Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Rafiki Yangu Ananitendea Hivi?

Mbona Rafiki Yangu Ananitendea Hivi?

SURA YA 10

Mbona Rafiki Yangu Ananitendea Hivi?

“Kerry alikuwa rafiki yangu mkubwa. Nilikuwa nikimpitia kila siku baada ya kazi kwa kuwa hakuwa na gari. Hata hivyo, muda si muda nilianza kuona kwamba ananitumia vibaya.

“Alikuwa akijitoma tu ndani ya gari langu huku akizungumza kwenye simu ya mkononi au kutuma ujumbe mfupi. Hakushukuru kamwe kwa kupewa lifti, naye akaacha kuchangia pesa za mafuta. Sikuzote alikuwa akiwachambua-chambua wengine. Nilijuta kwamba nimemvumilia kwa muda mrefu hivyo!

“Siku moja nilimwambia Kerry kwa fadhili kwamba sitampitia tena baada ya kazi. Tangu wakati huo, hakutaka tena kuniona. Naamini kwamba alitaka tu kuwa rafiki yangu kwa sababu ya faida alizopata kutokana na urafiki wetu. Hilo linaniumiza sana!”—Nicole.

INAWEZA kuwa hivyo kwa marafiki wenye uhusiano wa karibu sana. Siku moja ni marafiki wasioachana; siku ya pili hata hawasemezani. Kwa nini urafiki kama huo uvunjike haraka hivyo?

● Katika kisa cha Jeremy, mambo yalibadilika wakati rafiki yake wa karibu alipohamia eneo lililokuwa kilomita 1,600 hivi kutoka kwao. “Alipohama, hakunipigia simu tena,” Jeremy anasema, “na jambo hilo lilinihuzunisha sana.”

● Kerrin alianza kuona utu wa msichana ambaye alikuwa rafiki yake mkubwa kwa miaka mitano ukibadilika. “Nilihangaishwa sana na mtazamo na maneno yake,” anasema Kerrin. “Alianza kuchambua na kudharau mambo niliyoyaona kuwa ya maana. Nilipojaribu kuzungumza naye kuhusu jambo hilo, alisema kwamba ninajifanya mtakatifu, mimi si mwaminifu, na kwamba urafiki wetu hauna maana kwake!”

● Urafiki kati ya Gloria na rafiki yake wa karibu uliisha ghafula na bila mawasiliano yoyote. “Mwanzoni, tulipatana sana,” Gloria anasema, “naye aliniambia kwamba nilikuwa kama dada yake. Kisha, bila sababu yoyote, aliacha kufanya mambo pamoja nami, huku akitoa visingizio.”

● Matatizo kati ya Laura na Daria yalianza wakati Daria alipomnyakua mchumba wa Laura. “Daria alikuwa akizungumza naye kwa simu kwa saa nyingi, hata ingawa alijua kwamba kijana huyo ni mchumba wangu,” anasema Laura. “Nilisalitiwa na rafiki yangu mkubwa na kupoteza mchumba wangu wakati uleule!”

Tatizo Lilikuwa Nini?

Kila mtu hukosea. Kwa hiyo, si ajabu kwamba mara kwa mara rafiki anaweza kusema jambo ambalo linaweza kukuumiza. Huenda hata unakumbuka pindi fulani ambapo wewe mwenyewe uliwaumiza wengine. (Mhubiri 7:22) “Sisi sote hatujakamilika, na mara kwa mara tunaweza kukwaruzana,” anasema msichana anayeitwa Lisa. Kwa kawaida, mazungumzo mafupi yanaweza kuziba pengo ambalo limesababishwa na kutoelewana kidogo.

Hata hivyo, katika visa vingine, pengo katika urafiki halisababishwi na tukio moja tu bali linatokea wakati mnapotambua hatua kwa hatua kwamba mna mapendezi tofauti kinyume na mlivyokuwa mkifikiri. Kumbuka kwamba kadiri unavyokua ndivyo mapendezi yako yanavyobadilika—na ndivyo na ya rafiki yako. Unaweza kufanya nini ukitambua kwamba urafiki wenu umeanza kupoa?

Jinsi ya Kufufua Urafiki

Tuseme nguo unayoipenda sana imeraruka. Utafanya nini? Utaitupa au utaishona? Bila shaka, hatua utakayochukua itategemea nguo hiyo imeraruka kiasi gani na unaithamini kadiri gani. Ikiwa kwa kweli unaipenda sana nguo hiyo, haikosi utatafuta njia za kuirekebisha. Inaweza kuwa hivyo pia kuhusiana na urafiki uliovunjika. Mengi yanategemea tatizo lenyewe na jinsi ambavyo unathamini uhusiano huo. *

Kwa mfano, ikiwa umeambiwa au kutendewa kwa njia isiyo ya fadhili, unaweza kufunika jambo hilo kwa kufuata shauri la Zaburi 4:4: “Semeni moyoni mwenu, kitandani mwenu, na kunyamaza.” Kwa hiyo, kabla ya kuutupilia mbali urafiki huo, fikiri kwa uzito. Je, alitenda hivyo kwa makusudi? Ikiwa huna hakika, kwa nini usichukulie kwamba rafiki yako hakuwa na nia mbaya? Katika visa vingi, unaweza kuacha ‘upendo ufunike dhambi nyingi.’—1 Petro 4:8.

Pia, unaweza kuchunguza ikiwa ulichangia tatizo hilo. Kwa mfano, rafiki akifunua siri uliyomwambia, je, inawezekana kwamba hukutenda kwa hekima kwa kumtwika mzigo mzito hivyo? Unaweza pia kujiuliza ikiwa wewe mwenyewe ulichangia dhihaka unazopata, labda kwa kuongea kupita kiasi au kusema mambo ya kipumbavu. (Methali 15:2) Ikiwa ndivyo, jiulize, ‘Je, ninahitaji kufanya mabadiliko ili rafiki yangu aniheshimu?’

“Ningependa Tuzungumze”

Hata hivyo, namna gani ukiona kwamba huwezi kupuuza jambo lililotokea? Basi, huenda ikafaa kuzungumza na rafiki yako. Lakini uwe mwangalifu usifanye hivyo ukiwa umekasirika. Biblia inasema: “Mtu mwenye ghadhabu huchochea ugomvi, lakini yule ambaye hakasiriki upesi hutuliza mabishano.” (Methali 15:18) Kwa hiyo, kabla ya kujaribu kutatua tatizo hilo, kwanza tulia.

Unapoenda kuzungumza na rafiki yako, kumbuka kwamba kusudi lako si ‘kulipa uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Badala yake, lengo lako ni kutatua tatizo hilo na kurudisha urafiki. (Zaburi 34:14) Kwa hiyo, sema yaliyo moyoni. Unaweza kusema, “Tulikuwa marafiki. Sielewi kilichotokea. Ningependa tuzungumze.” Baada ya kujua kilichosababisha tatizo lenyewe, huenda ikawa rahisi kuwa marafiki tena. Hata rafiki yako asipotaka kuzungumza, angalau unaweza kufarijika kwa kujua kwamba wewe umejaribu kurudisha amani.

Baada ya kufanya yote hayo, kumbuka kwamba “kuna rafiki wanaoelekea kuvunjana vipande-vipande,” hata hivyo, kuna “rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Methali 18:24) Ni kweli kwamba hata marafiki wakubwa wanaweza kukwaruzana mara kwa mara. Hilo likitukia, fanya yote uwezayo kurekebisha uhusiano wenu. Ndiyo, kuwa tayari kutatua hali za kutoelewana zinazotokea, kunaonyesha kwamba unaendelea kukomaa.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 8

KATIKA SURA INAYOFUATA

Huenda baadhi ya rafiki zako wanatumia saa nyingi wakipiga gumzo katika Intaneti. Ni nini kinachowavutia hivyo?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Huenda kusiwe na haja ya kurudisha uhusiano wa karibu na watu fulani, hasa ikiwa hawajiendeshi kwa njia inayomfaa Mkristo.—1 Wakorintho 5:11; 15:33.

MAANDIKO MUHIMU

“Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.

PENDEKEZO

Kabla ya kukata kauli, msikilize kwanza rafiki yako.—Methali 18:13.

JE, WAJUA . . . ?

Rafiki wazuri hutambua kwamba rafiki zao wanahitaji nafasi ya kupumua. (Methali 25:17) Lakini, uhusiano unaweza kuvunjika mtu anapodai rafiki yake atumie muda mwingi kupita kiasi pamoja naye.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikihitaji kuzungumza na rafiki yangu kwa sababu ameniumiza, nitaanza kwa kusema ․․․․․

Hata ikiwa nimekasirika kwa sababu ya jambo ambalo rafiki yangu ametenda, nitajitahidi kudumisha amani kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Kwa nini nyakati nyingine pengo hutokea kati ya marafiki?

Ikiwa rafiki yako amekuumiza, ni mambo gani ambayo unaweza kuamua kusahau badala ya kuzungumza naye, na ni mambo gani ambayo unahitaji kuyatatua kwa kuzungumza naye?

Ikitokea kwamba umeumizwa na rafiki, ni mambo gani yenye faida unayoweza kujifunza kutokana na hali hiyo?

Unaweza kufanya nini ili kupunguza uwezekano wa kuumizwa na rafiki?

[Blabu katika ukurasa wa 95]

“Ikiwa ningeweza kuanza upya, singekuwa mwenye kudai mno. Ningemsikiliza zaidi na kumuunga mkono badala ya kukazia fikira kasoro zake. Sasa nimetambua kwamba ili urafiki ufaulu, kinachohitajiwa ni kutatua matatizo na magumu yanayotokea.’’—Keenon

[Picha katika ukurasa wa 94]

Kama vile nguo iliyoraruka inavyoweza kurekebishwa, ndivyo na urafiki uliovunjika