Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ananifaa?

Je, Ananifaa?

SURA YA 3

Je, Ananifaa?

Tafadhali jibu maswali yanayofuata:

Ni sifa gani ambazo sasa unaona kwamba yule atakayekuwa mwenzi wako wa ndoa anapaswa kuwa nazo? Katika orodha iliyo hapa chini tia alama hii ✔ kando ya sifa nne unazoona kuwa muhimu zaidi.

□ Mwenye sura nzuri □ Anayethamini mambo ya kiroho

□ Mwenye urafiki □ Mwenye kuaminika

□ Anayependwa na wengi □ Mwenye maadili mema

□ Mcheshi □ Anayeweka miradi na kuifikia

Ulipokuwa na umri mdogo, je, kuna wakati ulipohisi kwamba unampenda sana mtu fulani ambaye hakukuwa na matumaini yoyote ya kuwa na uhusiano naye? Katika orodha iliyo juu, tia alama hii × kando ya sifa ya mtu huyo iliyokuvutia zaidi wakati huo.

KATIKA sifa zote zilizoonyeshwa juu, hakuna yoyote iliyo mbaya. Kila moja inaweza kukuvutia. Hata hivyo, je, si kweli kwamba unapompenda mtu ambaye hakuna matumaini yoyote ya kuwa na uhusiano naye, ambaye hata hajui kwamba unampenda, unakazia fikira sifa za nje, kama zile zilizo upande wa kushoto?

Lakini unapoendelea kukomaa, unaanza kutumia utambuzi kuchunguza sifa za ndani, kama zile zilizo upande wa kulia. Kwa mfano, unaanza kutambua kwamba msichana anayevutia zaidi katika mtaa wenu hata si mwaminifu au mvulana anayependwa zaidi darasani hata hana maadili mema. Ikiwa umepita upeo wa ujana, inaelekea hutachunguza sifa za nje tu unapojibu swali hili, “Je, ananifaa?”

Kwanza Jifahamu

Kabla hujafikiria mtu anayekufaa, unahitaji kujifahamu vizuri. Ili kujichunguza zaidi, jibu maswali yanayofuata:

Nina sifa gani nzuri? ․․․․․

Nina udhaifu gani? ․․․․․

Nina mahitaji gani ya kihisia na ya kiroho? ․․․․․

Kujifahamu si kazi rahisi, lakini maswali kama hayo yaliyo hapo juu yanaweza kukusaidia. Kadiri unavyojifahamu, ndivyo utakavyoweza kupata mtu ambaye atakusaidia kuboresha sifa zako nzuri badala ya kuzidisha udhaifu wako. * Namna gani ikiwa unafikiri kwamba tayari umekwishampata mtu huyo?

Je, Yeyote Tu Anafaa?

“Ningependa tuwe marafiki!” Maneno hayo yanaweza kukushtua au kukusisimua—ikitegemea ni nani anayeyasema. Tuseme umekubali ombi hilo. Kadiri muda unavyopita, ni kwa njia gani unaweza kujua kama anakufaa?

Tuseme unataka kununua viatu vipya. Unaenda dukani na kuona viatu vinavyokupendeza. Unapima viatu hivyo kwa kuvivaa, lakini kwa kusikitisha, vinakubana sana. Utafanya nini? Je, utavinunua tu? Au utatafuta vingine? Bila shaka, jambo la hekima ni kuvirudisha na kutafuta vingine. Si jambo la busara hata kidogo kuvaa viatu ambavyo vinakubana!

Ndivyo ilivyo pia kuhusu kuchagua mwenzi wa ndoa. Kadiri muda unavyopita, utavutiwa na watu mbalimbali. Lakini si yeyote tu anayekufaa. Ukweli ni kwamba unahitaji mtu ambaye utafurahia kuwa pamoja naye—mtu ambaye utu wenu na miradi yenu inafaana. (Mwanzo 2:18; Mathayo 19:4-6) Je, umempata mtu kama huyo? Ikiwa umempata, unaweza kujua jinsi gani ikiwa anakufaa?

Kutoangalia Mambo Kijuujuu

Ili kujibu swali hilo, kwanza mtazame mwenzako pasipo upendeleo. Hata hivyo, uwe mwangalifu! Huenda ukaona tu mambo unayotaka kuona. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Jaribu kutambua jinsi rafiki yako alivyo kikweli. Jitihada zinahitajika. Na hilo halipaswi kukushangaza. Kwa mfano: Wazia kwamba unataka kununua gari. Utalichunguza kadiri gani? Je, utatosheka tu na sura ya nje? Je, halingekuwa jambo la busara kulichunguza kwa undani zaidi—labda kujitahidi kujua mengi iwezekanavyo kuhusu hali ya injini yake?

Kutafuta mwenzi ni jambo zito zaidi kuliko kuchagua gari la kununua. Hata hivyo, wengi wanaoanzisha urafiki wa kimapenzi hawachunguzi mambo kwa undani. Badala yake, wao hutaja tu mambo yanayowapendeza wote wawili: ‘Tunapenda muziki uleule.’ ‘Tunapendezwa na mambo yaleyale.’ ‘Tunakubaliana katika kila jambo!’ Hata hivyo, kama ilivyotajwa awali, ikiwa kwa kweli umepita upeo wa ujana, hutachunguza mambo kijuujuu tu. Unahitaji kumtambua “yule mtu wa siri wa moyoni.”—1 Petro 3:4; Waefeso 3:16.

Kwa mfano, badala ya kukazia fikira mambo mnayokubaliana, huenda mkapata kujuana hata zaidi kwa kuona inavyotokea mnapokosa kukubaliana. Kwa maneno mengine, anatenda jinsi gani kutoelewana kunapotokea? Je, anasisitiza maoni yake? Je, ‘analipuka kwa hasira’ na kuanza ‘kutukana’? (Wagalatia 5:19, 20; Wakolosai 3:8) Au anaonyesha usawaziko, kwa kukubali mambo ili kuwe na amani wakati ambapo hakuna kanuni yoyote inayovunjwa?—Yakobo 3:17.

Jambo lingine unalopaswa kufikiria ni: Je, mtu huyo anapenda kukusukuma ufanye mambo anayotaka, kukutawala, au ni mwenye wivu? Je, anadai umwambie kila kitu unachofanya? Msichana mmoja anayeitwa Nicole anasema hivi: “Mimi husikia kuhusu watu wenye urafiki wa kimapenzi wanaozozana kwa sababu mmoja wao amekasirika kwa kuwa mwenzake hampigii simu na kumweleza mahali alipo. Kwa maoni yangu, hiyo ni dalili ya matatizo.”—1 Wakorintho 13:4.

Mambo kama hayo ambayo yametajwa yanakazia fikira utu na mwenendo. Hata hivyo, ni muhimu pia kujua sifa za rafiki yako. Wengine wana maoni gani kumhusu? Ingefaa kuzungumza na watu ambao wamemfahamu kwa muda fulani, kama vile watu wakomavu kutanikoni. Kwa njia hiyo utajua ikiwa ‘anashuhudiwa vema.’—Matendo 16:1, 2.

Kuandika maoni yako kuhusu rafiki yako katika mambo yafuatayo, kwa kutegemea habari ambazo tumezungumzia kufikia sasa, kunaweza kukusaidia kumfahamu vizuri zaidi.

Utu ․․․․․

Mwenendo ․․․․․

Sifa ․․․․․

Pia utafaidika kwa kuchunguza sanduku lenye kichwa “ Je, Atakuwa Mume Anayenifaa?” katika ukurasa wa 39 au “ Je, Atakuwa Mke Anayenifaa?” katika ukurasa wa 40. Maswali yaliyo humo yatakusaidia kujua ikiwa rafiki yako atakuwa mwenzi wa ndoa anayekufaa.

Namna gani ikiwa baada ya kufikiria kwa uzito, unaona kwamba huenda mtu huyo asikufae? Ikiwa ndivyo, basi una uamuzi mzito wa kufanya:

Je, Tuvunje Urafiki Wetu?

Nyakati nyingine, kuna faida kuvunja urafiki. Fikiria kisa cha Jill. Anasema, “Mwanzoni nilifurahi kwamba mpenzi wangu alikuwa akitaka kujua niko wapi, ninafanya nini, na niko na nani. Lakini ilifikia hatua ya kwamba singeweza kuwa na mtu mwingine yeyote isipokuwa yeye. Hata aliona wivu nilipokuwa pamoja na watu wa familia yetu—hasa baba yangu. Nilipovunja uhusiano huo, nilihisi kana kwamba nimetua mzigo mzito sana!”

Sarah alikuwa pia katika hali kama hiyo. Alianza kutambua kwamba John ni mwenye dhihaka, mwenye kudai mno, na asiye na heshima. Sarah anakumbuka hivi: “Siku moja alikuja kwetu akiwa amechelewa kwa saa tatu! Alimpuuza mama yangu aliyemfungulia mlango, kisha akasema: ‘Twende. Tumechelewa.’ Si kwamba yeye amechelewa, bali ‘Tumechelewa.’ Alipaswa kuomba msamaha au kueleza sababu ya kuchelewa. Isitoshe, alipaswa kumwonyesha heshima mama yangu!” Ni kweli kwamba kisa kimoja chenye kuvunja moyo au tabia fulani isiyopendeza haimaanishi kwamba urafiki wenu hautadumu. (Zaburi 130:3) Hata hivyo, Sarah alipotambua kwamba John alikuwa na mazoea ya kukosa heshima, aliamua kuuvunja urafiki wao.

Kama ilivyokuwa katika visa vya Jill na Sarah, ungefanya nini ukitambua kwamba mpenzi wako hastahili kuwa mwenzi wako wa ndoa? Ikiwa ndivyo ilivyo, usipuuze hisia zako! Ijapokuwa ni vigumu kukubali ukweli wa mambo, huenda ikafaa kuvunja urafiki huo. Andiko la Methali 22:3 linasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” Kwa mfano, ikiwa rafiki yako anaonyesha dalili moja au zaidi kati ya zile zilizo katika ukurasa wa 39 na 40 huenda ikafaa kuvunja urafiki huo—angalau mpaka tatizo lenyewe lirekebishwe. Ni kweli, huenda isiwe rahisi kuvunja urafiki. Lakini ndoa ni muungano wa kudumu. Afadhali kuumia kwa muda mfupi sasa kuliko kujuta maisha yako yote baadaye!

Kumjulisha Uamuzi Wako

Unaweza kuuvunja urafiki wenu jinsi gani? Kwanza, chagua kikao kinachofaa. Ni kikao gani kinachofaa? Fikiria jinsi ambavyo wewe mwenyewe ungependa kutendewa katika hali kama hiyo. (Mathayo 7:12) Je, ungependa kujulishwa uamuzi huo mbele ya watu? Sivyo. Isipokuwa iwe lazima, haingefaa kuvunja urafiki huo kwa kuacha ujumbe kwenye mashini ya kujibu simu, kutuma ujumbe mfupi kwenye simu, au kupitia barua-pepe. Badala yake, chagua mahali na wakati unaofaa ili kuzungumzia jambo hilo zito.

Unapaswa kusema nini? Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo ‘wasemezane kweli.’ (Waefeso 4:25) Hivyo, njia bora ni kutumia busara na kuwa thabiti. Sema waziwazi kwa nini unahisi kwamba urafiki huo hautadumu. Huhitaji kutaja orodha ndefu ya makosa au kumshambulia kwa mashtaka. Badala ya kusema, “Wewe hufanyi” hili au lile au “Hujapata kamwe” kufanya hivi au vile, afadhali kutumia maneno yanayoonyesha hisia zako kama vile, “Mimi ninahitaji mtu ambaye . . . ” au “Mimi ninaona kwamba hatuwezi kuendelea kuwa marafiki kwa sababu . . . ”

Huo si wakati wa kuyumba-yumba au kushawishiwa ubadili maoni yako. Kumbuka kwamba kuna sababu nzito ambazo zimekusukuma ufikie uamuzi wa kuvunja urafiki huo. Kwa hiyo uwe mwangalifu rafiki yako akijaribu kutumia ujanja kubadili maoni yako. “Nilipovunja urafiki wetu,” anasema msichana mmoja anayeitwa Lori, “mvulana niliyekuwa na urafiki naye alianza kujifanya kwamba ana huzuni kila wakati. Nafikiri alifanya hivyo ili nimhurumie. Nilimsikitikia. Lakini sikuruhusu jambo hilo libadili uamuzi wangu.” Kama Lori, uwe na hakika kuhusu unachotaka. Shikamana na uamuzi wako. Acha siyo yako imaanishe siyo.Yakobo 5:12.

Matokeo ya Kuvunja Urafiki Huo

Usishangae ukihuzunika sana kwa muda fulani baada ya kuvunja urafiki huo. Huenda hata ukahisi kama mtunga-zaburi aliyesema: “Nimeingiwa na wasiwasi, nimeinama kupita kiasi; nimetembea huku na huku kwa huzuni mchana kutwa.” (Zaburi 38:6) Huenda marafiki wenye nia nzuri wakajaribu kukusaidia kwa kukutia moyo uanzishe tena urafiki huo. Uwe mwangalifu! Wewe ndiwe utakayeathiriwa na matokeo ya uamuzi wako, si marafiki hao. Kwa hiyo, usiogope kuwa imara—hata ingawa huenda ukahuzunishwa na yaliyotokea.

Uwe na hakika kwamba muda si muda huzuni yako itatoweka. Kwa sasa, unaweza kuchukua hatua zinazofaa, kama zile zifuatazo, ili kushughulikia hali hiyo.

Mweleze mtu unayemwamini jinsi unavyohisi. * (Methali 15:22) Sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. (Zaburi 55:22) Jishughulishe na mambo mengine. (1 Wakorintho 15:58) Usijitenge na watu! (Methali 18:1) Bila kukawia, anza kushirikiana na watu ambao watakujenga. Jitahidi kufikiria mambo ambayo yanajenga.—Wafilipi 4:8.

Baada ya muda, huenda ukapata rafiki mwingine. Na utakapofanya hivyo utakuwa na maoni yenye usawaziko zaidi. Huenda wakati huo jibu lako kwa swali hili “Je, ananifaa?” litakuwa ndiyo!

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 31

KATIKA SURA INAYOFUATA

Ikiwa tayari mna urafiki wa kimapenzi, ni mipaka gani mnayoweza kuweka kuhusiana na kuonyeshana mahaba?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Unaweza kujifunza hata zaidi juu yako mwenyewe kwa kuchunguza maswali katika Sura ya 1 chini ya kichwa kidogo “Je, Uko Tayari Kufunga Ndoa?

^ fu. 45 Wazazi wako au watu wazima wengine kama vile wazee Wakristo wanaweza kukusaidia. Huenda hata ukagundua kwamba wao pia walipatwa na hali kama hiyo walipokuwa vijana.

MAANDIKO MUHIMU

“Kwa matendo yake, mvulana hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” —Methali 20:11.

PENDEKEZO

Fanyeni pamoja mambo yanayofunua sifa za mtu:

● Jifunzeni Neno la Mungu pamoja.

● Chunguzaneni mnapokuwa katika mikutano ya kutaniko na katika huduma.

● Shirikini katika kusafisha Jumba la Ufalme na katika miradi ya ujenzi.

JE, WAJUA . . .?

Uchunguzi mbalimbali unaonyesha kwamba ndoa kati ya watu wa dini tofauti mara nyingi huishia kwenye talaka.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikivutiwa na mtu asiye mwamini, nita ․․․․․

Nikitaka kujua sifa za mtu ambaye nina urafiki wa kimapenzi naye, ninaweza ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Ni sifa gani nzuri ulizo nazo zinazoweza kufanya ndoa yenu ifanikiwe?

Ni sifa gani muhimu ambazo ungependa mwenzi wako wa ndoa awe nazo?

Ni matatizo gani yanayoweza kutokea ukifunga ndoa na mtu wa dini nyingine?

Unaweza kujua jinsi gani utu, tabia, na sifa ya mtu ambaye una urafiki wa kimapenzi naye?

[Blabu katika ukurasa wa 37]

“Jinsi rafiki yako anavyowatendea watu wa familia yao, ndivyo atakavyokutendea.’’—Tony

[Sanduku katika ukurasa wa 34]

“Msifungwe Nira Isivyo Sawa”

“Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” Huenda unakubaliana na kanuni hiyo ya Biblia, inayopatikana katika 2 Wakorintho 6:14. Hata hivyo, huenda bado ukavutiwa na mtu asiye mwamini. Kwa nini? Labda unavutiwa na sura yake tu. Mvulana anayeitwa Mark anasema: “Kuna msichana niliyekuwa nikimwona kila siku wakati wa mazoezi. Kila mara alihakikisha kwamba amekuja kuzungumza nami. Haikuwa vigumu kuanzisha urafiki naye.”

Ikiwa unajijua vizuri na unasadiki kwamba viwango vya maadili unavyofuata vinafaa—na ikiwa una ukomavu wa kutosha kutotawaliwa na hisia zako—basi unajua jambo unalopaswa kufanya. Kwa kweli, mtu huyo—hata awe mwenye kuvutia jinsi gani, hata awe mwenye kupendeza namna gani, au hata aonekane kuwa na sifa nzuri kadiri gani—hatakusaidia kuboresha urafiki wako na Mungu.—Yakobo 4:4.

Bila shaka, ikiwa tayari urafiki wa kimapenzi umeanza, haitakuwa rahisi kuuvunja. Ndivyo msichana mmoja anayeitwa Cindy alivyogundua. Anasema: “Nililia kila siku. Nilimfikiria mvulana huyo nyakati zote, hata wakati wa mikutano ya Kikristo. Nilimpenda sana hivi kwamba nilihisi afadhali nife kuliko kumwacha.” Hata hivyo, muda si muda, Cindy alifuata shauri lenye hekima la mama yake kuhusu kutokuwa na urafiki wa kimapenzi na mtu asiye mwamini. Anasema: “Ni vizuri kwamba niliuvunja urafiki huo. Nina hakika kabisa kwamba Yehova atanitimizia mahitaji yangu.”

Je, uko katika hali kama ya Cindy? Ikiwa ndivyo, si lazima ung’ang’ane ukiwa peke yako! Unaweza kuzungumza na wazazi wako. Ndivyo Jim alivyofanya alipojikuta akivutiwa na msichana fulani shuleni. Anasema: “Mwishowe niliwaomba wazazi wangu wanisaidie. Kufanya hivyo kulinisaidia sana kushinda hisia zangu.” Wazee wa kutaniko wanaweza kukusaidia pia. Usiogope kuzungumza na mmoja wao kuhusu mambo unayokabili?—Isaya 32:1, 2.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 39]

 Ukurasa wa Mazoezi

Je, Atakuwa Mume Anayenifaa?

Sifa za Msingi

□ Anatumia jinsi gani mamlaka yoyote aliyo nayo?—Mathayo 20:25, 26.

□ Ana miradi gani?—1 Timotheo 4:15.

□ Je, sasa anajitahidi kufikia miradi hiyo?—1 Wakorintho 9:26, 27.

□ Anawatendea jinsi gani watu wa familia yao?—Kutoka 20:12.

□ Rafiki zake ni nani?—Methali 13:20.

□ Anapenda kuzungumza juu ya nini?—Luka 6:45.

□ Ana maoni gani kuhusu pesa?—Waebrania 13:5, 6.

□ Anapenda kujiburudisha na mambo gani?—Zaburi 97:10.

□ Anaonyesha namna gani kwamba anampenda Yehova?—1 Yohana 5:3.

Sifa zenye Manufaa

□ Je, ana bidii?—Methali 6:9-11.

□ Je, ana usawaziko kuhusu matumizi ya pesa?—Luka 14:28.

□ Je, anashuhudiwa vema?—Matendo 16:1, 2.

□ Je, anawajali wengine?—Wafilipi 2:4.

Dalili za Matatizo

□ Je, anakasirika upesi?—Methali 22:24.

□ Je, anajaribu kukushawishi ushiriki katika mwenendo mpotovu kingono?—Wagalatia 5:19.

□ Je, anapenda kupigana au kuwatusi wengine?—Waefeso 4:31.

□ Je, ni lazima anywe pombe ili awe na furaha?—Methali 20:1.

□ Je, ni mtu mwenye wivu, anayejifikiria mwenyewe tu? —1 Wakorintho 13:4, 5.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 40]

 Ukurasa wa Mazoezi

Je, Atakuwa Mke Anayenifaa?

Sifa za Msingi

□ Anaonyesha jinsi gani ujitiisho katika familia na kutanikoni?—Waefeso 5:21, 22.

□ Anawatendea jinsi gani watu wa familia yao?—Kutoka 20:12.

□ Rafiki zake ni nani?—Methali 13:20.

□ Anapenda kuzungumza juu ya nini?—Luka 6:45.

□ Ana maoni gani kuhusu pesa?—1 Yohana 2:15-17.

□ Ana miradi gani?—1 Timotheo 4:15.

□ Je, sasa anajitahidi kufikia miradi hiyo?—1 Wakorintho 9:26, 27.

□ Anapenda kujiburudisha na mambo gani?—Zaburi 97:10.

□ Anaonyesha namna gani kwamba anampenda Yehova?—1 Yohana 5:3.

Sifa zenye Manufaa

□ Je, ana bidii?—Methali 31:17, 19, 21, 22, 27.

□ Je, ana usawaziko kuhusu matumizi ya pesa?—Methali 31:16, 18.

□ Je, anaripotiwa vema?—Ruthu 3:11.

□ Je, anawajali wengine?—Methali 31:20.

Dalili za Matatizo

□ Je, ni mgomvi?—Methali 21:19.

□ Je, anajaribu kukushawishi ushiriki katika mwenendo mpotovu kingono?—Wagalatia 5:19.

□ Je, anapenda kupigana au kuwatusi wengine? —Waefeso 4:31.

□ Je, lazima anywe pombe ili awe na furaha?—Methali 20:1.

□ Je, ni mtu mwenye wivu, anayejifikiria mwenyewe tu?—1 Wakorintho 13:4, 5.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Si kiatu chochote tu kinachoweza kukutosha; vivyo hivyo si mtu yeyote tu atakayekufaa

[Picha katika ukurasa wa 31]

Unapochagua gari, je, unafikiri ni muhimu kulichunguza kwa undani badala ya kuangalia sura yake ya nje tu? Hivyo basi unahitaji kuwa mwangalifu hata zaidi unapochagua mwenzi wa ndoa!