Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 14

“Tumefikia Kauli Moja”

“Tumefikia Kauli Moja”

Jinsi baraza linaloongoza lilivyofikia uamuzi na jinsi uamuzi huo ulivyoyaunganisha makutaniko

Matendo 15:13-35

1, 2. (a) Ni maswali gani mazito ambayo baraza linaloongoza la kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza linahitaji kuyashughulikia? (b) Ni nini kilichowasaidia ndugu hao kufanya uamuzi unaofaa?

 KIMYA kimetanda! Mitume na wazee waliokusanyika katika chumba kimoja jijini Yerusalemu watazamana, wakijua kwamba suala lililo mbele yao ni zito. Suala la tohara limetokeza maswali kadhaa mazito. Je, Wakristo wako chini ya Sheria ya Musa? Je, kunapaswa kuwa na tofauti yoyote kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo wa Mataifa?

2 Wanaume hao wanaoongoza wamesikia uthibitisho mbalimbali. Wanakumbuka unabii wa Neno la Mungu na mambo yaliyoonwa yenye kusadikisha, yanayoonyesha baraka za Yehova. Kila mmoja ameeleza waziwazi maoni yake na wana habari zote wanazohitaji ili kufanya uamuzi. Roho takatifu ya Yehova iko juu yao. Je, wanaume hao watakubali mwongozo wa roho hiyo?

3. Tunaweza kufaidikaje kwa kuchunguza masimulizi ya Matendo sura ya  15?

3 Ili kukubali mwongozo wa roho takatifu, wanaume hao wanahitaji kuwa na imani ya kweli na ujasiri. Huenda uamuzi wao ukazidisha chuki ya viongozi wa dini ya Kiyahudi. Isitoshe, wangekabili upinzani kutoka kwa watu fulani ndani ya kutaniko ambao waliazimia kuwalazimisha watu wa Mungu waendelee kuishika Sheria ya Musa. Baraza linaloongoza litafanya nini? Acheni tuone. Tunapochanganua habari hii, tutaona jinsi wanaume hao waaminifu walivyoweka mfano mzuri unaoweza kuigwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo. Ni mfano ambao sisi pia tunapaswa kuiga tunapohitaji kufanya uamuzi au tunapokabili hali fulani ngumu katika maisha yetu ya Kikristo.

“Maneno ya Manabii Yanaunga Mkono Jambo Hilo” (Mdo. 15:13-21)

4, 5. Yakobo alinukuu maneno gani ya manabii?

4 Mwanafunzi Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, akaanza kuzungumza. a Inaonekana alikuwa mwenyekiti katika mkutano huo. Huenda maneno yake yalikuwa muhtasari wa mambo waliyokubaliana wakiwa baraza. Yakobo akawaambia hivi wanaume waliokusanyika: “Simioni amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo.”​—Mdo. 15:14, 15.

5 Huenda baada ya kusikiliza hotuba ya Simioni, au Simoni Petro, na uthibitisho uliotolewa na Barnaba na Paulo, Yakobo alikumbuka maandiko kadhaa yaliyotaja jambo hilo muhimu lililozungumziwa. (Yoh. 14:26) Baada ya kusema “maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo,” Yakobo akanukuu maneno ya Amosi 9:11, 12. Kitabu hicho kiliorodheshwa kati ya Maandiko ya Kiebrania yanayoitwa “Manabii.” (Mt. 22:40; Mdo. 15:16-18) Utaona kwamba maneno yaliyonukuliwa na Yakobo yanatofautiana kidogo na yale yaliyo katika kitabu cha Amosi leo. Huenda Yakobo alinukuu Septuajinti, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania.

6. Maandiko yaliwasaidiaje akina ndugu kujua mapenzi ya Mungu?

6 Kupitia nabii Amosi, Yehova alitabiri kwamba angesimamisha “kibanda cha Daudi,” yaani, ukoo wa kifalme ambao hatimaye ungetokeza Ufalme wa Kimasihi. (Eze. 21:26, 27) Je, Yehova angeshughulika tena kwa njia ya pekee na Wayahudi wa asili? Hapana. Unabii huo unasema kwamba “watu wa mataifa yote” watakusanywa pamoja wakiwa “watu wanaoitwa kwa jina [la Mungu].” Kumbuka, Petro alitoa ushahidi kwamba Mungu “hakutofautisha hata kidogo kati yetu [Wakristo Wayahudi] na wao [Watu wa Mataifa walioamini], bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.” (Mdo. 15:9) Kwa hiyo, mapenzi ya Mungu ni kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa, wawe warithi wa Ufalme. (Rom. 8:17; Efe. 2:17-19) Hakuna unabii wowote ulioongozwa kwa roho unaoonyesha kwamba waamini wasio Wayahudi walipaswa kwanza kutahiriwa au kugeuzwa imani kabla ya kuwa warithi wa Ufalme.

7, 8. (a) Yakobo alipendekeza nini? (b) Yakobo alimaanisha nini aliposema “uamuzi wangu”?

7 Akichochewa na uthibitisho huo wa Maandiko na mambo yenye kusadikisha aliyosikia, Yakobo akapendekeza hivi: “Kwa hiyo uamuzi wangu ni kutowataabisha watu wa mataifa wanaomgeukia Mungu, bali kuwaandikia wajiepushe na vitu vilivyochafuliwa na sanamu, na uasherati, na vitu vilivyonyongwa, na damu. Kwa maana tangu nyakati za kale kuna watu ambao wamekuwa wakihubiri kumhusu Musa katika kila jiji, kwa sababu yeye husomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.”​—Mdo. 15:19-21.

8 Yakobo aliposema “kwa hiyo uamuzi wangu,” je, alikuwa akitumia mamlaka yake—labda kwa sababu alikuwa mwenyekiti wa mkutano huo—ili kuwalazimisha wale ndugu wengine wakubaliane na jambo analosema? Hapana! Katika Kigiriki, neno linalotafsiriwa “uamuzi wangu,” linaweza pia kumaanisha “nafikiria” au “maoni yangu ni.” Hivyo basi, Yakobo hakuwa akitoa uamuzi kwa niaba ya baraza zima, bali, baada ya kusikia ushahidi uliotolewa na Maandiko yaliyochunguzwa alipendekeza hatua inayoweza kuchukuliwa.

9. Pendekezo la Yakobo lilikuwa na manufaa gani?

9 Je, Yakobo alitoa pendekezo zuri? Bila shaka, kwa sababu baadaye mitume na wazee waliamua kufuata pendekezo hilo. Uamuzi huo ungetimiza nini? Kwa upande mmoja, ‘haungewataabisha’ Wakristo wasio Wayahudi kwa kuwalazimisha kufuata matakwa ya Sheria ya Musa. (Mdo. 15:19) Kwa upande mwingine, uamuzi huo ungeheshimu dhamiri za Wakristo Wayahudi, ambao kwa muda mrefu walisikia “Musa . . . [akisomwa] kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.” b (Mdo. 15:21) Kwa kweli pendekezo hilo lingeleta umoja kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa. Zaidi ya yote, lingempendeza Yehova Mungu kwa kuwa linapatana na kusudi lake. Hiyo ilikuwa njia nzuri ya kutatua tatizo lililohatarisha umoja na hali njema ya kutaniko zima la watu wa Mungu! Nao ni mfano mzuri kwa kutaniko la Kikristo leo!

Albert Schroeder akitoa hotuba katika kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1998

10. Baraza Linaloongoza leo, linafuata jinsi gani mfano uliowekwa na baraza linaloongoza la karne ya kwanza?

10 Kama tulivyoona katika Sura ya 13, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo hufuata mfano uliowekwa katika karne ya kwanza, kwa kumtegemea Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, na Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, ili kupata mwongozo katika mambo yote. c (1 Kor. 11:3) Wanafanyaje hivyo? Albert D. Schroeder, aliyetumikia katika Baraza Linaloongoza tangu mwaka wa 1974 hadi alipofikia mwisho wa maisha yake hapa duniani Machi 2006, alieleza: “Baraza Linaloongoza huanza mkutano wao wa Jumatano kwa sala ili kuomba mwongozo wa roho ya Yehova. Baraza Linaloongoza huhakikisha kwamba kila jambo linalozungumziwa na uamuzi unaofanywa unapatana na Neno la Mungu Biblia.” Naye Milton G. Henschel, aliyekuwa mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza ambaye alikufa Machi 2003 na kwenda mbinguni, aliwauliza swali lenye kuchochea fikira wahitimu wa darasa la 101 la Shule ya Gileadi. Aliwauliza, “Je, kuna tengenezo lingine duniani ambalo Baraza lake Linaloongoza hutumia ushauri kutoka katika Neno la Mungu, Biblia, kabla ya kufanya maamuzi muhimu?” Hakuna.

“Kuwatuma Wanaume Waliochaguliwa” (Mdo. 15:22-29)

11. Uamuzi wa baraza linaloongoza ulifikaje makutanikoni?

11 Baraza linaloongoza huko Yerusalemu, lilifanya uamuzi wa pamoja kuhusu suala la tohara. Hata hivyo, ili akina ndugu makutanikoni watende kwa umoja, walihitaji kujulishwa uamuzi huo kwa njia iliyo wazi na yenye kutia moyo. Ni njia gani iliyotumiwa? Masimulizi hayo yanaeleza: “Ndipo mitume na wazee, pamoja na kutaniko lote wakaamua kuwatuma wanaume waliochaguliwa kutoka miongoni mwao waende Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba; waliwatuma Yuda aliyeitwa Barsaba, na Sila, wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu.” Pia, wanaume waliotumwa walipewa barua ambayo ingesomwa katika makutaniko yote ya Antiokia, Siria, na Kilikia.​—Mdo. 15:22-26.

12, 13. Ni mambo gani mazuri yaliyotimizwa baada ya (a) Yuda na Sila kutumwa? (b) baraza linaloongoza kutuma barua?

12 Wakiwa “wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu,” Yuda na Sila, walistahili kuliwakilisha baraza linaloongoza. Wanaume wanne wangethibitisha kwamba habari waliyokuwa nayo haikuwa tu jibu la swali lililoulizwa bali ni maagizo ya baraza linaloongoza. Kuwepo kwa ‘wanaume hao waliochaguliwa’ kungesaidia kuleta umoja kati ya Wakristo Wayahudi waliokuwa Yerusalemu na Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa waliokuwa katika maeneo mengine. Huo ulikuwa mpango mzuri na wenye upendo. Bila shaka, ulichangia umoja na amani kati ya watu wa Mungu.

13 Barua hizo zilikuwa na maagizo yaliyokuwa wazi kwa ajili ya Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa kuhusu suala la tohara na mambo waliyopaswa kufanya ili kupata baraka na kibali cha Yehova. Sehemu muhimu ya barua hiyo ilisema: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumeona ni vizuri tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi ila mambo haya ya lazima: kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu, na damu, na vitu vilivyonyongwa, na uasherati. Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa. Afya njema kwenu!”​—Mdo. 15:28, 29.

14. Inawezekanaje kwa watu wa Yehova kufanya kazi kwa umoja katika ulimwengu huu uliogawanyika?

14 Leo, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 8,000,000, katika makutaniko zaidi ya 100,000 ulimwenguni pote, wanaamini na kutenda kwa umoja. Kwa kuwa ulimwengu wa leo umejaa misukosuko na migawanyiko, inawezekanaje kuwa na umoja huo? Kwanza kabisa, umoja huo unatokana na mwongozo ulio wazi ambao Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, anatoa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” yaani, Baraza Linaloongoza. (Mt. 24:45-47) Umoja huo pia unawezekana kwa sababu ndugu ulimwenguni pote hufuata kwa hiari mwongozo wa Baraza Linaloongoza.

“Wakashangilia kwa Sababu ya Kutiwa Moyo” (Mdo. 15:30-35)

15, 16. Suala la tohara lilitatuliwaje, na kwa nini uamuzi uliofikiwa ulikuwa na matokeo mazuri?

15 Kitabu cha Matendo kinaendelea kusema kwamba ndugu hao waliotumwa kutoka Yerusalemu walipofika Antiokia, “wakakusanya kundi lote pamoja na kuwapa barua hiyo.” Akina ndugu waliitikiaje mwongozo huo wa baraza linaloongoza? “Baada ya kuisoma[barua hiyo], wakashangilia kwa sababu ya kutiwa moyo.” (Mdo. 15:30, 31) Isitoshe, Yuda na Sila “wakawatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwaimarisha.” Wanaume hao wawili walikuwa “manabii,” kama vile Barnaba, Paulo na wengine walioitwa manabii—walipewa jina hilo kwa sababu walikuwa wakitangaza au kujulisha mapenzi ya Mungu.​—Mdo. 13:1; 15:32; Kut. 7:1, 2.

16 Ilionekana wazi kwamba Yehova alibariki uamuzi wa baraza linaloongoza na hivyo suala hilo likatatuliwa vizuri. Kwa nini matokeo yalikuwa mazuri? Kwa sababu ya mwongozo ulio wazi na unaotegemea Neno la Mungu na roho takatifu uliotolewa na baraza linaloongoza kwa wakati unaofaa. Sababu nyingine ni kwamba makutaniko yalijulishwa moja kwa moja na kwa upendo kuhusu uamuzi huo.

17. Waangalizi wa mzunguko leo hufuata mfano gani?

17 Leo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hufuata mfano huo kwa kuwapa ndugu ulimwenguni pote mwongozo kwa wakati unaofaa. Uamuzi fulani unapofanywa, makutaniko hujulishwa moja kwa moja na kwa njia inayoeleweka wazi. Njia moja ni kupitia ziara za waangalizi wa mzunguko. Ndugu hao wanaojitolea kwa moyo wote, hutembelea makutaniko wakiyatia moyo na kutoa mwelekezo. Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, wao pia hutumia wakati mwingi “wakifundisha na kutangaza habari njema ya neno la Yehova, wakiwa pamoja na wengine wengi.” (Mdo. 15:35) Kama Yuda na Sila, wanawaimarisha akina ndugu na kuwatia ‘moyo kwa hotuba nyingi.’

18. Watu wa Yehova wanawezaje kuendelea kupokea baraka zake?

18 Kwa upande mwingine, ni nini kitakachoyawezesha makutaniko ulimwenguni pote kuendelea kuwa na amani na umoja katika ulimwengu uliogawanyika leo? Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi baadaye: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii . . . Zaidi ya hayo, tunda la uadilifu hupandwa katika hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yak. 3:17, 18) Hatujui ikiwa kilichomchochea kuandika hivyo ni ule mkutano wa Yerusalemu au la. Hata hivyo, matukio yanayozungumziwa katika Matendo sura ya 15 yanaonyesha wazi kwamba Yehova hubariki roho ya umoja na ushirikiano.

19, 20. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba kulikuwa na amani na umoja katika kutaniko la Antiokia? (b) Paulo na Barnaba wangeweza kufanya nini sasa?

19 Ni wazi kwamba kulikuwa na amani na umoja katika kutaniko la Antiokia. Badala ya kubishana na ndugu waliotumwa kutoka Yerusalemu, akina ndugu wa Antiokia walithamini sana kutembelewa na Yuda na Sila. Ndugu wa Antiokia hawakuwaruhusu waondoke. Hata hivyo, “baada ya kukaa huko kwa muda fulani, ndugu hao wakawaacha warudi kwa amani kwa wale waliokuwa wamewatuma,” yaani, warudi Yerusalemu. d (Mdo. 15:33) Bila shaka, ndugu waliokuwa Yerusalemu walifurahi pia walipowasikia Yuda na Sila wakisimulia matokeo ya safari yao. Fadhili zisizostahiliwa za Yehova ziliwawezesha kuutimiza mgawo wao!

20 Paulo na Barnaba, ambao walibaki Antiokia, wangeweza sasa kukazia fikira kazi ya kuhubiri kama vile waangalizi wa mzunguko wanavyofanya wanapotembelea makutaniko. (Mdo. 13:2, 3) Ndugu hao ni baraka kubwa sana! Hata hivyo, Yehova aliwatumia waeneza-injili hao wawili wenye bidii kutimiza mambo gani zaidi? Tutaona katika sura inayofuata.

Leo, Wakristo hufaidika kutokana na maagizo kutoka kwa Baraza Linaloongoza na wawakilishi wake

a Ona sanduku lenye kichwa “ Yakobo—‘Ndugu ya Bwana.’”

b Yakobo alirejelea kwa busara maandishi ya Musa ambayo zaidi ya kuwa na Sheria, yalitia ndani masimulizi ya jinsi Mungu alivyoshughulika na watu wake na maoni yake kabla ya Sheria kutolewa. Kwa mfano, maoni ya Mungu kuhusu damu, uzinzi, na ibada ya sanamu yanaonekana wazi katika kitabu cha Mwanzo. (Mwa. 9:3, 4; 20:2-9; 35:2, 4) Hivyo, Yehova alionyesha kanuni zinazowahusu wanadamu wote iwe ni Wayahudi au Watu wa Mataifa.

c Ona sanduku lenye kichwa “ Jinsi Baraza Linaloongoza Lilivyopangwa Leo.”

d Katika mstari wa 34, tafsiri fulani za Biblia husema kwamba Sila aliamua kubaki Antiokia. (Union Version) Hata hivyo, inaonekana kwamba maneno hayo yaliongezwa baadaye.