Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?

Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?

SURA YA 5

Kwa Nini Uendelee Kuwa Bikira?

“Kuna mkazo mwingi wa kufanya ngono.”—Kelly.

“Ninahisi kana kwamba nina kasoro kwa kuwa bado mimi ni bikira.”—Jordon.

“BADO wewe ni bikira?” Swali hilo linaweza kukushtua! Katika sehemu nyingi, kijana ambaye bado ni bikira anaweza kuonwa kuwa mtu wa ajabu au mwenye kasoro. Ndiyo sababu vijana wengi wanafanya ngono mapema maishani!

Kuvutwa na Tamaa, Kusukumwa na Marika

Ikiwa wewe ni Mkristo, unajua kwamba Biblia inakuambia ‘ujiepushe na uasherati.’ (1 Wathesalonike 4:3) Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kwako kudhibiti tamaa zako za ngono. Kijana mmoja anayeitwa Paul anakiri hivi: “Nyakati nyingine, mimi huanza tu kufikiri kuhusu ngono bila sababu yoyote hususa.”

Uwe na hakika kwamba hizo ni hisia za kawaida. Hata hivyo, kudhihakiwa na kusumbuliwa sikuzote kwa sababu ya kuwa bikira si jambo la kupendeza! Kwa mfano, namna gani marafiki wako wakikwambia kwamba wewe si mwanamume au mwanamke halisi ikiwa hujafanya ngono? “Marafiki huzungumzia ngono kana kwamba ni raha tupu na jambo la kawaida,” Ellen anasema. “Ikiwa hujihusishi na ngono unaonwa kuwa mshamba.”

Lakini huenda marafiki wako wasikuambie matokeo ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Kwa mfano, Maria ambaye alifanya ngono na mvulana aliyekuwa rafiki yake anakumbuka: “Baadaye nilifedheheka na kuona aibu. Nilijichukia na kumchukia mvulana huyo.” Hali kama hizo hutokea mara nyingi kuliko vijana wengi wanavyofikiri. Ukweli ni kwamba, kufanya ngono kabla ya ndoa mara nyingi hutokeza maumivu ya kihisia na madhara makubwa!

Hata hivyo, msichana anayeitwa Shanda anauliza, “Kwa nini Mungu aliwapa vijana tamaa za ngono akijua kwamba hawapaswi kuzitosheleza kabla ya ndoa?” Hilo ni swali zuri. Lakini fikiria mambo yafuatayo:

Je, tamaa za ngono tu ndizo hisia zenye nguvu unazopata? Hapana. Yehova Mungu alikuumba na uwezo wa kuwa na tamaa na hisia nyingi mbalimbali.

Je, ni lazima utosheleze kila tamaa mara tu inapotokea? Hapana, kwa sababu Mungu alikupa pia uwezo wa kudhibiti matendo yako.

Basi, tuseme nini? Huenda huwezi kuzuia tamaa fulani zisitokee, lakini unaweza kudhibiti matendo yako. Kwa hakika, kutosheleza tamaa yako ya ngono kila mara inapotokea ni kosa na ni kutotumia akili sawa tu na kumpiga mtu kila mara unapokuwa na hasira.

Ukweli ni kwamba Mungu hakukusudia tutumie vibaya nguvu zetu za uzazi. Biblia inasema: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe [au, mwili wake mwenyewe] katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Kama vile kuna “wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia,” vivyo hivyo kuna wakati wa kutosheleza tamaa za ngono na wakati wa kuepuka kufanya hivyo. (Mhubiri 3:1-8) Vyovyote vile, wewe tu ndiwe unayeweza kudhibiti tamaa zako!

Lakini namna gani mtu akikudhihaki kwa kusema hivi kwa mshangao, “Eti bado wewe ni bikira?” Usiogope. Ikiwa mtu huyo anataka tu kukuaibisha, unaweza kusema: “Ndiyo, bado mimi ni bikira, na ninafurahia jambo hilo.” Au unaweza kusema, “Hilo ni jambo la kibinafsi ambalo silizungumzii na wengine.” * (Methali 26:4; Wakolosai 4:6) Kwa upande mwingine, huenda ukahisi kwamba mtu anayekuuliza swali hilo anahitaji kujua zaidi. Hivyo, unaweza kuamua kumweleza msimamo wako unaotegemea Biblia.

Je, unaweza kufikiria njia nyingine za kujibu unapoulizwa hivi kwa dhihaka “Eti bado wewe ni bikira?” Ikiwa ndivyo, andika majibu hayo hapa chini.

․․․․․

Zawadi Yenye Thamani

Mungu anahisi jinsi gani watu wanapofanya ngono kabla ya ndoa? Wazia kwamba umemnunulia rafiki yako zawadi. Lakini kabla hata hujampa zawadi hiyo, anaifungua kwa sababu ya udadisi! Ungeudhika, sivyo? Wazia basi jinsi ambavyo Mungu angehisi ikiwa ungefanya ngono kabla ya ndoa. Anataka ungoje mpaka utakapofunga ndoa ili ufurahie zawadi ya ngono.—Mwanzo 1:28.

Unapaswa kufanya nini kuhusu hisia zako za ngono? Jizoeze kuzidhibiti. Inawezekana! Mwombe Yehova akusaidie. Roho yake inaweza kuzidisha uwezo wako wa kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Kumbuka kwamba Yehova “hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” (Zaburi 84:11) Kijana mmoja anayeitwa Gordon anasema: “Ninapoanza kufikiria kwamba hakuna ubaya wowote wa kufanya ngono kabla ya ndoa, ninakumbuka hatari za kiroho na kutambua kwamba uhusiano wangu na Yehova ni wenye thamani sana hivi kwamba siwezi kuruhusu uharibiwe na dhambi yoyote ile.”

Ukweli ni kwamba kuwa bikira si jambo la kushangaza wala haimaanishi kwamba una kasoro. Kwa upande mwingine, upotovu katika ngono unasababisha aibu, kuvunjika moyo, na madhara mengine. Kwa hiyo, usiruhusu propaganda ya ulimwengu ikudanganye kufikiri kwamba una kasoro ukishikamana na viwango vya Biblia. Kwa kutunza ubikira wako, unatunza afya yako, hisia zako, na zaidi ya yote, uhusiano wako pamoja na Mungu.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 24

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Wakati mmoja, Yesu aliamua kunyamaza Herode alipomuuliza maswali. (Luka 23:8, 9) Mara nyingi hakuna haja ya kujibu maswali ya upuuzi.

MAANDIKO MUHIMU

“Ikiwa yeyote . . . amefanya uamuzi huu katika moyo wake mwenyewe, kutunza ubikira wake mwenyewe, yeye atafanya vema.”—1 Wakorintho 7:37.

PENDEKEZO

Epuka kushirikiana na watu ambao hawafuati viwango vya juu vya maadili, hata wakidai kwamba wana imani kama yako.

JE, WAJUA . . .?

Ni vigumu sana kwa watu wenye mwenendo mpotovu kingono kuacha tabia hiyo eti kwa sababu wamefunga ndoa. Lakini kuna uwezekano mkubwa kwamba wale ambao ni washikamanifu kwa viwango vya Mungu vya maadili kabla ya kufunga ndoa watakuwa washikamanifu kwa wenzi wao baadaye.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa ninataka kutunza ubikira mpaka nitakapofunga ndoa, ninahitaji ․․․․․

Ikiwa rafiki zangu wanafanya iwe vigumu kushikilia azimio langu, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Kwa maoni yako, unafikiri ni kwa nini watu huwadhihaki wale ambao ni mabikira?

Kwa nini inaweza kuwa vigumu kutunza ubikira?

Kuna faida gani za kutunza ubikira mpaka wakati utakapofunga ndoa?

Ni jinsi gani unaweza kumweleza mdogo wako faida za ubikira?

[Blabu katika ukurasa wa 51]

“Mimi huepuka kishawishi cha kufanya ngono kwa kukumbuka sikuzote kwamba ‘hakuna mwasherati au mtu asiye safi aliye na urithi wowote katika ufalme wa Mungu.’’’ (Waefeso 5:5)—Lydia

[Sanduku katika ukurasa wa 49]

Ukurasa wa Mazoezi

Ni Nini Hasa Kinachotokea Baadaye?

Mara nyingi marafiki wako na burudani zinazopendwa wanatumia ujanja kuficha matokeo mabaya ya kufanya ngono kabla ya ndoa. Ona mambo matatu yanayofuata. Unafikiri ni nini hasa kitakachowapata vijana hawa?

● Mwanafunzi mmoja anajigamba kwamba amefanya ngono na wasichana wengi. Anasema kwamba ni raha na hakuna madhara yoyote. Ni nini hasa kitakachotokea baadaye—kwake na kwa wasichana hao? ․․․․․

● Sinema inaisha ikionyesha vijana wawili ambao hawajafunga ndoa wakifanya ngono ili kuonyeshana upendo. Ni nini kinachoweza kutokea baadaye kihalisi? ․․․․․

● Unakutana na mvulana mwenye sura ya kuvutia anayetaka ufanye ngono naye. Anakuambia kwamba hakuna mtu atakayejua. Ukikubali na kisha ujaribu kuficha jambo hilo, ni nini hasa kinachoweza kutokea baadaye? ․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 54]

Kufanya ngono kabla ya ndoa ni kama kufungua zawadi kabla ya kukabidhiwa