Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 11

Nyimbo zilizoongozwa na roho ambazo zinafariji na kufundisha

Nyimbo zilizoongozwa na roho ambazo zinafariji na kufundisha

Daudi na wengine watunga nyimbo kwa ajili ya ibada. Kitabu cha Zaburi kina nyimbo 150

KITABU kikubwa zaidi katika Biblia ni mkusanyo wa nyimbo takatifu. Kitabu hicho kilichukua miaka 1,000 hivi kuandikwa. Kitabu cha Zaburi kina maneno yenye kupendeza na yenye kuchochea sana ya imani kuliko kitabu kingine chochote. Nyimbo hizo za sifa zinafunua hisia mbalimbali za wanadamu, kama vile, shangwe, shukrani, huzuni, sikitiko, na toba. Ni wazi kwamba mtunga-zaburi alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu naye alimtumaini. Fikiria baadhi ya mambo yaliyo katika nyimbo hizo.

Yehova ana haki ya kutawala, kuabudiwa na kusifiwa. Katika Zaburi 83:18 tunasoma: “Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Zaburi nyingi zinamsifu Yehova kwa kazi zake za uumbaji, kama vile mbingu zenye nyota, viumbe vya ajabu duniani, na jinsi mwanadamu alivyoumbwa kwa njia ya ajabu. (Zaburi 8, 19, 139, 148) Zaburi nyingine humtukuza Yehova kuwa Mungu ambaye huwawaokoa na kuwalinda washikamanifu wake. (Zaburi 18, 97, 138) Na katika zaburi nyingine anatajwa kuwa Mungu mwenye haki, anayewafariji walioonewa na kuwaadhibu waovu. —Zaburi 11, 68, 146.

Yehova huwasaidia na kuwafariji wanaompenda. Huenda zaburi inayojulikana sana ni ya 23. Katika zaburi hiyo, Daudi anamtaja Yehova kuwa Mchungaji mwenye upendo anayewaongoza, kuwalinda, na kuwajali kondoo wake. Zaburi 65:2 inawakumbusha waabudu wa Mungu kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala.” Wengi ambao wametenda dhambi nzito wamefarijiwa sana na Zaburi ya 39 na ya 51. Katika zaburi hizo, Daudi anatubu kwa unyoofu dhambi nzito alizofanya nayo maneno yake yanaonyesha wazi anaamini kwamba Yehova husamehe. Zaburi 55:22 inatuhimiza tumtegemee Yehova na kumtupia mizigo yetu yote.

Yehova ataubadili ulimwengu kupitia Ufalme wa Masihi. Sehemu mbalimbali za kitabu cha Zaburi zinamhusu moja kwa moja Masihi, Mfalme aliyeahidiwa. Zaburi ya 2 inatabiri kwamba Mtawala huyo ataharibu mataifa maovu yanayompinga. Zaburi ya 72 inaonyesha kwamba Mfalme huyo ataondoa njaa, ukosefu wa haki, na uonevu. Kulingana na Zaburi 46:9, Mungu atakomesha vita na kuharibu silaha zote za vita kupitia Ufalme wa Kimasihi. Katika Zaburi ya 37, tunasoma kwamba waovu wataharibiwa, lakini waadilifu wataishi milele duniani, wakifurahia amani na upatano.

—Inatoka kwenye Kitabu cha Zaburi.