Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 12

“Wakizungumza kwa Ujasiri kwa Mamlaka ya Yehova”

“Wakizungumza kwa Ujasiri kwa Mamlaka ya Yehova”

Paulo na Barnaba waonyesha unyenyekevu, uvumilivu, na ujasiri

Matendo 14:1-28

1, 2. Ni mambo gani yanayotokea, Paulo na Barnaba wakiwa Listra?

 KUNA vurugu jijini Listra. Mwanamume aliyezaliwa kilema anarukaruka kwa shangwe baada ya kuponywa na watu wawili asiowajua. Watu wanastaajabishwa na jambo hilo, na kuhani wa Zeu anawaletea mashada ya maua watu hao wawili ambao umati unaamini kuwa ni miungu. Ng’ombe-dume wanavuta pumzi kwa nguvu na kutoa mlio huku kuhani huyo akiwa tayari kuwachinja. Mara moja Paulo na Barnaba wanamkataza asifanye hivyo. Wanayararua mavazi yao, wanaruka ndani ya umati na kuwasihi sana wasiwaabudu.

2 Kisha, Wayahudi wapinzani kutoka Antiokia ya Pisidia na Ikoniamu wakafika. Wakawachongea kwa chuki na kuwapotosha watu wa Listra. Umati huohuo, uliotaka kumwabudu Paulo, sasa ukamzunguka na kumpiga kwa mawe mpaka akapoteza fahamu. Baada ya hasira yao kupoa, wanamburuta Paulo, wanamtoa nje ya malango ya jiji, na kumwacha afe.

3. Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?

3 Ni nini kilichosababisha vurugu hiyo? Wahubiri wa habari njema leo wanaweza kujifunza nini kutokana na matukio hayo? Wazee Wakristo wanawezaje kuiga mfano wa Barnaba na Paulo ambao walivumilia katika huduma yao, na ‘kuzungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova?’​—Mdo. 14:3.

“Umati Mkubwa . . . Wakawa Waamini” (Mdo. 14:1-7)

4, 5. Kwa nini Paulo na Barnaba walienda Ikoniamu, na ni nini kilichotokea huko?

4 Siku chache zilizotangulia, Paulo na Barnaba walikuwa wametupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia baada ya Wayahudi wapinzani kuwachochea watu wawatese. Lakini, badala ya kuvunjika moyo, wanaume hao wawili “wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao” wakaaji wa jiji hilo walioukataa ujumbe wao. (Mdo. 13:50-52; Mt. 10:14) Paulo na Barnaba wakaondoka kwa amani na kuacha mambo mikononi mwa Mungu. (Mdo. 18:5, 6; 20:26) Wamishonari hao wawili hawakupoteza shangwe yao, bali waliendelea na safari yao ya kuhubiri. Wakasafiri karibu kilomita 150 kuelekea upande wa kusini-mashariki na kufika nchi tambarare yenye rutuba iliyo katikati ya safu za milima ya Taurus na Sultan.

5 Mwanzoni, Paulo na Barnaba waliamua kukaa Ikoniamu. Jiji hilo lenye utamaduni wa Kigiriki ni mojawapo ya majiji ya mkoa wa Galatia, katika milki ya Roma. a Jiji hilo lilikuwa na Wayahudi wengi mashuhuri na idadi kubwa ya wageuzwa imani wasio Wayahudi. Kulingana na desturi yao, Paulo na Barnaba waliingia ndani ya sinagogi na kuanza kuhubiri. (Mdo. 13:5, 14) “Wakazungumza vizuri hivi kwamba umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki wakawa waamini.”​—Mdo. 14:1.

6. Kwa nini Paulo na Barnaba walipata matokeo mazuri, nasi tunawezaje kuwaiga?

6 Kwa nini Paulo na Barnaba walipata matokeo mazuri? Paulo aliyajua Maandiko vizuri. Aliyahusianisha kwa ustadi na historia, unabii, na Sheria ya Musa ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. (Mdo. 13:15-31; 26:22, 23) Barnaba aliwajali sana watu. (Mdo. 4:36, 37; 9:27; 11:23, 24) Wanaume hao hawakutegemea uelewaji wao wenyewe bali walizungumza “kwa mamlaka ya Yehova.” Unawezaje kuwaiga wamishonari hao unapohubiri? Kwa kufanya mambo yafuatayo: Lijue kabisa Neno la Mungu. Chagua Maandiko yatakayowavutia wasikilizaji wako. Tafuta njia za kuwafariji wale unaowahubiria. Na sikuzote mafundisho yako yategemee mamlaka ya Neno la Yehova, bali si hekima yako.

7. (a) Habari njema huwa na matokeo gani? (b) Ikiwa familia yenu imegawanyika kwa sababu ya habari njema, unapaswa kukumbuka nini?

7 Hata hivyo, si kila mtu jijini Ikoniamu aliyefurahi kusikia ujumbe wa Paulo na Barnaba. Luka anasema hivi: “Wayahudi ambao hawakuamini wakawachochea watu wa mataifa na kuwafanya wawachukie akina ndugu.” Paulo na Barnaba waliamua kukaa huko na kutetea habari njema, na “wakatumia muda mrefu wakizungumza kwa ujasiri.” Hata hivyo, “umati wa jiji ulikuwa umegawanyika; baadhi yao walikuwa upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume.” (Mdo. 14:2-4) Ndivyo ilivyo leo, ujumbe wa habari njema huleta umoja kwa watu fulani, lakini kwa wengine huleta mgawanyiko. (Mt. 10:34-36) Ikiwa familia yenu imegawanyika kwa sababu ya habari njema, kumbuka kwamba mara nyingi upinzani hutokea kwa sababu ya uchongezi au uvumi usio na msingi. Mwenendo wako unaweza kubadili mtazamo wa wale wanaokupinga.​—1 Pet. 2:12; 3:1, 2.

8. Kwa nini Paulo na Barnaba waliondoka Ikoniamu, nasi tunaweza kujifunza nini?

8 Baada ya muda, wapinzani huko Ikoniamu wakapanga njama ya kuwapiga mawe Paulo na Barnaba. Wamishonari hao wawili walipopata habari, waliamua kwenda kuhubiri katika eneo lingine. (Mdo. 14:5-7) Leo, wahubiri wa Ufalme hutumia busara. Tunaposhambuliwa kwa maneno, sisi huendelea kuhubiri kwa ujasiri. (Flp. 1:7; 1 Pet. 3:13-15) Lakini tukiona kwamba kuna uwezekano wa kutendewa kwa jeuri, tunaepuka kufanya jambo la kipumbavu linaloweza kuhatarisha uhai wetu au wa waabudu wenzetu.​—Met. 22:3.

“Mgeuke . . . Mje kwa Mungu Aliye Hai” (Mdo. 14:8-19)

9, 10. Jiji la Listra lilikuwa wapi, na ni mambo gani tunayojua kuhusu wenyeji wake?

9 Paulo na Barnaba wakaelekea Listra, eneo la milki ya Roma lililokuwa kilomita 30 hivi kusini-magharibi mwa Ikoniamu. Jiji la Listra lilikuwa na uhusiano wa karibu sana na Antiokia ya Pisidia, lakini jiji hilo halikuwa na Wayahudi wengi maarufu. Ingawa wenyeji walizungumza Kigiriki, lugha yao ya asili ilikuwa Kilikaonia. Paulo na Barnaba walianza kuhubiri katika eneo la umma huenda kwa sababu jiji hilo halikuwa na sinagogi. Petro alimponya mtu aliyezaliwa kilema jijini Yerusalemu. Paulo pia alimponya mtu aliyezaliwa kilema jijini Listra. (Mdo. 14:8-10) Kwa sababu ya muujiza ambao Petro alifanya, umati mkubwa wa watu ukaamini. (Mdo. 3:1-10) Lakini muujiza ambao Paulo alifanya ulikuwa na matokeo tofauti kabisa.

10 Kama tulivyoona mwanzoni mwa sura hii, yule mtu aliyekuwa kilema aliporuka na kuanza kutembea, mara moja umati wa wapagani huko Listra ukafikiri kwamba wao ni miungu. Walimwita Barnaba Zeu, mkuu wa miungu, naye Paulo wakamwita Herme, mwana wa Zeu na msemaji wa miungu. (Ona sanduku lenye kichwa “ Jiji la Listra na Madhehebu ya Zeu na Herme.”) Hata hivyo, Barnaba na Paulo waliazimia kuusadikisha umati kwamba wanazungumza na kutenda kwa mamlaka ya Yehova, Mungu wa kweli, bali si kwa mamlaka ya miungu ya kipagani.​—Mdo. 14:11-14.

“Mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia.”—Matendo 14:15

11-13. (a) Paulo na Barnaba waliwaambia nini wenyeji wa Listra? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Paulo na Barnaba?

11 Licha ya mambo hayo yote, Paulo na Barnaba walijitahidi kufikia mioyo ya wasikilizaji wao kwa njia bora zaidi. Katika kisa hiki, Luka anaeleza njia yenye mafanikio iliyotumiwa kuwahubiria wapagani habari njema. Ona jinsi Paulo na Barnaba walivyowasihi wasikilizaji wao: “Wanaume, kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu kama wenu. Nasi tunawatangazia habari njema, ili mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo. Katika vizazi vilivyopita aliruhusu watu wa mataifa yote waendelee kutembea katika njia zao, ingawa hakujiacha bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno, akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.”​—Mdo. 14:15-17.

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno hayo yenye kuchochea? Kwanza, Paulo na Barnaba hawakujiona kuwa bora kuliko wasikilizaji wao. Hawakujifanya kuwa watu wenye uwezo wa pekee. Badala yake, walikubali kwamba walikuwa na udhaifu uleule kama wa wapagani waliowasikiliza. Ni kweli kwamba Paulo na Barnaba walikuwa wamepokea roho takatifu na kuwekwa huru kutokana na utumwa wa mafundisho ya uwongo. Pia, walikuwa na tumaini la pekee la kutawala pamoja na Kristo. Hata hivyo, walijua kwamba watu wa Listra wangeweza kupata zawadi hizohizo ikiwa wangemtii Kristo.

13 Tunawaonaje wale tunaowahubiria? Je, tunaona wako sawa na sisi? Tunapowasaidia wengine kujifunza kweli za Neno la Mungu, je, tunawaiga Paulo na Barnaba kwa kuepuka kujitafutia sifa? Charles Taze Russell, mwalimu stadi aliyeongoza kazi ya kuhubiri mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20, aliweka mfano mzuri. Aliandika: ‘Hatujitafutii sifa wala heshima kwa sababu ya habari tunazoandika; wala hatutaki kuitwa Viongozi au Marabi.’ Ndugu Russell alikuwa mnyenyekevu kama Paulo na Barnaba. Vivyo hivyo, tunapohubiri, kusudi letu ni kuwasaidia watu wamgeukie “Mungu aliye hai” si kujitafutia utukufu.

14-16. Ni masomo gani mengine tunayojifunza kutokana na mambo ambayo Paulo na Barnaba waliwaambia watu wa Listra?

14 Jambo la pili tunaloweza kujifunza kutokana na mazungumzo hayo ni; Paulo na Barnaba walibadilika kulingana na hali. Wayahudi na wageuzwa imani waliokuwa Ikoniamu walijua mengi kuhusu Maandiko au jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli, lakini watu wa Listra walijua mambo machache au hawakujua kabisa mambo hayo. Hata hivyo, wale waliowasikiliza Paulo na Barnaba walikuwa wakulima. Jiji la Listra lilikuwa na hali nzuri ya hewa na mashamba yenye rutuba. Watu hao wangeweza kuona uthibitisho wa kutosha wa sifa za Muumba kupitia mambo kama vile majira ya mavuno, na wamishonari hao walitumia jambo hilo kama msingi wa kuwahubiria.​—Rom. 1:19, 20.

15 Je, sisi pia tunaweza kubadilika kulingana na hali? Ingawa mkulima anaweza kupanda mbegu ileile katika mashamba tofauti, anahitaji kutumia mbinu tofauti za kuutayarisha udongo. Huenda udongo fulani ukawa laini na tayari kwa ajili ya kupanda mbegu, lakini udongo mwingine ukahitaji matayarisho zaidi. Vivyo hivyo, tunapanda mbegu ileile, yaani, ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu. Hata hivyo, kama Paulo na Barnaba, tutajitahidi kutambua hali na dini za watu tunaowahubiria. Jambo hilo litatusaidia kuwahubiria ujumbe wa Ufalme kulingana na hali zao.​—Luka 8:11, 15.

16 Tunaweza kujifunza jambo la tatu kutokana na masimulizi kuhusu Paulo, Barnaba, na watu wa Listra. Licha ya jitihada zetu, wakati mwingine mbegu tunazopanda zinanyakuliwa au kuanguka kwenye miamba. (Mt. 13:18-21) Jambo hilo likitokea, usikate tamaa. Kama Paulo alivyowakumbusha wanafunzi huko Roma, “kila mmoja wetu [kutia ndani kila mtu tunayezungumza naye Neno la Mungu] atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”​—Rom. 14:12.

“Wakawakabidhi kwa Yehova” (Mdo. 14:20-28)

17. Baada ya kuondoka Derbe, Paulo na Barnaba walienda wapi, na kwa nini?

17 Paulo alipoburutwa na kutolewa nje ya jiji la Listra akiwa mahututi, wanafunzi walimzunguka, akasimama, akaingia jijini na kukaa hapo usiku kucha. Siku iliyofuata, Paulo na Barnaba wakaanza safari ya kilomita 100 kwenda Derbe. Wazia maumivu makali ambayo Paulo alikuwa nayo wakati wa safari hiyo, kwani saa chache zilizopita alikuwa amepigwa mawe! Hata hivyo, yeye na Barnaba walivumilia, na walipofika Derbe, wakafanya “watu wengi kuwa wanafunzi.” Kisha, badala ya kwenda nyumbani kwao huko Antiokia ya Siria, “wakarudi Listra, Ikoniamu, na Antiokia [ya Pisidia].” Kwa nini? Ili kuwatia nguvu “wanafunzi na kuwatia moyo wabaki katika imani.” (Mdo. 14:20-22) Waliweka mfano mzuri sana! Walitanguliza mahitaji ya kutaniko badala ya starehe zao. Waangalizi wanaosafiri na wamishonari wa siku zetu wanaiga mfano wao.

18. Wanaume wazee huwekwa rasmi jinsi gani?

18 Zaidi ya kuwatia nguvu wanafunzi kwa maneno na mfano wao, Paulo na Barnaba waliwaweka rasmi “wazee kwa ajili yao katika kila kutaniko.” Ingawa Paulo na Barnaba ‘walitumwa na roho takatifu’ katika safari hiyo ya umishonari, walisali na kufunga, nao “wakawakabidhi [wazee hao] kwa Yehova.” (Mdo. 13:1-4; 14:23) Ndivyo ilivyo leo. Kabla ya mapendekezo, baraza la wazee husali na kuchanganua ili kutambua ikiwa ndugu anatimiza sifa za Kimaandiko. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9; Yak. 3:17, 18; 1 Pet. 5:2, 3) Jambo kuu si muda ambao amekuwa Mkristo. Badala yake, maneno na mwenendo wake unapaswa kuonyesha wazi kwamba roho takatifu inafanya kazi katika maisha yake. Mtu anastahili kutumikia akiwa mwangalizi ikiwa anatimiza sifa zilizo katika Maandiko. (Gal. 5:22, 23) Mwangalizi wa mzunguko huwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma.​—Linganisha 1 Timotheo 5:22.

19. Wazee wanawajibika kwa nani, na wanawaigaje Paulo na Barnaba?

19 Wazee waliowekwa rasmi wanajua kwamba wanawajibika mbele za Mungu. (Ebr. 13:17) Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, wazee wanaongoza katika kazi ya kuhubiri. Wanawatia nguvu Wakristo wenzao kwa maneno yao. Wanatanguliza faida za kutaniko badala ya starehe zao.​—Flp. 2:3, 4.

20. Tunanufaikaje tunaposoma ripoti kuhusu kazi ya uaminifu ya ndugu zetu?

20 Mwishowe Paulo na Barnaba waliporudi kwenye makao yao huko Antiokia ya Siria, walisimulia “mambo mengi ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao, na kwamba alikuwa amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.” (Mdo. 14:27) Tunaposoma kuhusu kazi ya uaminifu ya ndugu zetu Wakristo na jinsi ambavyo Yehova amebariki jitihada zao, tunatiwa moyo kuendelea ‘kuzungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova.’

a Ona sanduku lenye kichwa “ Ikoniamu—Jiji la Wafrigia.”