Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuzungumza Jinsi Gani na Wazazi Wangu?

Ninaweza Kuzungumza Jinsi Gani na Wazazi Wangu?

SURA YA 1

Ninaweza Kuzungumza Jinsi Gani na Wazazi Wangu?

“Nilijaribu sana kuwaambia wazazi wangu ninavyohisi, lakini hawakunielewa, nao wakanikatiza nikizungumza. Haikuwa rahisi kuwafunulia hisia zangu, nao hata hawakutaka kunisikiliza!”—Rosa.

ULIPOKUWA na umri mdogo, huenda ulikuwa na uhuru wa kuzungumza na wazazi. Uliwaambia kila kitu. Ulisema maoni yako waziwazi na kwa uhuru nawe ulifuata mashauri waliyokupa.

Lakini sasa huenda unaona kwamba wazazi wako hawakuelewi hata kidogo. “Siku moja, tukiwa mezani, nilianza kuwaeleza wazazi wangu jambo fulani lililokuwa likinisumbua huku nikitokwa machozi,” asema msichana mmoja anayeitwa Edie. “Ijapokuwa walinisikiliza, hawakunielewa.” Ikawaje? “Nilienda kitandani na kuendelea kulia!”

Kwa upande mwingine, huenda nyakati nyingine ukaamua kutowafunulia wazazi wako hisia zako. “Mimi huzungumza na wazazi wangu kuhusu mambo mengi,” asema Christopher. “Lakini nyakati nyingine sitaki wajue kila kitu.”

Ni vibaya kutofunua mambo fulani yanayokuhusu? Si vibaya, ikiwa hutendi kwa hila. (Methali 3:32) Hata hivyo, iwe kwamba wazazi wako hawakuelewi ama huwaelezi mambo waziwazi, ukweli ni kwamba: Unahitaji kuzungumza na wazazi wako, nao wanahitaji kukusikiliza.

Usivunjike Moyo!

Kwa njia fulani, kupashana habari na wazazi wako ni kama kuendesha gari. Unapokuta kizuizi barabarani, huvunji safari yako; badala yake, unatafuta njia nyingine. Fikiria mifano miwili.

KIZUIZI CHA 1 Unahitaji kuzungumza, lakini ni kana kwamba wazazi wako hawakusikilizi. “Naona vigumu kuzungumza na baba yangu,” asema msichana anayeitwa Leah. “Nyakati nyingine ninaweza kuzungumza naye kwa muda kisha anasema, ‘Samahani, ulikuwa unazungumza na mimi?’”

SWALI: Vipi ikiwa kwa kweli Leah anahitaji kuzungumzia tatizo fulani? Anaweza kutumia angalau njia tatu.

Njia A

Kumfokea baba yake. Leah anasema kwa hasira: “Nakwambia jambo muhimu! Sikiliza!”

Njia B

Kuacha kabisa kuzungumza na baba yake. Leah anaacha kabisa kuzungumzia matatizo yake.

Njia C

Kungoja hadi wakati mwingine unaofaa na kujaribu tena kuzungumzia tatizo lake. Leah anazungumza na baba yake uso kwa uso baadaye, au anamwandikia barua akimweleza tatizo lake.

Unafikiri Leah anapaswa kutumia njia gani? ․․․․․

Acheni tuchunguze kila moja ya njia hizo tuone matokeo ambayo zinaweza kuwa nayo.

Akili ya baba ya Leah iko mbali, naye hatambui kwamba Leah amevunjika moyo. Kwa hiyo, ikiwa Leah atachagua Njia A, huenda baba yake akaona kwamba anafoka bila sababu. Huenda njia hiyo isimfanye baba yake amsikilize, wala haitaonyesha kwamba Leah anamheshimu. (Waefeso 6:2) Hivyo basi, kwa kweli njia hiyo haitakuwa na matokeo mazuri.

Huenda Njia B ikaonekana kuwa rahisi kati ya zote, hata hivyo, siyo njia bora. Kwa nini? Kwa sababu “mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Methali 15:22) Ili kutatua matatizo yake inavyofaa, Leah anahitaji kuzungumza na baba yake, na ili amsaidie, anahitaji kuelewa mambo ambayo Leah anapambana nayo maishani. Kukataa kuzungumza hakutimizi lolote.

Hata hivyo, akitumia Njia C, Leah haruhusu kizuizi kimfungie njia. Badala yake, anajaribu kuzungumzia jambo hilo wakati mwingine. Na akiamua kumwandikia baba yake barua, huenda Leah akatulia mara moja. Pia, kuandika barua kunaweza kumsaidia achague maneno yanayofaa anayotaka kumwambia baba yake. Atakaposoma barua hiyo, baba ya Leah ataelewa kile ambacho Leah alikuwa anajaribu kumwambia na hilo litamsaidia kuelewa vizuri zaidi matatizo ya Leah. Hivyo basi, Njia C itakuwa na manufaa kwa Leah na baba yake pia.

Leah anaweza kutumia njia gani nyingine? Jaribu kufikiria njia moja nawe uiandike hapa chini. Kisha, andika matokeo ambayo njia hiyo inaweza kuwa nayo.

․․․․․

KIZUIZI CHA 2 Wazazi wako wanataka kuzungumza, lakini wewe hutaki. “Hakuna kitu kinachoudhi kama kuulizwa maswali mengi baada ya kutoka shuleni ukiwa umechoka,” asema msichana anayeitwa Sarah. “Ninachotaka hasa ni kusahau kabisa mambo yaliyotokea shuleni, lakini hata kabla sijapumzika wazazi wangu wanaanza kuniuliza: ‘Umeshindaje? Ulipata matatizo yoyote?’” Wazazi wa Sarah wanauliza maswali hayo kwa kuwa wanamjali. Hata hivyo, ananung’unika, “Ni vigumu kuzungumza kuhusu shule nikiwa nimechoka akili na mwili.”

SWALI: Sarah anaweza kufanya nini katika hali hiyo? Sawa na kisa kilichotangulia, ana angalau njia tatu.

Njia A

Kukataa kuzungumza. Sarah anasema: “Tafadhali, niacheni. Sitaki kuzungumza sasa hivi!”

Njia B

Kuzungumza. Ingawa anaona kwamba anasumbuliwa, Sarah anajibu maswali ya wazazi wake akinung’unika.

Njia C

Kuacha kuzungumzia mambo ya shule mpaka wakati mwingine, lakini aendeleze mazungumzo kuhusu mambo mengine. Sarah anapendekeza wazungumzie mambo ya shule wakati mwingine, atakapokuwa ametulia. Kisha anasema hivi kwa unyoofu: “Na wewe je? Umeshindaje leo?”

Unafikiri Sarah anapaswa kutumia njia gani? ․․․․․

Acheni tuchunguze tena kila moja ya njia hizo na kuona matokeo yanaweza kuwa nini.

Sarah amechoka akili naye hataki kuzungumza. Akichagua kutumia Njia A, hali yake haitabadilika, lakini pia atajiona kuwa na hatia kwa kuwafokea wazazi wake.​—Methali 29:11.

Isitoshe, wazazi wake hawatafurahishwa na kufoka kwa Sarah, wala kimya kitakachofuata. Huenda wakafikiri kwamba Sarah anawaficha jambo fulani. Huenda hata wakajaribu kumlazimisha azungumze, na bila shaka, hilo litamvunja moyo Sarah hata zaidi. Mwishowe, njia hiyo haitafanikiwa.

Bila shaka Njia B ni afadhali kuliko Njia A. Angalau Sarah na wazazi wake wanazungumza. Lakini kwa kuwa mazungumzo yao hayatoki moyoni, wala Sarah wala wazazi wake hawatapata kile wanachotaka, yaani, mazungumzo yaliyo wazi na huru.

Hata hivyo, akitumia Njia C, Sarah atatulia kwa kuwa mazungumzo kuhusu shule yameachwa kwa sasa. Wazazi wake watafurahi na kuthamini jitihada zake za kutaka kuzungumza nao. Inaelekea njia hiyo itakuwa na matokeo mazuri zaidi kwa kuwa wote wanatumia kanuni inayopatikana kwenye Wafilipi 2:4, inayosema: ‘Mtu asitafute faida yake mwenyewe tu bali faida ya mwenzake.’—Biblia Habari Njema.

Epuka Kuwachanganya Wazazi Wako

Kumbuka, nyakati nyingine maneno unayosema na ujumbe ambao wazazi wako wanapata hutofautiana. Kwa mfano, wazazi wako wanakuuliza kwa nini unaonekana huna furaha. Unawajibu, “Sitaki kuzungumzia hilo.” Hata hivyo, ujumbe wanaopata wazazi wako ni: “Siwaamini, na kwa hiyo siwezi kuwaambia. Afadhali nizungumze na rafiki zangu kuhusu tatizo hili lakini si ninyi.” Jaribu zoezi lifuatalo kwa kuandika majibu yako. Wazia kwamba una tatizo zito, na mzazi wako anataka kukusaidia.

Ukisema: “Usijali. Nitajua la kufanya.” ․․․․․

Huenda ujumbe wanaopata wazazi wako ni:․․․․․․

Jambo ambalo lingekuwa afadhali ni:․․․․․․

Jambo kuu ni nini? Chagua maneno yako kwa uangalifu. Yaseme kwa sauti inayoonyesha heshima. (Wakolosai 4:6) Waone wazazi wako kuwa marafiki wala si maadui. Na kwa kweli: Ili kupambana inavyofaa na matatizo unahitaji marafiki.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Namna gani ikiwa tatizo si kuzungumza na wazazi, bali kwamba kila mara mnapozungumza ubishi unatokea?

ANDIKO MUHIMU

“Nitasema kadiri ya unyofu wa moyo wangu; ninayoyajua nitayasema kwa uaminifu.”​—Ayubu 33:3, BHN.

PENDEKEZO

Ikiwa unaona ni vigumu kuketi na kuzungumza na mzazi (wazazi) wako kuhusu tatizo fulani, lizungumzie mnapotembea, mnapoendesha gari, au mnapoenda madukani pamoja.

JE, WAJUA . . . ?

Vile tu unavyoona ni vigumu kuzungumza na wazazi wako kuhusu mambo mazito, huenda wao pia wanaona ni vigumu au hawastahili kuzungumza nawe mambo hayo.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Wakati ujao nitakapohisi kwamba sitaki tena kuzungumza na wazazi wangu, nita . . .

Mzazi wangu akinisukuma nizungumzie habari ambayo sitaki kuizungumzia, nitamwambia

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini ni muhimu kuchagua wakati unaofaa wa kuwa na mazungumzo?​—Methali 25:11.

● Kwa nini kuna faida ya kuzungumza na wazazi wako?​—Ayubu 12:12.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

“Si rahisi nyakati zote kuzungumza na wazazi wako, lakini baada ya kuzungumza nao, unasikia ni kama umeondolewa mzigo mzito akilini mwako.”—Devenye

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kama vile kizuizi hakipaswi kuwa mwisho wa safari, unaweza kutafuta njia ya kuzungumza na wazazi wako!