Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?

Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?

SURA YA 23

Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?

“Baba alisema anaenda kurekebisha gari, lakini hakuwasiliana nasi mchana kutwa. Mama alijaribu kumpigia simu. Hakuijibu. Muda si muda, nikamwona mama akiwa na wasiwasi huku akijitayarisha kuondoka. ‘Naenda kumtafuta baba yako,’ akasema.

“Baadaye, Mama alirudi peke yake. Nikamuuliza, ‘Kwani hukumpata?’ Akajibu, ‘Hapana.’

“Ndipo nikagundua kwamba Baba amerudia mazoea yake ya zamani. Ni kama tu ilivyokuwa wakati uliopita. Wajua, baba yangu ni mraibu wa dawa za kulevya. Kufikia wakati aliporudi nyumbani, tulikuwa na wasiwasi mwingi. Siku iliyofuata, sikuzungumza naye hata kidogo, jambo ambalo liliniumiza sana.”—Karen, 14.

MAMILIONI ya vijana huishi na wazazi ambao ni waraibu wa dawa za kulevya au pombe. Ikiwa mmoja wa wazazi wako ni mtumwa wa mazoea hayo, huenda unaona aibu, unavunjika moyo, au hata kukasirika.

Kwa mfano, mbele ya watu, baba ya Mary alionekana mzuri sana. Lakini kwa siri, alikuwa mlevi sugu, naye alikuwa akiwatusi na kuwatendea kwa ukatili washiriki wa familia yake. Mary anakumbuka hivi kwa uchungu: “Watu walikuwa wakitujia na kutupongeza kwamba baba yetu ni mzuri ajabu, na kwamba tuna raha kama nini kuwa na baba kama huyo.” *

Ikiwa mzazi wako ni mraibu wa pombe au dawa za kulevya, unaweza kufanya nini?

Uraibu Unasababishwa na Nini?

Kwanza, ni vizuri kuelewa kwa undani tatizo la wazazi wako. Methali 1:5 inasema hivi: “Mtu mwenye uelewaji ndiye anayepata mwongozo stadi.” Kwa hiyo, ingefaa kuelewa uraibu ni nini, ni akina nani huwa na mazoea hayo, na kwa nini.

Kwa mfano, mraibu si mtu ambaye hunywa kupita kiasi mara mojamoja. Badala yake, ni mtu mwenye tatizo la kudumu la kunywa kupita kiasi. Anatawaliwa na pombe, na akianza kunywa, hawezi kujizuia. Uraibu wake unaathiri familia, kazi, na afya yake. *

Ijapokuwa huenda ikawa mtu fulani anapenda tu kunywa kupita kiasi, nyakati nyingine hisia zinahusika. Waraibu wengi hujiona kwamba hawafai kitu. (Methali 14:13) Baadhi yao walilelewa na wazazi ambao pia walikuwa na mazoea ya kunywa kupita kiasi. Watu kama hao hunywa pombe ili kujisahaulisha uchungu na makovu ya utotoni. Huenda sababu hizohizo zikamfanya mtu aanze kutumia dawa za kulevya.

Bila shaka kunywa au kutumia dawa za kulevya kunazidisha tu matatizo ya mtu, kwa kuwa akiwa katika hali hiyo, akili yake haifanyi kazi vizuri nazo hisia zake si za kawaida. Ndiyo sababu huenda mzazi wako akahitaji kusaidiwa na wataalamu ili aweze kushinda zoea hilo.

Usitarajie Mengi Kupita Kiasi

Ni kweli kwamba kujua tu kwa nini mzazi wako anafanya jambo fulani linalokuaibisha, hakuondoi tatizo lenyewe. Hata hivyo, kuelewa kwa kiasi fulani tatizo lake kunaweza kukusaidia kumwonea huruma mzazi wako.

Kwa mfano, ungetazamia mzazi ambaye amevunjika mguu acheze mpira wa miguu pamoja nawe? Namna gani ikiwa unajua kwamba mzazi wako aliumia akifanya jambo fulani lisilofaa? Haikosi ungevunjika moyo. Hata hivyo, unajua kwamba hataweza kucheza mpira nawe mpaka atakapopona. Kuelewa hilo kunaweza kukusaidia usitarajie mengi kupita kiasi kutoka kwa mzazi wako.

Vivyo hivyo, mzazi ambaye hunywa kupita kiasi au ambaye hutumia dawa za kulevya ni mlemavu kihisia na kiakili. Ni kweli kwamba amejisababishia mwenyewe “ulemavu” huo. Na una haki ya kukasirishwa na mwenendo huo. Hata hivyo, hadi mzazi wako atakapotafuta msaada wa kushinda zoea hilo, hataweza kukuandalia mahitaji yako vizuri. Kuuona uraibu wake kama ulemavu fulani kunaweza kukusaidia usitarajie mengi kupita kiasi kutoka kwake kwa sasa.

Mambo Unayoweza Kufanya

Ukweli ni kwamba, utaendelea kusumbuliwa na mwenendo wa mzazi wako mpaka atakapobadili maisha yake. Unaweza kufanya nini kabla ya wakati huo?

Usijilaumu kwa sababu ya tatizo la mzazi wako. Mzazi wako—wala si mwingine yeyote—ndiye mwenye lawama. Andiko la Wagalatia 6:5 linasema hivi: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” Kwa hiyo, si kazi yako kutatua tatizo la mzazi wako au kumwepusha na matokeo ya tatizo hilo. Kwa mfano, hakuna haja ya kumdanganya mkubwa wake kazini kwa niaba yake au kumwinua anapoanguka nje kwa sababu ya ulevi.

Mhimize mzazi wako atafute msaada. Huenda tatizo kubwa la mzazi wako ni kukubali kwamba ana tatizo. Ulevi unapokuwa umemtoka na ametulia, yule mzazi mwingine pamoja na watoto wakubwa katika familia wanaweza kumwambia mzazi huyo mlevi jinsi mwenendo wake unavyoathiri familia na mambo anayohitaji kufanya.

Pia, kuandika majibu ya maswali yafuatayo kunaweza kumsaidia mzazi mwenye tatizo hilo: Familia yangu itakuwaje nikiendelea kulewa au kutumia dawa za kulevya? Matokeo yatakuwa nini nikiacha zoea hili? Ninapaswa kufanya nini ili nipate msaada?

Ukiona dalili ya matata, ondoka. Andiko la Methali 17:14 linasema hivi: “Kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.” Usijihatarishe kwa kuingilia mabishano kati ya wazazi wako. Ikiwezekana ingia chumbani mwako au uende kwa rafiki yako. Ikiwa kuna uwezekano wa jeuri kutokea, huenda msaada kutoka nje ukahitajika.

Si vibaya kuwa na hisia. Vijana fulani hujiona kuwa na hatia kwa sababu ya kumchukia mzazi ambaye ni mraibu. Ni kawaida kuchukizwa kwa kiasi fulani, hasa ikiwa uraibu wa mzazi wako unamzuia kukuonyesha upendo na kukutegemeza. Ni kweli, Biblia inakuamuru umheshimu mzazi wako. (Waefeso 6:2, 3) Hata hivyo, mamlaka yake ndiyo unayoheshimu, kama vile unavyoheshimu mamlaka ya polisi au hakimu. Haimaanishi kwamba unaunga mkono mwenendo wa mzazi wako. (Waroma 12:9) Wala haimaanishi kwamba wewe ni mbaya kwa sababu unachukia tabia yake ya kulewa au kutumia dawa za kulevya; vyovyote vile, uraibu ni tabia yenye kuchukiza sana!—Methali 23:29-35.

Tafuta marafiki wenye kujenga. Maisha ya nyumbani yanapojaa vurugu, ni rahisi kuzoea hali hiyo na kufikiri kwamba hiyo ndiyo kawaida. Hivyo, hakikisha unachangamana na watu walio na hali nzuri ya kiroho na kihisia. Pindi unazokuwa na washiriki wa kutaniko la Kikristo, zinaweza kuwa zenye kutia moyo na kutegemeza kwelikweli, na pia kukupa nafasi ya kupumzika kutokana na mahangaiko ya familia yenu. (Methali 17:17) Ushirika mzuri wa familia za Kikristo unaweza kukusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu maisha ya familia, na kuondolea mbali maoni yasiyofaa ambayo huenda ukawa nayo kwa sababu ya jinsi hali ilivyo katika familia yenu.

Tafuta msaada kwa ajili yako mwenyewe. Kuna faida ya kuwa na mtu mzima mkomavu unayemwamini ambaye unaweza kumweleza hisia zako. Wazee wa kutaniko wako tayari kukusaidia ukihitaji msaada. Biblia inasema kwamba wanaume hao wanaweza kuwa “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha mwamba mzito katika nchi iliyochoka.” (Isaya 32:2) Hivyo, usiogope au kuona aibu kuwaendea ili kupata faraja na mashauri.

Andika hapa hatua utakazojaribu kwanza kati ya hatua sita zilizozungumziwa. ․․․․․

Huenda huwezi kubadili hali nyumbani kwenu, hata hivyo unaweza kubadili jinsi hali hiyo inavyokuathiri. Badala ya kujaribu kuwaongoza wazazi wako, kazia fikira mtu unayeweza kumwongoza, yaani, wewe mwenyewe. Mtume Paulo aliandika: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe.” (Wafilipi 2:12) Kufanya hivyo, kunaweza kukusaidia kuwa na maoni yanayofaa, na huenda hata kunaweza kumsaidia mzazi wako atafute usaidizi.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Namna gani ikiwa wazazi wako wanabishana kila wakati? Unaweza kufanya nini?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ikiwa unatendewa vibaya na mzazi mwenye mazoea ya kulewa, tafuta msaada. Zungumza na mtu mzima ambaye unamwamini. Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, unaweza kuongea na mzee wa kutaniko au Mkristo mwingine mkomavu.

^ fu. 11 Ingawa mraibu wa pombe anayezungumziwa ni wa kiume, kanuni zilizozungumziwa zinawahusu waraibu wa kike pia.

MAANDIKO MUHIMU

Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.Methali 19:11.

PENDEKEZO

Badala ya kumchukia mzazi wako, chukia mwenendo wake mbaya.—Methali 8:13; Yuda 23.

JE, WAJUA . . .?

Katika Biblia, neno ‘heshimu’ linaweza kumaanisha tu kutambua mamlaka halali. (Waefeso 6:1, 2) Hivyo, kumheshimu mzazi hakumaanishi kwamba nyakati zote utakubaliana na mwenendo wake.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Mzazi wangu akianza matusi au ugomvi, nita ․․․․․

Ninaweza kumtia moyo mzazi wangu atafute usaidizi kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Ni nini huwafanya watu fulani wawe waraibu wa pombe au dawa za kulevya?

Kwa nini huwezi kulaumiwa kwa sababu ya uraibu wa mzazi wako?

Katika hali unayokabili, ni hatua gani unazoweza kuchukua?

[Blabu katika ukurasa wa 192]

“Ninajua kwamba huenda siku moja mwenendo wa wazazi wangu ukaniabisha, lakini najua pia kwamba nikimtegemea Yehova, atanipa nguvu za kuvumilia.’’—Maxwell

[Sanduku katika ukurasa wa 198]

Mzazi Akiacha Kumtumikia Yehova

Mmoja wa wazazi wako akiacha kuishi kulingana na viwango vya Biblia—labda hata anasema kwamba hataki kushirikiana na kutaniko la Kikristo—unaweza kufanya nini?

Kumbuka kwamba Yehova hatakulaumu kwa sababu ya mwenendo wa mzazi wako. Biblia inasema: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”Waroma 14:12.

Epuka kujilinganisha na vijana wengine ambao hali zao ni nzuri zaidi. (Wagalatia 5:26) Kijana mmoja ambaye baba yake aliiacha familia yake anasema: “Badala ya kufikiria tu hali yenu mbaya, ingekuwa afadhali kukazia fikira jinsi unavyoweza kushughulika na hali hiyo.”

Endelea kumheshimu mzazi huyo, na kutii maagizo yake maadamu hayapingani na viwango vya Mungu. Amri ya Yehova kwamba watoto wawaheshimu wazazi wao, haitegemei ikiwa mzazi ni mwamini au si mwamini. (Waefeso 6:1-3) Unapowaheshimu na kuwatii wazazi wako, hata ikiwa wana mazoea fulani yasiyofaa, unaonyesha kwamba unampenda Yehova.—1 Yohana 5:3.

Shirikiana sana na kutaniko la Kikristo. Humo unaweza kufarijiwa na familia kubwa ya kiroho. (Marko 10:30) Kijana mmoja anayeitwa David aliogopa kwamba huenda washiriki wa kutaniko wakamwepuka yeye na familia yao kwa sababu baba yake alikuwa ameacha kumtumikia Yehova. Hata hivyo, David aligundua kwamba maoni yake hayakuwa na msingi. Anasema: “Hatukuachwa peke yetu. Hilo lilinisadikisha kwamba kutaniko linatujali kikweli.”

[Picha katika ukurasa wa 194]

Kuuona uraibu wa mzazi wako kama ulemavu fulani kunaweza kukusaidia kutotarajia mengi mno kutoka kwake