Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini Ili Kujiondolea Upweke?

Nifanye Nini Ili Kujiondolea Upweke?

SEHEMU YA 9

Nifanye Nini Ili Kujiondolea Upweke?

Ingawa hali ya hewa ni shwari, huna mipango yoyote. Lakini, marafiki wako wote wana mipango. Wenzako wanakula raha. Kwa mara nyingine tena, hawakukualika! Kutoalikwa huvunja moyo, lakini unaweza kuvunjika moyo hata zaidi unapoanza kufikiria ni kwa nini hukualikwa. Huenda ukawaza, ‘Labda nina kasoro fulani. Kwa nini hakuna mtu anayetaka kuwa pamoja nami?’

LABDA, mara kwa mara, umejikuta katika hali kama ile inayotajwa katika ukurasa unaotangulia. Huenda ukaona kana kwamba kuna pengo kubwa sana kati yako na vijana wenzako. Kila mara unapojaribu kuanzisha mazungumzo pamoja nao, unashikwa na kigugumizi. Unapopata nafasi ya kuchangamana na marafiki, unalemewa na haya. Kwa nini jambo rahisi kama kuchangamana tu na marafiki liwe gumu hivyo?

Badala ya kubaki peke yako ng’ambo moja ya pengo hilo, unaweza kujenga madaraja. Acha tuone jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

Pengo la 1: Kuwa na maoni yasiyofaa juu yako mwenyewe. Vijana fulani hujidharau sikuzote. Wanaamini kwamba hakuna mtu anayependezwa nao na kwamba hawana lolote la kuchangia katika mazungumzo. Je, hivyo ndivyo unavyojiona? Ikiwa ndivyo, maoni hayo yanaweza tu kuzidisha pengo hilo linalokutenganisha na vijana wenzako.

Daraja: Kazia fikira vipawa ulivyo navyo. (2 Wakorintho 11:6) Jiulize, ‘Nina sifa gani nzuri?’ Fikiria vipawa fulani au sifa nzuri ulizo nazo na uziandike hapa chini.

․․․․․

Bila shaka, umepungukiwa katika mambo mengine na ni vizuri kukumbuka hilo. (1 Wakorintho 10:12) Lakini pia, una mengi unayoweza kuchangia. Kujua vipawa ulivyo navyo kunaweza kukupa ujasiri unaohitaji wa kuondolea mbali maoni yasiyofaa kujihusu.

Pengo la 2: Haya. Ungependa kuanzisha mazungumzo, lakini nafasi inapojitokeza, unakosa la kusema. “Mimi huwa na haya kila wakati,” analalamika Elizabeth mwenye umri wa miaka 19. “Mimi hushindwa kabisa kuzungumza na watu katika mikutano ya Kikristo, nami huvutiwa sana na wale wanaoweza kufanya hivyo!” Ikiwa hali yako inafanana na ya Elizabeth, huenda ukaona ni vigumu kuziba pengo hilo.

Daraja: Pendezwa kikweli na wengine. Usijali—haimaanishi uwe kasuku. Anza kwa kupendezwa na mtu mmoja tu. Kijana anayeitwa Jorge anasema: “Jambo rahisi kama vile kuwajulia watu hali au kuwauliza kuhusu kazi yao kunakuwezesha kuwajua vizuri zaidi.”

Pendekezo: Usizungumze tu na watu wa umri wako. Biblia inataja mifano mbalimbali ya watu waliokuwa na urafiki mkubwa kama vile Ruthu na Naomi, Daudi na Yonathani, na Timotheo na Paulo. (Ruthu 1:16, 17; 1 Samweli 18:1; 1 Wakorintho 4:17) Pia, kumbuka kwamba mazungumzo yanahusisha pande mbili, si upande mmoja tu. Watu hupenda watu wanaowasikiliza. Kwa hiyo, ikiwa wewe ni mwenye haya, kumbuka kwamba huhitaji kutawala mazungumzo!

Andika majina ya watu wazima wawili ambao ungependa kuwajua vizuri zaidi.

․․․․․

Mbona usimfikie mmoja wa watu ulioandika na kuanzisha mazungumzo naye? Kadiri unavyojitahidi kutafuta nafasi za kuzungumza na watu mbalimbali katika “ushirika mzima wa akina ndugu,” ndivyo upweke wako utakavyopungua.—1 Petro 2:17.

Pengo la 3: Tabia zisizopendeza. Kwa kawaida watu “wajuaji” hupenda kutumia matusi, dhihaka na kuwavunjia wengine heshima. Pia, kuna watu ambao hupenda ubishi na kusisitiza wengine wafuate maoni yao. Kwa kuwa wanajiona kuwa ‘waadilifu kupita kiasi,’ wao humshutumu mtu yeyote asiyefikia viwango vyao. (Mhubiri 7:16) Bila shaka, hungependa kuwa karibu na watu kama hao! Hata hivyo, inawezekana kwamba pengo limetokea kwa sababu hivyo ndivyo ulivyo? Biblia inasema: “Mpumbavu husema maneno mengi,” na pia “katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa.”—Mhubiri 10:14; Methali 10:19.

Daraja: Jifunze kuwa na “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Hata ikiwa hukubaliani na maoni ya mwingine, onyesha subira na umruhusu azungumze. Kazia fikira mambo mnayokubaliana. Ukiona kwamba ni lazima ueleze maoni yako yanayotofautiana na yake, fanya hivyo kwa upole na kwa busara.

Zungumza na wengine vile ambavyo ungependa wazungumze nawe. Biblia inashauri: “Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika na kubishana.” (Wafilipi 2:14) Mambo kama ubishi, utani usiofaa, kuwatusi wengine au kuona hawafai kitu, huzidisha pengo. Watakupenda zaidi ‘maneno yako yakiwa na neema sikuzote.’—Wakolosai 4:6.

Je, Uazimie Kupata Marafiki Hata Iweje?

Baada ya mazungumzo hayo mafupi, na kujichunguza, huenda umeona njia mbalimbali za kujenga madaraja ya kuziba pengo lililopo kati yako na wengine. Bila shaka, unapaswa kuona mambo kihalisi. Usitazamie kupendwa na kila mtu. Yesu alisema kwamba watu fulani hata watawachukia wale wanaotenda mema. (Yohana 15:19) Kwa hiyo, kuazimia kufanya urafiki na kila mtu ni kazi bure.

Hata hivyo, unaweza kujitahidi kuwavutia wengine bila kulegeza viwango vyako vinavyotegemea kanuni za Biblia. Samweli aliyeishi nyakati za Biblia aliazimia kabisa kufanya yale yanayompendeza Mungu. Matokeo? Aliendelea “kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.” (1 Samweli 2:26) Ukitia bidii, hata wewe utafanikiwa!

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 8

Unaweza kupata habari zaidi kwa kutazama DVD ya “Young People Ask—How Can I Make Real Friends?” inayopatikana katika lugha zaidi ya 40

KATIKA SURA INAYOFUATA

Rafiki yako wa karibu anabadilika ghafula na kuwa adui. Utafanya nini?

MAANDIKO MUHIMU

Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.Methali 11:25.

PENDEKEZO

Endeleza mazungumzo. Kwa mfano, mtu akikuuliza kama ulifurahia mwisho-juma, usimjibu tu ndiyo. Eleza ni nini kilichokufurahisha. Kisha mwulize yeye alifanya nini.

JE, WAJUA . . . ?

Biblia inaonyesha kwamba huenda Musa, Yeremia, na Timotheo walikuwa watu wenye haya.—Kutoka 3:11, 13; 4:1, 10; Yeremia 1:6-8; 1 Timotheo 4:12; 2 Timotheo 1:6-8.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Pengo kubwa linalonizuia ni ․․․․․

Nitajitahidi kuziba pengo hilo kwa․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini huenda Wakristo fulani wakawa wapweke?

● Ni nini kinachoweza kukusaidia kuwa na maoni yaliyosawazika kujihusu badala ya kuwa na maoni yasiyofaa nyakati zote?

● Unaweza kumfariji jinsi gani ndugu au dada kijana anayelemewa na upweke?

[Blabu katika ukurasa wa 88]

“Dada mmoja Mkristo alijaribu kufanya urafiki nami, lakini mwanzoni sikutaka. Baadaye tulipoanza urafiki, nilijiona kuwa mpumbavu sana! Mwishowe akawa rafiki yangu wa chanda na pete hata ingawa alikuwa amenizidi umri kwa miaka 25!’’—Marie

[Picha katika ukurasa wa 87]

Unaweza kuziba pengo linalokutenganisha na vijana wenzako kwa kujenga daraja