Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa na Nyuso Mbili—Kuna Ubaya Gani?

Kuwa na Nyuso Mbili—Kuna Ubaya Gani?

SEHEMU YA 16

Kuwa na Nyuso Mbili—Kuna Ubaya Gani?

□ Kunywa pombe

□ Kufanya urafiki na watu ambao wazazi wako wanaona hawafai

□ Kusikiliza muziki usiofaa

□ Kwenda kwenye karamu za kupindukia

□ Kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri

□ Kutazama sinema zenye jeuri au upotovu wa kiadili au kucheza michezo ya video yenye jeuri

□ Kutumia lugha chafu

TAZAMA orodha iliyo katika ukurasa unaotangulia. Je, wewe hufanya yoyote kati ya mambo hayo bila wazazi wako kujua? Ikiwa ndivyo, haikosi unajua kwamba kile unachofanya si sawa. Huenda hata ukasumbuliwa na dhamiri. (Waroma 2:15) Hata hivyo, si rahisi kuwafunulia wazazi wako mambo hayo. Na unapofikiria jinsi ambavyo wazazi wako watahisi, huenda ukaamua kutowaambia, ukifikiri hivi: “Pilipili wasizozila, zawawashia nini?” Lakini, je, unajua kwamba hayo ni maisha ya unafiki? Kwa nini vijana wengi huficha jinsi walivyo?

Kutaka Kujitegemea

Biblia inasema kwamba mwishowe “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Bila shaka, maneno hayo yanawahusu wanawake pia. Kila mtu anatamani kukua na kujifanyia maamuzi. Lakini wazazi wanapowakataza kufanya mambo ambayo machoni pao hayafai au ni mabaya, vijana fulani huasi.

Ni kweli kwamba wazazi fulani huonekana kuwa wakali mno. Msichana anayeitwa Kim alilalamika hivi: “Kwetu, kutazama sinema ni marufuku.” Kisha akasema, “Baba ametukataza kabisa tusisikilize karibu muziki wa aina zote!” Wanapowekewa vizuizi wanavyoviona kuwa vimepita kiasi, vijana fulani huanza kutamani maisha ya vijana wenzao ambao wanaonekana kuwa na uhuru mwingi zaidi.

Msichana anayeitwa Tammy anataja sababu nyingine inayowafanya vijana fulani kuwa na nyuso mbili: Wanafanya hivyo ili wakubaliwe na wanafunzi wenzao. “Nilianza kwa kutumia lugha chafu shuleni,” Tammy anakumbuka. “Hilo lilifanya nijione kuwa sawa na vijana wenzangu. Baadaye nilianza kuvuta sigara. Nikawa pia na mazoea ya kulewa. Kisha nikaanza kufanya urafiki na wavulana kisiri kwa sababu wazazi wangu walikuwa wakali sana nao hawakutaka niwe na rafiki yeyote wa kiume.”

Mvulana anayeitwa Pete alikuwa katika hali kama hiyo: “Nililelewa katika familia ya Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, niliogopa sana kudhihakiwa.” Pete alifanya nini? Anasema, “Nilijaribu kutafuta umaarufu. Nilipokuwa nikieleza kwa nini sipati zawadi wakati wa sherehe za kidini, nilidanganya na kutunga hadithi za uwongo.” Kwa kuwa Pete alikuwa amelegeza msimamo wake katika mambo madogo-madogo, muda si muda alijikuta ametumbukia katika dhambi nzito zaidi.

Hakuna Siri Mbele za Yehova

Watu wanafiki wamekuwako tangu zamani. Waisraeli fulani wa kale walijaribu kuishi maisha ya unafiki wakifikiri hakuna anayeweza kujua. Hata hivyo, nabii Isaya aliwaonya hivi: “Ole wao wanaojizamisha ndani sana katika kuficha shauri kutoka kwa Yehova, na ambao matendo yao yamefanyika mahali penye giza, huku wakisema: ‘Ni nani anayetuona, na ni nani anayejua habari zetu?’” (Isaya 29:15) Waisraeli walisahau kwamba Mungu anaona matendo yao. Mwishowe, aliwahukumu kwa sababu ya makosa yao.

Ndivyo ilivyo leo pia. Hata ukiwaficha wazazi wako mwenendo wako usiofaa, huwezi kumficha Yehova Mungu. Andiko la Waebrania 4:13 linasema: “Hakuna kiumbe kisichokuwa wazi machoni pake, bali vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” Basi kuna haja gani ya kujifanya? Kumbuka, huwezi kumfumba Mungu macho kwa kujifanya tu kwamba unamwabudu eti kwa sababu unahudhuria mikutano ya Kikristo. Yehova anajua wakati ambapo watu ‘wanamheshimu kwa midomo yao, bali mioyo yao iko mbali naye.’—Marko 7:6.

Je, unajua kwamba wale wanaoishi maisha ya unafiki wanamhuzunisha Yehova? Inawezekana kweli? Bila shaka! Waisraeli wa kale walipoiacha Sheria ya Mungu, ‘walimtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.’ (Zaburi 78:41) Lazima awe na uchungu sana leo anapoona vijana waliolelewa “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” wakifanya kisiri mambo yasiyofaa!—Waefeso 6:4.

Nyoosha Mambo

Kwa kweli, una wajibu mbele za Mungu, wazazi wako, na kwako mwenyewe kuungama mambo ambayo umekuwa ukifanya sirini. Ni kweli, kwamba, huenda ukapatwa na aibu baada ya kuungama au hata kuadhibiwa. (Waebrania 12:11) Kwa mfano, ikiwa umezoea kusema uwongo na kudanganya, itakuwa vigumu kwa wazazi wako kukuamini. Kwa hiyo, usishangae wakikuwekea vizuizi vingi hata zaidi kuliko mwanzoni. Hata hivyo, kufunua maisha yako ndilo jambo linalofaa. Kwa nini?

Fikiria mfano huu: Wazia kwamba wewe na familia yenu mko katika matembezi. Pasipo wazazi wako kujua, unabaki nyuma kinyume na maagizo yao, unakengeuka na kupotea. Ghafula, unaanza kudidimia katika mchanga. Je, utaona aibu kuomba msaada? Je, utaamua kukaa kimya eti kwa sababu huenda wazazi wako wakakuadhibu kwa sababu ulipuuza amri yao? Hapana! Utapiga kelele kwa sauti yako yote.

Vivyo hivyo, ikiwa unaishi maisha ya unafiki, unahitaji msaada haraka. Kumbuka, maji yakimwagika, hayazoleki. Hata hivyo, unaweza kuganga yajayo. Ingawa huenda ikawa vigumu kufichua ukweli kuhusu maisha yako, ni jambo la busara kuomba msaada kabla ya madhara makubwa kutokea kwako mwenyewe na kwa familia yenu. Ikiwa kwa kweli unajuta kwa sababu ya mambo ambayo umefanya, Yehova atakuonyesha rehema.—Isaya 1:18; Luka 6:36.

Kwa hiyo, waambie wazazi wako ukweli. Elewa kwamba umewaumiza. Kubali nidhamu wanayokupa. Ukifanya hivyo, utawafurahisha wazazi wako na Yehova Mungu. Pia, utapata kitulizo cha kuwa na dhamiri safi.—Methali 27:11; 2 Wakorintho 4:2.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Wewe na wanafunzi wenzako mna mapendezi yaleyale. Hata hivyo, je, kuna uhitaji wowote wa kuwa mwangalifu?

MAANDIKO MUHIMU

Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.Methali 28:13.

PENDEKEZO

Usipunguze uzito wa makosa yako, lakini kumbuka pia kwamba wewe si mkamilifu. Na iwapo utakosea, Yehova yuko tayari kukusamehe.—Zaburi 86:5.

JE, WAJUA . . . ?

Hisia za hatia zina faida; zinaweza kumfanya mtu arekebishe mwenendo usiofaa. Lakini anayeendelea kutenda dhambi anaiharibu dhamiri yake. Inakufa ganzi, kama ngozi iliyochomwa na kuwa na makovu.—1 Timotheo 4:2.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa nimekuwa nikiishi maisha ya unafiki, nitazungumza na ․․․․․

Naweza kunufaika na nidhamu yoyote ninayopata kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini vijana fulani wana nyuso mbili?

● Unafiki una matokeo gani mabaya?

● Kuacha kuishi maisha ya unafiki kuna faida gani?

[Blabu katika ukurasa wa 140]

Nafikiri vijana wanapaswa kujitambulisha kuwa Wakristo walio na maadili mazuri. Wanapaswa kufanya hivyo mapema iwezekanavyo. Kadiri wanavyosita kufanya hivyo, ndivyo itakavyokuwa vigumu zaidi.’’—Linda

[Picha katika ukurasa wa 141]

Ikiwa unadidimia katika maisha ya unafiki, unahitaji kuomba msaada