Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 1

Muumba Ampa Mwanadamu Paradiso

Muumba Ampa Mwanadamu Paradiso

Mungu aumba ulimwengu na viumbe; aumba mwanamume na mwanamke wakamilifu, awaweka katika bustani nzuri, na kuwapa amri wanazopaswa kutii

“HAPO mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Maneno hayo yamesemwa kuwa maneno maarufu zaidi ya ufunguzi ambayo yamepata kuandikwa. Katika maneno hayo rahisi lakini yenye kujaa maana, Biblia inamtambulisha mhusika mkuu wa Maandiko Matakatifu—Mungu mweza-yote, Yehova. Mstari huo wa kwanza wa Biblia unafunua kwamba Mungu ndiye Muumba wa ulimwengu wote kutia ndani dunia yetu. Mistari inayofuata inaeleza kwamba katika vipindi virefu vya wakati, vinavyoitwa siku, Mungu alitayarisha makao yetu hapa duniani, akitokeza vitu vyote vya ajabu vilivyo katika ulimwengu.

Mwanadamu ndiye kiumbe kikuu zaidi duniani alichoumba Mungu. Aliumbwa katika mfano wa Mungu—akiwa na uwezo wa kuonyesha sifa za Yehova mwenyewe, kama vile upendo na hekima. Mungu alimuumba mwanadamu kutoka katika mavumbi ya dunia, na kumwita Adamu. Kisha, akamweka katika paradiso—bustani ya Edeni. Mungu mwenyewe ndiye aliyetayarisha bustani hiyo na kuweka miti yenye kupendeza ya matunda.

Mungu aliona kwamba mwanamume huyo anahitaji mwenzi. Akitumia ubavu wa Adamu, Mungu alimfanyiza mwanamke na kumleta kwa mwanamume huyo ili awe mke wake. Mwanamke huyo aliitwa Hawa. Akiwa na shangwe kubwa, Adamu akasema kishairi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” Mungu akaeleza: “Ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”—Mwanzo 2:22-24; 3:20.

Mungu aliwapa Adamu na Hawa amri mbili. Kwanza, aliwaagiza walime na kutunza makao yao ya kidunia na hatimaye kuijaza dunia. Pili, aliwaambia wasile tunda la mti mmoja tu katika bustani yote hiyo, “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:17) Ikiwa wangekosa kutii, wangekufa. Kupitia amri hizo, Mungu alimpa mwanamume na mwanamke huyo njia ya kuonyesha kwamba wanamkubali kuwa Mtawala wao. Pia, kutii kwao kungeonyesha upendo na shukrani zao. Hawakuwa na sababu yoyote ya kuukataa utawala wake wenye fadhili. Wanadamu hao wakamilifu hawakuwa na kasoro yoyote. Biblia inatuambia: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.”—Mwanzo 1:31.

—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 1 na 2.