Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uichunguze Biblia?

Kwa Nini Uichunguze Biblia?

Je, wewe unaifahamu Biblia? Hakuna kitabu kingine chochote katika historia ambacho kimesambazwa sana kama Biblia. Ujumbe wake umewafariji na kuwapa tumaini watu wa tamaduni zote, nao wamefaidika na mashauri yake maishani. Hata hivyo, watu wengi leo hawaijui Biblia vizuri. Iwe wewe ni mfuasi wa dini fulani au sivyo, huenda kuna mambo fulani ambayo ungependa kujua kuhusu Biblia. Broshua hii imekusudiwa kukusaidia kupata picha ya ujumla kuhusu Biblia.

KABLA ya kuchukua Biblia na kuanza kuisoma, ingefaa kujua mpangilio wake. Biblia, ambayo pia huitwa Maandiko Matakatifu, ni mkusanyo wa vitabu au sehemu 66, kuanzia Mwanzo mpaka Ufunuo.

Biblia ilitungwa na nani? Hilo ni swali ambalo limewasumbua watu wengi. Ukweli ni kwamba Maandiko hayo yaliandikwa na wanaume wapatao 40 katika kipindi cha miaka 1,600 hivi. Hata hivyo, wanaume hao hawakudai kamwe kuwa watungaji wa Biblia. Mmoja wao aliandika: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Mwandikaji mwingine alisema: “Roho ya Yehova ndiyo iliyosema kupitia mimi, na neno lake lilikuwa kwenye ulimi wangu.” (2 Samweli 23:2) Kulingana na waandikaji hao, Yehova Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia naye anataka kuwa na uhusiano wa karibu na wanadamu.

Kuna jambo lingine muhimu linalohitajika ili kuielewa Biblia. Biblia ina ujumbe mmoja wa msingi: kutetewa kwa haki ya Mungu ya kuwatawala wanadamu kupitia Ufalme wa mbinguni. Katika broshua hii, utaona jinsi ujumbe huo unavyojitokeza kuanzia kitabu cha Mwanzo mpaka Ufunuo.

Ukiwa na hayo akilini, sasa chunguza ujumbe ulio katika kitabu maarufu zaidi ulimwenguni, Biblia.

^ fu. 9 Kuna njia mbalimbali za kutaja tarehe. Katika broshua hii, herufi W.K. zinamaanisha “Wakati wa Kawaida” na K.W.K. zinamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.” Herufi hizo zinatumiwa katika chati iliyo sehemu ya chini ya kurasa.