Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje Ikiwa Sisi Ni Maskini?

Nifanyeje Ikiwa Sisi Ni Maskini?

SURA YA 20

Nifanyeje Ikiwa Sisi Ni Maskini?

Kijana mmoja katika Ulaya Mashariki anayeitwa Gregory, hana pesa za kununua nguo au vifaa vya elektroniki ambavyo vijana wengine katika nchi zilizoendelea wanavyo. Anafadhaishwa sana na hali yake hivi kwamba anataka kuhamia Austria. Je, unafikiri akina Gregory ni maskini?

□ Ndiyo □ Hapana

Kijana Loyiso anaishi katika kijiji cha nchi moja kusini mwa Afrika, maelfu ya kilomita kutoka Ulaya Mashariki. Kwa kuwa wanaishi katika kibanda kidogo, Loyiso anaowaonea wivu vijana katika mji ulio karibu, ambao kulingana naye wanaishi maisha ya “anasa,” kwa kuwa wana maji ya bomba na umeme. Je, akina Loyiso ni maskini?

□ Ndiyo □ Hapana

BILA shaka, neno “umaskini” linarejelea hali tofauti katika nchi mbalimbali. Kwa mfano, huenda Gregory alijiona kuwa maskini hohehahe, lakini kwa kulinganishwa na Loyiso, anaishi maisha ya anasa. Ukweli ni kwamba hata ikiwa ninyi maskini kadiri gani, haikosi kuna wengine walio maskini zaidi. Hata hivyo, ikiwa huna nguo nzuri za shule au hamna vitu vya msingi kama vile maji ya bomba, huenda ukauliza, ‘Kujua kwamba kuna wengine walio maskini zaidi kunanisaidiaje?’

Vijana fulani wanaolelewa katika familia maskini hujiona kuwa hawafai, nao hujaribu kusahau matatizo yao kwa kunywa pombe au kutumia dawa za kulevya. Lakini, kufanya hivyo hufanya mambo yawe mabaya zaidi. Wale wanaokunywa pombe kupita kiasi hutambua kwamba “inauma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka.” (Methali 23:32) Maria, msichana kutoka katika familia ya mzazi mmoja, nchini Afrika Kusini, anasema, “Kuhepa matatizo huzidisha matatizo.”

Huenda usianze kunywa pombe au kutumia dawa za kulevya, hata hivyo, huenda usione uwezekano wa kuboresha hali yenu. Unaweza kupata wapi msaada? Shauri la Biblia lenye hekima ni kama ufunguo unaoweza kukuweka huru na minyororo ya kutokuwa na tumaini, na kukuwezesha kuwa na mtazamo unaofaa. Jinsi gani?

Kazia Fikira Vitu Ulivyo Navyo

Jambo moja la maana ni kukazia fikira, vitu ulivyo navyo, bali si vitu ambavyo huna. Vitu kama vile nyumba na familia yenye upendo ni vyenye thamani kuliko pesa! Methali moja ya Biblia inasema: “Afadhali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo kuliko ng’ombe-dume aliyenoneshwa pamoja na chuki.” (Methali 15:17) Vijana Wakristo wana kitu fulani chenye thamani sana—“ushirika mzima wa akina ndugu.”—1 Petro 2:17.

Jaribu pia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu vitu vya kimwili. Huenda mnaishi katika nyumba ndogo, au hata katika kibanda. Labda wewe huvaa nguo zenye viraka au matambara. Na pengine wewe hutamani kula vyakula tofauti-tofauti. Lakini je, unahitaji mavazi ya kisasa au nyumba ya kifahari ili kumpendeza Mungu? Je, unahitaji kula mapochopocho ili uishi na kuwa na afya nzuri? Hapana. Mtume Paulo alijifunza jambo la maana kuhusiana na hilo. Kuna wakati alipokuwa na mali nyingi, na kuna wakati alipokuwa na umaskini. (Wafilipi 4:12) Alikata kauli gani? “Kama tunacho chakula na mavazi, tunapaswa kuridhika navyo.”—1 Timotheo 6:8, BHN.

Eldred, aliyelelewa katika familia maskini nchini Afrika Kusini, anasema: “Tuliridhika na ukweli wa kwamba familia yetu ilikuwa na uwezo mdogo wa kifedha na kwamba hatungepata kila kitu tulichohitaji.” Eldred anakumbuka kwamba suruali yake ya shule iliporaruka, mama yake alikuwa akiipiga kiraka, naye alifanya hivyo tena na tena na tena! “Nililazimika kuvumilia kuchekwa,” Eldred anasema. “Lakini jambo la maana ni kwamba nguo zetu zilikuwa safi na zingevalika.”

Jiheshimu

James, mwenye umri wa miaka 11, aliishi na mama na dada yake katika mtaa wa mabanda karibu na Johannesburg, Afrika Kusini. Walikuwa fukara. Hata hivyo, James alikuwa na nguvu na wakati, naye alifurahia kutumia nguvu na wakati wake kuwasaidia wengine. Kila mwisho wa juma, James alijitolea kusaidia kujenga Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwao. Kazi hiyo ilimsaidia kuwa na jambo la kufanya badala ya kukaa tu bila kusudi, pia ilimpa uradhi na kumfanya ajiheshimu. Anasema: “Baada ya kushinda mchana kutwa nikisaidia katika ujenzi wa jumba hilo, nilihisi nimeridhika sana!”

Kazi nyingine muhimu ni ile ya kuwafundisha wengine Biblia nyumba kwa nyumba. (Mathayo 24:14) Vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova hufanya kazi hiyo kwa ukawaida. Kwa kufanya hivyo wanawapa watu tumaini la maisha bora wakati ujao, nao hujiheshimu zaidi. Ni kweli kwamba hawachumi pesa kutokana na kazi hiyo. Lakini kumbuka ujumbe wa Yesu kwa Wakristo wa kutaniko la kale la Smirna. Walikuwa maskini kimwili. Hata hivyo, kwa sababu ya hali yao nzuri ya kiroho, Yesu alisema hivi kuwahusu: “Ninajua dhiki na umaskini wako—lakini wewe ni tajiri.” Mwishowe, imani yao katika damu ya Yesu iliyomwagwa ingewawezesha kupata utajiri mkubwa zaidi, yaani, taji la kutoweza kufa.—Ufunuo 2:9, 10.

Tazama Mbele

Uwe tajiri au maskini, unaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Biblia inasema: “Mtu tajiri na maskini wamekutana. Mtengenezaji wao wote ni Yehova.” (Methali 22:2) Kujua hilo kumesaidia maelfu ya vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova kukabiliana na umaskini. Wanatambua kwamba furaha haitokani na kuwa na vitu vingi vya kimwili, bali inatokana na kufanya urafiki pamoja na Yehova Mungu, anayewakaribisha wote wanaotaka kumtumikia. Mungu anatoa ahadi ya uzima katika ulimwengu mpya unaokuja ambao hautakuwa na umaskini.—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Kwa sasa, tumia vitu ulivyo navyo kwa hekima. Tazama mbele. Jiwekee hazina za kiroho. (Mathayo 6:19-21) Ona umaskini kuwa tatizo ambalo unaweza kukabiliana nalo!

MAANDIKO MUHIMU

Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.Luka 12:15.

PENDEKEZO

Jiepushe na kucheza kamari, kuvuta sigara, na ulevi. Ikiwa wengine katika familia yenu wana mazoea hayo, wawekee mfano kupitia mwenendo wako.

JE, WAJUA . . .?

Hata hali zako ziwe namna gani, kanuni za Biblia zinaweza kukusaidia kuwa na sifa ya kuridhika.—Wafilipi 4:12, 13; 1 Timotheo 6:8; Waebrania 13:5.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ingawa sina vitu vingi vya kimwili, nina ․․․․․

Kwa hiyo ninaweza kuwasaidia wengine kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini huenda mtu anayejiona kuwa “maskini” asionwe hivyo na wengine?

● Kwa nini si vizuri kutumia dawa za kulevya, pombe, au dawa nyinginezo ili kuhepa matatizo?

● Ni hatua gani unazoweza kuchukua ili kukabiliana na umaskini?

[Blabu katika ukurasa wa 168]

Ingawa nilihisi nimefungwa kwa minyororo ya umaskini, nilijua kwamba dawa si kujiunga na genge au kuiba ili nijiruzuku. Leo hii, watu wengi wa umri wangu ambao walijiingiza katika mambo hayo sasa ni watu wasiofaa kitu, watumwa wa pombe na dawa za kulevya, au wako gerezani.’’—George

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 164]

Ukurasa wa Mazoezi

Nihamie Ng’ambo?

Vijana fulani hutaka kuhamia ng’ambo ili wachume pesa za kuwategemeza au kutegemeza familia zao. Wengine huhama ili kujifunza lugha ya kigeni, kupata elimu zaidi, au ili kuhepa matatizo yaliyo kwao. Vijana fulani Wakristo wamehamia nchi ambazo zina uhitaji wa wahubiri. Uamuzi wa kuhamia nchi ya kigeni ni mzito na haupaswi kuchukuliwa vivi hivi tu. Kwa hiyo, ikiwa unafikiria kuhamia ng’ambo, soma na utafakari maandiko yaliyo hapa chini. Jiulize maswali haya na uandike majibu kwenye karatasi. Kisha sali upate msaada wa kufanya uamuzi.

◻ Ni mambo gani ya kisheria yanayohusika?—Waroma 13:1.

◻ Itanigharimu kiasi gani cha pesa kuhamia ng’ambo? —Luka 14:28.

◻ Ninafanya nini sasa kinachoonyesha kwamba nitaweza kushughulikia mahitaji yangu ya kimwili nikiwa ng’ambo?—Methali 13:4.

◻ Nimepata ushauri gani kutoka kwa watu wazima ambao wameishi ng’ambo?—Methali 1:5.

◻ Wazazi wangu wana maoni gani kuhusu jambo hilo? —Methali 23:22.

◻ Kwa nini ninataka kuhamia ng’ambo?—Wagalatia 6:7, 8.

◻ Ikiwa nitaenda kuishi na watu wengine, je, watanitia moyo niendeleze mazoea mazuri ya kiroho?—Methali 13:20.

◻ Huenda nikakabili hatari gani za kiadili, kimwili, na kiroho?—Methali 5:3, 4; 27:12; 1 Timotheo 6:9, 10.

◻ Kwa kweli, ni faida gani ninazotazamia kupata nikiishi ng’ambo?—Methali 14:15.

[Picha katika ukurasa wa 167]

Shauri la Biblia ni kama ufunguo unaoweza kukuweka huru na minyororo ya kutokuwa na tumaini