Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 18

Yesu Afanya Miujiza

Yesu Afanya Miujiza

Yesu, kupitia miujiza aliyofanya, alionyesha jinsi atakavyotumia nguvu zake akiwa Mfalme

MUNGU alimwezesha Yesu kufanya mambo ambayo wanadamu wengine hawangeweza kufanya. Yesu alifanya miujiza mingi—mara nyingi mbele ya watazamaji wengi. Miujiza hiyo ilionyesha kwamba Yesu ana nguvu kuliko adui zake na pia kuliko vizuizi vingine ambavyo wanadamu wasio wakamilifu hawangeweza kamwe kushinda kwa mafanikio. Fikiria mifano kadhaa.

Njaa. Muujiza wa kwanza wa Yesu ulikuwa kubadili maji yawe divai. Katika pindi nyingine mbili, alilisha maelfu ya watu kwa mikate na samaki wachache. Pindi zote hizo kulikuwa na chakula cha kumtosha kila mtu na hata kubaki.

Ugonjwa. Yesu aliwaponya watu “kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu.” (Mathayo 4:23) Aliwaponya vipofu, viziwi, wenye ukoma, wenye kifafa, vilema, viwete, na wasiojiweza. Hakuna ugonjwa uliomshinda.

Dhoruba kali. Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri katika Bahari ya Galilaya, dhoruba kali ilizuka. Wanafunzi waliogopa sana. Yesu aliitazama dhoruba hiyo na kusema: “Nyamaza, utulie!” Nayo dhoruba hiyo ikatulia. (Marko 4:37-39) Pindi nyingine, alitembea juu ya maji kulipokuwa na dhoruba yenye kuogopesha.—Mathayo 14:24-33.

Roho waovu. Roho waovu wana nguvu kuliko wanadamu. Watu wengi wameshindwa kujitoa katika mtego wa adui hao hatari wa Mungu. Hata hivyo, tena na tena, Yesu alipowaamuru watoke watu, roho hao hawangeweza tena kuendelea kuwasumbua. Hakuwaogopa. Badala yake, walitambua mamlaka yake nao walimwogopa.

Kifo. Kifo ni adui ambaye hakuna mwanadamu anaweza kumshinda. Ndiyo sababu kinaitwa “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Hata hivyo, Yesu aliwafufua wafu. Alimfufua kijana wa mjane na binti ya wazazi waliokuwa na huzuni. Katika kisa cha pekee, Yesu alimfufua rafiki yake mpendwa, Lazaro, mbele ya umati wa waombolezaji, ijapokuwa alikuwa mfu kwa karibu siku nne! Hata adui za Yesu walikiri kwamba alifanya muujiza huo.—Yohana 11:38-48; 12:9-11.

Kwa kuwa wote waliosaidiwa na Yesu hatimaye walikufa, kwa nini alifanya miujiza yote hiyo? Miujiza ya Yesu ilitimiza mambo mazuri yenye kudumu. Ilithibitisha kwamba unabii wote wenye kupendeza kuhusu utawala wa Mfalme wa Kimasihi una msingi. Hakuna haja ya kuwa na shaka kwamba Mfalme aliyewekwa na Mungu hawezi kuondolea mbali njaa, magonjwa, hali hatari ya hewa, roho waovu, au kifo chenyewe. Tayari amethibitisha kwamba Mungu amemkabidhi nguvu za kufanya hivyo.

—Inatoka kwenye Kitabu cha Mathayo, Marko, Luka na Yohana.