine wameathiriwa. Kwa njia gani? Kwa mfano, baada ya Mkristo mmoja kutazama sinema kuhusu uchawi, alisema, “Nilitazama tu sinema hiyo, lakini sikuwa nikiwasiliana na pepo.” Kwa nini maoni hayo ni hatari?

16. Kwa nini ni hatari kuchagua burudani zenye mambo ya uchawi?

16 Ingawa kuna tofauti kati ya kuwasiliana na pepo na kutazama mazoea hayo, haimaanishi kwamba hakuna hatari ya kutazama mambo ya uchawi. Kwa nini? Fikiria hili: Kulingana na Neno la Mungu, inaonekana kwamba Shetani na roho wake waovu hawawezi kusoma fikira zetu. * Kwa hiyo, kama ilivyotajwa mwanzoni, ili kujua mawazo yetu na kutambua udhaifu wowote wa kiroho tulio nao, roho waovu huchunguza kwa makini matendo yetu kutia ndani burudani tunayochagua. Mwenendo wa Mkristo unapoonyesha kwamba anafurahia sinema au vitabu kuhusu watu wanaowasiliana na pepo, mizungu, kupagawa, au mambo mengine yanayohusiana na kuwasiliana na pepo, anawajulisha roho waovu jambo fulani. Anawafunulia udhaifu wake! Hivyo, roho waovu wanaweza kuzidisha mashambulizi yao juu ya Mkristo huyo ili kutumia udhaifu ambao amewafunulia mpaka watakapofaulu kumshinda. Kwa hakika, watu fulani ambao walianza kuvutiwa na mazoea ya kuwasiliana na pepo kwa sababu ya burudani zenye mambo ya uchawi mwishowe walijihusisha na mazoea hayo ya kuwasiliana na pepo.—Wagalatia 6:7.

Tafuta msaada wa Yehova unapokuwa mgonjwa

17. Shetani anaweza kutumia hila gani kuwashawishi wagonjwa?

17 Mbali na kutumia kwa ujanja tamaa yetu ya burudani, Shetani anatumia pia uhitaji wetu wa kupata matibabu. Jinsi gani? Mkristo ambaye afya yake inazidi kuzorota hata baada ya kujaribu kila njia ya kupata matibabu, anaweza kukata tamaa. (Marko 5:25, 26) Shetani na roho wake waovu wanaweza kutumia hali hiyo. Wanajua kwamba Neno la Mungu linaonya kuhusu kutafuta “usaidizi wa wale wanaozoea kufanya mambo yenye kudhuru.” (Isaya 31:2) Ili kumfanya Mkristo apuuze onyo hilo, roho waovu wanaweza kumshawishi mgonjwa ambaye hana tumaini lingine, atafute matibabu au kutumia mbinu zinazohusisha “nguvu za uchawi” au kuwasiliana na pepo—jambo ambalo ni hatari sana. Hila hiyo ya roho waovu ikifanikiwa, inaweza kudhoofisha uhusiano wake pamoja na Mungu. Kwa njia gani?

18. Ni aina gani za matibabu ambazo Mkristo anapaswa kuepuka, na kwa nini?

18 Yehova aliwaonya hivi Waisraeli waliogeukia “nguvu za uchawi”: “Mnaponyoosha mikono yenu, mimi huficha macho yangu kutoka kwenu. Hata mjapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi.” (Isaya 1:13, 15) Bila shaka, sikuzote tunataka kuepuka jambo lolote linaloweza kufanya sala zetu zizuiwe na kutopata msaada kutoka kwa Yehova—hasa tunapokuwa wagonjwa. (Zaburi 41:3) Kwa hiyo, ikiwa matibabu fulani au njia ya kupima ugonjwa inahusisha mazoea fulani ya kuwasiliana na pepo, Mkristo wa kweli anapaswa kuikataa. * (Mathayo 6:13) Kwa kufanya hivyo, ataendelea kupata msaada wa Yehova.—Ona sanduku “ Je, Kweli Ni Kuwasiliana na Pepo?

HADITHI KUHUSU ROHO WAOVU ZINAPOONGEZEKA

19. (a) Ibilisi amewadanganya watu wengi waamini nini kuhusu nguvu zake? (b) Wakristo wa kweli wanapaswa kuepuka hadithi gani?

19 Ingawa watu wengi katika nchi za Ulaya na Amerika hawaoni hatari za nguvu za Shetani, mambo ni tofauti katika maeneo mengine ya ulimwengu. Katika sehemu hizo, Shetani amewadanganya wengi waamini kwamba ana nguvu nyingi kuliko zile ambazo kwa kweli anazo. Watu wengi wanakula, wanafanya kazi, na kulala wakiogopa roho waovu. Kuna hadithi nyingi sana kuhusu matendo makubwa ya roho waovu. Mara nyingi watu husimulia hadithi hizo kwa njia yenye kupendeza; zinawasisimua watu. Je, tunapaswa kueneza hadithi hizo? Hapana, watumishi wa Mungu wa kweli huepuka kufanya hivyo kwa sababu mbili muhimu.

20. Ni kwa njia gani mtu anaweza kueneza propaganda za Shetani, bila hata kujua?

20 Kwanza, kwa kueneza hadithi kuhusu mafanikio ya roho waovu, mtu anaunga mkono jitihada za Shetani. Jinsi gani? Neno la Mungu linathibitisha kwamba Shetani anaweza kufanya kazi zenye nguvu, lakini pia linaonya kwamba anatumia “ishara za uwongo” na “udanganyifu.” (2 Wathesalonike 2:9, 10) Kwa kuwa Shetani ndiye mdanganyifu mkuu, anajua jinsi ya kuchochea akili za wale wanaopenda mambo ya kuwasiliana na pepo na jinsi ya kuwafanya waamini mambo yasiyo ya kweli. Watu hao wanaweza kuamini kwamba kwa kweli waliona na kusikia mambo fulani na wanaweza kusimulia mambo hayo kana kwamba ni ya kweli. Kisha, hadithi hizo hutiwa chumvi zinaposimuliwa tena na tena. Ikiwa Mkristo angeeneza hadithi hizo, angekuwa akifanya mapenzi ya Ibilisi—“baba ya uwongo.” Angekuwa akieneza propaganda za Shetani.—Yohana 8:44; 2 Timotheo 2:16.

21. Mazungumzo yetu yanapaswa kukazia nini?

21 Pili, hata ikiwa Mkristo amewahi kuwasiliana na roho waovu zamani, ataepuka kuwatumbuiza waamini wenzake kwa kuwasimulia hadithi hizo tena na tena. Kwa nini? Tunahimizwa hivi: ‘Mtazameni kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ (Waebrania 12:2) Ndiyo, tunapaswa kumkazia fikira Kristo, bali si Shetani. Alipokuwa duniani, Yesu hakuwatumbuiza wanafunzi wake kwa kuwasimulia hadithi za roho waovu, ingawa angeweza kusema mambo mengi kuhusu yale ambayo Shetani anaweza kufanya au yale ambayo hawezi kufanya. Badala yake, Yesu alikazia fikira ujumbe wa Ufalme. Hivyo, tunaweza kumwiga Yesu na mitume kwa kuzungumza juu ya “mambo makuu ya Mungu.”—Matendo 2:11; Luka 8:1; Waroma 1:11, 12.

22. Tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuchangia ‘shangwe mbinguni’?

22 Ni kweli kwamba Shetani anatumia hila mbalimbali, kutia ndani kuwasiliana na pepo, ili kujaribu kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Hata hivyo, kwa kuchukia maovu na kushikamana na yaliyo mema, hatumpi Ibilisi nafasi ya kulegeza azimio letu la kukataa katakata namna zote za kuwasiliana na pepo. (Waefeso 4:27) Wazia ‘shangwe itakayokuwa mbinguni’ tukiendelea “kusimama imara kupinga hila za Ibilisi” mpaka wakati ambapo hatakuwapo tena!—Waefeso 6:11.

^ fu. 16 Majina ya Shetani (Mpinzani, Mchongezi, Mdanganyifu, Mjaribu, Mwongo) hayadokezi kwamba ana uwezo wa kusoma mioyo na akili zetu. Kwa upande mwingine, Yehova anatajwa kuwa “mchunguzaji wa mioyo,” na Yesu anatajwa kuwa yule ‘anayechunguza figo na mioyo.’—Methali 17:3; Ufunuo 2:23.

^ fu. 18 Unaweza kupata habari zaidi katika makala yenye kichwa “Mtihani wa Afya Kwako?” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1994, ukurasa wa 19-22, na makala “Maoni ya Biblia: Uchaguzi Wako wa Matibabu—Je, Ni Muhimu?” katika toleo la Amkeni! la Januari 8, 2001.