Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 15

Nabii Aliye Uhamishoni Apata Maono ya Wakati Ujao

Nabii Aliye Uhamishoni Apata Maono ya Wakati Ujao

Danieli atabiri kuhusu Ufalme wa Mungu na Masihi atakayekuja. Ufalme wa Babiloni waanguka

DANIELI, kijana mwenye utimilifu wa pekee, alipelekwa uhamishoni Babiloni kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. Yeye na Wayahudi wengine—waliohamishwa kutoka katika ufalme ulioshindwa wa Yuda—walipewa kiasi fulani cha uhuru na wale waliowateka. Kwa muda mrefu aliokuwa Babiloni, Danieli alibarikiwa sana na Mungu, hata akaponyoka kifo katika shimo la simba na kupokea maono yaliyomwezesha kuona wakati ujao ulio mbali. Unabii muhimu zaidi wa Danieli ulikazia Masihi na utawala Wake.

Danieli apata kujua Masihi atafika wakati gani. Danieli aliambiwa wakati ambapo watu wa Mungu wangeweza kutazamia “Masihi Kiongozi” afike—Majuma 69 ya miaka baada ya amri ya kujengwa upya kuta za Yerusalemu kutolewa. Juma la kawaida lina siku saba; juma la miaka ni miaka saba. Amri hiyo ilitolewa muda mrefu baada ya wakati wa Danieli, yaani, mwaka wa 455 K.W.K. “Majuma” hayo 69 yalianza wakati huo na kuendelea kwa muda wa miaka 483, hadi mwaka wa 29 W.K. Katika sehemu inayofuata ya broshua hii, tutaona kilichotokea mwaka huo. Danieli aliona kimbele kwamba Masihi “angekatiliwa mbali,” au kuuawa, ili kufanya upatanisho wa dhambi.—Danieli 9:24-26.

Masihi angekuwa Mfalme mbinguni. Katika maono yasiyo ya kawaida ya mbingu zenyewe, Danieli alimwona Masihi, akirejelewa kuwa “mtu fulani kama mwana wa binadamu,” akikaribia kiti cha ufalme cha Yehova mwenyewe. Yehova alimkabidhi “utawala na heshima na ufalme.” Ufalme huo ungedumu milele. Danieli alipata kujua jambo lingine lenye kusisimua kuhusu Ufalme wa Kimasihi—Mfalme huyo angetawala pamoja na wengine, kikundi kinachoitwa “watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi.”—Danieli 7:13, 14, 27.

Ufalme utaharibu serikali za ulimwengu huu. Mungu alimpa Danieli uwezo wa kufasiri ndoto ambayo ilimkanganya Nebukadneza, mfalme wa Babiloni. Mfalme huyo aliona sanamu kubwa yenye kichwa cha dhahabu, kifua na mikono ya fedha, tumbo na mapaja ya shaba, miguu ya chuma, na nyayo za mchanganyiko wa chuma na udongo. Jiwe lililokatwa kutoka katika mlima lilipiga nyayo dhaifu za sanamu hiyo na kuivunjavunja. Danieli alieleza kwamba sehemu mbalimbali za sanamu hiyo ziliwakilisha mfuatano wa serikali mbalimbali za ulimwengu, kuanzia Babiloni iliyowakilishwa na kile kichwa cha dhahabu. Danieli aliona kimbele kwamba wakati wa utawala wa serikali ya mwisho ya ulimwengu huu mwovu, Ufalme wa Mungu ungechukua hatua. Ungezivunja-vunja serikali zote za ulimwengu huu. Kisha utawale milele.—Danieli, sura ya 2.

Akiwa mzee sana, Danieli alijionea kuanguka kwa Babiloni. Mfalme Koreshi alilipindua jiji hilo kama manabii walivyotabiri. Punde baadaye, Wayahudi wakaachiliwa huru kutoka uhamishoni—wakati barabara ulioahidiwa, baada ya ile miaka 70 ya ukiwa wa nchi yao. Wakiongozwa na magavana, makuhani, na manabii waaminifu, Wayahudi walijenga upya Yerusalemu na kulirekebisha hekalu la Yehova. Hata hivyo, ni nini ambacho kingetokea baada ya ile miaka 483 kumalizika?

—Inatoka kwenye Kitabu cha Danieli.