Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Mhubiri Mpendwa:

Wazia kwamba wewe ni mmoja wa mitume ambao wamesimama kwenye Mlima wa Mizeituni. Yesu anatokea mbele yako. Kabla tu ya kurudi mbinguni, anasema hivi: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Ungefanya nini?

Huenda ungeona huo kuwa mgawo mkubwa usioweza kuutimiza. Huenda ukauliza, ‘Sisi—tukiwa kikundi kidogo tu cha wanafunzi—tunawezaje kutoa ushahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia”?’ Huenda ukakumbuka onyo ambalo Yesu alitoa kabla ya kufa: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia; ikiwa wamelishika neno langu, watalishika lenu pia. Lakini watawatendea mambo yote haya kwa ajili ya jina langu, kwa sababu hawamjui Yule aliyenituma.” (Yoh. 15:20, 21) Ukitafakari maneno hayo, huenda ukajiuliza, ‘Ninawezaje kutoa ushahidi kamili huku nikipingwa na kuteswa?’

Leo, tuko katika hali kama hiyo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna wajibu wa kutoa ushahidi kamili “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia,” kwa “watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:19, 20) Tunawezaje kutimiza kazi hiyo licha ya upinzani kutoka kwa watu?

Kitabu cha Matendo ya Mitume kina masimulizi yenye kusisimua kuhusu jinsi mitume na Wakristo wenzao katika karne ya kwanza, walivyotegemezwa na Yehova kutimiza mgawo wao. Kitabu unachosoma kimekusudiwa kukusaidia kuchanganua rekodi hiyo na kuwazia akilini mfululizo wa matukio yaliyo katika kitabu hicho cha Biblia. Utashangaa kuona jinsi hali nyingi za watumishi wa Mungu katika karne ya kwanza zinavyofanana na hali za watumishi wake leo. Utaona kwamba ulinganifu huo hauhusu tu kazi tunayofanya, bali pia jinsi tunavyoifanya. Kutafakari mambo hayo kutaimarisha imani yako kwamba Yehova Mungu anaendelea kuongoza sehemu ya kidunia ya tengenezo lake.

Tunatumaini na kusali kwamba kuchunguza kitabu cha Matendo kutakuhakikishia kwamba Yehova atakusaidia na nguvu za roho yake takatifu zitakutegemeza. Hivyo, azimia kuendelea “kutoa ushahidi kamili” kuhusu Ufalme wa Mungu na kuwasaidia wengine waipate njia ya wokovu.​—Mdo. 28:23; 1 Tim. 4:16.

Ndugu zako,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova