Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Jinsi ya Kushughulika na Mtu Aliyetengwa na Ushirika

Jinsi ya Kushughulika na Mtu Aliyetengwa na Ushirika

Inahuzunisha sana mtu wa ukoo au rafiki wa karibu anapotengwa na ushirika wa kutaniko kwa sababu ya kutotubu dhambi. Hata hivyo, tunaweza kuonyesha kina cha upendo wetu kwa Mungu na ushikamanifu wetu kwa mpango wake kupitia jinsi tunavyofuata maagizo ya Biblia kuhusu jambo hilo. * Fikiria maswali mbalimbali yanayohusu habari hii.

Tunapaswa kushughulika jinsi gani na mtu aliyetengwa na ushirika? Biblia inasema: “Mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.” (1 Wakorintho 5:11) Kuhusu yeyote ambaye “hakai katika fundisho la Kristo,” Biblia inasema: “Msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kumsalimu. Kwa maana yeye anayemsalimu anashiriki katika matendo yake maovu.” (2 Yohana 9-11) Hatuchangamani wala kushirikiana kiroho na watu waliotengwa na ushirika. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1982, ukurasa wa 17, lilisema: “Kusema neno fupi tu la ‘Jambo’ (Habari?) kunaweza kuwa ndiyo hatua ya kwanza inayopanuka na kuwa mazungumzo na hata kuwa urafiki. Je! tungetaka kuichukua hatua hiyo ya kwanza kumwelekea mtu aliyetengwa na ushirika?”

Je, tunapaswa kumwepuka kabisa? Ndiyo. Kuna sababu mbalimbali za kufanya hivyo. Kwanza, ni njia ya kuonyesha ushikamanifu kwa Mungu na Neno lake. Tunamtii Yehova nyakati zote, iwe ni rahisi au ni vigumu kufanya hivyo. Kumpenda Mungu hutuchochea kutii amri zake zote, nasi tunatambua kwamba yeye ni Mungu mwenye haki na upendo na kwamba sheria zake hutuletea faida. (Isaya 48:17; 1 Yohana 5:3) Pili, kumwepuka mkosaji asiyetubu hutulinda sisi na pia kutaniko kwa ujumla lisipatwe na uchafu wa kiroho na kiadili na jina la kutaniko lisiletewe suto. (1 Wakorintho 5:6, 7) Tatu, kushikamana kwa uthabiti na kanuni za Biblia kunaweza hata kumfaidi aliyetengwa na ushirika. Kwa kuunga mkono uamuzi wa halmashauri ya hukumu, huenda tukamchochea mkosaji ambaye kufikia wakati ambapo hatua hiyo ilichukuliwa hakukubali msaada kutoka kwa wazee. Kupoteza ushirika wenye thamani pamoja na wapendwa wake kunaweza kumsaidia arudiwe na “fahamu zake,” aone uzito wa kosa lake, na kuchukua hatua za kumrudia Yehova.—Luka 15:17.

Tunaweza kushughulika jinsi gani na mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika? Katika hali kama hiyo, uhusiano wa karibu kati ya watu wa familia unaweza kuwa jaribu kali la ushikamanifu. Tunaweza kushughulika jinsi gani na mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika? Hatuwezi kuzungumzia hali zote zinazoweza kutokea, lakini acheni tuchunguze mbili.

Katika visa fulani, mtu wa familia aliyetengwa na ushirika huenda bado anaishi katika nyumba moja na wazazi wake na ndugu na dada zake. Kwa kuwa kutengwa na ushirika hakuvunji uhusiano wa kifamilia, shughuli na mambo ya kawaida ya familia yataendelea. Hata hivyo, kupitia mwenendo wake, mtu huyo amechagua kuvunja kifungo cha kiroho kati yake na watu wa familia ambao ni waamini. Kwa hiyo, watu wa familia ambao ni washikamanifu hawataendelea kumshirikisha katika mambo ya kiroho. Kwa mfano, mtu huyo aliyetengwa na ushirika akijiunga na familia wakati inapokutana ili kujifunza Biblia, hatashiriki. Hata hivyo, ikiwa aliyetengwa si mtu mzima, wazazi wake bado wana jukumu la kumfundisha na kumtia nidhamu. Hivyo, wazazi wenye upendo wanaweza kupanga kujifunza naye Biblia. *Methali 6:20-22; 29:17.

Katika visa vingine, huenda mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika anaishi kwake mbali na familia yao. Ingawa huenda mara mojamoja kukawa na uhitaji wa kuchangamana naye ili kushughulikia jambo fulani la familia, pindi kama hizo zinapaswa kuwa chache. Watu wa familia ambao ni washikamanifu hawatafuti visingizio vya kuchangamana na mtu aliyetengwa na ushirika ambaye anaishi nje ya familia. Badala yake, ushikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake unawachochea kuunga mkono mpango wa Kimaandiko wa kutenga na ushirika. Ushikamanifu wao unaonyesha kwamba wanamjali mkosaji, nao unaweza kumsaidia afaidike kutokana na nidhamu aliyopata. *Waebrania 12:11.

^ fu. 1 Kanuni za Biblia zinazohusu kutengwa na ushirika zinawahusu pia wale wanaojitenga wenyewe na ushirika wa kutaniko.

^ fu. 2 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu watoto waliotengwa na ushirika ambao bado wanaishi pamoja na wazazi wao, katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2001, ukurasa wa 16-17, na Novemba 15, 1988, ukurasa wa 2020.

^ fu. 3 Ili upate habari zaidi kuhusu kushughulika na watu wa ukoo ambao wametengwa na ushirika, ona shauri la Kimaandiko lililo katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1988, ukurasa wa 26-31, na la Januari 1, 1982, ukurasa wa 18-24.